Makapuku Forum

Makapuku Forum

Mkuu hapa unaongelea ugumu wa maisha kwa ujumla au individually?
Kwa ujumla mkuu.
Nahitaji tubadilishane uzoefu wa maisha ili kila moja afaidi mbinu za mwenzie...mfano ukiwa mfanyakazi siku zote mshahara huwa hutoshi, nini kifanyike sambamba na kazi yako angalau kupunguza makali ya maisha au kama huna ajira utafanyaje ili utoke kimaisha?
 
SEHEMU YA KUMI NA MOJA
SEHEMU YA KUMI NA MOJA
KITENDO cha kujikuta namweka mama yangu mzazi na Anitha katikia mzani mmoja ili nijue nini cha kufanya na nani wa kuanzia kilinivuruga akili akili. Kuna mda nililazimika kusema kwa sauti ilhali hakuna yeyote aliyekuwa akinisikiliza. Nilihaha huku na kule katika mkoa ule wa Iringa na bado hali ilikuwa tete.
Sikuwa na ndugu, rafiki na hata jamaa wa karibu wa kuweza kumshirikisha lolote lile. Niliketi chini ya ule mti na pasipokutarajia nikapitiwa na usingizi. Bila shaka kutokana na mawazo yaliyokuwa yanazidi badala ya kupungua.
Mimi naitwa marehemu!! Ni nani huyu anasimama nyuma ya haya mambo yote? Niliwaza baada ya kurejewa tena na uhai baada ya kifo cha usingizi!!
Mkononi nilikuwa na bahasha yangu ambayo thamani yake ilizidi kushuka badala ya kuongezeka. Bahasha ambayo badala ya kunipa tumaini iliishia kunipa dalili tu ya matumaini kisha yakatoweka pasipo kutimia. Bahasha ambayo sasa imenionyesha picha ya mtoto ambaye ameketi na ni picha hiyohiyo kutoka katika barua pepe aliyonitumia Anitha.
Anitha ambaye sasa sipo naye tena na sijui ni kitu gani kimemsibu!!
Mbaya zaidi nimetumiwa ujumbe kuwa NITAMFUATA…sasa namfuata wapi mimi eeh!!
Na huku mama anatishiwa kukatwa kichwa iwapo tu kichwa change hakitaonekana!! Mimi ambaye nipo hai.
Washenzi wameamua kuigusa familia yangu ili nijitokeze waniue!!! Ni hili nililitambua kichwani mwangu.
Mbaya zaidi sikuwa tayari kujitokeza kwa mtu yeyote yule kabla sijajiweka salama.
Kilichonipa faraja ni maneno ya Anitha usiku ule tuliokutana kwa mara ya kwanza tangu atoroke nyumbani kwao.
“Pesa ni kila kitu!!” nikafanya tabasamu na kisha nikautazama ule mfuko wenye pesa zilizohifadhiwa katika usalama wa hali ya juu!!
Asante sana Anitha!!! Sijui kama zisingekuwepo pesa hizi ningekuwa katika mawazo gani mengine!! Nilijisemea. Na hapo nikanyanyuka na kupiga hatua nyingi kuelekea popote pale na sikuwa nikitambua majina ya mitaa mingi!!
Kufikia hapo nikaamini kuwa nilikuwa nahitaji kwa namna yoyote ile mwenyeji wa mkoa huo aweze kuwa mwanga wangu. Lakini kigumu zaidi nililazimika kupata mwenyeji asiyenifahamu!!
Jambo gumu kabisa, utajuaje mtu hakufahamu!!!
Nikaghairi.
Maamuzi ya pili yakawa ‘jino kwa jino’.
Nikapanga safari ya kwenda Morogoro. Kwanza niwakabili jino kwa jino hao watu wanaotishia amani ya mama yangu halafu kitakachofuata hapo na lolote liwe lakini walau nimpiganie mama yangu!!!
Kwa Anitha sikujua wapi naanzia hivyo huenda ni vyema kupata moja kuliko kukosa yote, isitoshe Anitha alikuwa ni askari aliye tayari kufia vitani akitetea haki!!
Nikalala bila kula chochote, asubuhi sana nikadamkia katika stendi ya Iringa.
Baridi ilikuwa kali sana!! Na basi lilikuwa halijafika, hali ile ya hewa ikanikumbusha jijini Dar es salaam, siku ambayo nakutana na mauzauza ya Ezekiel wawili mmoja mzima na mwingine maiti.
Kisha baada ya masaa kadhaa nakumbwa na kashfa ya kulawiti hadi kuua!!
Uchachu ukanikumba mdomo baada ya kuwaza siku hiyo. Nikatafuta sigara nikawasha na kuanza kupuliza kama siku ile!!!
Nilipopiga funda nne, basi likawasili. Nikaionea huruma ile sigara lakini nikalazimika kuizima kisha kuisagia chini!!
Nikaelekea garini!! Nikapata siti ya dirishani. Nilikuwa sijielewi hata kidogo lakini nilijua naikaribia shari.
Kelele za vijana wauza maji, soda na vinywaji vingine hazikunifurahisha bali kunibughuzi. Mara huyu apige mayowe haya mwingine alalamike vile ilimradi tu bughudha.
“Pata Bajia, Sambusa za leoleo, sambusa za moto mtoto anapoozewa, sambusa za nyama achana na zile za Singida mwawekewa nyama ya punda, usisikie ya watu wahehe wala mbwa…uzushi mtupu kula mwenyewe ujionee kisha ukahadithie. Ukinunua moja nakupa na picha ya huyo ng’ombe aliyechinjwa!! Usiwasikilize wazushi, niulize mimi mama lao!!” hizi zilikuwa porojo nyingine tena, sauti hii ilipangilia maneno hasa na ilikuwa ikirudia mara kwa mara bila kukosea hata kidogo!! Abiria waliokuwa garini wakajikuta wanacheka, lakini katika kucheka huko wengine wakataka kununua kweli. Mimi nikajituliza huku nikijilazimisha kusahau kama nimesikia porojo zile sikuwa na hamu ya bajia wala sambusa za nyama ambazo yule mama alipinga kabisa kuwa sio nyama ya mbwa!!!
Baada ya muda kidogo sauti ile ilihamia katika gari ndani! Mama aliendelea kutuliwaza abiria na maneno yake. Nikavutiwa kunyanyua kichwa nimtazame vyema anafanania vipi huyu mama mwenye uwezo wa ajabu vile wa kukariri.
Lahaula!! Sura haikuwa ngeni machoni mwangu!! Alikuwa ni mama ama niite mwanamke ambaye siku kadhaa nyuma tulisafiri naye wakati tunatoka jijini Dar es saalam, porojo zake zikatufanya tuijue kiasi Michigani.
Sasa alikuwa katika basi letu!!
Nikataka kumpuuzia lakini imani ikanivuta kumuamini kiasi, nikaisshusha vyema kofia yangu ikaniziba sura yangu. Na mimi nikaomba huduma ya sambusa.
Akajongea nilipokuwa huku akiendelea kuhamasisha juu ya sambusa zake.
“Anti samahani naweza kuuliza?” nilianza kujenga hoja.
“Wahehe, Wabena, Wakinga asili yetu ustaarabu na ukarimu, ukitukera hatulipi kisasi siye twajinyonga tu!! Niambie bila shida baba yangu!!” alinijibu huku akinifungia sambusa tatu kama nilivyomwagiza.
“Hivi ni wewe tumesafiri wote majuzi kutoka Dar tuka….”
Kabla sijamalizia tayari alikwisha nitambua.
“Wa Michigani nyieeee ni wewe looh, yukwapi bibi yako yule mbona ana wivu sana yule.” Alinieleza kwa sauti ya chini nikasikia peke yangu.
“Hayupo leo mamangu kuna matatizo yamemkumba…”
“Alienda Michigani ama?” aliniuliza kwa sauti tulivu, sasa hakuwa katika utani wowote ule. Uso wake ulionyesha wasiwasi na ni kama kuna kitu hakupenda kiwe kama anavyodhani. Hakutaka jibu langu liwe kweli.
“Hapana ni matatizo mengine tu, kwanini umewazia Michigan?” nilihoji huku nikiuficha wasiwasi wangu.
“Mh…..afadhali kama sio huko maana….ehee we nawe tena mbona unarudi mwenyewe Dar es salaam” alihoji na sasa alikuwa anatabasamu.
“Hata sirudi Dar ujue, hivi tunaweza kuongea kidogo.” Niliamua kutumia nafasi.
“Lakini bado dakika mbili gari linaondoka hapa.” Alinitahadharisha. Nikamweleza haikuwa muhimu kusafiri wakati sijazungumza naye.
Akakubaliana nami, tukatelemka chini huku akisifia sambusa zake.
Mwanga ulikuwa umeanza kuonekana na giza likaipisha nuru! Tukajiweka mbali na umati wa watu. Nikamweleza shida yangu.
Nikamweleza juu ya Anitha na kupotea kwake katika namna ya utata.
Sikumuamini kiundani na kumweleza juu ya hatia inayonikabili jijini dare s saalam juu ya mauaji. Nilimuacha yeye awe msemaji mkuu.
“Kaka Sambusa zangu zitaniozea lakini ujue.” Alinitahadharisha.
“Kwani kapu moja bei gani kwa ujumla.” Akanitajia bei, nikamweleza kuwa nitamlipa mara mbili. Na kama hakuamini vile nikajipekua na kutoka na kiasi alichotaja na ziada yake.
Macho yakamtoka pima na bado hakuonekana kunitambua!!
Mazungumzo yakaanzia pale, yule mwanamke akanieleza machache ayajuayo juu ya mkoa ule. Akapinga kabisa kuwa Anitha amechukuliwa kishirikina. Akapinga kuwa mkoa ule hauna mambo hayo ya kurogana.
“Tena basi bora angekuwa mwenyeji wa huku!! Yaani mgeni hana hata siku nne!! Mi nakataa kwa kweli labda tu kuna mwanaume amemuweka ndani wewe hujui.” Alinijibu kiuhakika zaidi. Nikatamani kumweleza japo kwa ufupi kuwa mimi ni nani lakini niliingiwa hofu.
Nikamuona kama anafikiria jambo kidogo na kisha akasema kwa sauti ya chini kama anayejisemea mwenyewe.
“Auuu labda mambo ya Anti Ezekiel yameanza tena…lakini hamna wala haiwezekani.”
Maneno yake yakanishtua, alikuwa ametaja jambo zito katika sauti ndogo!!
Anti Ezekiel!! Jina hili lilihusiana na mkasa wangu moja kwa moja. Nikakosa ustahimilivu nikahoji.
“Anti Ezekiel ndo nani kwani?”
“Jamaa aliyeleta uzushi huo na yeye ukimuuliza anakwambia jibu hili moja tu UKIJUA NA WEWE UNAPOTEA” alinijibu kwa utaratibu na hakutaka kulizungumzia zaidi.
“Nani anayesema habari hizo kwani?’ sikutaka jambo hili liishie juu ya juu. Nikambana.
“Simfahamu lakini wanasema ni kichaa mmoja hivi. Hakuna atakaye kuamini kuhusu hilo. Si unajua maneno ya vichaa, kwa jinsi nilivyosimuliwa ni kwamba watu walikuwa wakipotea, waganga wa jadi wakishinda kupata majibu yeye anasema ni upepo wa Anti Ezekiel. Mbona huu mwaka wa nne unafika sasa tangu zivume hizi habari.” Alinieleza kwa utulivu huku akiyatuliza macho yake usoni kwangu.
Maelezo yake yakazidi kunichanganya, sasa yule Ezekiel nd’o anafanya nini sasa, mara amekufa mara akaonekana Ubungo, sasa huku Iringa tena kuna Anti Ezekiel wao. Upuuzi huu. Nilihisi kuchanganyikiwa.
“Kwani kaka, Anitha yeye kapoteaje ghafla hivyo!! Tatizo lako ni moja tu wewe unanificha siri huku ukisahau kuwa mficha uchi hazai. Na mficha jipu usaha utamuumbua….” Alinipiga na maneno yale makali, nikajisikia aibu sana maana alikuwa amesema kweli.
“Sio kama nakuficha mama…hapana nimechanganyikiwa kabisa!!!”
“Unadhani suluhu n’do kukaa kimya kaka!!” alizidi kunibana.
Kabla sijasema lolote akachukua uwanja zaidi.
“Sam..” akaniita. Moyo ukapiga kwa nguvu kubwa!! Amenijuaje jina langu huyu mwanamke ilhali siku ya safari sikujitambulisha kwa lolote lile.
“Unajiuliza nimekujuaje?” alisema kilichokuwa katika akili yangu!!
“Sam mdogo wangu! Ama kaka yangu vyovyote vile, katika mawazo yako unadhani mimi ni mtu mbaya ama ninayeweza kuhatarisha amani yako ambayo tayari ipo hatarini. Sam mimi sipo hivyo, nd’o maana hata kwenye basi tulilopanda nilikutambua kuwa unasakwa kwa udi na uvumba lakini je nilisema neon lolote mie! Nilishakoma tabia ya kujifanya najua mambo, biashara yangu ya bajia na sambusa inanitosha sana.
Sihitaji kupata mamilioni kwa kumsukumiza kijana mwenzangu katika moto. Baba yangu amefia jela kwa kosa la kusingiziwa, nitajuaje kama na wewe wanakusingizia, ujue polisi watu wa ajabu sana, wanapenda sana kusaidiwa upelelezi lakini wewe sasa uwe na shida uwaombe msaada nd’o utakoma na kiherehere chako. kama walishindwa kuniruhusu tu kuongea na baba yangu!! Wakanitishia kunifunga, niwapendee nini mimi sasa!!
Mzeewangu akahusishwa na wanaume wengine wanane eti wamehusika kuteketeza Michigani?? Mimi nilikuwa mfanyakazi pale ndani, Michigani haikuwa ya kuteketezwa na watu masikini kama wale. Haya masikini ana haki, Michigani ikateketea na baba naye akafungwa!! Nd’o mimi unayeniona hapa sasa Iringa nd’o mama lao. Yaani sina ndugu wala shoga, napiga kazi tu kupata mkate wangu wa kila siku. Kama wewe usivyomwamini mtu kwa mkasa wako huu na mimi simwamini mtu.
Nilipokuona nikakutambua, machoni hukufanania na mlawiti na muuaji. Tena juzi niliposoma gazetini kuwa umekufa nd’o nikajua kabisa kuwa kuna mpango hapa si bure!! Kama kweli umekufa mbona upo hapa muda huu? “ sasa aliniuliza na kisha kunitazama usoni.
Sikuwa na nguvu za kukimbia, ganzi ilishika mwili mzima. Huyu mwanamke alikuwa ananijua vyema kuliko nilivyodhani!! Na ilikuwa kama bahati tu hakuweza kunichoma popote pale.
“Naiwa Jojina usiniite mama lao!!” akajitambulisha jina lake hatimaye.
Nisingekuwa na lolote la kujitetea, nisingeweza kulaghai tena. Jojina alikuwa ananitambua vyema!!
Nikajaribu kumwomba radhi, akanielewa huku akinisisitiza ni vyema niishi kwa tahadhari kubwa.
“Sasa huyu Anitha, sina hata la kukusaidia lakini kama maneno ya yule chizi yapo sahihi basi kile kitabia cha Anti Ezekiel kinaweza kuwa kimeondoka naye.” Alinieleza huku akijaribu kutabasamu.
“Chizi mwenyewe anayesema hivyo yupo wapi…..” nikaamua kuuliza.
“Mh!! Kwa kweli ni miezi mingi sana imepita tangu nimwone. Nitakudanganya nikikwambia kuwa yupo Iringa hii. Kuna watu wanadai alionekana Dar es salaam, sasa sijui kama ni kweli ama la!!” alinijibu baada ya kufikiria kwa sekunde kadhaa.
“Na uliwahi kumtambua hata jina lake kwani?”
“Alikuwa na majina mengi sana mara wengine wamwite mganga wa jadi mstaafu, wengine walimuita Zuzu…lakini kuna waliodai kumfahamu na wakasema jina lake halisi ni Kindole, wakamfupisha na kumwita Kindo!!!”
“Nini?” nilihamanika nisiamini kile ninachokisikia. Yaani Kindo nimjuaye ama Kindo mwingine, Kindo alikuwa kichaa? Mbona alikuwa timamu jijini Dar es salaam. Nilijiuliza katika nafsi yangu!!
“Na kama ni kweli alikufa basi ndo yaleyale ya Anti Ezekiel labda maana maneno huumba!!!” aligandamiza tena yule mama na kuzidi kunichanganya!!!
**JIFUNZE!! SIRI ni siri iwapo ni ya kwako wewe na moyo wako!! Usijidanganye kumshirikisha rafiki yako na kumwambia akutunzie siri hiyo. Wanadamu hubadilika, leo wamuona mwema na kumkabidhi siri zako kesho anazifanya siri hizo fimbo ya kukuchapia!!!
 
SEHEMU YA KUMI NA MBILI
SEHEMU YA KUMI NA MBILI

Nilishangazwa na majibu ya Jojina yaani ni kama alikuwa akijaribu kuniimbia mashairi ambayo yameunganika vyema yakijali uzani wa vina na masivina lakini yakikosa mstari wa mwisho kila mara.
Mara anieleze juu ya michigani, lakini mwishowe hiyo Michigani yenyewe haipo tena.
Anazungumzia mkasa wa Anti Ezekiel ikiwa hamjui wala hana uhakika juu ya kiumbe cha kuitwa jina hilo.
Huyohoyo anadai kuwa Kindo ambaye ana wazimu alikuwa akisema sana juu ya Anti Ezekiel lakini mwishowe huyo Kindo hayupo tena Iringa na mbaya zaidi hajulikani alipo nan i tetesi tu kuwa alioneka Dar mara ya mwisho.
Kama kweli ni huyo kindo Aliyeonekana dar basi kwa namna yoyote tunahangaisha vichwa kumzungumzia mtu aliyeuwawa siku kadhaa nyuma baada ya kuchukuliwa na watu wasiojulikana.
Hawa watu wasiojulikana nd’o hao hao waliomuua Ezekiel, ndo haohao waliomchukua mke wangu na hawa hawa wamenizushia kuwa nimekufa na wamemweka mama yangu katika wakati mgumu kupindukia.
Hawa watu nd’o wanadai kuwa nitamfuata Anitha, na nitamfuata mama Eva.
Hawa watu ni akina nani!!!
Swali hilo likanitia kati kati ya hasira na mtafaruku wa kimawazo. Hawa watu walikuwa wamenizidi ujanja na tayari walishacheza na akili ya watu wa kuaminika serikalini ili nisiaminiwe popote pale!!
“Kwa hiyo dada Jojina….huyo Kindo wewe uliwahi kumuona ama!!”
“Nd’o maanake, hapa Iringa nani ambaye hakumjua na wazimu wake yule bwana. Zaidi lilikuwa skendo lake la Michigan…….”
“Skendo la Michigani?? Kiaje skendo la Michigani, yaani unanichanganya kweli dadangu hujui tu!!”
“Nakuchanganya na kipi tena, nakujibu kila unachouliza kadri ya uwezo wangu!!....na ninajitahidi zaidi ili ikiwezekana leo nyumba yangu iwe na mgeni.” Akazungumza kwa madaha kisha akanitazama kwa jicho fulani nikaelewa maana yake…sikutaka kuyakuza mambo zaidi nikamuuliza kwa utulivu nini kilijiri huko Michigani.
“Wanaomfahamu huyo wa kuitwa Kindo wanadai kuwa alichanganyikiwa baada tu ya kutoka Michigani.”
Akanitazama kisha aakaendelea, “Kindo alikuwa muajiriwa huko Michigani, kilichomtoa huko hakijulikani lakini baada tu ya kutoka huko siku kadhaa mbele Kindo ana wazimu!! Lakini usiniulize maswali mengi maana mimi sijui lolote nazisikia simulizi hizi nikiwa nauza bajia zangu na sambusa za nyama.” Alinijibu kizembe, ni kama alikuwa amechoshwa na maswali.
Majira ya mchahna tulikuwa tukitembea kwa tahadhari, tukakipita chuo cha Tumaini na hapo akanieleza kuwa mahali niliposimama ndipo Michigani.
Nilikata tamaa kwa sababu hapakuwa na sehemu ya kuanzia, ni kama makumbusho tu ya kale ambayo yamevunjwa na kusahaulika zamani sana. Hapakuwa na ulinzi wala mtu yeyote aliyekuwa akijihangaisha na eneo lile. Na hakuna aliyehangaika kutuuliza ni kitu gani tulikuwa tunatafuta.
Sikuwa na la zaidi, nikaondoka na mama yule hadi nyumbani kwake, huko nia ikiwa moja tu kujua zaidi kuhusu Michigani.
Tulipofika alinionyesha picha za Michigani hiyo ya zamani ambayo iliteketea yote miezi mingi nyuma!!
Ilikuwa sehemu ya kuvutia, palikuwa na bwawa kubwa la kuogelea, hoteli ya kifahari iliyoitwa Michigani na bustani ya kisasa.
“Siku za sikukuu palikuwa panajaa sana hapa, sio unajua mambo ya watoto na wazazi wao??” aliniambia wakati tukiingalia picha ya Michigani.
“Ungeweza kuona maeneo mengi lakini si kila eneo tuliruhusiwa kupiga picha kirahisi, hata hii yenyewe ni basi tu niliipata kibahati. Watu wana mambo, visheria vya ajabu ajabu kama nini!!!” alilalamika. Lakini akiona ufahari na kisha kujisifu kuwa yeye ni mama wa mjini alifanikiwa ajuavyo.
“Wewe uliipataje sasa.”
Kabla ya kujibu swali hili akacheka.
Kama nilivyokueleza awali juu yam zee wangu kuchukuliwa na skendo hili la kuichoma Michigani jambo ambalo hata naenda kaburini nitalikana kwa nguvu zote. Kweli nilibahatika kuingia katika mahusiano na bwana mmoja mtu mkubwa kidogo pale Michigani, basi nikawa nahudumiwa kila kitu kwa bili yake, hakuwahi kunieleza kwa nini picha hazipigwi hata zile za kumbukumbu!! Mzee wangu akazinasa hizi habari, akaniweka kitako kunikanya kuwa Michigani kuna mazingaombwe yanayofanana na ushirikina. Kwani kila sikukuu ifikapo basi kuna watoto zaidi ya watano wanapotea na wasionekane tena. Baba alisisitiza kuwa anaifahamu vyema michigani kuwa watu wake si wazuri, akanisihi nijiweke mbali nisije kupoteza mtoto wangu kwa hila za wanadamu, mtoto huyo alikuwa akiitwa Justin na nilimzaa bahati mbaya tuseme. Baba yake alikimbia, maneno ya baba yakaja na ukweli ndani yake lakini nilikuwa nimechelewa na wala sikutaka kuamini hata kidogo kuwa mwanangu amepotea eti kisa Michigani, japo alipotea siku ya sikukuu pia.
Tulizunguka kwa waganga wa kienyeji lakini hakuna hata mmoja aliyesema ukweli wote walitulaghai. Baba alibaki kusema kichinichini kuwa Michigani hiyo Michigani!! Hakuwa na maelezo ya kutosha labda na yeye hakujua vyema kama mimi nilivyobisha bila kujua neon lolote hadi leo nipo ndotoni.
Nikiwa na mapenzi tele na Dulla huyo mtu mzito wa Michigani nikafikia hatua ya kumweleza hisia za mzee wangu juu ya mtoto wangu kupotea. Dulla akapinga na kusema kuwa baba anazeeka vibaya. Name nikamuunga mkono. Hiyo siku tulifurahi sana, akiwa kama mpenzi akanitembeza maeneo kadha wa kadha akiahidi pia kuwa atakuja nyumbani kujitambulisha kwa baba ili anioe moja kwa moja!! Kwa kuhitimisha furaha yetu akanipa picha hii inayoonyesha maeneo kadhaa ya Michigani.
Baada ya juma moja Michigani ikaungua moto!!!
Siku tatu baadaye baba yangu akaanza kusakwa, akapatikana na alivyopotezwa……alivyopotezwa!!!! Basi tu Mungu anajua” kufikia hapa Jojina akaanza kutokwa na machozi, ilikuwa ni kumbukumbu mbaya sana kwake, lakini ikiwa ni kumbukumbu yenye mafumbo makali ndani yake bila yeye wala mimi kujua majibu!!
“Kwa nini sasa Dulla hakukusaidia katika kumsaidia mzee wako asiende jela.” Nilimuuliza.
“Dulla…Dulla hakuonekana tena, masikini yaani wanadai kuwa hakuna hata mtu mmoja aliyekufa lakini nina mashaka kuwa huenda Dulla alikufa.”
“Kwanini una mashaka hayo sasa!!!”
“Kwa sababu sijawahi kumuona tena na kuna jamaa zake wa karibu walinihakikishai kuwa Dulla alikufa. Na hapo nikaamua kubadilika na kuwa mama lao. Kila biashara nafanya.” Alimaliza kwa mbwembwe huku akilazimisha tabasamu.
Maneno ya mama lao Jojina yalizidi kunivuruga, badala ya mwanga likawa giza tena. Mkasa mmoja haujaisha inaongezeka mikasa mingine lukuki.
Mtoto wa Jojina kupotea, kisha Michigani kuteketea, baba yake Jojina kupotezwa katika uso wa dunia katika namna ya kustaajabisha!!
Michigani ya kwenye picha haikuwepo tena duniani!!!
Kuna nini Michigani?
Swali halikupata jibu!!
“Dulla wangu jamani eeeh!!” alianza kulia chinichini huku akiwa ameikumbatia picha fulani ambayo hakuwa amenionyesha kabla. Nilimbembeleza taratibu, hadi alipoitua ile picha kisha tukahamia katika mazungumzo ya hapa na pale, akanichombeza name nikamchombeza lakini hapakuwa na muda wa kuendelea mbele zaidi. Akasikika muuza magazeti.
“Wacha wee hebu ngoja nikakwapua gazeti, halafu leo kachelewesha huyo. Kuna hadithi nafuatilia magazetini, nakuja Sam usiwe mpweke.” Alinisihi kisha akatoka nje.
Alipotoka nikaupangusa mdomo wangu, sikuwa nimefurahia kumbusu mdomoni, lakini ilinilazimu kufanya vile maana nilihitaji kujua mengi sana kutoka kwa mama lao. Nilikubali kumbusu lakini moyoni nikijiapiza kuwa sitaendelea zaidi japokuwa baridi la Iringa lilitia hamasa kuendelea zaidi.
Nikajiandaa kumkabili akirejea kwa maneno ya kumhadaa ili niondoke pale kwake, nikaupanga uongo nao ukapangika.
Alipoingia badala ya kuniparamia pale kitandani, akanitazama huku akistaajabu.
“Sam!!” aliniita, nikageuka kumtazama, hakuwa kimahaba tena.
“Mkeo….mh!! mkeo anajua ulipo?” aliniuliza, nikaketi kitako niweze kujua nini kinaendelea.
“Kwanini?” nilimuuliza kwa kiherehere nikitaka kujua kulikoni.
“Si ndio huyu Edna ama …mama Eva si nd’o hivyo!!” alizidi kunivuruga.
Uvumilivu ukanishinda nikasimama na kuangalia anachokisoma.
Ilikuwa picha ya mke wangu Edna ama mama Eva kama nilivyomzoea. Sura yake kama niijuavyo ilikuwa inatabasamu!!!
Chini ya ile picha iliandikwa kitu ambacho nilitumia sekunde nyingi kurudia kukisoma.
MAREHEMU EDNA KIMARO!!
Nguvu zikaniishia, nikajitahidi kujizuia lakini ikashindikana na hapo nikaanza kuona giza ..
Kisha…..kisha …..nikaona kitu cha ajabu sana nikatami kukitazama zaidi lakini sikuweza kiza kikazidi kutanda kisha kimyaaa!!!!
Baadaye nilijikuta katika mikono ya uvuguvugu kiza kinene, nikajigeuza huku na huku nikaisikia sauti ikikwaruzakwaruza huku ikiliita jina langu!!
Nilijaribu kuvuta kumbukumbu zaidi kuwa ni wapi nipo.
“Sam!!” sauti iliita tena!! Sasa haikuwa ikikwaruza, ilikuwa sauti ya mama lao. Name nilikuwa nimekumbatiwa vyema na ule uvuguvugu ulitoka kwake.
Feni ilikuwa ikinipuliza!!
Mama lao akanyanyuka na kuwasha taa.
Akanieleza kuwa nilipoteza fahamu!! Kisha bila kunipa nafasi ya kusema chochote akanisihi kuwa sitakiwi kuamini kila ninachokiona wakati wa matatizo.
“Sam sidhani kama mkeo anaweza kulemazwa akili kiasi hicho, yaani hapana kabisa..” alishindwa kuendelea akanirushia gazeti.
Nikaisoma ile habari.
Eti mke wangu alikuwa katika msafara wa kusafirisha maiti yangu kuelekea mjini Morogoro, walipofika chalinze wakapata ajali mbaya ambapo maiti ilipotelea katika korongo na mke wangu akiumia vibaya kabla ya kupoteza uhai!!
Mimi ni mwandishi, nikamshangaa mwandishi mwenzangu aliyelishwa sumu na watu wabaya hadi akafikia kuunda makala ile mbovu inayoenda kupotosha akili za watanzania wote.
Nilitamani walau kumfahamu jina lakini nikakuta makala ile imeitwa MAKALA MAALUMU ikiwa imeandikwa na MWANDISHI WETU
Upuuzi kabisa!!!
Picha ya mke wangu ikanifanya niingiwe hasira maradufu nani wapi pa kuzishusha hasira hizi. Nikaamua kumpigia simu mama yangu mzazi ili nijue ni nini kinatokea. Niliomba sana awe peke yake ili aweze kuzungumza name vyema.
Hakika alikuwa peke yake!!
“Sam weee!! Sam mwanangu, nilipokuzaa sikukuzaa uende kuyafanya haya wanayokuandikia. Najua kuwa wanajaribu tu kukuchafua.
Nitakuwa upande wako!! Si nilikuzaa kwa upasuaji na fomu ikasainiwa kufa ama kupona.
Basi ni hivyo hivyo nipo nawe katika kufa ama kupona.
Eti watu wa Dar es saalam wanadai waliuaga mwili wako, wafanyakazi wenzako waliuaga mwili wako. Tena wananipigia simu kwa kasi kweli wakinipa pole juu ya kifo chako.
Nasemaje Sam, watakukana wote lakini mimi nitakusimamia hadi mwisho..” hapa mama akasita kisha akacheka kidogo!! Na akamalizia na kauli moja ya kishujaa lakini kama anayesanifu.
“Eti maiti imepoteaaaa, walijua tu kuwa mama nd’o pekee awezaye kumtambua mwanaye hata asipokuwa na kichwa!! Kama wamemkamata akili huyo Edna wako ni huyo huyo, kama na baba yako ulevi wake unamsahaulisha magumu tuliyopitia ni yeye si mimi (kisha Akatukana kwa kikabila chetu)” nikajua kuwa mama amakasirika katika kiwango cha mwisho!!! Haikuwa kawaida yake kutokwa na matusi.
Nilishusha pumzi zangu na kupata ahueni, kuwa mama yangu habadilishwi mawazo hata kidogo.
Jojina alikuwa amejikita katika jiko la gesi akiandaa chai, na nilipomaliza kuzungumza na mama na yeye alikuwa ameketi kitandani akiwa na kikombe cha chai.
“Sam, umezungukwa na watu wabaya tena wenye nguvu sana. Yaani mtu anaunda ajali kama hii maksudi anaharibu gari, anachonga jeneza ilimradi tu kukuchafua na kuunda ukweli usiokuwepo!! Wanadamu wabaya sana, na ili ufanikiwe lazima haya mambo yaende hatua kwa hatua vinginevyoo!!!!!” aliishia hapo akanipatia chai, nikachemsha tumbo!!
Nikiwa katika kunywa chai na kumkumbuka mke wangu kipenzi, nikakumbwa na kumbukumbu juu yay ale mazingira ambayo alipotea!! Nilipokumbuka kule dar es salaam nikakumbuka kuwa wakati naona giza kuna kitu niliona….hakika kuna kitu nilikiona.
“Mama lao, kuna kitu nilikiona wakati nazimia kama usemavyo…yaani kuna kitu niliona jamanii..” nilimweleza huku nikikifinyafinya kichwa changu kutafuta kumbukumbu.
Aliniambia kuwa huenda ni katika usingizi mzito tu wa kuzimia lakini nilikana, kipo kitu cha msingi niliona waziwazi!!!
Nikatoka kitandani na kumwomba Mama lao anisimamishe sehemu niliyokuwa mara ya mwisho kabla ya kuzimia. Akafanya vile huku akicheka kimadaha, kanga yake moja maungoni.
Nilipokuwa pale nikamwomba anielekeze pia namna ambavyo nilianguka!! Alifanya kila nilichotaka.
Nikaenda hadi chini na hapo nikajikuta nikionana na kitu cha kustaajabisha na kutisha kwa wakati ule.
Japokuwa ilikuwa picha lakini ilitisha kuitazama, niliisogelea huku nikitetemeka.
Nikaiona picha ile inayotabasamu kama ambayo inanikebehi. Nikaishika huku nikitetemeka.
“Jojina huyu ni nani kwa jina?” nilimuuliza huku nikiwa nimeipakata ile picha katika viganja vya mikono yangu!!
Badala ya kunijibu alicheka kidogo. Nikashangaa maana picha ile ilinitisha mimi lakini yeye hakuiogopa.
“Jojina usicheke huyu ni nani huyu?”
“Anaitwa Dulla, nimwite hayati Dulla, mwanaume wangu nimpendaye akafa kabla…”
Sikumwacha amalize nikayaingilia maongezi.
“Jojina huyu hajafa, huyu na mwenzake mzungu walimteka mke wangu…niamini mama lao..huyu hajafa. Dulla si mtu mzuri niamini sijamfananisha hata kidogo. Dulaa kama ni kweli anaitwa hivyo, kwa jicho langu nilimwona akimchukua mke wangu! Kuna kitu Mama lao..” sasa ikawa zamu yake kuchanganyikiwa. Macho yalimtoka pima ……….
Tukabaki kutazamana.

**JIFUNZE. Mwenye pesa si mwenzako, haki haipo katika dunia hii. Mwenye pesa anayumbisha sheria, na jela anaenda maskini. Wanasema mwenye nguvu MPISHE……usiisake haki dhidi ya mwenye pesa maana haki yako itageuzwa HARAMU.
FUNIKA KOMBE MWANAHARAMU APITE!! Ile kanuni ya mnyonge mnyongeni ila haki yake mpeni!! Haina nguvu tena mbele ya pesa!!
 
SEHEMU YA KUMI NA TATU
SEHEMU YA KUMI NA TATU

SOTE tulitazamana bila shaka kila mmoja akiwaza lake juu ya kinachoendelea.
“Kwa hiyo baba alikuwa anasema ukweli juu ya Michigani eeh!!” alijisemea nami nikamuunga mkono kuwa kuna uwezekano mkubwa sana kuwa mzee wake alikuwa sahihi juu ya ubaya wa Michigani japo hakuwa anaweza kuielezea vizuri.
“Mwanangu Justin jamani. Kwa hiyo wamemuua ama?” aliniuliza kana kwamba mimi ni wakala wa hiyo Michigani na ninajua kila kitu. Sikumjibu kitu akaendelea kuzungumza na nafsi yake!!
Nilitumia fursa hiyo kumweleza juu ya mazungumzo baina yangu na mama. Nikamweleza ukweli juu ya namna alivyopotea anitha, na nikafikia hatua ya kumweleza hata zile picha alizonitumia Anitha kabla hajakamatwa na yeyote yule ambaye mimi simfahamu.
“Picha ya mtoto?? Picha ya mtoto kama huyo usemaye ilikuwa inapatikana maeneo fulani ndani ya Michigani, sasa ukiniambia kuwa Anitha alikamatwa ama alipotelea eneo hilo nashindwa kukuelewa maana miezi tisa iliyopita Michigan iliteketea” Jojina alinijibu baada ya kumweleza juu ya picha katika barua pepe aliyonitumia Anitha kabla hajakamatwa na watu waliovaa suti nyeusi!! Wawili nyuma yake na wawili mbele yake!!
Majibu ya Jojina yakasababisha jambo tunalolifanya liwe kama mchezo wa maigizo usiojulikana wapi unaanzia na wapi unapoishia.
“Kwa hiyo hapa mjini hakuna tena sehemu kama hii!!”
“Haipo kwakweli ujue sambusa zangu napeleka kila kona ya mji lazima ningekuwa nafahamu picha hiyo!!” alinijibu kwa kujiamini.
Hayo yakawa mazungumzo yetu ya mwisho kabla kimya hakijatanda na kila mmoja kusinzia!!


****


Asubuhi nilikuwa nimeamka na wazo kichwani!! Nikamshirikisha Jojina akanielewa bila shaka naye akaunga mkono!!! Kwa sasa na yeye alikuwa mhanga katika mambo niliyokuwa napitia, Jojina aliamini kuwa ni kweli mtoto wake naye alichukuliwa katika tetesi za Michigani na mazingaombwe yake.
Akaamua kuungana rasmi na mimi huenda njia nitakayopitia inaweza kuwa suluhu yake pia.
Lililomhamasisha zaidi ni suala la mimi kumuona Dulla ambaye alikuwa mpenzi wake akiwa hai!! Wakati alidhani kuwa ni marehemu.
Majira ya saa moja asubuhi tulikuwa ndani ya basi kuelekea mjini Morogoro!! Tulitaka kuwashuhudia hao viumbe ambao walikuwa wakingojewa nyumbani kwetu kwa ajili ya kuuleta mwili wangu tayari kwa maziko, mwili ambao unasadikika kutokuwepo tena na sasa walikuwa wakija na taarifa tu rasmi kwa wazazi wangu!!
Nilikuwa nimejivika kofia kubwa kama kawaida kuificha sura yangu!!
Majira ya mchana tulikuwa Morogoro tukipata chakula katika mgahawa usiokuwa na mlundikano wa watu!! Baada ya hapo kwa mwendo wa miguu tukaanza kupita mtaa mmoja hadi mwingine tukipatafuta kwa hadhari kubwa nyumbani kwetu nilipozaliwa. Hapakuwa mbali sana kutokea stendi ya Msamvu, hivyo ilituchukua dakika chache tu kuwasili katika eneo lile.
Tuliukuta umati mkubwa ukiwa pale nyumbani, nilisikitika sana kuona kuwa wale watu wote wamelishwa sumu na kuamini kuwa mimi nimekufa na huku nikihusika na mauaji na pia nikihusika katika kulawiti.
Lakini huenda umati ule ulijazwa zaidi na tukio la msafara wa kuleta maiti yangu nyumbani kupata ajali na kisha mtu mwingine kufa huku jeneza likiingia katika korongo na maiti kutoweka.
Nilifanikiwa kuwaona watu wawili ambao nilikuwa nafahamiana nao. Wote walikuwa waandishi wa habari!! Nilijisikia kwenda kuwasalimia lakini hofu ya kujizulia mambo magumu zaidi ikanikwamisha.
Jojina alikuwa makini kabisa kuangaza huku na kule, nia ya kuja naye pale ni kupata uhakika iwapo hiyo Michigani ni kweli inahusika na mikasa yote tunayopitia na tuliyopitia ama Michigani ni kitu kingine.
Iwapo atamuona mtu yeyote ambaye awali aliwahi kumwona Michigani nilimsihi anijuze kwa wakati ile tujue nini cha kufanya.
Namba yangu ya simu ilikuwa nyingine tena na aliyeitambua alikuwa ni Jojina pekee. Tulipoufikia umati tukatengana, kila mmoja akaenda upande wake huku tukipeana ahadi kuwa baadaye tutakutana kwa ajili ya kupeana taarifa juu ya nani kaona nini.
Zaidi ya wale waandishi wa habari kadha wa kadha watu wengine niliofanikiwa kuwaona ni ndugu wa karibu, lakini wao hawakunitambua!!
Nililiona kundi la watu likimuhoji mama yangu, aina ya nywele zao ilinipa majibu mara moja kuwa wale ni askari. Mama alikuwa anafanya viapo mara kwa mara, bila shaka kuna swali walikuwa wanamuuliza na kila alivyojibu wanadhani anadanganya.
Swali gani jingine kama si juu yangu??

“SAA MBILI USIKU, GIRAFFE HOTELI CHUMBA NAMBA 18 NITAACHA WAZI INGIA KWA TAHADHARI KABATINI”

Ulikuwa ujumbe kutoka kwa Jojina. Nikausoma na kuuelewa.
Hoteli ile ilikuwa inajulikana sana hivyo sikuhangaika, nikajihesabia mida hadi ukafika huo wakati. Roho ilikuwa inadunda na kuhisi kusalitiwa lakini kwa sababu niliamua kumuamini
Jojina nilipiga konde moyo.
Nikaanza kwa kuupenyeza umati hapa na pale hadi nikafika mahali mama yangu ameketi peke yake chini ya mti akilia kwa maumivu makubwa!!

Nilimgusa begani akageuka lakini sikuifunua kofia.
“Mama mimi Sam, usionyeshe dalili za kushtuka!!!” nilimwambia kwa utulivu, lakini kama kawaida ya wanawake nimemsihi atulie yeye akasimama wima.
“Mamaaa!!” nilimsihi, akabonyea tena chini.
“Usijishughulishe na mimi wakati huu tunapoongea.” Kweli akatazama mbele.
Nikamweleza kwa ufupi sana juu ya wakati ambao ninapitia, nikamwomba aniombee sana kwa Mungu!! Sikumjibu maswali yake yote, lakini nikamweleza kuwa naenda kulala na siku inayofuata nitamtafuta tuzungumze.
Nikampatia mkono wangu, akajikumbushia mazoea yake ya miaka nenda rudi!!
Akaubusu!!
Nikaondoka.
Muhudumu alikuwa anakula wakati mimi naingia pale ndani, akajiweka sawa aweze kunisikiliza. Nikaulizia vyumba akanieleza kuwa vipo, nikamsihi anipatie chumba upesi, akafanya hivyo.
Baada ya malipo nikapewa funguo wangu !!!
Badala ya kwenda chumbani kwangu, nikaenda chumba namba 18. Kweli nikalikuta kabati kubwa kabisa. Nikafungua na kuingia ndani yake.
Nikajipekua na kukuta dhana zangu kadhaa nilizonunua kabla ya kuingia pale zikiwa sawa.
Kisu kidogo na nyembe kadhaa kwa ajili ya kujilinda!! Iwapo litatokea lolote.
Likakatika saa la kwanza lakini la pili halikukatika mara wakaingia wanaume wanne mle ndani. Kupitia kitundu kidogo nikawa nawatazama, kabati lilikuwa limefungwa kwa ndani na funguo nikiwanayo mimi.
“Huyu mwanamke kumbe aliacha wazi, yukwapi kwani?”
“Analewa huko nimemwacha!!” ilijibu sauti nene kutoka kwa mtu mwenye kipara, sikuweza kuwaona vyema.
Waliketi na kuanza mazungumzo palepale.
Mwongeaji mkuu akiwa mwenye kipara!!
“Dulla eeh huu ujio wa ghafla ni kwako mshkaji wetu, na ishu ni moja tu, wanawake Dulla angalia wasije wakakuponza tena, huyu mwanamke huyu we unadai anakufahamu sijui, angalia Dulla wasije majamaa wakakutoa muhanga. Si unajua huyo bwege mwandishi amemvuruga kabisa bosi sasa hivi na haoni hatari kuua. Sasa wewe endekeza mambo ya wanawake halafu mwisho wakuchomeshe jamaa akumalize. Usije ukasema hatukukwambia, kama unaona tunaingilia uhuru wako Dulla sawa lakini kama unajipenda acha hizi mambo.” Alizungumza kwa sauti ya chini wenzake wawili wakawa wanatikisa vichwa kukubaliana naye.
“Yaani ipo hivi sawa huyu mwanamke hatoki humu ndani, nd’o mwisho wake sifanyi ujinga tena kama wakati ule wa Michigani ya juu ile.” Aliposema kauli hii vicheko vikatawala kisha maongezi ya hapa na pale. Kabla yule msemaji hajaingiza maongezi mengine.
“Hivi huyu bwege wa kujiita mwandishi hajui kuwa atakufa kifo kibaya sana akicheza. Yaani angezijua hasira za jamaa dah bora hata ajinyonge kuliko kuingia mikononi mwa bonge waiti.” Alisema kwa masikitiko bwana mwenye kipara, kisha akainama na hapo nikaweza kumwona Dulla. Alikuwa ni yuleyule mtekaji wa mke wangu.
“Mkewe anaipata suluba aisee hadi huruma. Halafu yule msaidizi akajifanya kumtetea siku ile kaambulia vinao na matusi, Bonge waiti ni habari nyingine jamani.” Dulla alizungumza, na baada nya hapo ikasikika hodi mlangoni. Sauti ya kilevi.
“Oya Malaya wako huyo, hakikisha unafanya tulivyozungumza Dulla. Anakujua sana huyu demu.” Kipara alimnong’oneza Dulla na maneno yale yakaonekana kumuingia.
Mlango ukafunguliwa, wale mabwana watatu wakatoka nje na ndani akabaki Dulla, kisha akaingia mama lao. Alikuwa amelewa chakari kimtazamo, aliyumbayumba huku akiimba nyimbo anazozijua yeye mwenyewe. Niliendelea kuyatazama haya yanayoendelea huku nikijiuliza juu ya Michigani na mkasa unaoendelea.
Bonge waiti!! Huyu ni nani katika mlolongo huu wa kustaajabisha!!
Taa haikuzimwa na jicho langu likaendelea kushuhudia mambo machafu kusimulia kati ya Dulla na Jojina. Lakini nililazimika kutazama huku nikichukua tahadhari nisije kugusa chochote kile ambacho kinaweza kutibua mipango yetu.
Ni vyema kuwa niliendelea tu kutazama kinachoendelea, maana ningeacha na kuona aibu huenda lingetokea baya na kisha nikajutia muda wangu!!
“Jojina, ujue nakupenda sana.”
“We wala hunipendi na kama unanipenda mbona ulinikimbia.” Alijibu Jojina kilevilevi.
Dulla akamtazama yule mwanamama jinsi anavyosinzia na hapo nikamuona akichukua mto, akawa anasitasita lakini hatimaye akaushusha na kuufunika uso wa Jojina kisha akaukandamiza.
“Jojina lazima ufe ili niendelee kuishi kwa amani nisamehe…nisamehe inanibidi tu kukuua kabla mimi sijauwawa.” Alisema huku akiwa anauma meno yake.
Akili ikafanya kazi harakaharaka, mikono ikiwa inatetemeka nikauzungusha funguo, na kisha kulikanyaga kabati kwa nguvu. Dull hakujiandaa kuupokea mshtuko huo, akaacha mara moja kile alichokuwa anafanya na sasa akawa anatazamana moja kwa moja na mtu ambaye yeye binafsi anaamini kuwa ni dhaifu na huenda alijinyonga tayari.
Mama lao alikuwa akihema kwa nguvu huku akikohoa bila kikomo.
Sikumpa nafasi ya kuzubaa zaidi, nikajirusha na kumkaba huku nikivuta picha ya mke wangu na mwanangu mpenzi.
“Wewe wewe!!” alianza kunisonta kwa kidole chake. Lakini sikutishika nikajivuta nyuma na kumwangushia kichwa kimoja, akatokwa na yowe la uchungu, nikataka kumpiga ngumi lakini akaniwahi akanikanyaga teke la tumboni.
Kisha zikafululiza ngumi mbili tatu, nikaanza kuona mawenge!!
Lakini zile zikawa ngumi za mwisho. Ikajha ile sababu ya muhimu kabisa niliyokuwa naingoja ya Jojina kuitwa mama lao!!
Nikiwa chini nikamuoa akimnyanyua Dulla juu juu. Kisha akamnasa vibao kama mtoto mdogo, na mkong’oto uliofuata pale ni yeye pekee anaweza kusimulia maumivu iwapo angepata nafasi ya kusimulia.
Lakini hakupata nafasi hiyo!!
“Justin yuko wapi?” aliuliza kwa jazba huku akiwa amemuunganisha Dulla mikono yake vyema.
Mama lao alikuwa mama kweli!!
Dulla akaanza kujiumauma, mama Lao akamweka sawa kisha akatuliza kisigino chake katika korodani za Dulla. Yowe likamtoka na mimi nikasisimka.
“Unasema ama husemi wewe mpumbavu.” Alifoka mama lao.
“Sijui alipo sijui chochote dear, mimi ni kibaraka tu nisamehe…”
“Kwanza koma kuniita dear, wewe kibaraka wa nani?”
“Bonge…bonge waiti…..”
“Nd’o nani na yupo wapi na ni shughuli gani mnajihusisha nayo?” alimbana swali.
Dulla badala ya kujibu akajitoa katika himaya ya Jojina na kujaribu kujitetea huku na kule.
Jojina alikuwa macho haswa, mimi binafsi sikujua nimekidondosha kile kisu muda gani lakini yeye alikikwapua kutoka kilipokuwa, Dulla akajikuta akigumia kwa maumivu, kisu kikiwa kimezamishwa mgongoni!!
“Hivi unajifanya umafia wangu umeusahau eeh!!” sasa alizungumza huku akikizungusha kile kisu kama akayechokonoa.
Mama lao alikuwa katili haswa!!
Dulla alikuwa anapiga kelele lakini zote ziliishia katika kiganja cha mama lao. Alikuwa amemziba vyema.
Maumivu aliyokuwa akiyapata hata wewe unaweza tu kuyakadiria!!
Mashuka yalikuwa yanazidi kuwa mekundu na mama lao hakujali hayo. Sura yake ilikuwa imechafuka kwa ndita zilizotangaza hasira.
“Justin mtoto wangu yupo wapi?” aliuliza tena kisha akamwacha Dulla azungumze.
Lakini hakuzungumza na badala yake alianguka na kupoteza fahamu!!!
“Bwege atatiharibnia akizinduka shenzi kabisa anazo picha zangu niliwahi kumpa.” Alisema Jojina kisha akafanya nisichotarajia.
Akazamisha kisu katika upande wa moyo wa Dulla.
“Kalale kwenye moto wa jehanamu muuaji mkubwa wewe.” Alisema kwa hasira. Kisha akasimama kitandani akavua nguo zake zote zilizolowana damu.
Akauendea mkoba wake akachukua nguo nyingine akavaa.
“Twen’zetu!!” alisema na hapo tukatoka nje.
Jojina akiyumba kama mlevi!!! Na hapo nikapata jibu kuwa kumbe hakuwa amelewa bali alikuwa mtaalamu katika kuigiza.
Nilimtazama kwa wasiwasiu mkubwa, sikujua kama anaweza kuwa jasiri kiasi hiki mwanamama huyo.
Alimpataje Dulla? Na alimshawishi vipi hadi kumuamini tena??
Hayo yalikuwa maswali niliyotarajia kumuuliza tukishafika nje ama kwenda popote pale na kuwa huru!!!
“Sam, najua unajiuliza tunaanzia wapi eeh!! Usijali mpenzi wangu, mimi naifahamu Iringa vyema. Na kama kweli kuna kitu kibaya huko michigani nitajua tu!! Nakuhakikishia kuwa kama mwanangu mimi Justin, mwanao, mkeo, na Anitha wako salama basi watatoka salama. Hukuwahi kujua kwanini naitwa mama lao, lakini utajua hatua kwa hatua…” aliniambia huku akinibinyabinya kiganja cha mkono wangu

**JIFUNZE: Hakuna mwanamke aliyehifadhi tumboni mwake, Malaya, jambazi ama muuaji.. kwa miezi tisa kisha akamzaa.
Mazingira nd’o huzaa tabia hizi, mwanadamu huongozwa na mazingira na nyakati. Katika maisha yetu kuna nyakati zinakuja na kutulazimisha kusema uongo ilimradi tu kukomboa kitu flani, na zinakuja nyakati za hasira na chuki na kutusukumia dhambini.
Ni kumwomba mungu tu atupe mioyo ya ujasiri sana!!!
 
SEHEMU YA KUMI NA NNE
SEHEMU YA KUMI NA NNE
Nilibaki katika mshangao kwa muda nikiendelea kujiuliza yule mwanamke ni wa aina gani. Awali nilidhani kuwa ni msema sana tu kutokana na haiba aliyoionyesha siku tulivyosafiri naye kutokea jijini Dar es salaam, mara ya pili tukakutana naye akiwa anauza sambusa na bajia, hapa akazidi kunishangaza lakini ninazidi kumfahamu.
Sasa namtambua kama mama lao!!
Hakika alikuwa mama lao!!
“Mabwege wamelewa wale hawajui kama mwenzao kajifia huko ndani shenzi kabisa!!!” Jojina alizungumza kama anayesema mwenyewe, nikageuza shingo na kuwaona wale jamaa waliovaa suti waliokuwa wakimsihi Dulla amuue Jojina. Kulingana na mavazi aliyokuwa amevaa Jojina, mavazi tofauti kabisa na yale aliyokuwa amevaa awali, ilikuwa ngumu kwa mtu yeyote kuweza kumtambua. Kasoro mimi tu!!
“Sam, umeyaokoa maisha yangu! Sikutarajia kama ungeweza kushawishiwa na ujumbe ule mfupi niliokutumia ukajileta kichwa kichwa katika chumba kile!! Vipi tungekuwa tumepanga kukuua labda, ama vipi ungegundulika kuwa upo ndani ya chumba kile!!
Umekuwa jasiri sana kujileta katika mdomo wa kifo bila hofu. Na sit u kujileta katika mdomo wa kifo, bado ulikuwa jasiri ulipoona yule bwana anataka kuniua hukuvumilia ukatoka ndani ya maficho na kumkabili. Ni wanadamu wachache sana wawezao kujihatarishia maisha yao kama wewe ulivyofanya.” Jojina alikuwa akininong’oneza kwa sauti ya chini huku akinivutia katika kifua chake. Tulikuwa nyumba ya kulala wageni tayari.
Nilimjibu kizembezembe huku nikijifanya usingizi umenitawala, nikambusu midomo yake kisha nikageukia upande wa pili nikimwacha jojina akipitisha mikono yake kutokea mgongoni mwangu na kisha kuiunganisha kwa mbele!! Akanikumbatia.
****
ASUBUHI majira ya saa nne, tulikiachia chumba. Mama lao akiwa amevaa kama alivyokuwa amevaa usiku uliopita huku mimi nikiwa nimebadili na kuvaa kaptula na fulana kubwa, kichwani nikiwa na kofia kama ilivyo kawaida tangu niingie matatani.
Safari yetu ilikuwa ya kuvizia maeneo ya nyumbani kwetu ili tuweze kujua ni kitu gani kinachoendelea, tulitambua fika kuwa lazima taarifa juu ya kifo cha Dulla zilikuwa zinafahamika kwa wenzake na kama kuna lolote litakuwa limeendelea basi mwanzo wake ni pale msibani.
Tuukuta umati mkubwa tofauti na siku ya kwanza, jambo hili halikuwa la kawaida hata kidogo, ni kweli msiba huu ulikuwa na utata ndani yake lakini haukuwa utata wa kuvuta umati mkubwa kiasi kile.
Tukajichanganya katika makundi kwa tahadhari kubwa!!
Jojina alikuwa wa kwanza kuchezwa machale, akiwa amevalia wigi kichwani lililombadili sura yake alinivuta katika kundi fulani kisha tukawapa migongo kama hatuna habari nao.
“Hawa polisi walichofanya ni uonevu, haiwezekani mara amekufa mara msafara umepata ajali, sasa wanasema sijui kuna wadau wake mama yake anawajua??? Huu ushenzi huu!! Mama ambaye hata Dar hajawahi kwenda anajua nini sasa.” Alilalamika bwana mmoja, nikageuka kumtazama sura ilikuwa ngeni.
“We! Bora tu unyamaze maana hii serikali yetu hii ukionekana tu unatetea jambo basi. Chanzo eti jana pale mazikoni mama amekataa kata kata kuwa mtoto wake ajafa na siku ile usiku alipopiga mayowe kuwa ameisikia sauti ya mwanaye. Hapo tu nd’o tatizo likaanzia siku aliyodai kuwa amemsikia kesho yuake nadhani nd’o ikatokea ajali. Kwanini serikali isikubane isitoshe huyu mwenyekiti wa mtaa ana chuki binafsi na familia ya marehemu.” Alinong’ona kijana mwingine na yeye sikuwa nikimfahamu. Maongezi yao yakanipa mwanga kuwa mama yangu alikuwa matatani.
“Sam…jikaze usipaniki utaharibu!!” Jojina aliwahi kugundua azma yangu maana kuna chembechembe za wazimu zilianza kunipanda kichwani na kujisikia nikikabiliwa na mzimu wa lolote na liwe. Ni heri Jojina aliniwahi kisha akanishika mkono na kunitoa mahali hapo.
Mama yangu alikuwa kila kitu kwangu!! Almanusura nimponyoke Jojina na kukimbia lakini ukakamavu wake aliweza kunihimili, sikuweza kufanya lolote.
“Sam, unatakiwa utambue kitu kimoja. Tupo katika mapambano ambayo hakuna ajuaye tunapambana. Hatuna msaada na jeshi letu linazidi kuporomoka, ameondoka Anitha, Mama Eva, Mzee Matata sijui, sasa ameondoka mama, ukiiruhusu akili yako kujikita katika wazimu basi ujue kuwa nitabaki peke yangu!! Siwezi kupambana peke yangu Sam siwezi hata kidogo, wewe ukiharibu tu tambua kuwa utajikuta umefungwa kamba wewe, Anitha, mama, Eva, mama Eva na mimi pia halafu nani wa kumfungua mwenzake, ama nd’o unataka kuanza kumlilia Mungu ilihali amesema jisaidie nami nitakusaidia, unataka kujiingiza katika janga maksudiu. Janga ambalo mwanga wake tumeanza kuuona, tunatambua kuwa kuna Michigani, tunajua kuhusu Anti Ezekiel kiasi fulani, tunalo la kusema kuhusiana na kindo. Halafu wewe unataka kuharibu.
Sam kwa jinsi walivyokusaka kwa muda mrefu nadhani unajua kuwa wakikukamata ……wakikukamata Sam. Si umezikwa kiuongouongo, wale watakuzika kweli. Mbaya zaidi Sam, hawa watu akina Bonge waiti wanaonekana kukubalika samba serikalini kwa lolote lile wanalodanganya. Sam unatakiwa kuwa imara, ni mimi na wewe iwapo hatatokea mwingine wa kutuunga mkono tunalo jukumu la kumwokoa mama, Eva, mama Eva, Justin kama yupo hai mwanangu, Anitha na wengine wote wenye haki.” Jojina alinieleza haya kwa hisia kali. Kila mstari wa neno lake ulikuwa ni fimbo inayoumiza, aliusema ukweli mtupu. Nikapepesa macho nisitazamane naye usoni lakini yeye alizidi kunikazima macho ili maneno yaniingie.
Jojina!! Jojina alikuwa Anitha mwingine!!
“Nimekuelewa sana dada yangu!!” niliamua kukubali yaishe.
“Tunaondoka dakika hii kuelekea Iringa ama popote pale lakini sasa hivi tunaondoka tukiwa na lengo moja tu kuitafuta Michigani popote ilipo, kumtafuta Bonge waiti kama kweli yupo, tunaondoka kwenda kuisaka amani!!!” alizungumza katika namna ya kuamrisha sasa hakunitazama machoni.
Nikatii!!
Tukaongozana mpaka stendi, bahati nzuri magari ya kuanzia safari Morogoro kwenda Iringa yalikuwepo mengi tu.
Tukaingia katika basi lililokuwa linakaribia kuondoka!!
Dakika kumi baadaye likaanza safari. Tulikuwa tumepata siti mbili za mwisho nyuma kabisa!!
Hatukujali kuhusu hilo. Kama kawaida tukaandikisha majina ya kughushi!!
Kimya kilitanda, hatukusemezana chochote kile. Kwa takribani dakika thelathini, sijui Jojina alikuwa anafikiria nini, lakini mimi nilikuwa nawaza juu ya Kusadikika iitwayo Michigani, mahali palipovunjwa na kuteketezwa sasa tunapatafuta, nikamuwaza pia Ezekiel wakati huu nikimfananisha na mzimu wa ajabu uliojileta katika maisha yangu!!
Ezekiel! Ezekiel asiyejulikana! Aidha yu hai ama amekufa.
Dakika chache baadaye gari likasimama na kuegesha pembeni.
“Kuchimba dawa mapema hivi!!” hatimaye Jojina akatokwa na neno la kwanza.
“Vibofu havifanani aisee.” Nikamjibu kiutani, akatabasamu.
Lile tabasamu halikudumu sana, akataka kusema neno lakini akaishia kutanua tu mdomo na asiseme chochote.
Sikujua nini kimemsibu.
Baada ya sekunde kadhaa sikuwa na haja ya kuuliza tena kulikoni!!
“Iwapo unajua kuwa umeandikisha jina lisilokuwa lako katika tiketi yako, jisalimishe mapema kabla haujapekuliwa!! Narudia tena, iwapo unajua umeandikisha jina lisilokuwa lako katika tiketi uliyonayo tafadhali ndugu jisalimishe mapema nje ya basi kabla upekuzi haujaanza!!” sauti kali ya kiaskari iliamrisha.
Jojina alijisajiri kama Prisca na mimi nilijisajiri kama Rama.
Majina feki!! Mungu wangu!! Kuna nini tena?
Nilimtazama Jojina alikuwa akijaribu kujificha asionekane kama anayeshangaa, lakini macho yangu yalipotua katika kifua chake niliweza kushuhudia jinsi moyo wake ulivyokuwa unadunda kwa kasi.
Sote tulikuwa tumepagawa, hasahasa mimi ambaye sura yangu ilikuwa takribani katika magazeti yote nchini. Vipi wakiniona hawa maaskari. Bila shaka nd’o safari ya jela na kifo moja kwa moja.
“Sam, zama chini zama wajinga watakagua, ingia nitakufukina na sketi yangu fanya fasta.” Jojina alininong’oneza. Sikungoja zaidi maana kama ni hatari tayari tulikuwa hatarini.
Nikazama chini wakati abiria wengine wakiwashangaa askari waliokuwa wakitoa lile tangzo na wengine wakijishughulisha katika kujisalimisha mbele.
Nikajibana na hatimaye Jojina akatanua miguu nikawa chini ya himaya ya miguu yake miwili, joto kali likanitoa jasho lakini bora joto, jinsi nilivyojibana chini ya viti vile niliumia sana mgongo!! Miguu ya Jojina ilikuwa inatetemeka haswa.
Tulikuwa matatani!!
“Wanakagua tiketi Sam. Omba Mungu sana” Jojina aliinama na kunong’ona nikamsikia lakini sikujibu, akazidi kutetemeka.
Zikapita dakika kadhaa akanong’ona tena.
“Sam wanayo picha sijui ni picha ya nani, hawakagui tiketi mafala hawa wanakagua sura Sam. Ni hatari Sam” Jojina akazidi kunitia hofu.
Niliendekea kudumu katika hali ile bila kujitingisha wala kukohoa. Hofu niliyokuwanayo katika mazingira haya ilikuwa mara kumi ya hofu ya siku moja iliyopita nilipokuwa kabatini nikiwasubiri akina Dulla, na hofu hii ilizidi ile hofu ya kumuona Jojina akiua mtu.
Wakati naitafakari hali inayonikabiri nmara nikaisikia sauti ya Jojina tena, safari hii ilizungumza kwa uoga zaidi.
“Sam…tumekwisha….mafala wana picha yangu aisee kumbe wananitafuta mimi!! Jiweke safi Sali sala zako za mwisho, wanatuua hawa!! Hawatuachi Sam”
Kauli hii haikuwa kavu, iliambatana na mkojo!!
Yule mwanamama jasiri alikuwa anajikojolea, ule mkojo wa moto kutoka kwa Jojina ukatua vyema katika uso wangu!! Nikataka kujitikisa lakini nikahofia kuharibu zaidi.
Hakika Jojina alikuwa ameogopa sana.
Na kama alivyosema kuwa tumekwisha ni kweli alimaanisha, maana jasiri akifikia hatua ya kujikojolea basi ujue amenyanyua mikono juu…

**KUMBUKA!! MUNGU alitumia ubunifu wa hali ya juu sana kuliko ubunifu wowote uliowahi kutokea popote pale, kipindi anamuumba mwanadamu. Alimpa kila kitu, lakini akamnyima uwezo wa kujua nini kitatokea katika sekunde moja ijayo mbele yetu.
Kwa sababu hatujui lijalo, ni vyema kujiweka tayari kila muda ikiwa hatujui siku wala saa!!!
 
SEHEMU YA KUMI NA TANO
SEHEMU YA KUMI NA TANO
Sikukarahishwa na ile mikojo ya mama lao badala yake fikra zangu ziligandiana maneno ya Jojina ambaye n’do alikuwa shuhuda wa kila kinachoendelea.
Alikuwa amekiri kuwa hatuna ujanja na tumekamatika. Niliisikia na kuiona vyema mikono yangu jinsi ilivyokuwa ikitetemeka, nilijaribu kujiimarisha lakini sikuweza.
“Wewe kaza uso wako nitazame!!!” niliisikia sauti ya askari ikiamrisha, Jojina akazidi kutetemeka, sasa hakuwa akijikojolea tena, bila shaka mikojo ilijiishia katika kibofu!! . .Mimi ndo nilikuwa kwenye mashaka zaidi.
Niliiona miguu ya yule askari ikiwa imesimama imara mbele ya siti ya mwisho kabisa, bila shaka alikuwa akiwakagua akina Jojina.
Niliusikia mkono wa Jojina ulishuka kwa kasi na kuanza kunipapasa, alinishika sikio mara anishike kichwa!! Nikajiuliza kulikoni na bado sikufanya jitihada za kumzuia asinipapase. Sikujua anachokihitaji ni kipi. Mara akanishika pua na hatimaye akapanda juu kidogo akainyofoa miwani katika macho yangu.
Nilistaajabu nisijue kama hii ni hofu inasababisha ama ni kipi kinamsibu mwanamama huyu!! Nilikuwa namwomba Mungu afanye muujiza wowote ule na ile iwe ndoto. Tatizo ni moja tu!
Mungu hapangiwi kazi!! Yeye huombwa tu. Nami nikalazimika kuomba huku nikitarajia majibu ya haraka haraka.
Hatimaye miguu ile ikageukia upande aliokuwa ameketi Jojina. Hofu ikaongezeka maradufu.
“Kwani kuna nini hapa jamani!!!” nniliisikia sauti ya Jojina, sikujua anamuuliza nani.,
“Tiketi yako ipo wapi mwanamke??” sauti kali ya kiaskari ilijibu.
“Tiketi…tiketi yangu mimi….. Joshua, we Joshua….. mpe kondakta tiketi yake.” Jojina alijibu nikabaki kuduwaa kule chini nisijue nini kinaendelea baina yao.
Jojina aliendelea kusema maneno maneno, bila shaka aliyajua mwenyewe mimi nikabaki katika fumbo!!!
Kimya kikatanda, nikamsikia yule askari akisonya na mara akageuza na kuondoka zake.
Nilistaajabishwa sana na muujiza huo.
“Usitoke…vumilia huko huko!!!” alinong’ona Jojina, nami nikajizi kujikaza. Gari likawashwa!! Safari ikaendelea na kile kilichotokea kikabaki kuwa cha kutetwa ndani ya basi.
Baada ya dakika kadhaa Jojina aliniruhusu nitoke kule chini, hii ni baada ya abiria kadhaa kuwa wameuchapa usingizi wasijue kama nilitokea kule chini.
“Jojina umewalaghai kitu gani wewe mwanamke!!” nilimuhoji kwa sauti ya chini.
Akaanza kwa tabasamu kisha akanieleza kitu kilichonifanya niamini kuwa si lazima uende shule ndipo uwe na uwezo mkubwa wa kimaamuzi kama wa mama lao.
“Yaani nilikuwa najua kuwa sitaweza kuchomoka hapa, yaani kitu nilikuwa nimesahau ni kwamba Dulla huwa ana picha zangu tena nyingi tu, na wale jamaa waliniona nikiwanaye na mbaya zaidi aliwatambulisha kwangu. Hivyo ule mzoga kwa namna yoyote ile lazima skendo za kuua ziwe juu yangu. Sasa nikajibweteka kimawazo nikiamini ni wewe wanakusaka. Alikuwa pale hivi siti ya nne nd’o nikaiona picha, wacha nichachawe mtu mzima!! Yaani nikajua tumekwisha. Aliponikaribia zaidi nikaamua kama ni kufaacha nife kishujaa, ndo pale nikakupapasa nikakutoa miwani yako harakaharaka nikaitundika katika uso wangu. Aliponifikia nikaanza kujisemesha, jamaa akaniondoa miwani, aisee kitu nilichofanya najua mwenyewe, nikabenjua macho yangu, hii bolti nyeusi ikapotea ikabaki hii nyeupe, hii michezo naijua sana tangu zamani, wakati nabenjua nilikuwa napapasa huku na kule na mara nimkamate mkono, mara nimshike kifua. Nadhani unajua kilichotokea hapo, wasafiri bila kutumia aki;li wakaanza kukoroma kuwa mimi sina uwezo wa kuona tena wakitumia lile neno kali kabisa, kipofu!! Askari akaishiwa hamu, akanirejeshea miwani yangu machoni, nikayaweka macho yangu sawa na kumwona jinsi alivyokuwa na wasiwasi. Lakini nadhani ile picha nikiwa na kipara na uhalisia huu nikiwa na wigi umemwacha hoi. Kipofu mwenye wigi, wakati picha ni mtu anayeona akiwa na kipara.
Akasonya na kuondoka zake!! Sam siamini hata kidogo kama…….” Akasita kuzungumza, akaniegemea na kunong’ona, “kuna bwege anatuchora….” Aliniambia na kisha akanionya kuwa nisifanye jitihada zozote za kupepesa macho.
“Pita upesai nenda kamwombe kondakta,,, mwambie ninaumwa tumbo….pameharibika Sam hapa nenda haraka.” Akanisihi, upesi nikasimama na kupita nikafanya hima na kumfikia kondakta. Nikamsihi kama nilivyoelekezwa, nikalalamika sana juu ya mgonjwa wangu asiyeweza kuona anaumwa tumbo.
Kondakta akanielewa, nikarejea na kumchukua Jojina katika namna ileile ya kumwongoza mimi mbele yeye nyuma, akiigiza kuwa hana uwezo wa kuona. Wakati huu niliweza kumtilia mashaka yule mtu ambaye Jojina alidai kuwa hana nia nzuri, nilimwona akinong’ona na mwenzake. Nikajifanya sijui lolote linaloendelea.
Tulipoufikia mlango mimi nikiwa mbele kama kawaida mara tukasikia sauti kali ikiamrisha.
“Ninakutilia mashaka wewe mama usiyeweza kuona. Simama hapo hapo ulipo!! Nayaongea haya kwa mamlaka niliyopewa na jeshi la polisi Tanzania.” Niliskia miguu ikiishiwa nguvu, nikaanza kutetemeka. Lakini haikuwa hivyo kwa mama lao.
Ghafla akanisukuma nikatangulia nje.
“Saaaam poteaaaaa!!!” ndo neno pekee alilotoa, akatupa miwani huko, akaikunja sketi yake. Akili ikafanya kazi vyema sikulemaa, mwanamama anakimbia sijapata kuona, kumbe ule unene ni gelesha tu.
Nikaanza kufuata nyuma, huku nyuma zikawa zinasikika kelele za abiria. Yule askari sikuisikia sauti yake. Na niisikie ili iweje tena.
Nikapenya kila alipopita Jojina, mimi nyuma.
“Simama la sivyo nafyatua risasi!!!” ilisikika sauti kwa mbali, almanusura nisimame kama yasingekuwa maneno ya Jojina.
“Sam usisimame hakuna kitu hapo Sam kimbia.” Alinisisitiza pasipo kugeuka nyuma.
Maneno yake yakanitia wazimu wa kukimbia nikakazana zaidi. Hakika hatukujua ni wapi tunakwenda!!
Taratibu nilianza kuchoka, na bado nilisikia vishindo kwa nyuma. Jojina alikuwa ameniacha tayari na vile tulikuwa tukipenya katika majani sikuweza kumwona kabisa. Hofu ikaanza kutanda, dalili za kukata tamaa zikanikumba.
“Jojinaaa…..Jojinaaa..” nilianza kuita lakini sikujibiwa.
“Simama kimburu Kenge, shenzi kabisa simama.” Sauti iliamrisha kwa nyuma. Nilikuwa nimechoka, nikasikia miguu ikigongwa kwa nyuma, nikayumbayumba kisha kama mzigo nikatua chini.
Meno yangu yakauma nyasi!!! Nikajitahidi kugeuka nikakutana na mwanaume akiwa ameshikilia pingu. Alikuwa anahema juu juu, ni yuleyule mwanaume ambaye tulikuwanaye ndani ya gari. Alikuwa ananitazama kwa jicho kali.
“Shetani mkubwa!!!” nikasikia sauti nyingine ikasikika ikitokea katika majani!!! Mimi na yule mwanaume mwenye pingu tukatahamaki, lakini hatukudumu sana mara yule mwanaume akaaguka chini akijishika kichwa, nikaona jiwe kubwa pembeni yake. Na hapo akatokea yule mama aliyejikojolea ndani ya gari.
Jojina kwa mara nyingine!!!
“Mshenzi mkubwa wewe ukipona nenda kamweleze mkuu wako wa kazi kuwa kuna watu wabaya anawafuga huko.” Alikoroma mama lao. Lakini huyo mtu aliyepewa nafasi ya kupona akataka kuleta ujanja, ambao Jojina aliutegemea kumbe, akasimama na kurusha teke, mama lao akaingiza mkono wake katika sketi yake, akatoka na jiwe jingine kazuga kama analirusha yule askari akajificha kwa kutumia mikono miwili huku akiruka kando.
Jojina akatabasamu wakati yule bwana anaitoa kinga yake usoni, hapohapo akalivurumisha lile jiwe.
Nilibahatika kuona meno kadhaa yakitoka katika kinywa cha yule bwana. Kufikia hapo mama lao hakuwa akizuilika.
“Auaye kwa upanga……” alisema huku akitua juu ya mwili wa yule bwana anayevuja damu,
“Atauwawa kwa upange vilevile” akamalizia huku akiishika ile pingu na kuanza kumcharaza nayo yule bwana usoni.
Kila alipoituliza paliumuka kisha damu!!
Akapiga kwenye taya, akapiga paji la uso!! Akapiga kila kona!!!
Kisha mbio zikaendelea. Kidogo nilikuwa nimepumzika. Nikaweza kukimbia zaidi, wakati huu tukiwa sambamba na mama lao Jojina.
“Niliwahi kuwa mwanariadha shule!!” alisema bila kunitazama.
Sikumjibu.
Hapakuwa na mtu anayetufuatilia kwa nyuma!!!
“Hivi unajua tunapoelekea lakini?” Jojina aliniuliza, hapo tukajikuta tunapunguza mwendo taratibu huku kila mmoja akikumbwa na kiwewe.
“Hata sijui ndugu ujanja wangu mimi Morogoro mjini tu Msamvu, Kihonda basi!!” nilimjibu na hatimaye tulikuwa tumesimama.
Jojina akajipekua na kutoka na simu yake katika koba lake ambalo hakuwahi kulitua hata mara moja tangu tuliposhuka garini na kuanza kutimua mbio.
“Simu imezima chaji aisee tungeweza hata kutumia ramani ya simu kama ingeweza kufaa.”
Akasonya kisha akairudisha simu yake mkobani.
Tukaendelea kutembea kuelekea mbele bila kufahamu kama ni salama ama hatari.
“HIFADHI YA TEMBO MIKUMI” Kibao kikatukaribisha baada ya mwendo mrefu.
“Mungu wangu tupo mbugani Sam!! Mbugani Mikumi hapa…” aliweweseka Jojina nami nikapagawa. Hapakuwa na ngojangoja zaidi tukaanza kukimbia kuelekea uelekea mwingine, tukapishana na makundi ya Swala, na kwa mbali kabisa tukaiona barabara. Tukaukaza mwendo zaidi hadi tulipoifikia ile barabara.
Ilikuwa barabara ya vumbi, na ilikuwa bahati yetu tena tukaonana na wanadamu. Tukauliza na kupewa uelekeo wa barabara ya kuelekea Iringa, tukakaza mwendo, miguu yangu ilikuwa hoi sana lakini sikukubali kuonekana lelemama.
“Sam hawa jamaa tunaopambana nao hawa wananikumbusha hekaheka za Tunduma huko.” Jojina akaanzisha maongezi, walau mwendo na maongezi wapunguza uchovu.
“Tunduma? Harakati zipi tena huko.”
“Wakati ule wa uchunaji ngozi bwana!! Yaani kuna mdogo wangu fulani hivi kidogo achunwe ngozi, mwanamama nikaingia ‘front’ kutetea damu aisee, yaani mafunzo ya mgambo niliyopitia yananibeba sana mara kwa mara. Nikamjua jamaa anayewafahamu mabwana waliomteka dogo, aisee akajifanya mbishimbishi, nilimpiga ngumi mbili akalegea huko nikamkamata, nikamuwasha vibao ka’ vinne hivi wacha apagawe!! Nikamzuga kama nampiga teke akasema atanipeleka, nikamshika ile staili inaitwa Tanganyika jeki, yaani nikamkamata suruali yake huku nyuma nikamyanyua akawa anatembelea vidole. Moja kwa moja hadi eneo la tukio, saa nane usiku hiyo mwanamke barabarani. Nimeficha kisu huku kwenye pindo la sketi, tumbili yeyote ajiweke mbele yangu nafyeka korodani zake namtia uhanithi mimi!!, nikafika pale, nikatia mkwara na jamaa akiwasihi, mbona walimtoa ndani, walikuwa nd’o wanajiandaa na safari ya kwenda Zambia wakamchune ngozi….nikaondoka naye mabwege wananishangaa tu!! Chezea mama lao wewe!!!” alimaliza simulizi hii kwa majigambo, nikamkodolea macho wakati huo tukiwa barabarani tayari.
Kichwani nikakiri kuwa huyu Jojina alikuwa na mengi zaidi ya nilivyomtambua.
Baada ya muda tukafanikiwa kuelewana bei na lori la mbao lililokuwa linaelekea Mafinga,
Jojina akawa siti ya mbele mimi nikawa nyuma huku na vijana wengine.
Safari hii haikuwa na mushkeri wowote ule.
Tukafika Iringa mjini majira ya saa nne usiku!!
Tukatembea kwa miguu kuitafuta nyumba ya Jojina.
Tukaifikia nyumba vyema, lakini mazingira haya yalikuwa tofauti kidogo!! Ni kama kuna aidha ukarabati ulikuwa umefanyika ama la yale makazi kuna mtu aliongeza ama kupunguza kitu.
Naam!! Tulipoufikia mlango palikuwa na kufuri!!
Nani amefunga sasa? Wakati sisi tulikuwa tukitumia kitasa cha kawaida!!
Hatukungoja usiku ule upite, tukazunguka kwa nyuma na kuifikia nyumba ya mmiliki wa nyumba zote pamoja na chumba alichokuwa amepanga mama lao!!
Mwenye nyumba alikuwa hajalala, kuna mambo ya faragha alikuwa anashughulika nayo na mkewe na bila shaka ujio wetu ulimshtua sana!!!
“Kulikoni Jojina…” aliuliza kwa sauti tulivu.
“Mimi n’do niulize kulikoni kama ni kodi yako nilimaliza mapema tu vipi tena kufuli jipya mlangoni kwangu!!”
Mwenye nyumba akaduwaa kabla hajauliza.
“Wewe mwanamama wewe mbona mnataka kunivuruga sasa. Si wamekuja kaka zako hapa na dada zako wengine kudai kuwa unahama wewe, tena wamekuja na simu yako wewe kuwa haurudi tena hapa. Tena kizuri zaidi walikuja na mwenyekiti wa mtaa na mjumbe, mimi nikawaruhusu wakachukua mizigo yako kuwa wanakuletea huko ulipo, sijui kwa mume wako wewe!! Mi hayo sijui na hapa wakaacha vitu vichache tu!!!” alijibu kwa kujiamini baba mwenye nyumba.
“Mungu wangu weeeee!! Bahasha!!!” ndicho kitu cha kwanza kabisa kukumbuka kuwa tulikiacha ndani ya chumba kila kabla ya kusafiri!!!
Jojina akalegea na kushuka chini.
Akakaa!!
Nikaungana naye katika fedheheko hili!!!
Bila kithibitisho kile ni wapi zaidi pa kujitetea?
Tumekwisha!!!!
Nilikiri kimoyomoyo!!!
 
mlikuwa nami mh. Bwana Kikofia bin laden katika moja na mbili
Tutaonana badae coz am gonna
a3ad11475874de4eb5df808bf3ebaa3d.jpg
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom