Makapuku Forum

Makapuku Forum

SEHEMU YA NNE
SEHEMU YA NNE

KILICHONISAIDIA ni uenyeji wangu katika mitaa ile, niliongeza kasi na kisha nikapinda mkono wa kushoto ghafla na baada ya hatua mbili nikayumba kulia na hapo nikakutana na kichochoro kingine na kwa mbali ulikuwa ni uwanja wa mpira. Uwanja ambao zilizuka vurugu siku kadhaa nyuma na kunikutanisha na Ezekiel na sasa nipo katika balaa.
Kulikuwa na wachezaji uwanjani wakiwa katika mazoezi, nikaona hiyo ni nafasi ya kipee ya kupata wasaidizi. Nikaanza kupiga mayowe kwa jitihada zote huku nikipepea mikono juu.
Kumbuka nilikuwa kifua wazi!! Wanasoka wale wakabaki kunishangaa mimi huku wengine wakisogea nyuma na pembeni kwa tahadhari ya lolote baya ambalo nilikuwa nakabiliwa nalo.
Walinipokea huku wakisubiri kuona ni kitu gani kinanifanya nirukwe akili vile.
“Majambaziii majambaziiii…..” nililalamika huku pumzi zikikata na hofu ikitanda zaidi.
Kusikia neno majambazi, tahadhari kubwa zaidi ikachukuliwa kila mmoja akawa katika mkao wa kujiokoa mwenyewe. Macho yakatazama pande kuu nne za dunia lakini hakuna kilichotokea. Umakini ukaongezeka hadi wa kutazama pande zote kumi na sita, thelathini na mbili na hadi sitini na nne. Hapakuwa na kitu chochote cha hatari kilichojongea pale uwanjani.
“Huyu chizi huyu labda…” mchezaji mmoja akatoa hoja hiyo. Wenzake wakamkanya na hapo wakamtambulisha kuwa mimi ni mwandishi wa habari katika gazeti fulani. Licha ya yeye kuduwaa, mimi niliduwaa maradufu. Kumbe najulikana sana.
Yule aliyetoa shutuma za kuwa mimi nina wazimu akagwaya!! Akaungana na wenzake kuendelea kungoja hayo majambazi.
Bado hayakutokea!!
Wakaanza kupungua mtu mmoja baada ya mwingine, nikahisi vichwani mwao wamekubaliana na wazo la yule mwenzao kuwa huenda nimepandwa na wazimu.
Hatimaye nikabaki peke yangu, kifua wazi!! Kifurushiu mkononi. Kila mmoja akaendelea na shughuli zake, hakuna ambaye alikuwa tayari kuniamini.
Nikiwa kifua wazi nikalazimika kuendelea kukimbia maana niliamini kuwa wale watu wabaya walikuwa wakinifuatilia.
Nilitembea kwa tahadhari huku nikiamini kuwa watu kadhaa waliokuwa wananifahamu walikuwa wakinishangaa. Nilipenya nyumba kadhaa hatimaye nikafika nyumbani kwa Enock, rafiki yangu ambaye kabla ya kuhamia kwake ni mimi nilimkaribisha jijini na akaishi nami chumba kimoja kabla sijaamua kuishi na mama Eva.
Nilimkuta mnkewe yeye alikuwa ametoka kidogo. Mke wake ambaye ni shemeji yangu alishtuka kuniona katika ile hali, nikiwa katika pensi na mkononi kifurushi kikiwa na makaratasi ambayo ni mimi pekee niliamini yalikuwa yana umuhimu.
Shemeji alinikaribisha ndani huku macho yake yakikwepa mara kwa mara kunitazama.
“Shem…hebu mwambie Enock akatishe zoezi la kuoga aje kunisikiliza” shemeji akaruka upesi na kuelekea bafuni, hakurejea tena badala yake Enock akiwa amevaa taulo alitokea sebuleni.
“Kaka nini tena hiki….kimetokea nini…mama Eva ama?? Yaani mmefikia huku.” Alizungumza upesiupesi asinipe nafasi ya kusema lolote, nikaamua kumkatisha, “Noki eeeh!! Hebu nisikilize bwana…..” nilifoka kisha nikamsimulia kwa ufupi kuwa haja yangu ya kwanza ilikuwa nguo. Hilo hapakuwa na utata, miili yetu iliendana hivyo ningeweza kuvaa nguo zake.
Akanitimizia hilo mara moja nikavalia palepale sebuleni. Na baada ya pale nikamwomba anipatie kiasi fulani cha pesa, uzuri ulikuwa mwisho wa mwezi na alitambua ni fadhila kiasi gani nimewahi kumtendea. Nikamtajia kiasi akaniahidi kunipa kiasi chote kama nilivyoomba.
“Mengineyo nitakupigia simu uje mahali tukae tuzungumze, hapa si mahali sahihi hata kidogo. Kuna watu wabaya wasije wakazua lolote la kuzulika.
Enock hakunielewa kabisa lakini hakuwa na la kufanya, nilikuwa nimefedheheka na akili yangu ilikuwa haijakaa mkao wa kusimulia juu ya Ezekiel kisha mazingaombwe ya kumuona akiwa Ubungo hai na kisha akiwa maiti anayeharibika kitandani baada ya nusu saa, mkasa wa mke wangu kuchukuliwa kisha kuachwa ujumbe, mkasa wa Selemani yule mtoto kukwapuliwa na watu wabaya kisha kuanza kunifukuza mimi. Ningeweza vipi kusimulia tukio lote kwa ufasaha wakati shemeji yangu alikuwa ameniona nikiwa kama tahira tayari aliponikaribisha ndani.
Hakika sikuweza!!
“Enock….shemeji yako yupo matatani hadi sasa sijui alipo, tukionana hiyo jioni ama muda wowote ule uje unishauri. Sijui kama yupo mwingine wa kunishauri zaidi yako” nilimnong’oneza Enock kisha nikajivika vyema kofia aliyonipatia, kifurushi changu nikakiweka katika mpangilio mzuri, badala ya ule mfuko mweusi sasa niliyapanga makaratasi yale katika bahasha kubwa ya kaki.
Dereva wa pikipiki akapigiwa simu, akafika hadi mlangoni. Nikapanda pikipiki na kuagana na Enock mwenye mashaka.
“Nipeleke Ubungo maji.” Nilimpa maelekezo.
“Shilingi ngapi?” nilimuhoji.
“Jamaa amesema atalipia kila kitu cha msingi nikupeleke popote utakapoenda.” Alinijibu.
Kisha akavaa ngao ya kichwani na kutokomea.
Wakati huo ilikuwa tayari saa saba mchana!!!
Upepo uliovuma wakati pikipiki ikizidi kushika kasi, kidogo ulinipa ahueni ya kufikiri. Nilijiona mtu kati ya watu. Lakini mtu asiyekuwa mkamilifu!!
Mke wangu alikuwa matatani. Na hawa jamaa hawakusema naenda kumchukua wapi. Baadaye kidogo nikatabasamu baada ya kugundua kuwa kile ninachokiandika kila siku sasa kilikuwa kinanitokea. Maisha ya kwenye simulizi!!
Tulipofika Ubungo maji nilishuka na kumshukuru yule bwana.
Baada ya kuondoka nikachukua daladala iliyonipeleka maeneo ya kimara. Nilifanya vile ili kukwepa kupatikana kirahisi iwapo tu mambo yatakuwa makubwa zaidi ya pale.
Nilichukua chumba maeneo ambayo yalikuwa yamejificha sana. Nikajiandikisha jina la uongo na hatimaye nikawa chumbani huru.
Nilihisi uchovu lakini sikutaka kulala, nikafungua bahasha yangu. Kitu cha kwanza kukitoa ilikuwa ni picha ndogo ya mtoto wa kiafrika alikuwa anatabasamu. Haikuandikwa chochote kwa mbele lakini nyuma yake iliandikwa ‘MICHIGAN’.
Jina likanichanganya sana, hii Michigan ya bara la Amerika ama Michigani ni jina la yule mtoto katika picha. Na inahusu nini sasa picha hiyo!!
Nikabakli na swali kuu la kwanza, nikaiweka kando ile picha nikakutana na makaratasi mengine, moja lilikuwa na maandishi yaliyoandikwa na mtu ambaye anajifunza kuandika ama ni maksudi aliamua kuhadaa kwa namna ile. “THE DON 20 MKAKATI WA KUDUMU” Halikuandikwa neno jingine zaidi.
Makaratasi yalikuwa mengi sana na pia picha mbalimbali, nyingine nikamuona Ezekiel, alikuwa amekumbatiana na mwanaume wa kizungu, kwa namna walivyokuwa Ezekiel alionekana kama hapendi kushikwa vile lakini ilimlazimu tu. Katika picha ya mzungu paliwekwa alama ya ‘x’….hapakuwa na maelezo kwa nyuma.
Katika kila karatasi nilijaribu kubashiri majibu yangu lakini hata moja halikuonekana kuendana na ukweli wowote bambao ungeweza kunivusha hatua moja mbele.
Ina maana Ezekiel alikuwa analazimishwa kuwa alivyokuwa?
Nani alikuwa anamlazimisha?
Michigan? Ni kitu gani hiki?
Picha ya yule mtoto na yule mzungu aliyewekewa alama ‘x’ zinahusika vipi?
Haya yalikuwa baadhi ya maswali yaliyolundikana katika kichwa changu!!
Kabla sijamaliza makaratasi mengine, nilihisi njaa kali, hapa ni baada ya kusimama. Nilipoangalia saa ilikuwa saa kumi na mbili na nusu jioni. Nikakumbuka sikuwa nimekula kwa siku nzima.
Ahadi ya kukutana na Enock nayo ikawa imekufa, kwa sababu simu yangu ya mkononi niliiacha ndani wakati naenda kuoga na sikurudi tena kuichukua.
Nikajikongoja hadi nje na kufanikiwa kupata chakula. Nikala kwa kadri ya mahitaji yangu na kisha nikalipia na kurejea chumbani ambapo nilioga na kujaribu kujinyoosha kidogo. Usingizi ulipoanza kuninyemelea nikajiahidi kuwa nitalala kidogo na kisha kuamka, nipitie tena makaratasi yaliyosalia ili siku inayofuata niende polisi kisha nifike kazini pia kutafuta watu waelewa ambao wangeshirikiana nami katika mkasa huu wa ajabu ambao hadi wakati huo ulikuwa umenitia matatani.
Haikuwa kama nilivyojiahidi, nilikuja kushtuka majira ya saa saa kumi na mbili asubuhi. Kitu cha kwanza kusikia zilikuwa ni kelele zilikzokuwa zinapigwa na mwanamke, nilizisikiliza kwa makini nitambue kama kuna hatari yoyote eneo lile lakini nikang’amua kelele zile hazikuwa na wasiwasi wowote na wala hazikuelezea uchungu wowote na badala yake zilikuwa zinaelezea raha fulani na huyo aliyezipiga hakujua kama alikuwa anapiga kelele na kusumbua wengine ambao walikuwa wamelala tena peke yao.
Nikaghafirika na kuwashangaa wawili hao waliokuwa wakifanya mapenzi kwa raha zao na kutupigia kelel wengine.
Nikachukua rimoti na kuwasha luninga bila dhumuni lolote ilimradi tu kukwepa kuzisikia kelele za mwanamke yule ambaye kwa lugha moja ningeweza kusema hajastaarabika.
Nilisimama na kujinyoosha viungo kisha nikauendea mlango wa bafuni, nikaingia kwa ajili ya kujistiri na haja ndogo. Niliacha mlango wazi, sikuwa na shaka kwa sababu nilikuwa mwenyewe.
Nikiwa maliwatoni, nilisikia vitu ambavyo akili yangu ilinituma kuwa ni muhimu nivisikilize, upesi nikarejea chumbani na kukuta mtangazaji akizungumza juu ya habari fulani ya kuvutia.
“……mwandishi huyo ambaye alitimua mbio baada ya tukio anasadikiwa kufanya mauaji hayo kwa makusudi. Mwanamke aliyemshuhudia kwa jicho lake akitokea chumbani mwa marehemu anadai mwandishi alitimua mbio baada ya tukio hilo. Uthibitisho zaidi wa suruali yake ambayo ilisheheni simu ya mkononi ambayo imethibitika ni mali yake, pochi iliyokuwa na pesa taslimu laki tatu, katika suruali palikutwa pia na sumu kali ya kuulia wanyama. Jitihada za kumpata yeye na mkewe waliyekuwa wanaishi naye ziligonga mwamba. Hata hivyo mtoto wao mdo aliyejitambulisha kwa jina la Eva amehifadhiwa na jeshi la polisi Tanzania. Huku upelelezi wa kuhakikisha Samson Josephat na mkewe wanaingizwa nguvuni kwa kosa hilo la mauaji.” Alipomaliza kusoma habari hiyo, ilionyeshwa picha kwa ukaribu kabisa, ilikuwa ni suruali yangu, na pochi ilikuwa yangu lakini sumu na zile pesa hazikuwa mali yangu!!!
Na mbaya zaidi waandishi na maaskari wakaaminishwa kuwa nguo zile zimekutwa katika chumba cha Ezekiel.
“Mungu wangu..kwani yule dada hakuniona kuwa nilikuwa nimevaa suruali yangu na shati zuri kabisa!!” nilijiuliza kwa sauti kama kwamba kuna yeyote wa kushirikiana nami katika mjadala huu.
Wakati nawaza juu ya mchezo huu wa ajabu na mchafu kuwahi kunikumba nikaikumbuka kauli ya mwisho ya mtangazaji…”Mtoto wao mdogo aitwaye Eva…..”
Mapigo ya moyo yakapiga maradufu!!
Eva alinizoea mimi na mama yake tu!! Hakuna mtu mwingine ambaye angeweza kuishi na Eva.
Mtoto wangu jamani!! Nilijikuta katika manung’uniko na majuto wakati sijui najutia jambo gani!!
Mambo yalikuwa yameharibika.
Wakati nahangaisha kichwa changu kufikiria ni jambo gani sahihi natakiwa kufanya, habari ile ikaendelea, wananchi kadhaa walikuwa wakihojiwa juu ya tukio lile, macho yangu yakamwona yule mchezaji aliyeniita mwehu. Alizungumza kwa hisia kubwa sana akinishutumu kuwa alihisi tu kuna jambo baya nimefanya lakini wenzake wakampinga!!
Nilitaka kumpiga ngumi lakini nikakumbuka kuwa kile ni kioo, yeye hayupo pale.
Kwa siku ile sikuiona sura yangu ikirushwa kwenye luninga lakini ningejuaje labda vituo vingine walirusha picha yangu!! Hii ni hatari sana.
Mke wangu yupo wapi?? Hii ni hila ya watu wabaya kwa sababu nimewakimbia basi wamemuunganisha na mke wangu katika tukio mili kuunda ukweli, maana kwa kumwacha yule angenitetea mpaka tone lake la mwisho la damu.
Lakini hakuwepo tena!!
Safari ya kwenda kituo cha polisi kutoa taarifa ikaishia pale na sasa nikawaza mengine, lakini hata yenyewe hayakujiweka katika mkondo mahususi!!!
Nikapagawa!!!
 
SEHEMU YA TANO
SEHEMU YA TANO

Nikiwa na utambuzi fika kuwa mambo yamenikalia vibaya mimi na familia yangu nikaamini kuwa huu ulikuwa wakati muafaka wa kuishughulisha akili yangu mara elfu moja zaidi nilivyojishughulisha kuandika simulizi ya KWAKO MPENDWA, simulizi ambayo ilinipa tunzo katika kampuni yangu.
Nilitambua kuwa thamani yangu haikuwepo tena na mtu pekee wa kuweza kuirejesha ni mimi pekee. Upesi bila kuoga nikavaa suruali yangu na kisha nikatoweka kutoka katika nyumba ile ya kulala wageni. Wakati natoka nilipishana na muhudumu wa kike ambaye alinipatia chumba siku iliyopita.
“Shkamoo….habari za asubuhi kaka…” alijing’atang’ata wakati wa kunipa salamu, kivipi binti ambaye tunalandana katika suala la umri anisalimie ‘shkamoo’ tena alionekana kubabaika waziwazi.
Sikumjibu chochote, badala yake nilitoka nje na kisha kutokomea mbali zaidi na nyumba ile.
Usafiri wangu kwa mara nyingine ukawa pikipiki. Nikapenya mitaa kadhaa na hatimaye nikafika Kibamba.
Nikiwa na kofia kichwani, nikafanikiwa kununua na miwani. Nikajipachika usoni. Sasa niliamini kuwa hakuna ambaye angeweza kunona. Ilikuwa mara yangu ya kwanza kuyaficha macho yangu nyuma ya miwani.
Nilitazama huku na kule hadi nikayafikia magazeti. Gazeti la kwanza kutazama lilikuwa ni Mwangaza. Gazeti ambalo nilikuwa nafanya kazi hapo.
SAMSON AMESINGIZIWA: ASEMA MATATA.
Nilijikuta natabasamu kidogo, Alfred Matata; huyu ndiye alikuwa mmiliki wa kampuni inayochapisha gazeti lile na kwa namna ya pili alikuwa bosi wangu. Aliniamini sana kupindukia na mara kwa mara alinishirikisha juu ya mambo yake ya siri.
Walau mwajiri wangu ameutambua upande wa ukweli, huyu ndiye ambaye angeweza kunisaidia mimi kujua naanzia wapi. Nikalipia lile gazeti nikapatiwa nakala yangu na kisha nikapuuzia vichwa vingine vya habari vilivyosisitiza kuwa mimi ni muarifu na ninasakwa kwa udi na uvumba.
“MATATA MATATANI KWA KUMTETEA MUUAJI” Kichwa hiki cha habari pia kilinivutia lakini nilipuuza baada ya kugundua kuwa lile ni gazeti la udaku.
“Pumbavu kabisa…” nilijisemea huku nikitowewka eneo lile na kuambaa upande mwingine wa barabara, nikafikia kwa mama lishe ambaye alikuwa akichochea moto kwa ajili ya kuanza rasmi kuisaka riziki yake, nikachukua nafasi katika dawati lililokuwa pale.
“Chai bado sana…” nilizungumza huku nikilifunua gazeti.
“Kidogo tu baba yangu, lakini kitafunwa tayari, maandazi yapo na mihogo hii hapa nageuza.” Alinijibu kwa staha. Nikaendelea kusoma kurasa za gazeti lile.
Nikaipitia taarifa kuhusu Matata kukanusha juu ya madai kuwa nimeua na kisha kukimbia. Kadri nilivyozidi kusoma moyo wangu ulisuuzika na lile barafu gumu la uchungu na wasiwasi lililokuwa limeniganda nikahisi likiyeyuka. Moyo wangu ukafanya majuto kidogo kwa kitendo changu cha kuwahi kujihusisha kimapenzi na binti wa mzee huyu, lakini cha kushukuru ni kwamba hakuwahi kugundua. Na hata baada ya kuanza kuishi kinyumba na Mama Eva, nikamtupilia mbali binti yule ambaye alidai ataendelea kunipenda kila siku.
Potelea mbali, sikuwahi kumpa mimba na wala sikuwahi kumfelisha katika masomo yake!!
Nikaimaliza makala ile huku nikipata mwanga juu ya wapi naenda kuanzia.
Kwa sababu mama Eva alikuwa amekamatwa kiujanjaujanja basi mzee Matata angeweza kuwa mtu sahihi wa kuanza kuzungumza naye na hata kumkabidhi makaratasi yale ili tusaidiane katika ufumbuzi.
Nikaanza kuifikiria safari ya kurejea jijini Dar es salaam kwa tahadhari kubwa ili niweze kuonana na mzee mwenye hekima,. Mzee Matata. Tena nilitakiwa kufanya maamuzi haraka sana kabla mambo hayajawa mazito na zile tetesi za kipuuzi kuwa mzee Matata matatani kwa kutetea muuaji hazijawa kweli.
Nilitambua kuwa kwa mujibu wa muda ingeweza kuwa saa mbili za asubuhi, hata mama muuza naye nilipomuuliza alinijibu kwa uhakika kana kwamba ana saa mkononi, akasema ni saa mbili.
Wakati huo nilikuwa namalizia pande la muhogo!! Nikagida chai na kufanya malipo kisha nikaambaa kuelekea kona nisizozifahamu, maeneo ambayo hayakuwa karibu sana na barabara.
Huko nikakutana na kibao kilichoonyesha nyumba ya kulala wageni!!
Eneo muafaka kabisa kwangu kwa wakati ule.
Nikaingia pale na kukutana na muhudumu.
“Vyumba havijafanyiwa usafi kaka hadi saa nne ndo wateja wa mwishomwisho wanatoka.” Alinijibu kichovu huku akijifuta tongotongo machoni.
Nilijipigia hesabu za kichwa na mara nikakumbuka kuwa wasiwasi wangu wa kurejea mjini, ulikuwa wa bure. Mwanzo nilihisi kuwa mzee Matata atakuwa kazini, lakini nikakumbuka kuwa asubuhi hiyo ilikuwa jumapili. Lazima angekuwa nyumbani kwake. Nikaondoka na kisha nikachukua pikipiki tena, bahasha yangu ikiwa kitu cha muhimu kupita chochote katika mwili wangu!!
Nikapepea hadi maeneo ya Shekilango!!
Nikafanya malipo na kuchepuka kwa hatua kubwa kubwa nikavuka barabara na kuingia vichochoro kadhaa, hatimaye nikatazamana na nyumba ya mzee Matata. Makala yake kuhusu mimi ikaendelea kunijengea uaminifu kwake, nikagonga hodi nikapokelewa na mlinzi ambaye alikuwa akinifahamu, sikutaka kuzungumza naye sana, nikaingia hadi ndani, nikaufikia mlango mkuu wa kuingilia.
Aliyenipokea alikuwa mke wa mzee Matata, akanikaribisha kwa ukarimu wote kama ilivyo kawaida yake, baada ya salamu akaniuliza kama nitakunywa chochote, nikataka kukubali lakini nikahisia nitapoteza muda wakati mihogo ya mama lishe bado ilikuwa tumboni.
Nikashukuru na hapo nikamuulizia mzee Matata.
“Ameenda kanisani.” Akanijibu kwa sauti tulivu huku akihangaika kupunguza sauti katika runinga iliyojiongeza sauti kimakosa.
Jibu la mwanamke huyu likanistaajabisha lakini nikajificha nisijulikane kama nimestaajabika, mzee Matata na kanisa wapi na wapi? Kila siku ofisini alikuwa akitukashfu sana watu tunaojifanya kuhudhuria kanisa wakati kanisa ni biashara. Mzee Matata hakuwahi kusifia lolote juu ya nyumba za ibada ambazo mkewe alikuwa muhudhuriaji mzuri sana na hata watoto walifuata nyendo za mama yao. Kasoro yeye tu!!
Iweje leo ameenda kuhudhuria ibada. Tena asubuhi yote ile.
Nikaguna lakini sikuuliza kingine nje ya uwezo wa yule mama, badala yake nikaulizia atarudi saa ngapi.
“Ibada huwa inamalizika saa sita, nadhani unaweza kukadiria.” Alinijibu, sasa alikuwa ananitazama machoni.
Nikapiga mahesabu yangu upesiupesi nikakutana na jibu la uongo!!
Ibada ipi ya kumalizika saa sita wakati kwa maelezo ya awali mzee Matata alitoka asubuhi sana.
Kwanini ananidanganya? Nilijiuliza huku nikijisikia vibaya kudanganywa na mama yule mtu mzima.
“Haya mimi nipo jikoni mara moja…rimoti hiyo unaweza kubadili chaneli” alitoa kauli hiyo huku akisimama na kujifunga kanga yake vyema kisha akatoweka.
Hakuelekea jikoni!!! Uongo mwingine. Mzee Matata kama nilivyokwisha elezea alikuwa mzee wangu wa karibu kuna kipindi mkewe akiwa masomoni niliishi nyumbani kwake, kwa siku kadhaa nilizijua kona nyingi sana. Na hata mtoto wake nilimpata kipindi hicho.
Nililifahamu jiko lilipokuwa, lakini mwanamke huyu hakwenda jikoni!!
Kwanini?
Wakati najiuliza na kuumiza kichwa juu ya hayo mara mtu alivamia sebuleni ghafla huku akiweka tahadhari juu ya uwepo wake katika sebule ile.
Nikashtuka kidogo, nikamtazama na kuwahi kutaka kumsalimia, lakini kabla sijasema lolote akaniziba mdomo. Mikono yake ya uvuguvugu iliyokuwa inanukia marashi haikunikera.
“Sam….wanasema umeua, umeua jana Sam. Sikia kama ni kweli umeua Sam, hapa si mahali sahihi hata kidogo pa wewe kukaa hata kwa sekunde moja. Baba na mama wametishwa sijui na nani? Wameambiwa wanatambua wewe ulipo Sam, kama mama amekwambia baba ameenda kazini ni uongo mtupu, amepeleka vyeti vyako vyote vya shule polisi amepeleka picha na kila kitu kuhusu wewe, alama yako ya dole gumba, jaribu kunielewa sam. Amepeleka kila kitu!!! Kila kitu sam….Sam pliiiz Sam unajua kuwa nakupenda, na kwa namna yoyote aidha umeua ama hujaua, sam nakutambua kama mwanaume mkarimu kupita wengi katika maisha yangu, sikukosea kukupenda sam, na nilikuahidi kuwa nitakupenda milele, Sam ukiendelea kuwa hapa watakufunga Sam. Sitaki kujua kwa nini uliua lakini sitaki kusikia ukihukumiwa kunyongwa. Mlizni getini aliambiwa ukionekana hapa asikuruhusu kutoka tena. Na makala aliyoiandika upesi upesi alitaka kukujenfea imani naye. Baba anatamani upatikane ili kampuni yake iendelee vizuri Sam….” Alishindwa kuendelea kuzungumza yule binti akaanza kutokwa na machozi. Bado alikuwa ameniziba mdomo. Alikuwa anatetemeka na uso wakle ulimaanisha kila alichokuwa anasema.
“Anitha…sikia Anitha ukilia si ndo utanipoteza mimi ama…nyamaza nambie nafanya nini, Anitha sijaua hii ni njama tu. Njama ya kuniteteketeza family yangu kutokana na siri nzito Anitha. Siri ambayo…..yaani aaah…Anitha nisaidie nitoke.” Nilimwambia kwa kunong’ona huku kiganja changu kikiwa kimejikita katika kubadili Chaneli hovyohovyo bila sababu za msingi, nilikaa mfumo wa nusu tako kitini nusu nyingine isieleweke kama ipo hewani ama imefanya mgomo wa kukaa.
Ni kama nilitaka kusimama.
“Sam….Sam…mama mama huyooo atajua….” Aliweka tahadhari na kisha akatimua mbio kuelekea vyumbani.
Na hapo akafika mama mwenye nyumba, nilirudisha miwani usoni asiweze kuisoma hofu yangu!!
“Anakuja baada ya kama nusu saa hivi, kumbe wametoka tayari. Pole kwa kumsubiri shemeji yangu jamani.” Alinikarimu, lakini sasa sauti yake ilikuwa katika namna ya maigizo na uso wake ukitangaza hasira.
Nikayaamini maneno ya Anitha, msichana ambaye aliwahi kuwa mpenzi wangu lakini kutokana na heshima kubwa niliyokuwanayo kwa mzee wake nikaamua kuyatupia mapenzi kando.
Sasa alikuwa amenionyesha maana ya upendo!! Anitha hakuwa ameamini hata kidogo juu ya tetesi za mauaji niliyofanya, na hata kama ni kweli alikuwa amesisitiza kuwa hatajali.
Mwanamke wa kipekee!!
Mama aliendelea kupiga porojo zake nami nikaweka tabasamu bandia, alisema anarejea baada ya nusu saa na Anitha alinieleza kuwa mlinzi alizuiwa asiniruhusu nitoke baada ya kuingia.
Hawa jamaa ni akina nani hawa? Inawezekana wakawa ni polisi kweli wameamini kirahisi hivyo kuwa nimeua?
Nilijiuliza na dakika kumi na tano zilikuwa zimekatika!!
Mama alikuwa akiongea maneno mengi tofauti na kawaida yake!! Nikajua hii ni njama nyingine ya kunihadaa, njama ya kunipotezea wakati ili mumewe afike na polisi ama na yeyote yule waweze kunikamata.
Na kama ni njama walikuwa wamefanikiwa haswa! Ningeaga vipi pale na kuweza kutoroka na kisha kujipanga upya.
Ghafla wazo likajikita katika ubongo.
“Hivi mama zile picha za sherehe ya kutimiza miaka hamsini zipo ujue siku ile mama Eva alinighasighasi hata sikuzitazama vyema…”
“Wacha weee!! Haukuziona kumbe ngoja nikuletee maana zipo katika albamu…nzuri hizo.” Alisifia huku akiondoka, nikaisoma akili yake kuwa yule mama alikuwa amejidanganya kuwa kwa kuangalia albamu ile nitakuwa nimemsaidia katika zoezi la kuuvuta muda maana kama ni maongezi hakika alikuwa ameishiwa.
Wakati huo zilisalia takribani dakika tisa itimie ile nusu saa aliyoisema mama huyu kuwa mzee Matata atarejea.
Alipotoka na mimi nikaishika vyema bahasha yangu na kusimama, kumbe Anitha alikuwa akinitazama kupitia alipokuwa amejificha.
“Anitha, kama wakinikamata usiachie hii bahasha iende kizembe. Humu kuna kila kitu!!” nilimwambia kwa sauti ya kukwaruza kwaruza. Na nikamwona macho yake yakilengwa na machozi. Sikugeuka tena.
Nikaondoka na kulifikia geti, geti lilikuwa limefungwa kwa kufuli lakini halikuwa limebanwa, nilipojongea nd’o kwanza mlinzi akalibana lile kufuli kisha akaendelea kuvuta sigara huku akipuliza moshi hewani.
Ametimiza wajibu!! Nilijisemea huku akili ikigoma kabisa kujua ni kipi nafanya kwa wakati huo. Nilijua kuwa Anitha ananitazama kwa huzuni kubwa, nilijua mama amekaribia kufika tena sebuleni akiwa na albamu, na kubwa zaidi nilitambua kuwa mzee Matata si rafiki tena bali adui mkubwa na muda wowote ule anawasili hapo kwa ajili ya kunikamata aidha akiwa na polisi ama akiwa amehadaika na njama za wale watu wabaya waliochanganyikana na wazungu!!!!
Miguu ilikuwa inatetemeka na bahasha ikaanza kulowa jasho, jasho jepesi kutoka katika kwapa lililokuwa limeibana vyema.
Nimekamatika!!

JIFUNZE: Rafiki hugeuka adui, usimwamini mtu kwa asilimia mia. Jiamini wewe kwa sababu kamwe huwezi kujidanganya na hata ukijidanganya utatambua kuwa unaponda maji kwenye kinu!!!! Yaani ni kazi bure……
Lakini moyo wa mwenzako ni kiza kinene!! Huwezi kujua……. JIFUNZE
 
bd91eb752dc85307b1ce722171507e9b.jpg
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom