[h=1]Macho ya Bundi- 20-[/h]ILIPOISHIA
Nilimuangalia mume wangu huku nikitokwa na machozi. Nilijaribu kusema jambo lakini ulimi ulikuwa mzito. SASA SONGA NAYO...
MUME wangu aliamua kujilaza kwenye kochi kisha kunitaka niwe karibu naye ili aniambie jambo. Nilipomsogelea alisema nisijali kwani maneno ya yule mwanamke, yaani Mei yasinitie wazimu.
Kwa nini amenidhalilisha?
Yule Mei japokuwa ni mkwe wangu sitataka akanyage hapa tena.
Unasema kweli? nilimuuliza mume wangu.
Nakuapia. Hakanyagi hapa. Ninachowaza ni mtoto wangu tu maana bado ni mdogo na najua hana uwezo wa kumtunza.
Nikuambie jambo?
Sema.
Yule amefanya hivyo kwa kuwa anataka mtoto wako amfanye mtaji, yaani apate matumizi ya kila siku kupitia mwanao
Thubutu, hapati kitu hapa!
Mara tulisikia breki ya gari ambalo lilisimama nje ya nyumba yetu. Nilichungulia na kumuona Mei akitoka huku uso ukiwa umevimba.
Aliingia ndani bila kubisha hodi.
Nimegeuza gari. Njiani nimemuuliza Pili kama umetoa fedha za matumizi ya mtoto akasema hujatoa, nikamuamuru dereva ageuze gari.
Tuliangaliana mimi na mume wangu kwa kuwa hayo tulikuwa tukiyazungumza dakika kama mbili zilizopita. Mume wangu aliinuka na kukaa kwenye kochi huku akiwa amekunja uso, aliniangalia nami nikakunja uso.
Lakini Mei kwani wewe ni mke wangu? Hayo mambo angefanya Pili siyo wewe.
Mimi nahusika mia kwa mia, kwani Pili anakwenda kukaa kwa nani?
Pili kwenda kukaa kwako ni wewe umejitakia, kwani mimi nimeshindwa kumlea?
Kwa maana hiyo unataka kuniambai hutoi?
Kwako Mei sitoi hata senti tano. Hapa umemchukua Pili kwa nguvu hata muda wa kumpa hizo fedha ingekuwa saa ngapi
Kwani kutoa fedha kunahitaji winji, kalete hizo fedha tuondoke zetu.
Nakuambia nenda kwenye gari na ukabaki na mtoto kisha mtume Pili aje hapa nimuelekeze cha kufanya.
Yaani unaniamuru kwamba niende nikamchukue mtoto ina maana unanigeuza mimi ni yaya siyo?
Hapana.
Sasa kwa nini unasema niende kwenye gari nikampakate mtoto, unanivunjia heshima Bwana Chinchi kuwa umemzalisha mwanangu?
Huyo ni mke wangu, wewe ulitaka nizae na nani?
Na huyo mkeo wa kwanza.
Baada ya kusema hivyo alinitibua nikasimama na kutaka kumuendea pale alipokuwa amesimama lakini Chinchi mume wangu akanizuia.
Hebu niache, nikamfundishe adabu huyu pimbi.
Nani pimbi.
Wewe pimbi, sasa hivi umeponea tundu la sindano na umerudia tena kosa lilelile, sasa nakuua kabisa.
Wakati nasema hivyo Pili aliingia ndani huku akiwa na mtoto wake.
Mama, sasa hivi ulikuwa umezimia na unarudia tena kutaka kugombana na mama mkubwa, unafanya vibaya mama.
Sifanyi vibaya, mimi napigania haki zako, huoni kwamba huyu bwana anataka kukutesa?
Hapana mama, mambo yangu na huyu bwana tuachie wenyewe tutayamaliza.
Acha kunifundisha cha kufanya, kosa mimi unadhani huyu bwana angekuoa, si angeendelea kukaa na huyu mwanamke tasa hapa ambaye anajaza choo tu!
Maneno hayo yalinifanya nitoke jikoni huku nikiwa nimeshika panga, hasira zilikuwa zimenikaa barabara kichwani. Haraka kama umeme mume wangu alinishika huku akipiga yowe:
Salome utaua, utaua mke wangu
Je, nini kilitokea baada ya hapo? Fuatilia