Macho ya Bundi- 27-
ILIPOISHIA
Nilimuona Mei akiingia huku akiwa amejiinamia. Ile anakaa tu kwenye kochi mume wangu naye akawa anaingia. Alipomkuta alihamaki.
"Nani kakuruhusu kuingia? Mei nilikupiga marufuku."
SONGA NAYO...
Niliingilia kati na kumueleza mume wangu kuwa Padri Kalo katusuluhisha..
"Nisamehe mume wangu. Nilimruhusu mlinzi amruhusu Mei kuingia hasa baada ya kupatanishwa na Padri Kalo, nilikueleza mume wangu. Tumsamehe tafadhali."
Wakati wote Mei alikuwa akibubujikwa na machozi ambayo alikuwa akiyafuta kwa upande wa kanga.
"Unalia nini rafiki yangu?" nilimuuliza.
"Nisamehe sana rafiki yangu."
"Nikusamehe nini?"
"Nimegundua ubaya wangu niliowafanyia."
"Upi?"
Alianza kunieleza jinsi alivyotaka kunitibulia ili niachane na mume wangu, alivyokwenda kwa waganga ili kuturoga kwa nia ya kusambaratisha ndoa yetu.
Alikiri pia kwamba alikwenda kwa waganga kufunga kizazi changu lakini alipoona nimepata ujauzito na kujifungua, akagundua kuwa alikuwa akidanganywa na yule mganga wake.
Ilikuwa ni simulizi ya kusisimua kwa sababu aliyekuwa akifanya hayo alikuwa ni rafiki yangu mkubwa ambaye hata kuolewa kwangu zaidi ya miaka minane nilimshirikisha kwa asilimia mia moja.
Aliniambia kuwa kila wakati alikuwa akimuambia Pili amuambie mume wangu kuwa mimi nina wanaume, natembea nao nje ya ndoa.
Lakini pia nakumbuka kuwa hata mimi alikuwa akinieleza (Mei) kuwa mume wangu alikuwa na wanaume wengi wa nje, hali iliyosababisha tugombane sana na mume wangu na nikawa nasusa kulala katika chumba chetu.
Kususa huko kulisababisha mume wangu ampate Pili mtoto wa Mei na niligundua hilo siku mume wangu aliponipa taarifa ya kumuoa Pili kimila.
"Mume wangu, Mei mimi ni rafiki yangu na wala sina kinyongo na aliyonifanyia. Nampenda na nitazidi kumpenda. Tumsamehe na mimi nimeshamsamehe, shetani alimpitia."
Tulikumbatiana na Mei na tukawa wote tunatoka machozi. Nilimuambia wasiwasi wangu kuhusu macho ya bundi, nyumbani na hospitali ambako nilikuwa nakutananao kwamba kumbe wala siyo wa kichawi.
Simu iliita ilikuwa inatoka kwa Pili. Niliipokea, nilipigwa na butwaa baada ya Pili kuniambia kwamba kuanzia sasa yeye siyo aliyekuwa mke wenzake bali mimi ni mama yake.
"Najua mama alifanya ubaya kwako na ndiye aliyenilazimisha nitembee na mumeo nikapata mimba. Naomba umsamehe," alisema Pili.
Nilimuambia kuwa nimeshamsamehe na hivi nipo naye hapa nyumbani. Pili japokuwa alikuwa mbali na sisi hukohuko Ulaya alisika akisema Wawoo kwa furaha.
Naye akasema alipiga simu kwanza kwangu kabla hata ya kumpigia mama yake mzazi na mume wangu ambaye amemuacha na kumsomesha.
Anasema ananiona kama mama yake na siyo mke mwenza, akasema kusudio lake la pili ni kutaka kuniarifu kwamba amepata mchumba hivyo anataka baraka zangu na anataka ndoa hiyo ifungwe hukohuko Ulaya anakosoma.
Nilimuambia anipigie baada ya dakika kumi ili niwaambie mama yake na mume wangu.
Baada ya kukata simu wenzangu wote wakawa wananishangaa kwani nilirukaruka kushangilia.
"Salome naona una jambo kubwa, ulikuwa unazungumza na nani?" Mume wangu aliniuliza.
Je, akimwaga habari hiyo nini kitatokea? Usikose kufuatilia mkasa huu wa kusisimua leo jioni ndio Fainali