Uwanja wa ndege uliojengwa kwenye kisiwa bandia waendelea kuzama baharini.
Uwanja mkubwa wa ndege wa Kimataifa wa Kansai, uliopo katika eneo la bahari ya Osaka Bay nchini Japan, umeingia katika hatari ya kutoweka baada ya kugundulika kuwa unaendelea kuzama kwa kasi isiyotarajiwa baharini.
Uwanja huo wa ndege, ambao ulijengwa kwa gharama ya pauni bilioni 14 sawa na dola bilioni 19 za Kimarekani, unahudumia zaidi ya abiria milioni 30 kwa mwaka na ni kitovu muhimu cha safari za anga kuelekea miji ya Osaka, Kyoto na Kobe.
Uwanja huo umejengwa kwenye visiwa viwili vya bandia na ulikuwa ukisifiwa kwa ubunifu wake wa kipekee unaoleta uimara dhidi ya matetemeko ya ardhi, ikiwa ni pamoja na barabara za kurukia ndege zinazoweza kupinda wakati wa tetemeko la ardhi ili kuzuia nyufa.
Tangu kufunguliwa kwake miaka 30 iliyopita, uwanja wa ndege wa Kansai umeshinda tuzo mbalimbali, ikiwemo ya Skytrax Kama uwanja bora wa ndege katika uhifadhi wa mizigo ya abiria, kutokana na rekodi ya kutopoteza hata begi moja katika kipindi cha miaka 30.
Hata hivyo, uwanja huo sasa unakumbwa na changamoto kubwa ya uharibifu wa miundombinu yake kutokana na kuzama. Kwa mujibu wa tovuti ya Essential-Japan, uwanja huo tayari umeshazama kwa zaidi ya mita 11.5 (futi 38) tangu kufunguliwa kwake mwaka 1994 – kiwango kilichozidi makadirio ya awali ambapo kilitarajiwa kuzama kwa mita 8 (futi 26) ndani ya kipindi cha miaka 50.
Wataalamu wanaeleza kuwa uzito mkubwa wa uwanja huo unaweka shinikizo kubwa kwenye tabaka la udongo wa mfinyanzi na tope linalounga mkono visiwa hivyo bandia, jambo linalosababisha uwanja huo kuendelea kuzama.
Mwaka 2018, Kansai Airport ililazimika kufungwa kwa muda baada ya Kimbunga Jebi kukata mawasiliano kati ya uwanja huo na eneo la nchi kavu, huku maji ya mafuriko yakifunika barabara za kurukia ndege na daraja linalounganisha uwanja huo na Osaka kuharibika vibaya.
Hadi sasa, Kansai Airports Group imeshachukua hatua za kuongeza kimo cha ukuta wa baharini ili kuzuia athari za mafuriko ya baadaye.
Licha ya changamoto ya kuzama, uwanja huo hivi karibuni umekamilisha ukarabati mkubwa wa Terminal 1 kwa ajili ya maandalizi ya ongezeko la wasafiri kuelekea maonesho makubwa ya Expo 2025 yanayotarajiwa kuanza Aprili 13 huko Osaka.
Katika taarifa yake, Kansai Airports Group imesema itaendelea kukabiliana na changamoto hiyo huku ikilenga “kukidhi mahitaji yanayoongezeka ya safari za anga na kuboresha usafiri kwa abiria.”
#airport #osakabay #kansaiinternationalairport #aviationlovers #aviationcareer #aviationtanzania✈ #aviationtanzaniaupdates #aviata #aviataupdates