Tafasiri Unavyoweza: Mabadiliko, Teuzi Poteleambali
...kipengele hiki kama unavyojua ni siasa na jamii, kifupi maisha ya jamii yetu kisiasa. Kwa hiyo tegemea mengi yanayofanana na haya na kama kipengele kinavyojulikana, unaruhusiwa kutafasiri unavyoweza, nchi huru hii, usiogope. Teuzi zinaendelea, na hadi sasa ni kama ndo rais anaunda timu yake baada ya uchaguzi. Kumbuka miaka mitatu ishakata sasa, teuzi na tenguzi zinaendelea na bahati mbaya hakuna jipya. Ni kama kutoka ndani ya nyumba yako, unaizunguka na kisha unarudia mlango ule ule. Mabadiliko ni kuja na kitu kipya, sio kile kile ukitegemea kupata kitu kipya. Tafasiri unavyoweza.
Tumeona wakuu wa bodi za umma, wale wale, wazee (na hapa haimaanishi kuwatenga wazee) waliotumikia umma kwa muda mrefu, ni wastaafu hawa, waachwe wale pensheni na kucheza na wajukuu, wasipewe majukumu ilhali kuna nguvu kazi kubwa tu yenye mawazo ya sasa wanaoweza kuleta maendeleo yanayoonekana na si maendeleo ya Dar peke yake. wizara ya mambo ya ndani imepata mtu mpya wa zamani, polisi aliyetuhumiwa kupokea rushwa na kaja na kituko cha bendera ya taifa kwenye mifuko ya kaunda suti, tumeachana na skafu tumekuja na mifuko. Mabadiliko mgando, usitegemee kipya na ukikaa kimya utapata tabu sana.
Teuzi potelea mbali, hizi ni aina ya teuzi za kuwakomoa wanaokukosoa, ni teuzi za mpe wasiyempenda kwa sababu tu anasema yanayokufurahisha. Unataka kufanikiwa, basi jisogeze na tega sikio kwa wanaokukosoa kwa nia ya kujenga. Unamteua waziri kisa tu kawasema vibaya watu wa kusini na kwa kupigilia msumali unaahidi kuanza kuwachapa shangazi zao, kwa wasio na shangazi tutegemee nini, kuwapiga wajomba au? Tafasiri unavyoweza