Kitila Mkumbo
BUNGE la bajeti la mwaka huu limekamilisha kikao chake kwa kishindo, kilichotokana na kufungiwa kwa Mbunge wa Kigoma Kaskazini, Zitto Kabwe (CHADEMA), kuhudhuria vikao vya Bunge hadi Januari 2008. Kabwe alifungiwa kwa kile kilichodaiwa kuwa, alilidanganya Bunge.
Baada ya mjadala wa takriban wiki moja kupitia vyombo mbalimbali vya habari na katika maisha ya kila siku ya wananchi, imedhihirika wazi kuwa kilichosababisha Zitto afungiwe si kusema uongo, bali msimamo wake wa dhati wa kusema ukweli na kutekeleza wajibu wake wa ubunge kama alivyoapa kwa mujibu wa katiba yetu.
Mengi yamesemwa kuhusu hatua iliyochukuliwa na Bunge. Wapo waliolaani sana, ambao ndio wananchi walio wengi; wapo pia waliopongeza uamuzi wa Bunge na hawa ni wale wateule wachache ndani ya CCM wanaodhani wao pekee ndio wana akili, na sisi wengine hamnazo.
Kwa upande wangu, naona kwamba yaliyompata Zitto ni matokeo ya mfumo wetu wa utawala uliojengwa na CCM tangu mfumo wa vyama vingi uanze. Utawala wa CCM umejikita katika kuwabeza watu wenye uwezo na dhamira ya kweli na kuwatukuza watu wenye kutafuta mafanikio kwa njia ya ujanjaujanja.
Utawala wa CCM umejijenga katika kufanya watu waamini uongo ndio ukweli na ukweli ni uongo.
Kwa hiyo, wakijitokeza watu wachache kama akina Zitto na wakapata nafasi adimu ya kuingia bungeni, wanatengenezewa kila aina ya ghiliba ili kuwachafua katika jamii na kuwakatisha tamaa wasifanye kazi zao za kisiasa sawasawa.
Tukirejea kidogo katika hoja ya Zitto iliyomsababishia kufungiwa kuhudhuria vikao vya Bunge, tunaona kwamba hoja ya msingi ya Zitto ilitokana na shaka aliyokuwa nayo juu ya uharaka uliosababisha kusainiwa kwa mkataba mpya wa madini, tena hotelini ughaibuni, huku kukiwa na agizo la rais la kusitishwa kusainiwa kwa mikataba mipya (moratorium), hadi pale mapungufu yaliyokuwemo katika mikataba ya zamani yatakapokuwa yamerekebishwa.
Hii ndiyo hoja ya msingi iliyowekwa mezani na Zitto. Sasa tazama mtoa hoja ya kupewa adhabu ya kifungo, Mudhihir Mudhihir, alivyochangia mada hii. Katika kujenga hoja yake ya kumfungia Zitto kuhudhuria vikao vya Bunge.
Mudhihir alirejea mchango wa Zitto alioutoa wakati akichangia hotuba ya bajeti ya Waziri wa Nishati na Madini tarehe 16/7/2007; na nanukuu baadhi ya maelezo yake kama ifuatavyo:
Mheshimiwa Spika, yaliyopo mbele yetu hapa ni mambo mawili tu. Moja la msingi ni tuhuma ambayo aliitoa Mheshimiwa Zitto tarehe 16/7/2007 ambayo ningependa niinukuu katika Hansard ukurasa 181 alisema hivi:
Mheshimiwa Spika, kutokana na majibu ya Mheshimiwa Waziri kuhusiana na Mkataba mpya wa Mgodi wa Buzwagi ambao Mheshimiwa Waziri ameeleza maelezo ambayo sio sahihi, amedanganya na ameeleza vitu ambavyo kwa kweli sivyo ambavyo vipo katika Mkataba ambao ameusaini.
Mheshimiwa Spika, hii ndio hoja ya msingi. Kwa mkataba ambao ameuona yeye hayo yaliyosemwa na Waziri sivyo vilivyomo mle. Sasa mnataka taarifa gani na mkataba anao na amesema aliyoyaona yeye mle sio aliyosaini Waziri. Mnatafuta taarifa gani tena? Kwa hiyo, mkataba huu alikuwa nao ndio maana akaweza kufananisha kwamba yaliyosemwa na Waziri siyo yaliyomo mle, hii ndio hoja ya msingi kudanganya. Sasa hii habari ya Kamati Teule ilikuwa ni mtoto wa hoja ya msingi.
Mheshimiwa Spika, sasa tunazungumza habari ya Kamati Teule tunaacha hoja ya msingi iliyotukusanyisha hapa leo kwamba Waziri alidanganya... Mwisho wa kunukuu.
Baada ya ya maelezo hayo, Mudhihir alirejea Kanuni ya 50(1) inayotoa adhabu kwa mbunge anayemsemea mwenzake uongo na akahitimisha hoja yake kwa maneno haya:
Mheshimiwa Spika, kutokana na ukiukwaji huu sijui taratibu zinakuwa wa Kanuni ya 50(1) ya kumsemea mwenzake uongo, ya kumpaka matope nahisi aliyedanganya ni huyu mtoa hoja kuliko yule aliyebambikiwa tuhuma hizi na kwa msingi huo utanielekeza kama nitakuwa nakosea ninaomba mimi nitumie kanuni ya 59(3) kwamba kwa tabia hii ambayo imefanywa na ndugu yetu Mheshimiwa Kabwe Zuberi Zitto asimamishwe kazi ya Ubunge kuanzia leo na mkutano wote wa tisa unaokuja, tukutane naye hapa Bunge la Januari. Mwisho wa kunukuu.
Kuna mambo mawili ya msingi ya kuzingatia katika hoja ya Mudhihir iliyosababisha Zitto kufungiwa kufanya kazi za ubunge.
Kwanza, hoja ya Mudhihir haikujengwa katika hoja ya msingi ya hoja binafsi ya Zitto aliyoiwasilisha bungeni kwa ajili ya majadiliano na maamuzi.
Hoja aliyowasilisha Mudhihir ilikuwa ni hoja nyingine tofauti, na ilipaswa kutazamwa tofauti na hoja ya Zitto.
Pili, hoja aliyoitoa Mudhihir ilikuwa ni hisia, rejea maneno yake hapo juu pale anaposema; nahisi aliyedanganya ni huyu mtoa hoja. Hapa akimaanisha Zitto.
Kwa hiyo, Zitto alihukumiwa kwa hoja tofauti na ile aliyowasilisha katika hoja yake binafsi akitaka Bunge liunde kamati teule na alihukumiwa kwa hisia tu zilizoonyeshwa na Mudhihir, bila uchunguzi wowote kama hisia hizi zilikuwa kweli au la.
Kama Bunge lingekuwa linafanya maamuzi yake kwa kuzingatia mantiki na uzito wa hoja badala ya misimamo ya vyama na sura za watoa hoja, lingeiona hoja ya Mudhihir kuwa ni hoja nyingine mpya ambayo angeshauriwa kuiwasilisha katika mkutano au kikao tofauti na kile kilichokuwa kinajadili hoja ya Zitto.
Vilevile, Zitto asingepaswa kuhukumiwa kwa hisia tu ambazo Mudhihir alizitoa; badala yake, Bunge lingechunguza kama hisia hizi zilikuwa za kweli au la.
Kuna jambo lingine la kujadili katika sakata hili.
Katika kumhukumu Zitto, Bunge lilijiweka katika hali inayoonyesha kuwa halipendi kabisa mambo ya uongo, hasa pale ambapo uongo huo unasemwa na mbunge au waziri.
Hata hivyo, nina shaka sana kama kweli Spika na Bunge letu, na hasa wabunge wa CCM wanachukizwa na tabia ya uongo. Hii ni kutokana na ukweli kwamba, mara kadhaa wabunge na hata mawaziri wamedanganya na hatukuona Spika au Bunge kwa ujumla wake likichukizwa, achilia mbali kuchukua hatua.
Mfano wa karibuni kabisa ni wa Waziri wa Fedha, Zakia Meghji. Sote tunakumbuka kuwa mwanzoni mwa Julai mwaka huu, baada ya kuanza kutumika kwa bajeti mpya iliyosabisha bei ya mafuta, bidhaa zingine na gharama ya maisha kwa ujumla kupanda, Waziri Meghji alilitangazia Bunge na wananchi kwa ujumla kuwa bei ya mafuta ingeshuka.
Lakini hadi unaposoma makala haya, bei ya mafuta haijawahi kushuka, sana sana inazidi kupaa. Sasa hii maana yake ni nini kama si alichosema waziri ni uongo? Ndani ya Bunge letu hili hili, kuna wabunge na hata mawaziri kadhaa ambao imekwishathibitika kuwa wamedanganya kuwa wana shahada za uzamivu (PhD) wakati si kweli.
Imekwishagundulika kwamba kuna watu katika Bunge letu wanaodai wana shahada za uzamivu walizozipata kwa njia ya mtandao kwa kipindi kifupi kisichozidi miezi sita na ambazo zilitolewa na vyuo visivyotambuliwa na taasisi yoyote ya kuhakiki shahada za elimu ya juu hapa duniani.
Pamoja na kugundulika huku, bado wabunge na mawaziri hawa wanaendelea kutumia vyeo vya udaktari, na kwa maana hiyo, wanadanganya kwa kujibebesha sifa wasizokuwa nazo.
Sasa akina Mudhihir kama kweli wana uchungu sana na kudanganywa kwa Bunge, kwa nini hawajatoa hoja binafsi za kuwafungia hawa wabunge na mawaziri kwa kuanzia na Waziri Meghiji kwa kudanganya kuwa bei ya mafuta ingeshuka?
Pengine cha kujiuliza ni kwa nini hasa Bunge letu lipo kama lilivyo? Au kwa maneno mengine, kwa nini Bunge letu linatoa maamuzi ambayo yanasababisha dhoruba katika jamii kwa kiwango tulichoshuhudia katika hili sakata la Zitto?
Majibu ya swali hili yanaweza yakawa mengi. Lakini kwa upande wangu, nafikiri kwamba jibu lake ni rahisi kabisa, nalo ni ukweli kwamba viongozi wetu tuliowachagua kupitia chama chao cha CCM, wamelewa sana kutokana na madaraka makubwa sana tuliyowabebesha.
Hapa ndipo unaingia msemo maarufu wa Kiingereza usemao kuwa; madaraka hulevya, na madaraka makubwa sana hulevya sana!
Viongozi wetu wamelewa madaraka kwa kiasi cha kuziba mifumo yao ya fahamu na hata sasa hawasikii, hawaoni wala hawawezi kunusa yale yanayoendelea katika jamii.
Kwa maana nyingine, viongozi wetu hawafikirii jinsi vile tunavyofikiri na wala hawaishi vile sisi tunaishi. Na ndiyo maana basi wananchi wanapowazomea wabunge kwa maamuzi yao yasiyofuata mantiki ya kawaida ya kufikiria, achilia mbali kanuni walizojitungia wao wenyewe, wao nao wanawashangaa wananchi kwa kumpongeza Zitto kwa ushujaa wake! Kwa kifupi viongozi wetu hawavai taswira tuliyonayo sisi wananchi!
Swali la pili la kujiuliza, iweje wabunge watokanao na CCM ambao ndio wengi, wawe wasemaji wa serikali wakati wale wa upinzania walio wachache ndio wanaonekana kuwa wasemaji wa wananchi kama inavyopaswa kuwa kwa mujibu wa kazi za ubunge?
Jibu kwa swali hili pia si gumu kulipata kama utarejea kidogo jinsi wabunge wa CCM walivyopatikana ukilinganisha na wale wa upinzani. Mchakato wa uchaguzi wa 2005 na hata chaguzi za kabla ya hapo zilizofanyika tukiwa katika mfumo wa vyama vingi, unatuonyesha kuwa wabunge wa CCM walio wengi walibebwa na chama chao.
Ndiyo kusema, wananchi wengi waliwachagua wabunge wa CCM si kwa kuwa waliowaona wanafaa kuwa viongozi wao, bali kwa kuwa CCM ilisema kuwa wanafaa. Kwa maana nyingine, wananchi waliichagua CCM na si wale wabunge moja kwa moja.
Wabunge wa CCM pia wanajua hili, kwamba wao walichaguliwa na CCM na wananchi walitumika kuhalalisha chaguo la CCM. Kwa hivyo, wabunge wa CCM wanajua aliyewapeleka bungeni si wananchi, bali ni CCM.
Kwa hiyo, inapokuja hoja ya moto kama ile ya Zitto, wabunge wa CCM wanajua wa kumtetea ni serikali ya CCM na si hao wananchi na mgodi wao wa Buzwagi.
Ukija kwa upande wa wabunge waliotokana na upinzani, tunajua kwamba hawa hawakubebwa na vyama vyao, bali wao ndio waliovibeba vyama vyao. Ndiyo kusema, kama sheria ingekuwa inaruhusu, wabunge wengi wa upinzani waliopo sasa wangeweza kuwa wamechaguliwa na wananchi bila kujali vyama vyao.
Kwa hiyo, hawa wanajua wa kumsemea bungeni si vyama vyao, bali wananchi wa Tanzania waliowatuma. Haishangazi basi hoja zote nzito nzito zinagusa maslahi ya wananchi bungeni zinabebwa na wabunge wa upinzani huku wale wenzao wa CCM wakiwaona kuwa ni nuksi!
Nimalizie makala haya kwa kutoa angalizo la kimafunzo katika sakata hili la Zitto. Kwanza, kwa maoni yangu tunapowalaumu wabunge wa CCM, nasi tukubali kupokea sehemu ya lawama hizo kwa kuipenda na kuiamini mno CCM kiasi kwamba miaka 15 baada ya kuanzishwa kwa mfumo wa vyama vingi, tumeendelea kuchagua wabunge na madiwani lundo kutoka chama hiki, CCM.
Tena sisi tulio Dar es Salaam, tukubali kubeba lawama zaidi kwa kushindwa kuchagua mbunge hata mmoja kutoka chama cha upinzani katika uchaguzi uliopita.
Vilevile tunapowashangilia akina Zitto, Wangwe, Dk. Slaa na wabunge wengine wa upinzani kwa kazi nzuri wanayoifanya bungeni, tunawajibika kuwarudishia heshima na shukrani wananchi wa Kigoma Kaskazini, Tarime, Karatu na majimbo mengine ya mikoani yaliyowachagua wabunge kutoka vyama vya upinzani, kwa wao kuwa wangamuzi wa mambo kuliko sisi wa Dar es Salaam!
Ndiyo kusema, kwa Tanzania linapokuja swala la ujanja na uelewa kisiasa, wenzetu wa vijijini wametuzidi. Tukiri kwanza ukweli huu ili tuweze kuwekana sawa.
Pili, sakata hili limetukumbusha kazi za ubunge ambazo tulianza kuzisahau baada ya kuanza mfumo wa vyama vingi.
Umahiri wa ujenzi wa hoja ulioonyeshwa na akina Zitto na wenzake kutoka vyama vya upinzani, unatukumbusha kuwa kazi ya msingi ya mbunge ni kutetea maslahi ya wananchi waliomchagua na nchi kwa ujumla, na kuhakikisha kuwa serikali iliyopo madarakani inatakeleza wajibu wake wa kuwatumikia wananchi kwa mujibu wa katiba.
Kwa hiyo, uchaguzi mwingine utakapofika tusiwachague watu kwa sababu tu wana uwezo wa kifedha wa kujenga visima vya maji au kutugawia unga wakati wa njaa; haya ni mambo mazuri, lakini si kazi za msingi za mbunge na kufanya haya si lazima mtu awe mbunge.
Mwisho, tunajifunza kwamba tunahitaji wabunge wengi wa aina ya Zitto ili kishindo cha hoja zao si tu kitikise nchi, bali kiweze kusababisha mabadiliko katika sera zinazotawala maisha yetu. Hivyo basi tukiendelea kutafakari madhila ya Bunge letu la sasa, tuweke nadhiri kuwa katika uchaguzi wa 2010, tutawachagua akina Zitto 200 na akina Mudhihir 0!