Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu imewaachia huru wanafunzi 17 na Mhitimu mmoja wa Vyuo Vikuu na Vyuo vya Kati mbalimbali Jijini Dar es salaam waliokuwa wakikabiliwa na mashtaka ya kughushi nyaraka na kujipatia mikopo ya Bodi ya Mikopo ya Elimu ya Juu (HESLB) kwa njia ya udanganyifu.
Uamuzi huo umetolewa na Hakimu Mkazi Mkuu, Romuli Mbuya baada ya kukubaliana na hoja za Wakili wa Utetezi, Peter Madereka kwamba hati ya mashtaka ilifunguliwa kinyume cha Sheria kwa kuwa haikuambatana na nyaraka zote za ushahidi kama inavyotakiwa.
Hata hivyo, Upande wa Mashtaka ulidai kuwa Sheria inaruhusu ushahidi kuwasilishwa siku nne kabla ya kusomwa kwa hoja za awali, lakini Mahakama haikukubaliana na hoja hiyo na kuiondoa hati ya mashtaka, hivyo kuwaachia huru Washtakiwa wote.
Hata hivyo, muda mfupi baada ya kuachiwa huru, washtakiwa hao walikamatwa tena na askari.
Kwa mujibu wa mashtaka yaliyokuwa yamewasilishwa Mahakamani, Washtakiwa hao walikabiliwa na jumla ya makosa 47, yakiwemo kughushi nyaraka, kutoa nyaraka za uongo na kujipatia mikopo ya HESLB kwa njia ya udanganyifu.
Ilidaiwa kuwa kati ya Juni 2024 na Novemba 2025 waliandaa na kuwasilisha nyaraka za uongo kupitia mfumo wa maombi ya mikopo ya elimu ya juu (OLAMS), wakidai wao au wazazi wao wana ulemavu ili waweze kupata mikopo ambayo hawakuwa na sifa ya kuipata.
Baadhi yao walidaiwa kujipatia mikopo ya kati ya shilingi milioni 1.8 na shilingi milioni 5.89 kwa kutumia taarifa hizo za uongo.