MAMA YANGU ADUI YANGU -33-
Hata baada ya kuacha kazi bado aliendelea kupata usumbufu kutoka kwa Emma kwa kupigiwa simu bila kuzingatia alikuwa na nani. Pia, alikuwa
akimtumia ujumbe wa vitisho kitu kilichosababisha abadilishe namba yake ya simu ambayo hata miye sikuwa nayo.
Taarifa hizo nakumbuka nilipewa na mmoja wa wasichana tuliyekuwa tukifanya naye kazi.
Kwa kipindi kile sikuwa na shida naye kwa vile nilijua ana namba yangu lazima angenipigia na kunipa michapo yote.
Niliamini alichokifanya kilikuwa na masilahi kwake.
Dereva alipofika alinichukua na kunipeleka hospitali. Tulipowasili tuliwakuta wagonjwa wengi, nilisubiri kwa saa nzima ndipo nilipata nafasi ya kuonana na dokta Hindu.
SASA ENDELEA...
Mwaija usione nimekuweka shoga yangu, nilitaka niwapunguze watu ili nipate nafasi nzuri ya kuzungumza na wewe kwa kina.
Hakuna tatizo shoga yangu.
Sikuwa na maelezo mengine ya kumueleza zaidi ya yale niliyomwambia kwenye simu. Baada ya kuniuliza maswali alinifanyia vipimo vyote kisha alipima ujauzito wangu na kukuta kila kitu kikiwa sawa.
Mmh! Sasa hiki kitakuwa nini? dokta Hindu alishtuka.
Hata najua!
Kila kitu kinaonesha kipo sawa, ujauzito pia uko sawa, inawezekana ni hali ya kawaida ambayo haiathiri kitu.
Nina wasiwasi hali hii inaweza kuendelea.
Mmh! Sidhani kwa vile nimecheki hakuna dalili zozote za damu kuendelea kutoka.
Mmh! Ilinitisha sana.
Ondoa wasiwasi ujauzito wako upo sawa hata viungo vya karibu na mfuko wa uzazi vipo sawa.
Baada ya kuona hakuna tatizo nilirudi nyumbani kidogo moyo wangu ulikuwa umetulia. Wazo la kumwambia mama nilikuwa nalo lakini kutokana na maelezo ya daktari niliamini huenda damu iliyotoka usiku wa kuamkia siku ile ilikuwa ya mwisho.
Nilirudi nyumba na kujipumzisha huku msichana wangu wa kazi akitaka kujua majibu ya hospitali.
Vipi dada za huko?
Mmh! Nzuri, majibu ni yaleyale.
Unamaanisha nini?
Hakuna tatizo.
Sasa na hizo damu?
Inaonekana zimekata.
Ooh! Afadhali yaani hata mimi nilikuwa na wasiwasi sana.
Nashukuru kuguswa na matatizo yangu.
Yaani dada wewe kama Mungu wangu.
Aah! Hapana siwezi kuwa Mungu wako.
Kweli dada umeniokoa kwenye mateso.
Pamoja na hilo, lakini nitabakia kuwa mwanadamu wa kawaida, pamoja na wema wangu niliamini siwezi kufikia hata robo ya utukufu wa mitume nini Mungu!
Basi wewe ni mtu muhimu sana kwangu.
Hapo sawa.
Kwa vile alikuwa ameniandalia juisi alinipatia na kunywa kisha nilijipumzisha. Siku ile nilishinda katika hali nzuri japokuwa wasiwasi wangu ulikuwa ni kuumwa na tumbo, lakini hali ile haikujitokeza mpaka jioni ilipoingia.
Usiku ulipofika nililala vizuri mpaka siku ya pili. Nilipoamka cha kwanza kilikuwa kuangalia nguo ya ndani ambayo nilishangaa kuikuta ikiwa safi. Nilijichunguza na kujiona nilikuwa sawa, nilikwenda kuoga na kuisikilizia ile hali ambayo pia siku ilikatika nikiwa sawa. Mchana wa siku ile dokta Hindu alinipigia simu kutaka kujua maendeleo ya hali yangu nikamjulisha kwamba nilikuwa nikiendelea vizuri.
Sikujiamini moja kwa moja niliendelea kuisikilizia hali ile kwa siku tatu bila kuona mabadiliko.
Wiki ilipokatika bila kuiona damu, niliamini kuwa nimepona na tatizo lile limeisha.
Baada ya wiki ya pili kukatika nikiwa katika hali nzuri, niliamini naweza kukutana kimwili na mpenzi wangu.
Kama kawaida siku hiyo alikuja jioni kabla ya kuondoka nilimuomba akidhi haja zangu.
Japokuwa alitaka tuendelee kusubiri mpaka mwezi ukatike lakini nilimhakikishia kwamba nilikuwa sawa. Alinikubalia na tukakutana, safari ya kwanza tulienda vizuri.
Safari ya pili tukiwa katikati ya tendo nilihisi tumbo likivurugika kama vile nilikuwa nikitaka kuhara na nikamuomba mzee Sambi anyanyuke kwanza.
Samahani mpenzi hebu toka.
Kuna nini?
Tumbo limenivurugika ghafla.
Aliponyanyuka nilihisi kama nimeshikwa na haja ndogo. Nilikimbilia msalani na kuchutama na kusukuma kwa nguvu.
Ajabu haja ndogo iligoma kutoka lakini maumivu ya kutaka kujisaidia yalikuwa makali.
Niliendelea kulazimisha kusukuma huku mvurugano tumboni ukiwa mkubwa. Niliamini lile ni tumbo la kuhara, niliendelea kusukuma haja kubwa ambayo niliamini lazima nitaharisha kutokana na tumbo lilivyokuwa likinivuruga.
Lakini baada ya kujikamua sana nilitoa kinyesi kidogo kama cha mbuzi na kunishangaza, tumbo lilivyokuwa likinivuruga kutoa kinyesi kama kile wakati nilijua nitaharisha.
Niliendelea kujikamua huku haja ndogo ikiuma lakini iligoma kutoka. Niliendelea kujikamua huku maumivu chini ya kitovu yakiwa makali sana.
Nilijiuliza kile ni nini? Nilijuta kulazimisha kufanya mapenzi, japokuwa hayakuwa ya nguvu zaidi ya kufanya kwa tahadhari kubwa.
Mzee Sambi alinifuata msalani baada ya kuniona nimechelewa kutoka na kuniuliza:
Vipi mpenzi?
Yaani hii hali wala siielewi.
Kwa nini?
Haja ndogo imenishika mpaka kinena kinauma lakini haitoki. Tumbo nalo limevurugika lakini choo hakitoki hata sijui...yaani mbona nateseka mtoto wa kike, nilisema huku nikiuma meno kwa uchungu.
Sasa itakuwa nini! Au twende hospitali?
Su...su...mmh, nilisema huku nikiuma meno na kusukuma kwa nguvu baada ya kusikia kama kitu kikisogea mithili ya mtu anayejifungua.
Niliuma meno na kusukuma kwa nguvu zote. Mara kitu kilifyatuka kwa mbele na kufuatiwa na damu nyingi nyeusi.
Niliendelea kujikamua, damu iliendelea kutoka ikiwa mabongemabonge na kufika robo ya sinki la choo.
Ilikuwa damu nyeusi iliyokuwa ikinuka kama kitu kilichokuwa kimeoza.
Wakati huo nilianza kuharisha mfululizo kitu kilichonifanya niishiwe na nguvu na kuanguka msalani.
***
Niliposhtuka nilijikuta nikiwa hospitali, niliponyanyua macho niliwaona watu kwa shida, macho yangu yalikuwa kama yana ukungu.
Hata hivyo, nilibaini kwamba kulikuwa na watu waliokuwa wamejazana kitandani kwangu huku nikiongezewa damu.
Uwezo wa kuona vizuri sikuwa nao kwa vile nilipojitahidi kutizama vizuri niliona kitanda kikizunguka na kunifanya nifumbe macho, nilikuwa nimeshikwa na kizunguzungu kikali.
Niliisikia sauti ya mama ikiniita:
Mwaija...Mwaija.
Nilimsikia lakini sikuwa na uwezo wa kufumbua mdomo japokuwa nilijitahidi kuitikia. Nilikuwa najisikia vibaya na kizunguzungu kilikuwa kikali sana.
Nilitulia nikiwa nimefumba macho, kizunguzungu nacho kilipungua taratibu na usingizi ulinipitia.
Niliposhtuka nilijikuta nikiwa kitandani na mama na dada zangu walikuwa pembeni wakionesha kuwa na nyuso zenye huzuni.
Mara aliingia daktari na kusogea kitandani kwangu.
Mwaija, aliniita kwa sauti ya upole.
Abee, safari hii sauti ilitoka.
Unajisikiaje?
Kizunguzungu.
Kitaisha tu, damu uliyopoteza ilikuwa nyingi.
Damu!? Nilishtuka.
Ndiyo, ulikuja ukiwa na hali mbaya sana, mpaka sasa hivi unazungumza kweli Mungu mkubwa.
Itaendelea Jumamosi ijayo ....