Tafasiri Unavyoweza: Mzaha Wa Viwanda, Shirikisha Wote.
...tunapenda kuona Tanzania ya viwanda, ndiyo, huu ni uchu wa kila mpenda maendeleo nchini na bila shaka ukibebwa mioyoni mwa kila mmoja, kwa utashi wa wengi kwa kutambua kuwa tunajenga nyumba moja basi mchango wa sekta ya viwanda utakuwa mkubwa na viwanda vitakuwa vingi. Kwa sasa ni maneno mengi tu ndo utasikia, takwimu za mdomoni mara kila mkoa utajenga viwanda 3000+, ukitaka kuvitafuta viwanda hivi utachoka, vingine ni miradi iliyoko kwenye karatasi wala hakuna hata anuani. Tafasiri unavyoweza.
Sera nzuri na inayoweza kufanya kazi sehemu husika ni ile inayoshabikiwa na wengi, je unakumbuka zama za miradi ya umma kufa baadhi ya sehemu? Wananchi wanahitaji barabara, wanajengewa kiwanja cha ndege. Hizi zilikuwa ni zama ambazo maenedeleo ya Rukwa yalipangwa na watu wanaoishi Dar, hawaijui Rukwa, hawajui mahitaji yake na hivyo wakipeleka mradi, ile dhana ya umiliki ya wana Makanyagio pale Mpanda inakuwa haipo, wanaukanyaga mradi na unakufa maana wananchi hawakuuhitaji.
Tunapoongelea viwanda tunaongelea uchumi mkubwa, tunaongelea miundombinu inayowezesha viwanda viwepo, vimee na vichangie pato la taifa, sio masuala ya vyerehani vinne na maduka ya kunyoa nywele. Tunaongelea utayari wa serikali kujipanga na kuhakikisha umeme wa uhakika, miundombinu rafiki ya usafiri, kodi zinazobebeka na ulinzi wa tunachozalisha (smart protectionism), sio unazuia bidhaa toka nje ilhali hatuwezi kuzalisha kukidhi soko. Tuache mzaha, kauli mbiu ya viwanda, ili ifanikiwe iwe ya kitaifa na sio kichama, tafasiri unavyoweza