Haya ni majibu yangu kwa Dk. Kitilya Mkumbo.
Wakati mwingine unaweza ukajiuliza hivi hizi PhD huwa zinatolewa kwa watu wenye uwezo kiasi gani, hasa unapokutana na wasomi wa ajabu ajabu. Siwezi kuamini kwamba miaka mingi baada ya kumaliza Chuo Kikuu cha Dar es Salaam hadi leo hii Daktari wa Falsafa ndugu yangu Kitilya ambaye amehamahama vyama kadhaa vya siasa akizungumzia suala la itikadi au falsafa. Huu ni mzaha wa hatari kwa msomi.
Kitilya amepata kuwa kada wa CCM na amepata kuwa Chadema pia ambako yuko sasa. Inavyoonekana huyu jamaa ni mtu anayefanya mambo yake pasipo kuongozwa na falsafa yoyote, ingawa yeye mwenyewe anapata jeuri ya kuwaonyesha wenzake njia kuhusu masuala yanayohusu falsafa.
Kumbe wewe si msomaji mzuri wa makala za Jenerali Ulimwengu ambaye umemtaja hapo juu. Siku zote Jenerali amekuwa akiwalalamikia ninyi wanasiasa kwamba mmepoteza mwelekeo kwa sababu mnaongozwa na matakwa ya kimadaraka na fursa za kimaslahi mnapoenda katika vyama vya siasa badala ya itikadi.
Ni jambo la kusikitisha kwamba kumbe wewe na Zitto Kabwe mliamua kujiunga na Chadema (mwenzako alijiunga akiwa na miaka 16 akiwa hajafikia umri wa kupiga kura au wa kuwa na maamuzi ya busara) mkiwa na lengo la kuitikisa hata itikadi ya chama hicho? Kwa hiyo mlijiunga na Chadema kwa sababu mlikuwa na fursa ya kufanya hivyo au kwa sababu mlivutiwa na haiba binafsi ya wazee wa chama hicho kama akina Mtei na wengine hata kabla hamjasoma katiba na itikadi za chama mnachotaka kujiunga nacho. Zinakwenda wapi siasa za nchi yetu ambazo kumbe hazina dira?
Katika hili la Itikadi na Falsafa naweza nikasema wazi kabisa kwamba kumbe Kitilya na Zitto ni 'mamluki ndani ya Chadema' na kwa hakika wanapaswa kuanza kuchunguzwa mienendo yao ili isije ikawa ni mapandikizi hatari katika chama. Future will Tell.
Nayatambua mabadiliko si ya kiitikadi bali ya kimtazamo na kisera ya vyama vya Democratic, Labour (New Labour), Republicans na vingine vingi kikiwapo Chama Cha Kikomunisti cha China. Nimesoma kwa ufasaha Thatcherism na Reaganism. Ni mwanafunzi mzuri wa falsafa za Hegel, Lenin, Karl Marx na wanazuoni wengi. Nimesoma ujamaa wa Nyerere na The Fabian Socialism aliko copy ujamaa wake na namna alivyoukarabati kutoka katika ukomunisti na Ufabian akirejea misingi ya ujima na kuiboresha. Mimi ni mwanafunzi mzuri wa Historia kwa level yangu.
Nakushauri Dakta Kitilya kwamba ni makosa kuangalia jina la chama na kuvutiwa nalo kabla haujasoma itikadi ya msingi ya chama husika. Kosa hili ndilo lililokufanya katika utu uzima uhame mara CCM mara Chadema na ukaondoka baada ya kukosa madaraka (Lilikupata ukiwa UVCCM). Hii ni fedheha ya kisiasa ambayo tunaivumilia kwa sababu tu ya uchanga wa demokrasia wetu.
Viongozi wa chama kimoja cha siasa wanaweza kutofautiana katika mitazamo, sera, mbinu na mipango na si katika itikadi. Haiwezekani mjamaa na bepari, mmoja akawa mwenyekiti na mwingine Naibu Katibu Mkuu ndani ya chama kimoja. Huu ni upofu ambao ndiyo msingi mkuu uliosababisha Zitto Kabwe kwa ushauri wako wewe na vijana wengine kadhaa niliowaita wajinga ndani ya Chadema aamue kugombea kwa staili hii ya kakakuona.
Napenda tu kukueleza dakta kwamba falsafa ya kimantiki inayoniongoza katika uandishi wangu siku zote ni 'ukweli kwanza'. Journalism haina ya leo imepita zama za cold war, kwa hiyo katika masuala kadhaa hakuna leftist writers au rightist writers kama unavyotaka iwe.
Ni kweli kwamba siku zote nimekuwa nikimuona Zitto kuwa ni hero wangu. Ukweli huo hautabadilika bado itabakia pale pale kwamba japo nimempinga kwa hili kama nilivyopata kumpinga kwa mengi tu, ninamheshimu.
Muulize Zitto atakueleza, hii ni makala ya pili au ya tatu kumkosoa (si kumshambulia), nimepata kufanya hivi huko nyuma kupitia safu yangu ya kawaida ya Tuendako kila Jumatano. Nimepata kumkosoa mara nyingi katika mazungumzo ya ana kwa ana au ujumbe wa simu ya mkononi ama yeye mwenyewe au kupitia kwa watu wake wa karibu na mara kadhaa kupitia kwa mama yake mzazi.
Kwa sababu hiyo basi, mimi si kasuku ambaye Zitto akiimba wimbo hata kama wimbo huo ni wa matusi nicheze eti kwa sababu Zitto ni hero wangu. Nitakuwa mpumbavu sana. Na hakika wenye mawazo ya namna hiyo ni watu wa kuwasikitikia.
Nimepata kumpinga Mbowe pia katika makala zangu nyingi na Zitto Kabwe na wengine ambao wamekuwa wakisoma makala zangu wanalitambua hilo.
Kimsingi nilikuwa nikisubiri nikuone ukichangia na nilipoona uko kimya zaidi ya kutuma ujumbe mmoja tu wa kunikejeli ukinitaka nichukue fomu ya kugombea, niliamua kuingia na kuwapa darasa baadhi ya vijana wajinga ndani ya Chadema kama wewe, ambao kwa sababu ya upofu wenu mmeamua kumfanya Zitto ngazi ya mafanikio yenu ili akipata nafasi ya uenyekiti ambao kwenu mmeufanya ni ulaji, aweze kuwateua kushika nafasi za juu. Huku ni kumuangusha Zitto sana.
Napenda niliweke hili wazi kwamba, siupingi hata kidogo uamuzi wa Zitto kugombea uenyekiti wa Chadema. Ninachokipinga ni timing yake na kimsingi utaratibu alioutumia kugombea kiti hicho ambao gazeti ninaloliongoza limeuita 'kakakuona'.
Nimeshangazwa na kushtushwa na uamuzi wa Zitto kuingia mitini na akachukua fomu 'mafichoni' na akairejesha kupitia kwa Msafiri Mtemelwa. Huu si ujasiri wa kiuongozi ambao Zitto alipaswa kuwa nao.
Staili hii ya Zitto ambaye anapokuwa Dar es Salaam anafanya vikao vya usiku na mchana na wanahabari (nikiwamo mimi) na wanasiasa wengine wa CCM na CUF huku akikataa kukutana na viongozi wenzake wa Chadema wakiwamo wakuu wake kama Mbowe na Dk. Slaa ni wa kusikitisha kama si wa kukemewa.
Mimi ni mwana habari, ninazijua hisia za viongozi wengine wa Chadema ambao ni watu makini kabisa kama Dk. Slaa, John Mnyika na John Mrema juu ya mwenendo huo wa Zitto. Hawa jamaa wote pamoja na kutambua uwezo mkubwa wa kuona mambo alionao kijana mwenzao huyo wanaujua udhaifu wake kama kiongozi (si kama Zitto)> Naamini wameamua kukaa kimya wakiogopa kukijeruhi chama chao. Mimi sina sababu ya kukaa kimya ni wajibu wangu kuandika hata kama nitapingwa na maelfu. Msome Ibsen 'The strongest man is the one who stands alone'
Ni kweli kwamba mimi ni judgemental. Inaonekana unaliogopa neno anguko ambalo ni linafafana na la Kiingereza la 'fall' ambalo ni la kawaida katika vyombo vya habari duniani kote.
Si kweli kwamba nimekuwa cynical au sadist. Hata hivyo ni kweli nimekuwa judgemental. Huo ni wajibu wangu kama Mhariri Mtendaji. Ninao wajibu wa kusimamia sera ya gazeti na kuonyesha njia. Unatumia maneno poor and unprofessional katika hoja ambazo wewe mwenyewe unaonekana dhahiri kuubeba udhaifu huo.
Mtu anaweza akaanguka na akasimama. Anguko si kifo, ni pigo la kipindi fulani na si la milele. Nashangaa wewe na Zitto mnafanya spinning kupitia JF ili kutimiza malengo yenu ya kisiasa ambayo kwa mtazamo wangu ni ya hatari (Nasisitiza huu ni mtazamo wangu).
Sipendi kujisifu, ninayo rekodi ya kuyaona matukio mengi na makubwa ya kisiasa kwa miaka mingi kabla hayajatokea. Waulizeni wanasiasa waliowatangulia ambao baadhi yao walipuuza maandishi yangu kwa matusi na kejeli kabla ya kufikwa na mianguko ya namna hii hii ambayo naiona inataka kumpata rafiki yangu na mwanasiasa ninayemuunga mkono siku zote; Zitto Kabwe.
Hata hivyo, yako mambo mengi tu ambayo nimepata kuyaandika kwa makosa na hayakutokea kama nilivyotafakari. Makosa kama haya wamepata kufanya wanazuoni na wachambuzi mbalimbali duniani. Inapotokea hali ya namna hiyo nimekuwa mwepesi siku zote kuomba radhi na kusonga mbele.
Nimemlinganisha Zitto na Mbatia kwa minajili ya kubeba ajenda ya vijana na kwa taarirfa yako, ulinganifu huu aliuanzisha huyo mgombea wako Zitto ambaye kwa maneno yake mwenyewe alipata kuniambia kuwa anasita kugombea ili asije akakiporomosha chama na kukizika kama alivyofanya Mbatia.
Kwa hiyo scenario niliyoanza nayo ni uchaguzi uliomng'oa Marando (aliyeonekana kapitwa na wakati kama Mbowe kwa mtazamo wenu) na kumpa wadhifa Mbatia (kijana kama Zitto zama hizo) na siyo historia ya misukosuko ya wakati wa Mrema. Nadhani Kitiliya somo la 'Comparative Analysis' linakupa shida sana si kidogo.
Unataka nieleze tatizo la Zitto kugombea ni nini? Nimekujibu kidogo hapo nyuma, lakini nianze kusema, tatizo kubwa la kwanza ni kupokea ushauri mbaya kutoka kwa watu wenye nia mbaya kama wewe na wengine walio ndani na nje ya Chadema. Pili 'timing' yake si sahihi kwake yeye na kwa chama chake, tatu msingi wa kugombea kwake ambao wapambe wake wamekuwa wakisema ni kumuonyesha jeuri Mbowe ambaye eti alikuwa na mpango wa kumng'oa.
Ni wazi kwamba iwapo Mbowe alikuwa akifirikia kumng'oa Zitto ndani ya Chadema basi uamuzi huo ungekuwa ni wa hatari kama ulivyo huu ushindani wao ambao umejengwa katika misingi ya chuki, fitina na uchonganishi.
Pili si kweli kwamba kwa kuandika kwa maana ya ku foresee baadhi ya mambo ya mbele (Dhima ya Safu ya Tuendako) hakumaanishi kuwa na wasiwasi bali kumtakia mema Zitto, Mbowe Chadema na kimsingi demokrasia ya vyama vingi iliyoanza kufufuka baada ya kupwaya kwa muda mrefu.
Nimeandika bayana kuhusu anguko la Zitto na si anguko la Chadema nikijua kwa uhakika kwamba Chadema itabakia imara ingawa Zitto na Mbowe wanaweza kuanguka kutokana na uchaguzi. Soma historia ya chaguzi ndani ya vyama duniani kote na uone iwapo haziandamani na mianguko ya watu.
Zitto anasema anataka kukiandaa chama kuchukua dola, dhana ambayo Mbowe amekuwa akiifanya kwa vitendo tangu akiwa mbunge alipoanzisha ziara za kukijenga chama kwa wabunge, kufanya ziara za kitaifa na baadaye akawaleta vijana wasomi ndani ya chama kabla ya kuja na sera mchanganyiko zilizoifikisha Chadema hapa kilipo leo.
Pili, Chadema inapaswa kuepuka aina yoyote ile ya mtikisiko ambao utawalazimisha viongozi wa juu wa chama hicho kuanza kujipanga upya kuendeleza operesheni mbalimbali za chama hicho. Uamuzi wa Zitto kuingia sasa na kwa staili ya 'kakakuona' inatia shaka sana na kwa hakika kama haitadhibitiwa inaweza ikawa 'break' kwa Chadema.
Hivi Kitilya ukiwa msomi ulitaka waandishi wote tuimbe wimbo wa Goo Zitto, Goo Zitto kama ambavyo wana mtandao walitufanyia kwa Kikwete mwaka 2005? Hivi unadhani umaarufu wa Zitto ni kielelezo tosha cha kuwa na uwezo wa kuongoza? Mbona akina Augustine Mrema na Kikwete wamepata kuwa maarufu wakubwa na leo tunaona matunda yake! Hamlioni hilo? Nilidhani makala yangu ingechukuliwa kama changamoto na si dharau.
Angalia Zitto unaanguka, unaangushwa na akina Kitilya, Kafulila, Umar, Msafiri na wengine wengi. Angalia Zitto, saa yako ya ushindi inakuja ndani ya Chadema na hakuna atakayeweza kukuzuia wakati wako ukifika. Leo hii baadhi yetu tumetuhubutu kwa kuwa tunathamini uwezo wako. There's always tomorrow.