Mkurugenzi wa Kampuni ya Hali
Halisi Publishers, Saed Kubenea
pamoja na Mwenyekiti wa
Jukwaa la Wahariri Tanzania
(TEF) Absalom Kibanda
wameionya serikali juu ya
uamuzi wa kulifuta gazeti la
MAWIO uliochukuliwa hivi
karibuni.
Kupitia tangazo la serikali lenye
notisi namba 55, serikali
ilichukua uamuzi wa kulifungia
MAWIO, Januari 15, 2016 huku
Waziri wa Habari, Utamaduni,
Sanaa na Michezo, Nape Nnauye
akisema gazeti hilo limekuwa
‘sugu’ kwa uchochezi tangu
2013.
Kubenea na Kibanda walikuwa
katika kituo cha Polisi cha Kati
ambapo ndiyo Makao Makuu ya
Kanda Maalum ya Dar es Salaam
wakiwasindikiza wahariri Jabir
Idrissa na Simon Mkina
walioitikia wito wa uliotolewa na
jeshi hilo siku tatu zilizopita.
Kibanda amewambia
wanahabari kuwa kitendo cha
jeshi la polisi kuwasaka ili
kuwakamata Jabir na Mkina
ambao ni wahariri ili kuwahoji
huku gazeti la MAWIO likiwa
limefungiwa, kinalenga
kuwatisha waandishi wa habari
nchini na kuzima uhuru wa
habari.
Ameulezea uamuzi huo wa
Waziri mwenye dhamana ya
masuala ya Habari, Nape, kama
uamuzi uliolishitua TEF na
wamewasiliana naye wakielezea
mshituko na masikitiko yao.
“Hatuwezi kuvumilia kufungiwa
kwa vyombo vya habari,
kukamatwa na kunyanyaswa
kwa waandishi, miaka miwili
iliyopita nilitakiwa kujisalimisha
makao makuu ya polisi,
nikafikishwa mahakamani na
nikashinda kesi, naelewa
maumivu ya mapambano haya,”
ameeleza Kibanda.
Kwa upande wake Kubenea,
amesema Serikali kupitia Nape
imechukua uamuzi wa kikatili
dhidi ya gazeti la MAWIO ili
kuzima sauti ya wananchi kwa
hoja zisizo na mashiko ikiwemo
ile ya uchochezi ambayo
imekuwa kisingizio cha
watawala kwa muda mrefu.
“Katika toleo la MAWIO lilimnukuu
Maalim Seif akijitangaza mshindi,
yeye hakuitwa mchochezi, Jecha
amefuta uchaguzi wakati hana
mamlaka ya kisheria wala ya
kikatiba hakuitwa mchochezi ila
gazeti kuandika ushindi
uliotangazwa na Seif
limefungiwa,” ameeleza Kubenea.
Kubenea ameongeza kuwa,
ubovu wa sheria ya magazeti ya
mwaka 1976 umekuwa
ukitumiwa na serikali kuviadhibu
vyombo vya habari vinavyofichua
maovu, huku mahakama
ikithibitisha mara kadhaa kuwa
madai ya uchochezi
yanayotolewa na serikali hayana
mashiko.
“Jabir ni Mwandishi aliyebobea
kitaaluma na uzoefu, ameandikia
magazeti ya Uhuru, Mzalendo,
Majira na New Habari huko kote
hakuitwa mchochezi wala
hakukamatwa.
“Nape alikuwa mmoja wa
waandishi na vyanzo vya taarifa
za MwanaHALISI kipindi hana
madaraka CCM, mbona
alishirikiana na sisi kuibua
maovu kama sisi ni
wachochezi?” alihoji Kubenea.
Jabir na Mkina wamekuwa
wakitafutwa na jeshi la polisi
kwa siku tatu mfululizo tangu
Jumamosi kwa tuhuma za
uchochezi huku jaribio la
kuwakamata likishindikana mara
kwa mara kutokana na kutojua
walipo mpaka walipoamua
kujisalimisha jana.
Mbali ya Kubenea na Kibanda,
walisindikizwa pia na Mhariri
Mtendaji wa gazeti la
MwanaHALISI, Ansbert Ngurumo
pamoja na wakili wao, Fredrick
Kihwelo.