Mkutano wa 13 wa Baraza la Washauri la China na Afrika ulifanyika hivi karibuni jijini Dar es Salaam, Tanzania. Mkutano huo ulifikia "Makubaliano ya Kukuza Maendeleo na Ushirikiano wa Kimataifa kati ya China na Afrika," unaojulikana pia kama "Makubaliano ya Dar es Salaam." Kama mafanikio muhimu ya China na Afrika katika harakati zao za kujiendeleza kisasa, makubaliano hayo yanavunja zaidi fikra potofu kwamba "maendeleo ya kisasa ni sawa na mambo ya kimagharibi."
"Makubaliano ya Dar es Salaam" yanapendekeza kuzingatia maendeleo kwanza na kuchunguza njia ya maendeleo ambayo ni huru, kuheshimiana na kufunzana, na inayotoa kipaumbele kwa watu, na hii ndio taswira ya kweli ya ushirikiano kati ya China na Afrika katika miaka ya hivi karibuni. Kama nchi kubwa zaidi inayoendelea, China siku zote imekuwa ikizingatia maendeleo ya pamoja kama msingi wa ushirikiano kati ya China na Afrika. Katika kipindi cha miaka 15 iliyopita, China imekuwa mshirika mkubwa zaidi wa kibiashara na mwekezaji mkubwa barani Afrika miongoni mwa nchi zinazoendelea.
Katika Mazungumzo ya Viongozi wa China na Afrika mwezi Agosti mwaka 2023, Rais Xi Jinping wa China aliahidi kuunga mkono kithabiti Afrika kujiendeleza kisasa na kupendekeza hatua tatu za kuunga mkono ukuaji wa viwanda wa Afrika, kilimo cha kisasa na ushirikiano wa kuandaa wataalam. Kwa hiyo, kufikiwa kwa "Makubaliano ya Dar es Salaam" kunaonyesha kuwa, ushirikiano kati ya China na Afrika umeingia kwenye kipindi cha maingiliano ya kina ya dhana za maendeleo kutoka mradi mmoja mmoja wa maendeleo.
Hali halisi imethibitisha kuwa mtindo wa maendeleo unaokuzwa na nchi za Magharibi katika nchi zinazoendelea kama vile za Afrika haujaleta matokeo yaliyotarajiwa, na badala yake kumesababisha Afrika kuingia katika mtego wa kutegemea misaada na mikopo. "Makubaliano ya Dar es Salaam" yaliyotolewa kwa pamoja na China na Afrika safari hii yanatokana na uzoefu muhimu wa jinsi China inavyojiendeleza kisasa, uchambuzi mpana wa historia na hali halisi ya Afrika, na pia jinsi dunia hii inavyoendelea kwa ujumla, jambo ambalo lina maana kubwa katika kuvunja dhana potofu kwamba "kisasa ni kimagharibi".
Katika miaka ya hivi karibuni, China imekuwa ikisisitiza ujenzi wa jumuiya ya hali ya juu yenye mustakabali wa pamoja kati ya China na Afrika. Maana ya hali ya juu, ni kuwa jumuiya yenye mustakabali wa pamoja kati ya China na Afrika haipaswi kutegemea mradi mmoja mmoja pekee, lakini pia inapaswa kuboresha kwa mapana dhana ya jumuiya yenye mustakabali wa pamoja wa China na Afrika - yaani, China na Afrika katika msingi wa matunda yaliyopatikana katika ushirikiano wa kivitendo, pande hizo mbili zitaendelea kufanya mazungumzo na ushirikiano katika nyanja kama vile utawala wa nchi na dhana za kutafuta maendeleo ya kisasa.
Mkutano mpya wa Baraza la Ushirikiano kati ya China na Afrika (FOCAC) utafanyika baadaye mwaka huu. Viongozi wa China na Afrika watakusanyika tena na kupanga kwa makini mpango mpya wa ushirikiano kati ya China na Afrika na kuzingatia kuwanufaisha watu wa pande zote mbili.
Kutolewa kwa "Makubaliano ya Dar es Salaam" ni hatua muhimu katika kubadilishana dhana ya maendeleo kati ya China na Afrika kwenye njia ya kujenga jumuiya ya hali ya juu ya China na Afrika yenye mustakabali wa pamoja, na kutahimiza ushirikiano wa kina kati ya China na Afrika ili kuhudumia vizuri maendeleo ya China na Afrika mtawalia.