Mada maalum ya ndege toka FB

Mada maalum ya ndege toka FB

DAR ES SALAAM - Mwanamuziki nyota wa Bongo Flava, Diamond Platnumz, amesema alidhurumiwa kiasi cha Shilingi Bilioni 4 alicholipia kwa ajili ya kununua ndege yake binafsi aina ya Bombardier Challenger 603.

Akizungumza katika mahojiano na Wasafi Media yaliyorushwa kupitia YouTube na majukwaa mengine ya Wasafi, Diamond alieleza kuwa ndoto yake ya kumiliki ndege binafsi pamoja na helikopta ilipata pigo baada ya wakala aliyemtegemea kutoweka na fedha hizo.

Kulingana na Diamond, ndege hiyo binafsi "Private Jet" na Helikopta hiyo hazikuwa za matumizi yake binafsi tu, bali zlikuwa ni sehemu ya uwekezaji ambao ungetumika kukodiwa na kumwingizia mapato.

Hata hivyo, baada ya kukamilisha malipo ya awali, aligundua kuwa wakala husika hakuwa mwaminifu. Alitoweka na fedha bila kuwasilisha chombo hicho cha usafiri kama walivyokubaliana.

Kutokana na changamoto hiyo, msanii huyo amesema bado anategemea kukodi ndege kutoka Kenya kila anapofanya ziara kubwa za kimataifa barani Afrika. Hii inagharimu mamilioni ya fedha kwa kila safari.

Alitoa mfano kuwa safari moja ya kukodi Private Jet kutoka Tanzania kwenda Nigeria inagharimu takriban dola laki 150, ambayo ni karibu na shilingi milioni 400.

Diamond alisema kama angekuwa na ndege yake binafsi, basi hata waandaaji wa matamasha wangelazimika kuikodi kutoka kwake. Pia alisisitiza kuwa hawezi kwenda kufanya show yoyote barani Afrika bila kutumia private jet.

Akifafanua kuhusu ukimya wake tangu tukio litokee, Diamond alisema alifuata ushauri wa kisheria. Alibainisha kuwa mamlaka husika zinaendelea na uchunguzi wa kina ili kuona uwezekano wa kurejesha fedha zake na kupata haki yake, badala ya kujadili suala hilo hadharani.
1786965030775.jpg
 
Rubani mmoja nchini Canada amepongezwa kwa ustadi mkubwa baada ya kufanikiwa kutua Helikopta kwa dharura kwa kutumia mbinu ya kuteleza angani bila nguvu ya injini, maarufu kama 'autorotation' kufuatia hitilafu ya kimitambo iliyotokea kwenye helikopta hiyo ya uzimaji moto ya aina ya Huey mnamo tarehe 14 Agosti 2026.

Wakati wa tukio hilo, hali ilikuwa ngumu zaidi baada ya ndoo ya kubebea maji kukwama kwenye ndoano na kumfanya rubani ashindwe kuiachia huru kama ilivyo kawaida wakati wa dharura.

Pamoja na changamoto hiyo kubwa ya ziada, marubani wa ndege hiyo walionyesha umahiri wa hali ya juu na kufanya utulivu ulioruhusu helikopta hiyo kutua salama na kwa ulaini mkubwa, jambo linalothibitisha viwango vya juu vya mafunzo na uwezo wa marubani hao katika kukabili majanga.
 
Uwanja wa ndege maarufu wa kimataifa wa Heathrow uliopo London, Uingereza, unamilikiwa na kuendeshwa na kampuni iitwayo Heathrow Airport Holdings Limited ambapo kampuni hiyo awali ilikuwa inajulikana kama British Airports Authority - BAA.

Kampuni ya Heathrow Airport Holdings yenyewe pia inamilikiwa na kampuni ya uwekezaji iitwayo FGP Topco Limited.

FGP Topco ni muungano wa makampuni makubwa ya uwekezaji kutoka nchi mbalimbali na ugawaji wa umiliki wake kwa sasa ni kama ifuatavyo;

~Ardian kutoka Ufaransa inamiliki asilimia 32.61
~Mfuko wa Uwekezaji wa Qatar unamiliki asilimia 20
~Mfuko wa Uwekezaji wa Umma wa Saudi Arabia unamiliki asilimia 15.01
~GIC ya Singapore inamiliki asilimia 11.20 ~Australian Retirement Trust inamiliki asilimia 11.18 na
~China Investment Corporation inamiliki asilimia 10

Awali uwanja wa ndege wa Heathrow ulikuwa chini ya serikali ya Uingereza kupitia British Airports Authority. Mwaka 1986 serikali ya Waziri Mkuu Margaret Thatcher ilibadilisha BAA kuwa kampuni binafsi na mwaka 1987 iliuza hisa zake katika soko la hisa.

Leo hii Heathrow, moja ya viwanja vikubwa zaidi vya ndege barani Ulaya unaongozwa kwa kusimamiwa kifedha na Mamlaka ya Anga ya Kiraia pamoja na kamouni za Masoko na Ushindani.
1787050498570.jpg
 
SYDNEY — Ndege ya Qantas ya aina ya Airbus A380 ilimaliza safari mbili za kuvuka Pasifiki bila kujulikana kuwa kulikuwa na taa ndogo ya matengenezo iliyoachwa ndani ya bawa lake la kushoto.

Kwa mujibu wa ripoti ya mamlaka ya usalama wa usafiri "Australian Transport Safety Bureau -ATSB" iliyotolewa hivi karibuni, tukio hilo lilitokea baada ya ukarabati wa mfumo wa kiyoyozi kwenye uwanja wa Sydney tarehe 7 Januari 2026.

Wahandisi walitumia taa ya kazi ya Makita yenye urefu wa takriban sentimita 33 ili kusaidia kuona kwenye sehemu nyembamba na zenye yenye joto ndani ya bawa.
Baada ya kumaliza kazi, walizima taa hiyo na kufunga mlango wa ukarabati bila kutoa taa.

Ndege hiyo ya ghorofa mbili, yenye namba ya usajili VH-OQK, ilifanya safari mbili ndefu za kimataifa za kubeba abiria kutoka Sydney kwenda Dallas-Fort Worth na kurudi , takribani kilomita 27,000.

Ripoti hiyo inaangazia udhaifu katika mifumo ya kufuatilia zana zinazotumika wakati wa matengenezo ya ndege.
1787066506690.jpg
 
DODOMA — Mamlaka ya Viwanja vya Ndege nchini imetoa rai kwa abiria wanaomiliki silaha kihalali na wanaokusudia kusafiri nazo kuzifuata taratibu za kuzikabidhi katika vituo vya Polisi vilivyopo viwanja vya ndege.

Akizungumza jana Agosti 19, 2026 jijini Dodoma wakati wa maadhimisho ya Siku ya Utamaduni wa Usalama wa Anga, Mkurugenzi wa Viwanja vya Ndege vya Dodoma na Msalato, Clemence Mbaruku Jingu, amesema utaratibu huo unalenga kulinda usalama wa abiria na shughuli za anga kwa ujumla.

“Silaha hizo baada ya kukabidhiwa zinahifadhiwa kwenye masanduku maalumu na kisha zinarejeshwa kwa abiria husika na maafisa wa Polisi anapofika mwisho wa safari yake,” amesema Mbaruku.

Pia ameeleza kuwa Serikali inaendelea kuimarisha ulinzi katika viwanja vya ndege nchini ikiwemo Msalato, kwa kuweka uzio wa ndani na nje, kamera za usalama na mashine za ukaguzi wa abiria na mizigo.

Naye Meneja Usalama wa Kiwanja cha Ndege Dodoma, Lydia Mwenisongole, amesema maadhimisho hayo yana jukumu la kutoa elimu kwa jamii kuhusu umuhimu wa usalama wa anga, na kwamba kuhakikisha usalama wa viwanja ni jukumu la kila mtu.
1787224196669.jpg
 
Watu saba wamefariki dunia nchini Kenya mnamo tarehe 19 Agosti 2026 kufuatia ajali ya helikopta ya kitalii iliyotokea karibu na Mlima Ololokwe katika Kaunti ya Samburu.

Ajali hiyo ilitokea majira ya saa 3:13 asubuhi wakati helikopta hiyo aina ya Eurocopter EC130 B4 ilipokuwa ikisafiri kutoka Hifadhi ya Wanyama ya Loisaba kuelekea eneo la Ewaso Nyiro.

Ndege hiyo inayomilikiwa na kampuni ya Lady Lori Helicopters ilikuwa ikisafirisha watalii chini ya usimamizi wa kampuni ya safari ya &Beyond.

Wote waliokuwa ndani ya ndege hiyo, wakiwemo abiria sita na rubani mmoja raia ya Kenya, walipoteza maisha.

Miongoni mwa waliofariki ni raia watano wa Marekani, akiwemo José Suárez ambaye ni mtendaji mkuu wa kituo cha televisheni cha Telemundo, pamoja na Mkuu wa Idara ya Ujasusi ya Ecuador, Michele Sensi-Contugi, aliyeambatana na mke wake.

Zoezi la uokoaji linaloongozwa na Shirika la Msalaba Mwekundu la Kenya liligeuka kuwa gumu kutokana na eneo hilo kuwa la milima isiyofikika kwa urahisi pamoja na moto mkubwa uliokuwa ukiwaka kwenye mabaki ya ndege.

Idara ya Uchunguzi wa Ajali za Anga nchini Kenya tayari imeanzisha uchunguzi rasmi ili kubaini chanzo kamili cha ajali hiyo.
1787225094172.jpg
 
Mnamo Mwezi Julai 2026, Kapteni Derrick Lockhart kutoka kampuni ya Airboat Rides ya Midway alifanya operesheni ya kipekee ya uokoaji baada ya kutumia Airboat kuwatoa kwenye kisiwa wafanyakazi wa Helikopta na kupakia kwenye Boat ndege hiyo iliyokwama katika Ziwa Jesup linalojulikana kwa kuwa na Mamba wengi.

Helikopta hiyo ilikuwa ikifanya kazi ya serikali ya kukagua viota vya mamba na kukusanya mayai ambapo ilipata hitilafu ya kiufundi.

Marubani walilazimika kutua kwa dharura kwenye kisiwa hicho kidogo ndani ya Ziwa Jesup, eneo linalokadiriwa kuwa na Mamba takriban 13,000.

Kulingana na taarifa, timu ya watu 14 ilishirikiana kupakia Helikopta hiyo yenye uzito takriban paundi 1,500 juu ya airboat.

Uamuzi huo wa haraka ulifanyika ili kukwepa dhoruba iliyokuwa inakaribia na kuhakikisha wote warudi salama nchi kavu.

Lockhart na timu yake walifanikiwa kukamilisha zoezi hilo bila madhara yoyote, na helikopta pamoja na wafanyakazi wake walirejeshwa salama kutoka eneo lile hatari lililojaa Mamba.
1787236941888.jpg
 
Shirika la ndege la Precision Air limekuwa la kwanza nchini Tanzania kupata idhini ya kutumia mfumo wa kielektroniki wa taarifa za safari za ndege "Electronic Flight Bag" (EFB).

Idhini hiyo imetolewa na Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania (TCAA) baada ya shirika hilo kukamilisha tathmini ya hatua tano na kuthibitisha kufuata matakwa yote ya kisheria na kiutendaji.

Mfumo huo unachanganya kazi za kabla, za wakati huo na baada ya safari katika jukwaa moja la kidijitali.
Pia unaruhusu marubani kupata ramani za urambazaji (navigation) mipango ya safari, hali ya hewa na taarifa nyingine muhimu bila kutumia karatasi.

Akizungumza baada ya kupokea idhini, Mkurugenzi Mtendaji wa Precision Air, Bw. Patrick Mwanri, amesema ni hatua kubwa katika mageuzi ya kidijitali na utunzaji wa mazingira.

“Ni uthibitisho wa dhamira yetu ya kutumia teknolojia kuboresha usalama, ufanisi na kupunguza athari za shughuli zetu kwa mazingira. Tunajivunia kuwa wa kwanza nchini kutumia mfumo huu,” amesema Bw. Mwanri.

Ameishukuru TCAA pamoja na timu za uendeshaji, usalama na ufundi za Precision Air kwa ushirikiano.

Precision Air inasema matumizi ya EFB yataongeza ufanisi, kuboresha upatikanaji wa taarifa kwa wakati halisi na kupunguza mzigo wa kazi za kiutawala.

Shirika hilo pia linashiriki katika mpango wa kimataifa wa kupima na kupunguza uzalishaji wa hewa ukaa "Carbon Emmissions) katika sekta ya anga.
1787245387855.jpg
 
Back
Top Bottom