Mtumishi wa Halmashauri ya Wilaya ya Kilosa, Mkoa wa Morogoro, idara ya maendeleo ya jamii, Mereciana Calvin (42), ameuawa nyumbani kwake eneo la Mamboya huku shingoni akiwa na majeraha ya kukatwa na kitu chenye ncha kali.
Akitoa taarifa ya mauaji hayo, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Morogoro, Hassan Omary alisema uchunguzi unaonyesha mtumishi huyo aliuawa Julai 17, mwaka huu saa 3:30 usiku na mwili ulikutwa sebuleni kwake jana asubuhi.
Alisema pamoja na mtumishi huyo kuuawa, pia baadhi vitu viliibwa ndani mwake, ikiwemo televisheni, godoro na simu ya mkononi aliyokuwa akiitumia.
Kutokana na tukio hilo, alisema Jeshi la Polisi kwa kushirikiana na vyombo vingine vya ulinzi wa usalama Wilaya na Mkoa wanaendelea na uchunguzi, ikiwa ni pamoja na kuwasaka waliohusika kutekeleza mauaji hayo.
Naye Mkuu wa Wilaya hiyo, Shaka Hamdu Shaka alisema tukio hilo ni la kusikitisha na lazima vyombo vya ulinzi na usalama vifanye kazi usiku na mchana ili kubaini chanzo cha mauaji hayo na wote waliohusika ili hatua za kisheria zichukuliwe dhidi yao.
"Ni tukio baya ambalo haliwezi kufumbiwa macho, nina imani na vyombo vyetu vya ulinzi na usalama, najua kupitia wataalamu wao watachunguza vizuri na watatoa majibu kuhusu tukio hili ambalo linaonekana wazi kuwa ni la kupanga," alisema Shaka.
Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Halmashauri hiyo, Kisena Mabuba alisema baada ya tukio hilo mwili wa Mereciana ambaye pia alikuwa mratibu wa Ukimwi wa Halmashauri umehifadhiwa katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Morogoro na taratibu za mazishi zinafanywa.
View attachment 2692906