MAMA YANGU ADUI YANGU - 43-
ILIPOISHIA:
"MAMA yako angeniona na kitu hicho angeanguka, ndiyo maana nilitakiwa nikuache na kuondoka haraka. Kama ningeendelea kuwepo kwenu, mama yako angekufa."
"Ni kwa nini?" niliuliza mkono wangu ukiwa shavuni.
SASA ENDELEA...
"Kwa sababu ya ubaya wake," alisema.
"Unafikiri kwa nini amekuwa na tabia hiyo?" nilimuuliza swali ambalo nilitakiwa nilijibu mimi mwenyewe.
"Ni roho mbaya na kupenda kushiriki mambo ya kishirikina yamemfanya apende kucheza michezo ya kichawi."
"Enhee, nini kiliendelea?"
"Kwanza nilikataa na kuamua kuachana na wazo hilo. Baada ya kubahatika kupata kazi katika mradi wa ujenzi wa Barabara ya Tanga.
"Nilifanya kazi kule kwa muda huku nikiwa na wazo la kutafuta njia mbadala tofauti na maelezo ya mganga.
"Lakini mganga alinieleza kama sijipendi nifanye kinyume na alivyonieleza. Baada ya kufanya kazi kwa muda nilipata nafasi ya kurudi nyumbani.
"Kabla ya kuja Dar nilirudi kwa mtaalamu ambaye alinieleza nifanye kama alivyonielekeza na kuniambia mambo nitakayoyakuta siku nitakayokuja kwenu na hali itakayojitokeza.
"Niliporudi Dar sikukaa, nilikuja kwenu na kila nilichoelezwa na mganga kilitokea ikiwa ni pamoja na mama yako kuanguka alipokuwa amekaa baada ya kushtuka aliponiona.
"Kwa kweli tukio lile lilinifanya nichukue uamuzi mgumu wa kukupa talaka na kukuacha na fumbo kuhusiana na talaka yako.
"Niliamini mama yako angekueleza lakini hakukueleza, nilipoondoka sikutaka kujua habari za nyuma. Leo unaponiona nina siku mbili na kesho naondoka kurudi nilipo, kwa yaliyonitokea nimejikuta sipendi tena kukaa katika jiji hili."
Mpaka Beka anamaliza kunieleza chanzo cha talaka yangu, macho yake yalikuwa yamejaa machozi. Si yeye tu, hata mimi muda wote nilikuwa nikilia huku nikitumia mtandio wangu wa kichwani kujifuta machozi.
Nilijitahidi kuzungumza japokuwa moyo wangu ulikuwa kama amechubuliwa katika kovu lililoanza kupona na maumivu yake yakawa mara mbili.
"Beka nakubaliana na wewe kwa asilimia mia kuwa, mama yangu anahusika lakini bado hukutakiwa kuutesa moyo wangu kwa maswali yasiyo na majibu.
"Najua pengine mimi ndiye niliyesababisha kwa kutoa siri ya kipato chetu kwa mama ila kwa vile ni mkeo ulitakiwa kuniweka wazi. Siamini kama kuna mwanadamu anaweza kuua bali kwa idhini ya Mungu.
"Hata kwenye riziki binadamu anaweza kuichelewesha si kuizuia kabisa.
"Beka ungekuwa wazi ningejua nifanye nini, pengine ukimya wako umenifanya nichungulie kaburi au ningezikwa ningali hai."
"Kwa nini?" Beka aliuliza macho yakiwa yamemtoka pima.
Nilimueleza yote yaliyotokea baada ya kunipa talaka, maisha niliyoishi na kufikia kuugua ugonjwa wa ajabu.
"Dah! Pole sana Mwaija, nina imani hata huyo bwana kuondoka kwake inawezekana mama yako amechangia."
"Inawezekana," nilimkubalia.
"Lazima ujiulize kwa nini mtu akukimbie wakati wa matatizo?" aliniuliza.
"Beka nashukuru kwa maelezo yako ambayo naamini yamechelewa kunifikia, nina imani leo hii tungekuwa pamoja."
"Ni kweli lakini sina wa kumlaumu bali wasiwasi wa nafsi yangu."
"Beka naomba nikapumzike kwa vile sijisikii vizuri, pia mwanangu nimemwacha muda mrefu."
"Ha! Mwaija una mtoto?" Beka alishtuka.
"Beka uliambiwa mi mgumba?"
"Mmh! Sawa," Beka alishusha pumzi nzito na kuinamisha kichwa.
"Beka naomba niondoke, kwani hali yangu siielewi nahisi mapigo ya moyo yananienda kasi," niliongea kwa shida kidogo.
"Hakuna tabu Mwaija kwa vile nina gari nitakupeleka."
"Hapana Beka, nitakodi teksi au nitamwita mume wangu anifuate."
"Kwa nini usumbuke nitakupeleka mara moja, kwa hali hii siwezi kukuacha peke yako."
"Hakuna tatizo."
Ilibidi nikubali kwa vile sikuelewa baada ya muda hali yangu ingeendeleaje. Kila nilivyofikiria nilikosa jibu na kujikuta moyo ukiniuma kama unataka kutoka na kuachana na mwili wangu.
Beka alinipeleka mpaka kwangu kwani hata nguvu za kutembea sikuwanazo. Nashukuru nilifika nyumbani salama na kuagana na Beka huku tukipeana namba za simu kwa ajili ya kuendelea kusalimiana kama marafiki si wapenzi tena.
Nilipofika ndani hali ilizidi kuwa mbaya, kila nilipoyakumbuka mambo yote yaliyokuwa yamejificha nyuma ya pazia.
"Kumbe mama yangu ndiye adui yangu!" nilijiambia mwenyewe moyoni.
Kichwa kiliniuma na mapigo ya moyo yalinienda kasi, nilimwambia msichana wa kazi amjulishe mume wangu kwa vile hata uwezo wa kupiga simu sikuwa nao.
Mume wangu baada ya kupewa taarifa alifika mara moja na kunikimbiza hospitalini. Niliambiwa kuwa presha ilikuwa juu sana na kuwafanya madaktari kupata kazi ya kuishusha.
Walifanikiwa baada ya saa mbili ndipo nilipata usingizi mpaka asubuhi. Taarifa zilimfikia mama, naye akawa wa kwanza kufika hospitalini na kufuatiwa na dada zangu.
Siri ya matatizo yangu sikumueleza mume wangu, alijua ni matatizo ya kawaida japokuwa hali ile haikuwahi kunitokea tangu aliponioa. Mama naye alishangaa na kutaka kujua presha ile ilisababishwa na nini.
Nilishindwa kumueleza ukweli, nilisingizia imetokea ghafla japokuwa mama alikataa katakata maelezo yangu.
"Hapana Mwaija, kwa maelezo aliyonipa mumeo nahisi kuna kitu mnanificha.Hebu niambie mama nini kimekusibu? Madaktari wamesema presha ile ingeweza kukupofua macho au kukufanya upooze mwili."
"Hata sijui nimejisikia tu mwili ukikosa nguvu na kumpigia simu mume wangu ambaye alinieleta hapa," bado niliificha siri ile.
"Mwaija mi' mtu mzima maisha ya ndoa nayajua, kama kuna kitu mumeo amekuudhi niambie ili tujue tufanye nini, sitaki yatokee ya mzee Sambi."
"Haki ya Mungu, kuhusu mume wangu utamuonea. Ananitunza kama malkia, hajawahi hata kunikemea tangu anioe na ananipenda kwa mapenzi ya dhati."
"Sasa tatizo ni nini?"
"Mama ni hali umenitokea tu, hata sielewi, pengine ni mawazo ya kutaka kuzikwa ningali hai, kila nikikumbuka moyo unanipaa," nilitengeneza uongo uliomfanya mama aamini.
"Lakini mwanangu mambo hayo si yameshaisha? Sasa hivi una ndoa yako nzuri, pia una mtoto, hebu achana na mambo hayo ili kuondoa kuishi kwa wasiwasi."
"Sawa mama nimekuelewa nitajitahidi kusahau."
"Itabidi ufanyiwe na kisomo."
"Hakuna tatizo."
Kila alilokuwa akilifanya mama na kutoa maneno yenye faraja, yaliufanya moyo wangu uzidi kuwa njia panda kwa kutoamini kama mbaya ni yeye.
Niliamini lile lilikuwa fumbo zito ambalo alilifahamu mama Amina peke yake, yeye ndiye aliyekuwa na majibu ya maswali yangu. Nilipanga nikitoka hospitali na kutulia, nimfungie safari ili akanieleze ukweli, nilikuwa radhi kumpa kiasi chochote atakachokitaka ili tu anieleze ukweli.
Baada ya hali yangu kuwa nzuri niliruhusiwa na kurudi nyumbani. Mume wangu naye alitaka kujua sababu ya tatizo lile kama alikuwa amelisababisha yeye. Naye nilimdanganya sababu ile ilitokana na kukumbuka hali iliyonitokea siku za nyuma.
Alinisihi nisiwaze vitu vilivyopita kwa vile ananitunza kama mboni ya jicho lake. Nilimhakikishia hali ile haitajitokeza tena, maneno yangu yalimfariji mume wangu na kurudisha tabasamu lililopotea baada ya kuwa na wasiwasi wa tatizo langu.
Nilijitahidi kuwa katika hali ya kawaida ili niweze kuwatoa wasiwasi wote na kunipa nafasi ya kuweza kwenda kwa mama Amina. Siku zilikatika nikiwa katika hali ya kawaida.
Baada ya wote kuamini kuwa nilikuwa sawa, nilifunga safari hadi kwa mama Amina ili kujua ukweli.
Aliponiona nikiwa katika afya njema na mwili wangu ukiwa umerudi kama zamani, alifurahi sana.
ITAENDELEA TENA JUMAPILI IJAYO...