Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa amewataka Wakuu wa Mikoa na Wakuu wa Wilaya wafanye ziara kwenye masoko na maduka ili kupata hali halisi ya bei za bidhaa na wachukue hatua kudhibiti upandaji holela wa bei hizo.
Waziri Mkuu ametoa maagizo hayo leo Ijumaa, Aprili 22, 2022 wakati akizungumza na viongozi wa mikoa na wilaya kuhusu maendeleo ya maandalizi ya Sensa ya Watu na Makazi kwenye kikao kazi alichokiendesha kwa njia ya mitandao (video conference) kutokea ofisini kwake Mlimwa, jijini Dodoma.
“Tumepata malalamiko kutoka kwa wananchi kwamba bidhaa nyingi zimepanda bei, ninyi ni Wenyeviti wa Kamati za Bei na Kamati za Kodi kwenye mikoa na wilaya zenu, upandaji wa bei sasa umekuwa holela, ni jukumu lenu kufanya ufuatiliaji wa bei za mazao katika masoko yenu"
Waziri Mkuu amesema ziko bidhaa ambazo zinazalishwa nchini kama vile nondo au saruji ambazo hazipaswi kupanda bei hasa baada ya kutolewa tamko na Waziri wa Fedha na Waziri wa Uwekezaji, Viwanda na Biashara kwamba wameshaongea na wenye viwanda na wakakubaliana kuwa bidhaa zote za ndani zinapata nafuu ya kodi.
“Sasa iweje hali iendelee kuwa vilevile?”, vyakula vinavyozalishwa nchini kama mchele, Shinyanga mchele mwingi, Tabora mchele mwingi, Mbeya nako mchele mwingi kuna sababu gani ya kupadisha mchele wakati unazalishwa nchini?, kama ni mahindi au mihogo inalimwa huko kwenu, umbali wa mazao yanakolimwa mnaujua, iweje bei zipande? mpite kwenye masoko na kwenye maduka mpate bei za kila siku za maeneo yenu"