THINKINGBEING
JF-Expert Member
- Aug 9, 2010
- 2,779
- 1,304
Leo katika taarifa ya habari ITV kwa mara ya Kwanza nimemsikia katibu mkuu wa CCM akikiri hadharani kwamba serikali inayoongozwa na chama chake inanuka rushwa ndio maana watu wanapenda CHADEMA.
Chanzo: Mwananchi
Katibu Mkuu wa CCM, Abdulrahman Kinana ametaja siri ya chama hicho kupoteza majimbo mbalimbali ya uchaguzi likiwamo la Iringa Mjini kuwa ni makosa yaliyofanyika wakati wa uteuzi wa wagombea.
Alisema jambo jingine linalowapa kiburi wapinzani lilitokana na vitendo vya rushwa vilivyofanyika ndani ya chama hicho kwa upande mmoja na kwa watendaji serikalini kwa upande wa pili.
Kinana alisema chama hicho kimeshajisahihisha na kimejipanga kudhibiti vitendo hivyo ndani ya chama na pia kitadhibiti rushwa kwa viongozi na watendaji serikalini kwa kuwachukulia hatua watakaobainika kujihusisha na vitendo hivyo viovu.
Alitoa kauli hiyo juzi alipokuwa akizungumza kwenye mkutano wa hadhara uliofanyika katika Uwanja wa Mwembetogwa Iringa katika siku ya mwisho ya ziara ya siku tano mkoani hapa.
"Chadema wasidhani wana wanachama hapa, CCM tumejua sababu zilizotufanya tupoteze majimbo kadhaa likiwamo hili la hapa Iringa Mjini, mosi ni makosa yaliyofanyika wakati wa uteuzi wa wagombea, watu walitaka mabadiliko hawakuyapata ndani ya chama ndiyo sababu wakalazimika kupiga kura za hasira kwa kuchagua upinzani," alisema Kinana na kuongeza:
"Chadema wasipate kiburi kwa kudhani wana watu… watu wote waliosimama kule juu si wanaChadema ni wanaCCM wamekwenda huko baada ya sisi ndani ya chama hususan ngazi za juu kufanya makosa, tulifanya makosa katika suala zima la uteuzi wa wagombea.
"Kwa sasa niwahakikishie wananchi wote na wakazi wa Jimbo la Iringa kuwa tumejisahihisha, hatutarudia makosa … natoa wito kwa wakazi wa jimbo hili kutuunga mkono katika uchaguzi mkuu ujao ili tuweze kupata mbunge atakayewasaidia kutatua kero zinazowakabili wananchi."
Katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2010, Frederick Mwakalebela alishinda kura za maoni ndani ya CCM katika Jimbo la Iringa Mjini, lakini jina lake likakatwa katika vikao vya juu vya chama hicho.
Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM, Nape Nnauye alimtuhumu Mbunge wa Iringa Mjini, Mchungaji Peter Msigwa kuwa alishirikiana na Chadema kutumia vibaya picha za tukio la mauaji ya aliyekuwa mwandishi wa Channel Ten, Daud Mwangosi kwa kuziuza nje na kujipatia kipato.
Akijibu tuhuma hizo, Msigwa alisema:
"Kiukweli nimeumizwa sana na propaganda hii, nasema kweli imeniuma sababu hata familia ya marehemu Mwangosi tumeendelea kushirikiana nayo, wale ni jirani zangu na yule mtoto mdogo mara nyingi anakuja kushinda pale nyumbani kwangu," alisema Msigwa.
Alisema suala hilo pamoja na mambo mengine, chama chake kitayajibu kwenye mkutano wake wa Oktoba 18, mwaka huu utakaofanyika mjini hapa.
Chanzo: Mwananchi