Wanamtandao
Ninawashukuru wote ambao kwa mda mmeelekeza masuala na matukio mbalimbali kwangu. Niombe radhi kuchelewa kujibu kwa sababu ya shughuli zilizokuwa zinatukabili. Sasa nimepata nafasi kidogo, nitajibu baadhi ya mambo ambayo naona ni ya haraka zaidi, na yanafaa kujadiliwa hadharani. Private messages nyingine nitazijibu moja kwa moja (bilaterally).
- Private messages ya TAYADI, tarehe 11 Juni
Kazi unaweza saaana!,, lakini Kwa hili la GHOROFA, Mafisadi wameiweka serikali pamoja na mama Tibaijuka MFUKONI. Hakuna anayefurukuta. Jengo litaendelea kuwepo tu!
Jibu. Asante kuona naweza ila nikuhakikishie sijawekwa mfukoni na mtu. Ila mwenye jengo kaenda mahakamani na kapewa injunction. Kesi ipo Mahakama Kuu, Kitengo cha Ardhi, Miscellaneous Land Application No. 42 of 2013. Tarehe 31 Mei, 2013, Mhe Jaji J.S. Mgeta alitoa amri ya kulinda status quo baada ya Bw. Mashauri, Mwanasheria wa Halmashauri ya Ilala (ambayo imeshitakiwa), kutopinga ombi la Bi. Rachel, Mwanasheria wa Mwekezaji (Ali Raza Investments Ltd), kwamba wakati kesi kuu ikisikilizwa jengo lilindwe. Mchakato wa kisheria unaendelea tukipata maamuzi tutawajulisha. Mbali ya taarifa hiyo, kwa mujibu wa sheria, siwezi kujadili zaidi jambo lililo Mahakamani. Tusubiri.
- Private Message ya Amani Ndoyella, ya 11 Juni, 2013
Ujumbe wako kuhusu Mradi wa Mji Mpya wa Kigamboni ni mrefu ila kwa ufupi, unalalamika kuwa wananchi hawashirikishwi katika maamuzi, watendaji wamenipotosha, fidia ya Shs milioni 141 kwa ekari ni ndogo wakati unadai mwekezaji atalipa Shs milioni 300 kwa eka, unataka wananchi mmojammoja waingie ubia, unalalamika sijwawahi kufika Kigamboni kukutana na wananchi kwa hiyo niliyoyasema Bungeni siyo sahihi. Unakiri nilikutana na Kamati yenu lakini pia unadai hamsikilizwi, Mwisho unailalamika kamati yenyewe, nkd.
Jibu: Kupanga miji ni kazi ngumu, inahitaji uzalendo. Ni changamoto na kero kwa wahusika wote. Ushirikishwaji umekuwepo tangu mradi ulipoanza mwaka 2008 ila tukubali umechelewa na hii ni changamoto. Mimi binafsi nimefanya mikutano mikubwa ya hadhara Kigamboni miwili, mbali na kukutana na Kamati ya Madiwani, Wabunge, na hata Kamati huru kama ile ya kwenu. Wananchi wamechagua wawawikilishi wao katika KDA, wakala wa Serikali kuu itakayoendesha mradi. Ofisi za KDA ziko huko huko Kigamboni. Mkurugenzi wake Bw. Vincent Shauri anapatikana hukohuko kujibu hoja zenu. Tunatambua usumbufu lakini na sisi tunajitahidi kutekeleza kazi hii kwa manufaa ya umma hasa vizazi vijavyo. Miji yetu ikiharibika hata na uchumi na maisha haviwezi kuwa bora.
Niliporejea kutoka Singapore, kwenye ziara ya Mhe. Rais, nilileta kwenye mtandao huu Master Plan ya mji mpya wa Singapore. Wengine hawakuelelwa mantiki ya post hiyo, hata wakadiriki kukebei kwa nini ninawasumbua?. Nilitaka kuonyesha kwamba adha za upangaji miji siyo Dar es Salaam tu, hata haya majiji yalioyoendelea sana kama Singapore yanapangwa upya kadri ya maendeleo yanavyosonga mbele (urban renewal programs). Utamaduni wa kulalamika hausaidii sana lakini utamaduni wa kujadili ni mzuri na ndiyo umuhimu wa jukwaa hili la JF. Kwa hiyo kuhusu Kigamboni nifafanue tu kwamba fidia tuliyotaja ni endelevu na mchakato wa kutoa malipo kwa wananchi wa Kibada unaendelea. Madai ya Shs milioni 300 kwa ekari ni uongo, na mwenye ushahidi mwambie akuonyeshe. Niliyoyasema Bungeni ni sahihi, ninakushukuru kwa kufuatilia.
Mwisho amani ndiyo msingi wa maendeleo kwa hiyo tuilinde. Tujiepushe na kauli za kutishia uvunjifu wa amani, hazina tija. Hoja tu ndiyo jambo la msingi.