Tangu mfumo wa vyama vingi umeingia Nchini mwetu, mwenendo wa kisiasa umekuwa ni wenye ushindani mkubwa hasa kwa miaka ya hivi karibuni. Kumeibuka vyama na wanasiasa ambao kwa njia moja ama nyingine wamekuwa wakileta ushindani mzuri katika siasa, hali ambayo imechangia kuleta fikra mpya katika uongozi wa vyama mbalimbali na hata serikali kwa ujumla.
Tumeshuhudia wanasiasa mbalimbali wenye fikra chanya za kimaendeleo kutoka ndani ya CCM na vyama vya upinzani, orodha yao ni ndefu. Vyama vya upinzani kwa ujumla vimekuwa vikijidhatiti na kujiimarisha ili kuchukua Dola wakati CCM nayo imekuwa ikijidhatiti ili kuendelea kuwa madarakani. Hali hii imesababisha siasa zetu kuwa ni zenye ushindani mkubwa hasa katika kipindi cha chaguzi mbalimbali.
kwa ujumla naweza kusema siasa zetu zinakua ingawa bado tunaendesha siasa za kizamani, siasa ambazo yule asiekubaliana na mawazo yako unamuona ni adui kiasi hata cha kutoaminiana. Hali hii imejitokeza baina ya vyama kwa vyama, lakini pia hata ndani ya vyama baina ya wanachama kwa wanachama. Hali ipo hivyo ndani ya vyama vyote hasa vyama vikubwa kama NCCR MAGEUZI, CUF, CHADEMA, CCM na kwa mbali TLP. Tumeshuhudia sakata la Maalim Seif Sharrif na Hamad Rashid, tumeyaona ya David Kafulila na NCCRR Mageuzi.
Bado tunaendelea kuyashuhudia ya Zitto Kabwe na CHADEMA. Ndani ya CCM pia hali si shwari. Ilifikia hatua ya Mwenyekiti wake ambaye pia ni Rais wa Nchi kutahadharisha kwamba chuki iliyopo imefikia hatua mbaya ya watu kutoaminiana kiasi cha kutopeana hata maji ya kunywa. Mheshimiwa Rais alikuwa sahihi kabisa. Kwangu mimi tahadhari hiyo ilipaswa ichukuliwe kwa uzito mkubwa na vyama vyote vyenye matatizo ya ndani. Siasa sio chuki, siasa ni maendeleo, hili linahitaji mjadala wake.
Pamoja na yote hayo ukweli uliopo ni kwamba Chama Cha Mapinduzi bado kinapendwa na Wananchi walio wengi ukilinganisha na vyama vingine. Hali hii itaendelea hivyo kwa muda mrefu hasa kama CCM itaendelea kufanya siasa za Mapinduzi kama ilivyokusudiwa (Mapinduzi ya Kifikra na Maendeleo). Wananchi wengi bado wana imani na CCM na Serikali yake. Tatizo kubwa kwa CCM ni baadhi ya Viongozi wake kujisahau na kufanya mambo ambayo ni kinyume na madhumuni ya CCM. Hali hiyo ndio iliyochangia CCM leo kuonekana ni Chama kinachopata shida sana kupata ushindi katika maeneo mengi ya miji mikubwa. Sababu zipo nyingi na zinaepukika.
Nasema ni baadhi ya viongozi kwa sababu ndani ya CCM kuna viongozi wasafi, wachapa kazi, wazalendo na pia wavumilivu. Rais Kikwete binafsi namuona kama mmoja wa Viongozi wa CCM wenye sifa hizo. Tukiacha propaganda za kwenye majukwaa ya kisiasa na kwenye mitandao ya kijamii, Kikwete anabaki kuwa Mwanasiasa Msikivu, Mzalendo na Mvumilivu, mwenye kujali matakwa ya wananchi ingawa kuna watu wanamkwamisha. Leo Nchi ipo katika mchakato wa kuandika Katiba mpya, ni kwa sababu ya maamuzi magumu yaliyofanywa na Kiongozi huyu. Kuongoza Nchi na Serikali kunahitajika chama cha siasa chenye misingi iliyojengeka toka chini kwenda juu. Kunahitaji chama cha siasa kisicho na migogoro ya mara kwa mara. Migogoro ndani ya vyama haiepukiki, lakini iwe ni migogoro yenye tija. Kinahitajika chama cha siasa kilicho ndani ya mioyo ya wenye Nchi ambao ni Wananchi wenyewe.
Tukiuzingatia UKWELI huo, bado CCM ina nafasi ya kuendelea kutuongoza kama Nchi. Maeneo ambayo CCM imeyapoteza kwa vyama vya upinzani, ni matokeo ya kutouona ukweli ndani ya CCM na badala yake kufanya kinyume na maamuzi ya wengi ndani ya Chama... Ni kama adhabu ambayo CCM imekuwa ikipewa na wanachama wake. Ni kama adhabu ambayo CCM imekuwa ikipewa na wananchi kwa niaba ya Serikali yake. Ni funzo ambalo likifanyiwa kazi, Wananchi wataendelea kuiamini kwa muda mrefu. Binafsi nina imani na CCM. Ni wakati sasa wa CCM kurudi katika misingi yake. Hayati Baba wa Taifa Mwalimu Julius Nyerere aliliona hili zamani na ndio sababu alitahadharisha na kutaka TUJISAHIHISHE!