Ni dhahiri kuwa serikali imeshindwa kuwa na amani na Lowassa kwa sababu wanazozijua wao vizuri sana tena tangu akiwa ndani ya CCM. Jinsi walivyohitimisha suala la Richmond wengine tulibakia na maswali mengi tu.
Baada ya hapo wamemuendeshea kampeni ya kufa mtu kumnasibisha na ufisadi papa - kuwa ndiye kinara wa ufisadi nchini! Haya, wakaenda mbali zaidi kumthibitisha ugonjwa. Push-ups zikapigwa majukwaani kuonyesha tofauti. Kampeni ikazidi kutumbukia kwenye majitaka kumdhalilisha kabisa utu wake.
Pamoja na yote akapata uungwaji mzito katika kampeni na uchaguzi mkuu wenyewe. Sasa ni mwendo wa makatazo, vitisho, mabomu ya machozi, hoja za kipuuzi za polisi, n.k. Manake hamna namna nyingine tena. Wamejitahidi kuwaambia wananchi kuwa Lowassa ndiye kubwa la mafisadi lakini wapi! Umati unaendelea kumfuata tu. Quite frustrating.
Pamoja na mkao wake wa kistaarabu, kwangu mimi bado sijamuona Lowassa kuwa mtu wa maana sana kimaadili. Hadi sasa namhesabu kama mmoja wa mtandao wa uongozi wa CCM uliojenga na kuuimarisha mfumo wa ufisadi unaoliangamiza taifa hadi Leo hii. Labda kuna siku atatoa msimamo wake rasmi dhidi ya mtandao huo.
LAKINI sikubaliani kabisa na juhudi za serikali na CCM kumgeuza Lowassa kuwa ndiye shetani wetu mkuu halafu wao eti ndio mnabii na mitume wetu waliodondoka toka mbinguni majuzi! TENA nina mashaka kuwa wanaogopa kuwa huenda jamaa ndio anajitoa kwenye mtandao ilhali ana siri zao nyingi. Hawana imani wala amani. Ni kuota majinamizi kwa kwenda mbele. Dawa pekee waliyobakia nayo nionavyo, ni kumfikisha Lowassa kwenye mahakama ya mafisadi kama kweli wana jeuri hiyo. Manake hapo ni lazima waweke "suicide pact".