Mshitakiwa katika kesi ya kumbaka, kumlawiti mtoto mwenye umri wa miaka mitatu (jina linahifadhiwa), amemlaumu shetani kwa vitendo vyake, baada ya kutiwa hatiani kwa makosa hayo, na Mahakama ya Mombasa.
Mtuhumiwa huyo Ramadhan Atenya, amemlaumu shetani kwa kitendo hicho akisema kuwa alipagawa na pepo mchafu na hivyo kujikuta akifanya kitendo hicho.
Hata hivyo, Hakimu Mkuu wa Mombasa, Martha Mutuku, alikataa madai na utetezi huo, na hivyo kuamua kuwa upande wa mashtaka umethibitisha kesi hiyo inayomkabili pasipokuwa na shaka yoyote.
“Madai ya shambulio la pepo mchafu, hayana uhusiano wowote na mtoto mdogo aliyedhulumiwa. Upande wa mashtaka umeonyesha kuwa mtuhumiwa kwa kweli ametenda makosa hayo,” amesema hakimu huyo.
Hakimu Martha amebainisha kuwa ushahidi uliowasilishwa na upande wa mashtaka umemtia hatiani mtuhumiwa na kwamba alitambuliwa kuwa ndiye alieyefanya makosa hayo.
Kiongozi wa Mashtaka, Alex Gituma, ameiomba mahakama impe mtuhumiwa huyo adhabu kali ili iwe fundisho kwa wengine wenye tabia kama hiyo.
“Watoto wamedhulumiwa kutokana na vitendo vya watu kama mtuhumiwa. Naomba mahakama hii isimuonee huruma mtuhumiwa. Anapaswa kutumika kama funzo kwa wengine ili kulinda watoto dhidi ya unyanyasaji wa kimapenzi,” amesema Gituma.
Awali, mahakama iliambiwa kuwa mtoto huyo wa miaka mitatu, alikuwa akicheza nje ya nyumba yao wakati alipofanyia vitendo hivyo vya kikatili na mshtakiwa huyo. Upande wa mashtaka umedai kuwa mtuhumiwa alitenda makosa hayo Februari 5, mwaka jana.
Mahakama imeelekeza mtuhumiwa aendelee kushikiliwa rumande akisubiri siku ambayo mahakama itatoa hukumu juu ya kesi hiyo.