Kakke
JF-Expert Member
- Dec 4, 2010
- 1,883
- 1,482
Na Mwinyi Sadallah
9th December 2011
Makanisa mawili yameharibiwa kwa kuchomwa moto na kubomolewa na watu wasiojulikana visiwani Zanzibar.
Tukio hilo lilisababisha polisi kurusha risasi hewani kutawanya watu waliokuwa wanabomoa kanisa usiku wakiwa na silaha za kienyeji katika eneo la Kianga, Mkoa Kusini Unguja.
Akizungumza na NIPASHE, Mchungaji wa Kanisa la Siloam, Boniface Kalyabukama, alisema lilibomolewa wiki iliyopita na watu waliotumia nyundo za kupasulia miamba ya mawe.
Mchungaji Kalyabukama alisema kanisa hilo limeharibika kabisa na kusababisha huduma zote za kiroho kuathirika.
Mchungaji huyo aliongeza kuwa, kutokana na kuharibika kwa kanisa hilo, waumini wake wapatao 80 sasa wanaendesha ibada katika Shule ya Jumuiya ya Wazazi ya CCM.
Alisema kundi la watu wenye silaha za kienyeji na tochi zenye mwanga mkali walivamia kanisa hilo majira ya saa 2:00 usiku na kufanya uhalifu huo, baada ya mlinzi, Isaya Eliah, kukimbia kwa usalama wake.
Mchungaji Kalyabukama alisema kuwa, wakati watu hao wakiwa katika hekaheka za kubomoa kanisa, polisi waliofika katika eneo la tukio ambapo walilazimika kurusha risasi nne hewani baada ya watu hao kukaidi amri ya kuwazuia kulibomoa.
Alisema kanisa hilo lenye uwezo wa kuchukua waumini 200 kwa wakati moja, lilijengwa kwa gharama ya Sh. milioni 25, baada ya Halmashauri ya Wilaya ya Magharibi kuwaruhusu waumini hao kujenga kanisa Agosti, mwaka huu.
"Tangu kukamilika kwa ujenzi wa kanisa na kuanza kutumika kwa ibada, kumeibuka kikundi cha watu kupinga kuwepo kwake katika eneo hilo la Kianga," alisema Mchungaji Kalyabukama.
Alisema anaamni polisi watatenda haki kwa kuwachukulia hatua watu waliohusika kwa vile wamevunja haki ya kikatiba ya kila mtu kufanya ibada kulingana na imani yake.
KANISA LINGINE LACHOMWA
Wakati huo huo, Kanisa la PEFA la Mtufaani, lililoko eneo la Mwera, katika wilaya ya Magharibi Unguja, limechomwa moto na watu wasiojulikana.
Mchungaji wa Kanisa hilo, Julius Magoho, jana alisema kuwa, lilichomwa moto wiki iliyopita majira ya saa moja usiku, baada ya kumwagwa mafuta ya taa juu ya paa la makuti.
Alisema alipokea taarifa za kanisa kuchomwa moto kupitia simu ya kiganjani na baada ya kufika alikuta watu wanaendelea kuzima moto huo.
Mchungaji Magoho alisema aliripoti tukio hilo polisi na baadaye siku iliyofuata wakagundua chupa iliyokuwa na mabaki ya mafuta ya taa karibu na eneo la kanisa.
Askofu wa kanisa hilo, Daniel Kwilemba, aliomba Polisi kuchukua hatua za kisheria kwa vile tukio hilo linakwenda kinyume cha katiba na misingi ya haki za binadamu.
Alisema kwamba vitendo vya hujuma dhidi ya makanisa vinazuia uhuru wa kuabudu na kuchochea chuki katika jamii na akaomba Serikali ya Mapinduzi Zanzibar (SMZ) kuvunja kimya na kukemea mwenendo huo.
Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Kusini, Agustine Ulomy, alithibitisha kutokea kwa matukio hayo na kufafanua kuwa mtu mmoja tayari ametiwa nguvuni kuhusiana na tukio la kubomolewa kanisa la Siloam.
Alimtaja mtuhumiwa huyo kuwa ni Mbaraka Khamis (60), mkazi wa Kianga na kwamba atafikishwa mahakamani baada ya uchunguzi kukamilika.
Kamanda Ulomy alisema uchunguzi wa awali unaonyesha kuwepo utata katika mradi wa ujenzi wa kanisa la Siloam, baada ya maelezo kuonyesha kwamba halmashauri iliruhusu walioomba eneo hilo kujenga ukumbi wa mikutano na sio kanisa.
Alisema utata huo unatokana na kijana aliyeuza eneo hilo na baba yake ambaye ndiye anayepinga kuwepo kwa kanisa katika eneo hilo.
Kuhusu kanisa la PEFA, Kamanda Ulomy, alisema moto ulioharibu kanisa hilo uliwahi kudhibitiwa na hivyo kuzuia madhara.
CHANZO: NIPASHE