Herbalist Dr MziziMkavu
JF-Expert Member
- Feb 3, 2009
- 42,318
- 33,116
Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), imesema kuwa matokeo ya Rais yatatangazwa kwenye majimbo badala ya kusubiriwa kutangazwa na NEC...
Mkurugenzi wa NEC, Rajabu Kiravu, alisema hayo jana jijini Dar es Salaam wakati wa mkutano na wawakilishi wa watu wenye ulemavu kwa ajili ya maandalizi ya uchaguzi mkuu unaotarajiwa kufanyika Oktoba, mwaka huu.
Alisema kuwa lengo la kufanya hivyo ni kuondoa hofu kwa wananchi wanaosubiri kujua matokeo.
Kiravu alisema kuwa NEC imeanza maandalizi ya uchaguzi ujao kwa kujipanga kikamilifu ili kuwepo na uwazi na haki sawa kwa mujibu wa sheria.
Alisema kwa sasa NEC inaboresha Daftari la Kudumu la Wapigakura ili iweze kupanga vituo vya kupigia kura wakati wa uchaguzi mkuu.
Alisema kwa mwaka huu vituo vitaongezeka kufikia vituo 55,000 kutoka 47,000 vya mwaka 2005.
Mkurugenzi huyo alisema asasi za kiraia zikiwemo za walemavu zina wajibu wa pekee wa kuelimisha umma hususan masuala muhimu yanayohusu uchaguzi.
Kwa mujibu wa Kiravu, uelimishaji huo ni ule unaolenga kumpa uelewa mpiga kura kuhusiana na namna ya kupiga kura, thamani ya kupiga kura, umihimu wa kutunza kadi ya kupigia kura na kujitokeza kwa wingi siku ya kupiga kura.
Alisema walemavu watapewa kipaumbele zaidi kwa kuwa ni watu kama watu wengine na wana haki za msingi na watapatiwa elimu kuhusu namna ya kushiriki katika uchaguzi huo.
Mkuu wa Mradi wa Shirika la Mpango wa Maendeleo wa Umoja wa Mataifa (UNDP), Oscar Harnam, alisema kuwa wamejitolea kwa ajili ya kuwasaidia walemavu kwenye uchaguzi na kuwapatia mahitaji watakayoyahitaji wakati wa uchaguzi.
Alisema takwimu zinaonyesha kuwa asilimia 8.2 ni watu wenye ulemavu ambao ni sawa na watu zaidi ya milioni 3 hivyo wanapaswa kushiriki.
CHANZO: NIPASHE