Zitto azua mjadala
• Wazee CHADEMA walinda mchakato usiingiliwe
na Waandishi Wetu
HATUA ya Naibu Katibu Mkuu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Zitto Kabwe, kuchukua fomu ya kugombea wadhifa wa uenyekiti, inaonekana kuibua mjadala katika anga la siasa hapa nchini.
Kuibuka kwa mjadala huo kwa kiwango kikubwa kumetokana na hatua ya mwanasiasa huyo kijana kuamua kukabiliana na Mwenyekiti wa sasa wa chama hicho, Freeman Mbowe.
Habari za uhakika ambazo Tanzania Daima Jumatano imezipata kutoka vyanzo vya kuaminika ndani ya CHADEMA, zinaeleza kwamba uamuzi huo wa Zitto unaonekana kuwashtua viongozi mbalimbali wa juu wa chama hicho.
Mbali ya hao, uamuzi huo wa Zitto kuchukua fomu ya kugombea uenyekiti wa chama hicho, unaonekana kugusa mijadala ndani ya vyama vingine vya siasa, kikiwamo Chama Cha Mapinduzi (CCM).
Makada kadhaa wa CCM waliozungumza na gazeti hili kwa nyakati tofauti juzi na jana walisema, mabadiliko ya uongozi ndani ya CHADEMA ni jambo linalofuatiliwa kwa karibu.
Kama ilivyokuwa kwa CCM, mchakato huo unaonekana kukigusa pia Chama cha Wananchi (CUF) ambacho ndani ya Bunge kimeunda serikali kivuli kwa ushirikiano na CHADEMA.
Hata hivyo, kikubwa kinachozusha mijadala na maswali, ni hatua hiyo ya Zitto kuamua kugombea akichukua fomu Kigoma na kutuma watu wa kumrejeshea pasipo yeye mwenyewe kukutana na viongozi wenzake wa juu.
"Uamuzi wa Zitto kuchukua fomu ya uenyekiti si jambo la ajabu hata kidogo. Kinachotatanisha ni kwamba, huyu jamaa ameamua kugombea kwa staili ya kakakuona.
"Ametoweka katika Ofisi za Makao Makuu kwa zaidi ya miezi mitatu, akasikika akiwa Kigoma na aliporejea Dar hakukutana na kiongozi mwingine yeyote hadi alipotuma watu kumrejeshea fomu juzi," alisema kiongozi mmoja wa juu wa CHADEMA aliyezungumza na gazeti hili kwa sharti la kutotajwa jina lake gazetini.
Jitihada za Tanzania Daima Jumatano kuwasiliana na Zitto kwa njia ya simu jana, hazikufanikiwa na taarifa zinasema alikuwa nchini Ujerumani kwa shughuli binafsi.
Hata hivyo, alipozungumza na Tanzania Daima Jumatano mwishoni mwa wiki kuhusu kuwapo kwa taarifa zilizokuwa zikimhusisha na kugombea wadhifa huo, Zitto alikiri kuwapo kwa shinikizo kutoka miongoni mwa viongozi wenzake ndani ya chama hicho.
"Nimekuwa nikipata shinikizo kubwa kutoka kwa baadhi ya watu ndani ya chama wanaonitaka nigombee uenyekiti. Nimekuwa nikitafakari sana na hadi sasa bado sijaamua kugombea au la," alisema Zitto siku ya Jumapili.
Alipoulizwa iwapo alikuwa amefanya mawasiliano yoyote na viongozi wenzake wa CHADEMA kuhusu yeye kuwa na mpango wa kugombea, Zitto alisema asingeweza kufanya uamuzi wowote kabla ya kumtaarifu Mbowe na Katibu Mkuu wake, Dk. Wilbrod Slaa.
Gazeti hili lilipowasiliana na Mbowe siku ya Jumapili na jana kuhusu uamuzi huo wa Zitto kugombea, mara zote mwanasiasa huyo aliwaelekeza waandishi wetu kuwasiliana na Ofisi ya Katibu Mkuu ambayo alisema ndiyo inayoratibu shughuli zote za uchaguzi wao.
Hata hivyo, pamoja na kutokuwa tayari kuingia kwa undani, jana Mbowe alilihakikishia gazeti hili kwamba tayari alikuwa amejaza na kurejesha fomu za kugombea uenyekiti katika Ofisi ya Katibu Mkuu.
Wakati Mbowe akikataa kutoa ufafanuzi mwingine wowote wa ziada, ofisa mmoja wa juu wa CHADEMA alilieleza Tanzania Daima Jumatano kuwa, uamuzi wa mwenyekiti huyo kuchukua fomu za kugombea, ulichagizwa na shinikizo au ushauri wa wazee wa chama hicho.
Kwa mujibu wa ofisa huyo, Mbowe alijaza fomu hizo baada ujumbe wa wazee hao wa chama uliowajumuisha, Profesa Mwesiga Baregu, Victor Kimesera na Bob Makani kukutana naye na kumshauri kugombea tena nafasi hiyo.
"Ninachoweza kukuthibitishia ni kwamba, Mbowe alikuwa amefikia uamuzi wa kutogombea uenyekiti hadi baada ya kushawishiwa na wazee ambao walimuomba kukivusha kwanza chama katika Uchaguzi Mkuu wa mwakani," alisema mtoa habari wetu.
Baadhi ya wanasiasa waliozungumza na Tanzania Daima Jumatano kwa nyakati tofauti tangu tetesi za Zitto kuwa na nia ya kugombea nafasi hiyo akichuana na mwenyekiti wa sasa, walieleza kuwa ingawa hatua hiyo inaonyesha jinsi demokrasia ilivyokaa ndani ya CHADEMA, kwa upande mwingine inaweza kukipeleka pabaya chama hicho.
Mmoja wa wanasiasa hao aliyezungumza na gazeti hila jana kwa sharti la kutoandikwa jina lake gazetini, alieleza kuwa hatua ya Zitto kuwania nafasi ya uenyekiti, ina lengo la kukidhoofisha chama hicho kwa sababu inaweza kuleta mgawanyiko miongoni mwa wanachama.
Alisema uwezekano wa kutokea kwa mgawanyiko ndani ya chama ni mkubwa, kwa sababu CHADEMA sasa imekuwa ikiangaliwa kwa jicho baya na vyama vingine vya siasa kutokana na mafanikio ambayo kimeyapata kwa muda mfupi.
"Zitto, kama mwanachama wa CHADEMA anayo haki ya kuwania nafasi yoyote ya uongozi ndani ya chama ilimradi ametimiza masharti, lakini uamuzi wake wa sasa ameuchukua wakati mbaya kwa sababu anaweza kutumiwa na maadui wa chama kukidhoofisha," alisema mwanasiasa huyo.
Mwanasiasa mwingine aliyetoa maoni yake kuhusu uchaguzi huo, ni kiongozi wa kambi ya upinzani bungeni, Hamad Rashid Mohamed, ambaye alieleza kuwa kujitokeza kwa Zitto kuchuana na Mbowe kuwania nafasi ya Mwenyekiti wa Taifa wa CHADEMA, ni dalili za kukomaa kwa demokrasia ndani ya chama hicho.
Hamad, ambaye pia ni Mbunge wa Wawi (CUF), alisema kujitokeza kwa wanasiasa wenye majina makubwa kuchuana kuwania nafasi ya kuiongoza CHADEMA, kunaonyesha jinsi demokrasia ilivyopea ndani ya chama hicho ingawa pia ni dalili za wazi za wanachama kutokubaliana na uongozi uliopo.
"CHADEMA wanaonyesha jinsi demokrasia ilivyopea ndani ya chama chao, lakini pia, unapoona mtendaji wa ngazi ya juu ndani ya chama anajitokeza kugombea nafasi inayoshikiliwa na kiongozi mwenzake, hiyo ni dalili ya wazi ya kutoridhishwa na uongozi uliopo.
"Hivyo, ingawa Zitto yupo sahihi, lakini hatua yake hiyo inaonyesha wazi kuwa anataka mabadiliko katika uongozi wa juu kwa kuwa haridhiki na jambo fulani," alisema Hamad.
Aidha, aliufananisha uchaguzi huo wa CHADEMA na ule wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) ambapo wanachama wake hujitokeza kwa wingi kuwania nafasi mbalimbali za uongozi, zikiwemo zile za ngazi za juu, lakini anapopatikana mshindi hurejea kuwa kitu kimoja.
Alisisitiza kuwa, chama chake na kambi nzima ya upinzani, vitakuwa tayari kushirikiana na kiongozi yeyote atakayechaguliwa kukiongoza chama hicho, kwa sababu ndiye atakuwa chaguo la wana CHADEMA.
Kwa upande wake, wakili wa kujitegemea na mmoja wa waanzilishi wa mageuzi hapa nchini, Mabere Marando, alieleza kuwa haoni tatizo kwa Zitto kujitokeza kuchuana na Mbowe kuwania nafasi ya juu ya uongozi ndani ya chama, kwa sababu demokrasia ndani ya vyama vya siasa inaelekeza hivyo.
"CHADEMA wanaonyesha jinsi demokrasia ilivyokomaa ndani ya chama chao, anapojitokeza mwanachama kumpinga kiongozi aliyepo, ndiyo kukomaa kwa demokrasia. Hapo atakayeshinda inajulikana ndiye anayependwa na wanachama, hivyo anakuwa na uhalali usio na shaka wa kuongoza," alisema Marando.
Kwa upande wake, Ndimara Tegambwage, mmoja wa wanasiasa wa mwanzo kujiunga na vyama vya siasa vya upinzani, alisema kujitokeza kwa Zitto kuchuana na Mbowe, kunaonyesha kuwepo kwa fursa ya kila mwanachama kugombea nafasi ya uongozi.
"CHADEMA wameonyesha kuwa wana uhuru, sioni kama hilo litaleta mgogoro, ilimradi mipango na taratibu zao za uchaguzi ndani ya chama zinafuatwa," alisema Ndimara.
Wakati huo huo, Katibu Mkuu wa CHADEMA, Dk. Willbrod Slaa, amesema licha ya baadhi ya wanachama wa chama chao waliojitokeza kuwania nafasi mbalimbali za uongozi kupokea vitisho kutoka kwa baadhi ya wanasiasa walio nje ya chama hicho, ya kuwataka kuondoa majina yao, hakuna mwanachama aliyetishika.
Akizungumza na waandishi wa habari jana makao makuu ya chama hicho, Dk. Slaa alisema uchaguzi huo unaangaliwa kwa namna tofauti tofauti na watu wa aina mbalimbali wakiwemo wanaoitakia mabaya CHADEMA.
Hata hivyo, hakuweka wazi vitisho vinavyotolewa kwa baadhi ya wagombea.
Alisema mchakato wa uchaguzi unaendelea vizuri ambapo watu wenye nafasi tofauti katika jamii wamejitokeza kugombea ngazi mbalimbali.
Aliyataja matabaka ya watu hao kuwa ni pamoja na wasomi na wafanyabiashara.
"Watu wanaogombea wamekuwa wengi sana, na hii ni faraja kwetu kwani inakuza demokrasia na inaonyesha kuwa Watanzania sasa wanazijua haki zao za kikatiba za kuchagua na kuchaguliwa," alisema Dk. Slaa.
Akizungumzia mchuano wa nafasi ya uenyekiti, alisema hadi jana wanachama waliochukua na kurudisha fomu za kuwania nafasi hiyo ni wawili aliowataja kuwa ni Mbowe na Zitto.
Hata hivyo, alieleza kuwa huenda idadi ya wagombea wa nafasi hiyo ikaongezeka baada ya kupokea fomu za wanachama wa mikoani walioomba kuwania nafasi za uongozi.
Kuhusu wagombea wa nafasi ya makamu mwenyekiti kwa upande wa Bara, Dk. Slaa alisema inawaniwa na wanachama watatu aliowataja kuwa ni Profesa Mwesiga Baregu, Anna Maulida Komu na Said Arfi.
Alisema CHADEMA kimeongeza vyombo vitatu ndani ya chama hicho ambavyo viongozi wake watapigiwa kura, na alivitaja kuwa ni Baraza la Wanawake (Bawacha) ambapo wamejitokeza wagombea 33, Baraza la Vijana (Bavicha) ambalo nafasi zake zinawania na vijana 33 na baraza la wazee lenye wagombea 13.
Dk. Slaa alizungumzia pia mikoa ambayo imezuiliwa kufanya uchaguzi ngazi ya mkoa kutokana na dosari mbalimbali ikiwemo mikoa ya Mbeya, Mara na Arusha ambayo imebainika rushwa kutumika na kutotimiza vigezo vya kufanya uchaguzi.
Katika hatua nyingine, aliyekuwa Katibu Mwenezi Taifa wa chama cha NCCR- Mageuzi, Joseph Selasini, jana alijiunga na CHADEMA na kukabidhiwa kadi ya uanachama na Dk. Slaa. Akizungumza baada ya kukabidhiwa kadi, Selasini alisema ameamua kujiunga CHADEMA baada ya kuona kuwa kinajali demokrasia na uhuru wa kweli.