Unajua Chadema sehemu kubwa ya umaarufu wake inatokana na kuonekana waziwazi kinawatetea wanyonge na kupambana na mafisadi, na hata CCM ilipata wafuasi kwa kupambana na mafisadi, na hata Igunga CCM ilishinda kwa kuwa imemuondoa fisadi na hiyo ndiyo hoja kuu kwa wananchi sasa bila kujali vyama vyao, kwa hiyo Chadema haiwezi kujiua kisiasa kubeba mafisadi," anasema kiongozi mmoja wa Chadema mkoani Arusha.
Tayari Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe, amekanusha waziwazi kutobeba watuhumiwa wa ufisadi na kwamba chama chake kimekuwa makini kisiasa wakati wote wa harakati zake nchi nzima.
Miezi michache iliyopita Katibu wa Itikadi na Uenezi wa NEC ya chama hicho, Nape Nnauye, akiwa Zanzibar, alibainisha kwamba mafisadi wana mikakati ya kuhusisha baadhi ya vyama vya siasa, magazeti na asasi za dini kujibu mapigo dhidi ya CCM, mambo ambayo yameshaanza kutokea ikiwamo kutukwana kwa viongozi wa CCM akiwamo Nape mwenyewe.
Huo ni umbea wenye lengo na dhamira chafu ya kuvuruga Chadema. Ni wajibu wetu kuibua mafisadi kwa kadiri tunavyopata ushahidi. Tulianza 2007 na tutaendelea kwa awamu," alisema na kuendelea:
Tuhuma dhidi ya Chadema kutumika ziliibuka siku chache baada ya maamuzi ya Halmashauri Kuu ya Taifa ya CCM (NEC) kutangaza kuwa imewataka wanachama wake watatu kujiondoa katika nyadhifa zao, ambako chama hicho kikuu cha upinzani kilifanya mkutano wake mkoani Tabora na kuonekana wazi kubadili mwelekeo.
Katika mkutano huo Chadema ilitoa orodha mpya ya mafisadi ikiwa na majina mapya.
Ilielezwa kwamba mkakati huo mpya ulilenga kuingiza majina mengi zaidi katika orodha ya mafisadi ili CCM ione uzito katika kutekeleza dhana ya kujivua gamba.
Akiongea na KuliKoni kwa njia ya simu, kiongozi mwingine wa Chadema alisema kwamba kinachoendelea CCM ni matatizo yao wenyewe na kwamba kwa vile chama hicho kililea ufisadi kwa muda mrefu makundi kilichoyazalisha yataendelea kutafunana kila kukicha.
Katika kudhihirisha mkakati huo mpya, kundi linaloaminika kumuunga mkono Mbunge wa Monduli, Edward Lowassa, lilionesha wazi wazi kuasi na kushambulia viongozi wenzao wa CCM na kusifia Chadema huku wakionesha kutetea watuhumiwa wa sakata la Richmond.
Aliyewashangaza wengi alikuwa Kaimu Mwenyekiti wa UVCCM, Benno Malisa, ambaye ni Mjumbe wa Kamati Kuu ya CCM kutamka hadharani kwamba serikali isiingilie vyama vya upinzani ikiwamo Chadema na kwamba wananchi waungane kutaka wanasiasa waliopinga Dowans wachukuliwe hatua kwa kupotosha umma.
Bila kujua hoja ya Chadema ni kutaka watuhumiwa waliohusika na mkataba wa Richmond akiwamo Lowassa wafilisiwe ili kulipa deni la Dowans, Malisa alitaka wapinzani kuungana na CCM kutaka walioipinga Dowans kuchukuliwa hatua.
Walioshiriki katika mkutano wa Malisa, ulioambatana na ufunguaji wa matawi bila kushirikisha uongozi wa CCM mkoa na wilaya ya Arusha, ni pamoja na Mbunge Catherine Magige, ambaye alielezwa kutamba kuwa haogopi polisi ambao walikataa kutoa kibali cha maandamano kwa maelezo kwamba ‘anawamudu.'
Wengine walioshiriki ni pamoja na Mwenyekiti wa UVCCM mkoa wa Arusha, James Millya, ambaye alimtukana waziwazi Nape kwa kumuita kichaa na kumshauri mwenyekiti wa Taifa wa CCM, Rais Jakaya Kikwete, aangalie upya uteuzi wake.
"Haya ni matusi kwa Rais Kikwete, haiwezekani kwa kiongozi wa nchi kuteua kichaa na inaweza kutafsirika kuwa Millya ana mashaka na uwezo wa Mwenyekiti wake wa chama. Na hii ni hatari sana kwa uhai wa chama chenyewe. Anadiriki hata kukashifu familia ya Rais! Huyu anastahili kufukuzwa uanachama, sijui anapata wapi hii jeuri," anasema kiongozi mmoja wa UVCCM.
Katika hotuba yake iliyowashangaza wengi Malisa aliitaka serikali na CCM kutoingilia mambo ya Chadema na kuwaacha wawafukuze madiwani wao walioonekana kushirikiana na CCM.
"Nimesikia kuna madiwani wamefukuzwa Chadema na kuna viongozi ambao si wana Chadema wanawakingia vifua, niwaombe tusiingilie mambo ya vyama vyao na tusitumie nafasi tulizopewa na dhamana hizi kuingilia yasiyotuhusu niwatake vijana wa CCM kisheria kata hizo zitaenda katika uchaguzi jiandaeni kugombea," alisema Malisa na kuongeza;
"Sisi kama Chama kinachoongoza, tujitahidi kuheshimu demokrasia na maamuzi ya vyama vingine, tusipende kutumia vyombo vya serikali kuwakomoa kwani siku ya mwisho wanaoumia ni wananchi na si vyama vya siasa.
"Nitumie nafasi hii kumuomba Mbunge wa Arusha Mjini kaka yangu Lema (Godbless) kuwa mstari wa mbele katika kuleta umoja na mshikamano hapa mjini (Arusha) na kumaliza tofauti za u-CCM na u-Chadema ili wakazi wa Arusha wapate maendeleo."
Kuhusu Dowans, Malisa alisema; "CCM tunalalamika wakati sisi wenyewe tunaibomoa nchi na chama chetu. Tazama sakata la Dowans, waliosema wao watatusaidia kupinga kulipa Dowans na ambao walitushauri na kutumia nafasi zao tusinunue mitambo ya Dowans nao sasa wanalalamika na kuanza kutafuta wachawi, wawajibike walitudanganya kama taifa leo tumeshindwa kesi mitambo ileile waliyosema haifai leo inatumika na kampuni ya Symbion, wanatufanya Watanzania mazuzu."
Malisa alitaka vijana wa CCM kuungana na wa vyama vya upinzani kuwawajibisha waliopinga Dowans kununuliwa.
Hotuba ya Malisa ambaye sasa anaonekana wazi kuwa upande wa mafisadi, ilijaa kejeli na dharau kwa serikali na uongozi wa CCM Taifa, hali iliyotafsiriwa kuwa ni uasi wa waziwazi.
Dhana ya uvuaji gamba iliwagusa Lowassa ambaye anahusishwa na mradi wa Richmond, Mbunge wa Bariadi Magharibi Andrew Chenge, na Rostam ambaye tayari amekwishajivua gamba kwa kuachia nafasi zake za CCM. Chenge amekuwa akihusishwa na sakata la ununuzi wa rada kwa bei isiyo halali na kwamba wakati akiwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali nchi hii iliingia mikataba mingi mibovu inayolitafuna taifa hivi sasa.