Makapuku Forum

SEVEN DAYS IN HELL (SIKU SABA KUZIMU)- 2 MTUNZI AZIZ HASHIM

ILIBIDI nisogee mpaka kwenye maegesho ya bodaboda nikiamini pale itakuwa rahisi kuzungumza na dereva yeyote ili aniwahishe kabla ile ‘ambulance’ haijapotea kabisa. Nilipopiga hatua moja, nilijiona kuwa mwepesi sana halafu tambo lilikuwa refu sana tofauti na kawaida.
Sehemu ambayo ningetembea hata hatua ishirini, nilipiga hatua mbili tu, nikawa nimeshafika pale kwenye bodaboda.

SASA ENDELEA…
“OYA mambo vipi mkubwa!” nilimsalimu dereva wa bodaboda aliyekuwa pembeni yangu kwa bashasha kubwa lakini hakuniitikia, akawa anaendelea kuifutafuta bodaboda yake.
Nilirudia kumsalimu lakini bado hakunijibu chochote na wala hakuonyesha kama ananisikia. Nilimgusa begani lakini bado ilikuwa ni kazi bure, aliendelea kufutafuta bodaboda yake, nikabaki nimepigwa na butwaa.
Ilibidi nimsogelee dereva mwingine wa bodaboda, naye nikamsalimia kwa bashasha lakini hakunijibu, nikarudia tena na tena lakini bado hali ilikuwa ileile, nikaenda kwa watatu ambaye alikuwa akipiga stori na wenzake, naye akaonyesha kutonisikia.
“Kwani imekuwaje? Mbona sielewi kinachoendelea?” nilijisemea huku nikianza kutetemeka kwa hofu kubwa, mwisho niliamua kufanya jambo moja, nilipaza sauti kwa nguvu nikiita ‘bodabodaaa!’ niliamini yeyote ambaye atakuwa wa kwanza kuniona basi nitamchukua huyohuyo lakini wapi! Kila mmoja aliendelea na mambo yake.
Ni hapo ndipo nilipogundua kwamba huenda nilikuwa sionekani kwa macho ya kawaida wala sauti yangu haisikiki licha ya ukweli kwamba mwenyewe nilikuwa najisikia vizuri tu.
“Sasa nitafanyaje?” nilisema huku nikigeuka kuitazama ile ‘ambulance’, tayari ilishapotea kwenye upeo wa macho yangu lakini akili zangu zilinituma kuamini kwamba lazima itakuwa imeupeleka mwili wangu Hospitali ya Taifa ya Muhimbili.
“Nataka nikashuhudie kila kitu kinachoendelea,” nilisema huku nikianza kutafuta mbinu nyingine ya kunifikisha hospitalini hapo. Sijui nilipata wapi akili hizo lakini nilijikuta tu nikiamua kuanza kutimua mbio kuelekea kule ile ambulance ilikoelekea.
Nilipopiga hatua chache tu, nilijikuta nikiwa napaa angani kwa kasi kubwa, nikawa naitazama mitaa ya jiji kutokea angani. Kuna wakati akili zangu zilinituma kuamini kabisa kwamba nilikuwa kwenye ndoto ya kutisha ambayo muda wowote itaisha lakini akili nyingine zikawa zinaniambia kwamba siyo ndoto, kila kitu kilikuwa kikitokea kwa uhalisia.
Wakati ambulance ikiwasili kwenye geti kuu la kuingilia Muhimbili, na mimi tayari nilikuwa nimeshafika eneo hilo, geti likafunguliwa na likaingia moja kwa moja mpaka kwenye eneo la ‘emergency’ ambalo wagonjwa wenye hali mbaya ndipo walipokuwa wanafikia.
Milango ya ambulance ilifunguliwa, manesi waliokuwa ndani ya ile ambulance pamoja na wengine waliokuwa pale mapokezi, walisaidiana kuushusha mwili wangu na kukimbizwa mpaka ndani, nikawa nashuhudia kila kitu kilichokuwa kinaendelea.
Harakaharaka nilianza kupewa huduma ya kwanza, nikamuona nesi mmoja akichukua mkasi na kukata shati nililokuwa nimevaa, nilipoliona jeraha lililokuwa kifuani wangu, nilisisimka mno. Nilijiuliza iweje mtu anifanyie ukatili mkubwa kiasi hicho, tena bila sababu ya msingi?
Japokuwa vitabu vya dini vinakataza kulipa kisasi, nilijikuta nikipandwa na ari kubwa ya kulipa kisasi, nilikuwa nimejeruhiwa sana. Niliwaona hata wale manesi akitetemeka kila walipokuwa wanalitazama jeraha langu.
Kwa bahati nzuri, madaktari wa kiume waliingia, huwa naamini siku zote kwamba sisi wanaume Mungu ametuumba na ujasiri mkubwa kuliko wanawake. Wakaanza kunifanyia kile ambacho
kitaalamu huwa kinaitwa ‘dressing’, yaani kusafisha jeraha kabla ya kuanza kutibiwa. Muda mfupi baadaye, tayari nilikuwa nimesafishwa jeraha hilo, nikahamishwa na kupelekwa chumba cha wagonjwa mahututi nikiwa bado sijitambui huku madaktari na manesi wakiendelea kuhangaika kudhibiti damu zilizokuwa zinaendelea kunitoka kwa wingi.
Nilipoingizwa kwenye chumba cha wagonjwa mahututi, harakaharaka niliunganishwa kwenye mashine ya kunisaidia kupumua huku dripu ikitiririka kwa kasi kuingia kwenye mishipa yangu.
“He has lost a great deal of blood, he need an urgent transfusion,” (Amepoteza damu nyingi sana, anahitaji kuongezewa damu haraka iwezekanavyo) alisema daktari mmoja kwa Kiingereza, kwa kuwa na mimi shule ilikuwepo kiasi chake kichwani, nilimuelewa vizuri.
Niendelee kusisitiza kwamba wakati haya yote yakitokea, katika ulimwengu wa kawaida sikuwa na fahamu hata kidogo, nilikuwa nimefumba macho na kulala pale kitandani kama maiti, nikiwa nimeunganishwa na mashine ya kunisaidia kupumua lakini katika ulimwengu mwingine ambao hata sijui niuiteje, nilikuwa nimesimama kwenye pembe moja ya ile wodi, nikishuhudia kila kilichokuwa kinaendelea.
Kazi ya kuokoa maisha yangu iliendelea, madaktari na manesi wakawa wanapishana huku na kule, huyu kabeba dawa, huyu kabeba chupa ya damu, huyu mikasi na sindano, ilimradi kila mmoja alikuwa bize.
Nilijisikia ahueni kubwa ndani ya moyo wangu kuona watu ambao pengine hata hawakuwa wakinijua, wakipigana kuokoa maisha yangu. Niliendelea kuwatazama wanavyohangaika, kuna wakati machozi ya uchungu yalikuwa yakinitoka kwa sababu ya kilichotokea, nikawa naendelea kujiuliza maswali mengi yaliyokosa majibu.
Nilivuta kumbukumbu ya jinsi mambo yote yalivyoanza kutokea.
***
Januari 16, 2012
Mikocheni, Dar es Salaam.
“Haloo!”
“Haloo, nani mwenzangu.”
“Mh! Kwani namba yangu hujaisevu Moses, mbona una visa wewe.”
“Samahani, utakuwa umekosea namba, mimi siitwi Moses wala sikufahamu.”
“Ooh! Basi samahani kaka yangu nitakuwa nimechanganya namba. Samahani sana.”
“Usijali, kuwa makini,” yalikuwa ni mazungumzo kati yangu na mtu aliyepiga simu na kunifananisha.
Nilikata simu na kubonyeza kitufe kwenye rimoti ya runinga yangu kubwa (flat screen) niliyokuwa nimekata sauti (mute) baada ya kuona simu yangu inaita. Nikawa naendelea kutazama muvi kwani miongoni mwa vitu nilivyokuwa navipenda, ilikuwa ni kutazama muvi, kuangalia mpira na kusikiliza muziki, hasa muda ninaokuwa nyumbani baada ya kutoka kazini.
Haukupita muda mrefu, simu yangu ikawa inaita tena, nilikasirika kwa sababu muvi ilikuwa imefika sehemu nzuri na sikutaka inipite hata sehemu moja, safari hii nilibonyeza kitufe cha ‘pause’ kuisimamisha ili isiendelee, nilipotazama namba ya mpigaji, ilikuwa ni ileile ya yule mtu aliyedai kukosea namba.
“Samahani mpendwa najua nakusumbua, nimeangalia vizuri simu yangu na kugundua kuwa ni kweli nilikosea namba wakati nakupigia.”
“Usijali dada, tufanye yameisha.”
“Ahsante kwa kunisamehe kaka yangu, japo sikujui lakini unaonekana mstaarabu sana. Mimi naitwa Shenaiza sijui mwenzangu unaitwa nani.”
“Naitwa Jamal au kwa kifupi Jay,” nilimjibu kwa kifupi kwa sababu niliona kama ananiletea stori zisizo na kichwa wala miguu.
“Ooh! Nimefurahi kukufahamu kaka Jamal. Unaishi wapi vile?”
“Mikocheni,” nilimjibu na safari hii niliamua kubonyeza tena rimoti, muvi ikaendelea kwani niliona hana chochote cha maana cha kuniambia, nikawa nimeiweka simu sikioni huku nikiendelea kuangalia muvi.
“Mbona kuna kelele kwani uko wapi?” alihoji msichana huyo lakini sikumjibu chochote, naona baadaye alijishtukia mwenyewe, akaamua kukata simu. Nikaiweka simu pembeni na kuendelea kutazama muvi.
Baadaye ilipoisha, nilichukua simu yangu na kugundua kuwa kulikuwa na meseji nyingi zimeingia bila mwenyewe kushtukia, nikaanza kuzisoma moja baada ya nyingine.
Nilishangaa kugundua kwamba ukiachilia mbali meseji mbili za rafiki zangu, Justice na Prosper, nyingine zote zilikuwa zimetoka kwa yule msichana aliyekosea namba ya simu, nikashusha pumzi ndefu na kuanza kuzisoma, moja baada ya nyingine nikiwa
na shauku kubwa ya kutaka kuona ameandika nini.
Je, nini kitafuatia? Meseji zinahusu nini? Usikose next issue.
 
Hii ntaisoma baadae shem ..
 
ILIPOISHIA:
NILISHANGAA kugundua kwamba ukiachilia mbali meseji mbili za rafiki zangu, Justice na Prosper, nyingine zote zilikuwa zimetoka kwa yule msichana aliyekosea namba ya simu, nikashusha pumzi ndefu na kuanza kuzisoma, moja baada ya nyingine nikiwa na shauku kubwa ya kutaka kuona ameandika nini.
SASA ENDELEA…
YA kwanza ilisomeka: “Samahani kaka Jamal naomba tuchati kama hutajali.” Nikaisoma na kuirudia zaidi ya mara mbili, sikuelewa maana ya yeye kuomba tuchati ni nini kwa sababu tayari nilishamwambia amekosea namba na mwenyewe akakiri hilo.
Hakuishia hapo, meseji nyingine ikasomeka: “Nina tatizo kubwa nilikuwa nahitaji mtu wa kumshirikisha ndiyo maana nikawa nimempigia simu ndugu yangu mmoja aitwaye Moses lakini baada ya kusikia sauti yako, naamini na wewe unaweza kuwa na busara na kunisaidia nini cha kufanya.”
“Mbona hunijibu?” ilisomeka meseji nyingine, nikawa naendelea kuzisoma moja baada ya nyingine ambapo msichana huyo alianza kulalamika kwamba nimemdharau ndiyo maana nilikuwa sitaki kujibu meseji zake, mwisho akaniambia nisimfikirie vibaya na kama ameniudhi anaomba nimsamehe.
Nilishusha pumzi ndefu baada ya kumaliza kusoma meseji zote, nikatafakari kwa kina nikiwa sijui lengo la msichana huyo ni nini hasa. Sina desturi ya kumdharau mtu hata mara moja, hasa anaponiambia ana matatizo. Huwa naamini kwamba hata kama huwezi kumsaidia mtu kwa namna nyingine, ushauri wa kimawazo unaweza kuwa msaada tosha kwake.
Ilibidi nichukue simu yangu na kupiga namba ya yule dada aliyeniambia kwamba anaitwa Shenaiza. Ilipoanza kuita tu, harakaharaka alipokea, nikamueleza kwa nini nilichelewa kujibu meseji zake.
“Nilikuwa na kazi naifanya ndiyo maana sijakujibu, nisamehe kwa hilo,” nilimwambia, harakaharaka akaniambia nisijali na anashukuru kwa kuwa nimempigia kwani tayari alishaanza kujisikia vibaya ndani ya nafsi yake. “Umeniambia una tatizo, naweza kukusikiliza tafadhali,” nilimuuliza kwa sauti ya kiungwana, nikamsikia akishusha pumzi ndefu kisha akaniuliza mahali nilipo.
“Nipo nyumbani, Mikocheni.”
“Mimi nipo Ilala, tunaweza kuonana tafadhali kama hutajali.”
“Mh!” niliguna, nilishindwa kuelewa msichana huyo anataka nini. Haikuwa kawaida yangu kuonana na watu nisiowajua, yaani dakika chache zilizopita mtu anakupigia simu na kukueleza kwamba amekosea namba, muda mfupi tena baadaye anakueleza kwamba ana shida muhimu na anataka kuonana na wewe? Nilijiuliza maswali mengi yaliyokosa majibu.
Nimewahi kusikia visa vya watu wengi hasa jijini Dar es Salaam ambao walitekwa na kwenda kufanyiwa vitu vibaya baada ya kutegeshewa wanawake. Wengi wanaamini ni wanaume wachache sana wanaoweza kuepuka kishawishi cha mwanamke anayekupigia simu na kuomba kuonana na wewe, hata kama hamfahamiani.
“Hapana, haitawezekana dada’angu, tuzungumze tu kwa simu, leo nina kazi sana,” nilimkatalia kijanja. Msichana huyo aliendelea kung’ang’ania akitaka kuonana na mimi lakini kwa sababu za kiusalama, niliendelea kushikilia msimamo wangu.
Alipoona nimekuwa mgumu, aliniomba basi nipange siku na mahali ambapo tutaonana kwa sababu anahisi kwamba huenda nina wasiwasi naye, nikamwambia asiwe na wasiwasi siku nitakayokuwa na nafasi nitamtaarifu.
“Ila naomba iwe haraka, nina tatizo kubwa mwenzio,” alisema huku sauti yake ikionyesha kwamba alikuwa na huzuni kali ndani ya moyo wake. Nilikata simu na kujilaza kitandani, nikashusha pumzi ndefu na kuendelea kujiuliza maswali mengi yaliyokosa majibu.
Kwa muda mfupi tu niliozungumza naye, tayari tulikuwa kama watu ambao tumefahamiana miaka mingi iliyopita. Sauti yake ilionyesha alikuwa na jambo zito ndani ya moyo wake lakini sikutaka kuwa mwepesi na kujiingiza kichwakichwa, nilikuwa tayari kutoa msaada wowote ambao angeuhitaji lakini pia nilihitaji kuwa na uhakika na maisha yangu.
Muda uliendelea kuyoyoma, kwa kuwa siku hiyo nilikuwa mapumziko nyumbani baada ya kazi za wiki nzima, niliutumia muda wangu mwingi kufanya usafi ndani kwangu, kufua nguo za kazini pamoja na za kushindia na baada ya kumaliza, nilirudi na kuendelea kutazama muvi. Jioni nilitoka na kwenda kwenye mgahawa uliokuwa jirani na pale nilipokuwa naishi, japokuwa nilikuwa nimekamilika kimaisha, nilikuwa mvivu sana kwenye suala zima la kupika kama walivyo vijana wengi ambao hawajaoa.
Kwa hiyo shughuli nyingine zote nilikuwa nikizifanya kwa mikono yangu isipokuwa jambo moja tu; kupika. Japokuwa nilikuwa na umri ambao ningeweza kuwa na msichana wa kunisaidia majukumu madogomadogo ya nyumbani, namaanisha mpenzi lakini nilikuwa nimeamua kuishi ‘single’ hasa kutokana na maumivu makubwa ya moyo niliyoyapata katika uhusiano wangu uliopita.
Tangu nilipoanza kuwa na akili za kikubwa, nilikuwa nimetoka na wasichana wawili tu, tena kwa nyakati tofauti lakini mambo niliyokutana nayo, yalinifanya nisitamani tena kuwa na mpenzi. Nikaamua kutuliza moyo mpaka umri wa kuoa utakapofika na huo ndiyo ulikuwa msimamo wangu.
Baada ya kupata chakula cha jioni, nilirudi nyumbani kwangu na kuendelea na mapumziko yangu. Majira ya kama saa tatu za usiku, yule msichana alinitumia tena ujumbe akinitakia usiku mwema, nami nikamjibu na tukawa tumeishia hapo kwa siku hiyo.
Kesho yake asubuhi, niliwahi kuamka na kuanza kujiandaa kuelekea kazini kama kawaida. Mahali nilipokuwa nafanya kazi, hapakuwa mbali sana na nyumbani kwangu kwa hiyo nilikuwa nikipanda daladala au wakati mwingine nikiwa na fedha za ziada, nakodi Bajaj au bodaboda.
Nilikuwa nikifanya kazi kwenye kampuni ya ukandarasi ya Collins Constructors & Civil Engineering, Mbezi Beach nikiwa kwenye kitengo cha usanifu wa ramani za majengo au kwa Kiingereza Architecture.
Sikuwa nimeanza kazi muda mrefu kwa sababu ndiyo kwanza nilikuwa nimehitimu masomo yangu ya chuo kikuu. Nikiwa kazini, niliendelea na majukumu yangu kama kawaida, ilipofika majira ya kama saa nne, muda ambao kwa kawaida huwa tunapumzika dakika chache kwa ajili ya kifungua kinywa, Shenaiza alinipigia simu kwa lengo la kunijulia hali, tukazungumza kawaida tu kisha akakata simu.
Niliendelea na kazi na kutokana na ubize wangu, sikushika tena simu mpaka saa kumi na moja jioni, muda ambao kwa kawaida huwa tunatoka kazini. Niliposhika simu yangu, nilikutana na ‘missed calls’ nyingi za Shenaiza na ujumbe mmoja ulionishtua sana moyo wangu. Aliniambia kwamba anahisi anakaribia kufa.
Ujumbe uliishia hivyo tu, nikashindwa kuelewa alikuwa anamaanisha nini? Ilibidi nimpigie, simu yake ikawa inaita tu bila kupokelewa. Nilipiga tena na tena lakini hakukuwa na majibu, nikapatwa na wasiwasi mkubwa ndani ya moyo wangu.
Sikujua msichana huyo amepatwa na nini, nikajihisi kuwa na hatia kwa sababu pengine kama ningekubali kuonana naye jana yake alipotaka nifanye hivyo, ningeweza kuelewa nini kinachomsumbua na pengine ningeweza kumsaidia.
Niliondoka kazini nikiwa ni kama nimechanganyikiwa, sikuwa namjua Shenaiza lakini sijui kwa nini nilihisi kama matatizo yake yalikuwa yakinihusu sana. Nikiwa kwenye kituo cha daladala nikiendelea kusubiri usafiri, ujumbe mfupi uliingia kwenye simu yangu, ulisomeka:
“Mwenye simu hii amelazwa Hospitali ya Amana, Ilala. Hali yake ni mbaya, hawezi kuzungumza.”
Je, nini kitafuatia? Usikose next issue
 
Weka moja moja tupate mda wa kusoma shem
 

Similar Discussions

Cookies are required to use this site. You must accept them to continue using the site. Learn more…