Majambazi yateka mitaa D`Salaam, yapora, yaua

Herbalist Dr MziziMkavu

JF-Expert Member
Feb 3, 2009
42,268
33,040
headline_bullet.jpg
Yalifunga mitaa usiku saa mbili
headline_bullet.jpg
Yakapora duka moja moja
headline_bullet.jpg
Yakaua raia wawili kwa risasi




Vilio, simanzi na majonzi, vilitawala jana katika eneo la Vingunguti Faru, jijini Dar es Salaam, wakati wa shughuli za mazishi ya miili ya mfanyabiashara, Fadhili Adam na mganga wa tiba za jadi aliyefahamika kwa jina moja la Musa, waliouawa kwa kupigwa risasi na majambazi.
Vijana hao waliuawa katika eneo hilo usiku wa kuamkia jana na kusababisha wingu zito la huzuni kutanda katika eneo hilo wakati wote wa msiba.
Pia, shughuli zote za biashara katika eneo hilo, jana zilisimama kwa ajili ya kuomboleza msiba wa vijana hao, huku maelfu ya watu wakifurika nyumbani kwa marehemu Fadhili katika Msikiti wa Kisengo, Vingunguti ambako shughuli za kuandaa miili ya vijana hao kwa ajili ya mazishi zilifanyika.
Katika tukio hilo la juzi usiku lililozua hofu na tafrani kubwa miongoni mwa majirani na wapita njia, majambazi hao waliobeba silaha za moto wanaokadiriwa kufikia saba, pia walipora fedha taslimu na bidhaa katika maduka kadhaa ya eneo hilo kwa nyakati tofauti.
Fadhili, ambaye alikuwa ni mfanyabiashara wa duka na mkazi wa eneo hilo, alizikwa katika makaburi ya Kwa Mnyamani.
Musa, ambaye mauti yalimkuta akiwa katika eneo la shughuli zake, alikuwa akiishi Moshi Bar, Ukonga, jijini Dar es Salaam, alizikwa katika makaburi ya nyumbani kwake. Wote walizikwa jana jioni.
Akizungumza na Nipashe katika eneo la msiba, mmoja wa majirani wa Fadhili, Mohamed Khatib, alisema majambazi hayo yalivamia maduka hayo majira ya saa 1.30 usiku, wakati umeme ukiwa umekatika katika eneo lote la Vingunguti.
Alisema umeme ulikatika kwa saa zisizopungua nne; kuanzia saa 11.00 jioni hadi 2.00 usiku na majambazi hayo yakavamia maduka wakati eneo lote la Vingunguti likiwa katika giza zito.
Mohamed (26), alisema kabla ya majambazi hayo kuvamia duka hilo na kuwaua vijana hao, walitokea eneo la bondeni, ambako walipora katika duka la mfanyabiashara aliyemtaja kwa jina la Mangi.
“Walipofika dukani kwa Fadhili, walimkuta mdogo wake, Ahmad. Wakamuuliza yuko wapi muuza duka? Muda huo Fadhili alikuwa nje anabeba mzani mkubwa akisaidiana na Musa kuuingiza dukani,” alisema Mohamed na kuongeza:
“Ahmad alipoulizwa vile, hakujibu, badala yake alitoka nje na kumwambia Fadhili, kaka, hawa ni wezi na kisha akakimbia. Majambazi hao walikuwa kama saba hivi. Baada ya kuambiwa vile na Ahmad, Fadhili na Musa walijaribu kukimbia, ndipo majambazi hayo yakawapiga risasi na kufia hapo hapo.”
Mohamed alisema wakati hayo yakijiri, yeye alikuwa anatoka kwenye shughuli zake na kwamba, aliyaona majambazi hayo, lakini alijua ni watu wa kawaida.
Hata hivyo, alisema baadaye alisikia milio ya risasi ikirindima katika eneo hilo na baada ya majambazi hayo kutoweka, alikwenda katika eneo hilo na kushuhudia miili ya vijana hao ikiwa imelala.
Naye Ahmad Juma, alisema ilikuwa saa 1:45 usiku juzi alipokuwa amekaa nje ya duka hilo.
“Wakatokea watu wanne, ambao siwajui. Wa mbele alikuwa amebeba bunduki na mfuko wa karatasi. Wakauliza mhusika yuko wapi? Nikainuka, nikaingia ndani, nikatokea mlango wa uwani,” alisema Ahmad (15) na kuongeza:
“Baba (Juma Swaleh) akatoka ndani akaniuliza kuna nini? Wakati huo Musa alikuwa anaingiza mzani dukani. Nikamwambia kuna majambazi. Baada ya kumjibu hivyo, nikakimbilia kujificha nyumba ya pili. Baadaye, Baba akaamriwa na majambazi hayo kulala chini, wakampiga na kumjeruhi mguuni. Baadaye nikasikia mlio wa risasi, nilipotoka nje nikakuta kaka na Musa wamekufa.”
Naye Bartalome Shayo, ambaye ni mfanyabiashara wa duka katika eneo hilo, alisema alivamiwa na majambazi hayo saa 1.30 usiku wakati akiwa amekaa na rafiki zake dukani.
“Walikuja watu saba, watatu wakiwa wamebeba bunduki. Wanne wakaingia dukani wakatuamuru tukae na tusalimishe simu zetu zote. Walipotuamuru hivyo, nikakimbilia dukani, nikakuta wameingia watu wale,” alisema Shayo.
Alisema katika tukio hilo, majambazi hayo yalipora vocha za simu zenye thamani ya Sh. 200,000 na Sh. 400,000 za mauzo ya soda.
Shayo alisema pia, wateja wote waliokuwa dukani kwake wakati huo, waliporwa simu tatu na fedha taslimu, ambazo thamani yake haijajulikana.
Alisema polisi wa doria hawakufika hadi alipokwenda katika kituo kikuu cha polisi kutoa taarifa za tukio hilo.
Jeshi la polisi Mkoa wa Ilala, limethibitisha kutokea kwa tukio la mauaji ya watu hao.
Kamanda wa Polisi wa mkoa huo, Fasutine Shilogile, alisema jana jioni kuwa watu hao waliuawa usiku wa kuamkia jana katika eneo hilo na kundi la watu wapatao sita wanaodhaniwa kuwa ni majambazi ambao walivamia kwenye duka.
Kamanda Shilogile alisema kuwa tukio hilo likitendeka, umeme ulikuwa umekatika katika eneo hilo.
Alisema watu hao walivamia eneo hilo kwa lengo la kupora mali zilizopo kwenye duka hilo na kwamba baada ya kufika walifyatua risasi kadhaa ambazo ziliwajeruhi watu wawili na kusababisha vifo vyao.
Alisema watu hao walifariki dunia wakati wakikimbizwa katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili (MNH) na kwamba miili yao imehifadhiwa hapo.
Kamanda Shilogile alisema mpaka jana polisi hawakufanikiwa kumkamata mtu yeyote.
Alisema kwa mujibu wa mmiliki wa duka ambalo lilivamiwa, majambazi hao walipora fedha za mauzo Sh. 500,000.



CHANZO: NIPASHE
 
pumbaf polisi wanaishia kutoa taarifa tu kila siku,tumechoka kuwasikiliza taarifa,taarifa,taarifa,mbona hawakamati majambazi jamani tanzania yaani inachokesha nasikia kufakufa ,sijui nihamie wapi mie nibadili kabisa na uraia mungu nisaidie.:angry:
 
Hivi polisi kama hawatoshi kuweza kufanya doria katika vitongoji (na hiyo ni Dar!), kwa nini wasifanye harambee ya kuvutia vijana (tena wasomi) kujiunga na jeshi hilo (yaani recruitment drive)? Pia, kama tatizo ni usafiri, badala ya kuchangisha hela za khanga, t-shirt na mbege kwa nini watu wasiombwe kuchangia manunuzi ya magari ya polisi (hata ya mtumba)?

Milioni 200 zilizopatikana kwa ajili ya CCM Kilimanjaro zinaweza kununua magari kama 20 ya matumizi ya doria.
 
0 Reactions
Reply
Back
Top Bottom