Tafasiri Unavyoweza: Shawishi Bila Maguvu
...kama kuna sifa moja kubwa ambayo viongozi wengi wanaikosa hapa kwenda ni sifa ya ushawishi. Uwezo wa kumshawishi mtu mwingine afanye unalodhani ni sahihi kwako, kwake na kwa jamii nzima. Hili linakosekana kwa wengi na tunachoona sasa ni maguvu badala ya ushawishi unaokubalika na wengi. Imezoeleka sasa na tumeona namna ushawishi wa watawala kwa wananchi unazidi kupungua kila kukicha na badala yake ni mabavu na vitiso vya kitoto. Fikiria kuhusu zile harakati za maandamano mtandaoni, badala ya kujadili hoja misuli ilitumika ya mikono na shingo iliwatoka viongozi wa dola kiasi wakajikuta wanakosa hata akili za kutoa ujumbe ikabaki ni vitisho tu.
Unamuangalia kiongozi uso wake umejikunja, hauna nuru, misuli ya shingo inamtoka kila anapotaka kuwasiliana na umma. Anataka aabudiwe, hataki majadiliano. Uoga huu kwa mtizamo mwingine ni dalili za mtu anayetaka kukuibia, hataki ufikiri, shuruti inatawala. Serikali ya kambale, kila mmoja anasharubu, dola inajipanga kukuvunja miguu, bunge limekuwa kwaya/kasuku kuimba kinachoimbwa na dola na mahakama inaambiwa kuna muhimili uliojichimbia zaidi. Umma umefungwa na wachache wanajiona wana haki na akili kuliko wengine na kila mtu anajaribu kusema tuko kwenye njia sahihi (right track), kama kasuku unarudia ulichosikia.
Kiongozi badala ya kusikiliza anajiandaa kujibu, anajiona yuko sahihi kwa sababu tu kazungukwa na vyombo vya dola na si ajabu ukimwambia asikilize atakufuata na vifaru. Ni suala la muda tu utaona kuwa kwa kuwa ushawishi ni mdogo basi msafara wa kiongozi utakuwa ukitanguliwa na vifaru na magari ya delaya ili kumfikisha kiongozi kuongea na wananchi! Tafasiri unavyoweza. Nimeandika sio kukushawishi, nimeandika usome