KESI YA MKE WA BILIONEA MSUYA: Mamantilie alivyoshirikishwa gwaride kutambua mshtakiwa

Oldmantz

JF-Expert Member
Jan 24, 2023
430
996
Dar es Salaam. Mkulima kutoka Songea mkoani Ruvuma, Sophia Amir Shemzigo, ameieleza Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam kuwa alikuwa mmoja wa watu walioshiriki katika gwaride la utambuzi wa mshtakiwa wa kwanza, Miriam Steve Mrita katika kesi ya mauaji ya Aneth Msuya.

Mkulima huyo alieleza ushiriki wake katika gwaride hilo, wakati akitoa ushahidi wake mahakamani hapo akiwa shahidi wa 18 wa upande wa mashtaka katika kesi hiyo.

Aneth aliyeuawa Mei 25, 2016 kwa kuchinjwa nyumbani kwake Kibada, Kigamboni, wilayani Temeke, jijini Dar es Salaam, alikuwa mdogo wa aliyekuwa mfanyabiashara tajiri maarufu wa madini mkoani Arusha, marehemu Erasto Msuya, maarufu kama Bilionea Msuya

Washtakiwa katika kesi hiyo ni Miriam Steven Mrita, ambaye ni mshtakiwa wa kwanza na mjane wa Bilionea Msuya aliyeuawa kwa kupigwa risasi eneo la Mijohoroni, wilayani Hai mkoani Kilimanjaro Agosti 7, 2013.

Mwingine ni Revocatus Everist Muyella (mshtakiwa wa pili)
Kesi hiyo namba 103 ya mwaka 2018, inasikilizwa na Jaji Edwin Kakolaki, na washtakiwa wote wanakabiliwa na shtaka moja tu la mauaji wakituhumiwa kuwa ndio waliohusika katikamauaji ya Aneth.

Kwa mujibu wa ushahidi wake alioutoa mahakamani hapo jana akiongozwa na mwendesha mashtaka, Wakili wa Serikali Generose Montana, wakati alipotakiwa kushiriki katika gwaride hilo la utambuzi wa mtuhumiwa, alisema alikuwa akiishi Kurasini Dar es Salaam yeye na mumewe.

Wakati huo alikuwa akijishughulisha na biashara ya kupika na kuuza chakula maarufu kama mamantilie eneo la JKT Mgulani

Katika simulizi ya ushahidi wake alisema kuwa siku ya tukio, Agosti 7, 2016 wakati anatoka kudai madeni yake eneo la Polisi Kilwa Road, aliitwa na askari Polisi kushiriki kwenye gwaride la utambuzi naye akakubali.

Askari huyo alimchukua akampeleka nyuma ya kituo cha Polisi ambako alikutana na wenzake (wanawake wengine) saba na yeye akawa wa nane.

Walipangwa (yeye na wenzake) mstari na askari wa kiume akawaeleza kuwa amewaita kwa kuwa kuna gwaride la utambuzi, kwamba kuna mtuhumiwa wa mauaji anatakiwa kutambuliwa.

"Mtuhumiwa wa jinsia ya kike aliletwa na askari wa kike akaambiwa achague nafasi ya kukaa kwenye ule mstari, naye akachagua kukaa nafasi ya tano kutoka kulia na mimi nilikuwa nafasi ya nne kutoka kushoto na wa sita kutoka kulia", alisema shahidi huyo.

Hivyo pamoja na mtuhumiwa katika mstari huo, walikuwa jumla tisa na wote walikuwa wanafanana, yaani wakiwa weupe, wanene na wenye urefu wa kimo cha kati, si wafupi wala warefu.

Wakiwa mstarini baadaye aliletwa msichana na askari wa kike ambaye aliambiwa apite nyuma na mbele ya gwaride (mstari walikokuwa wamepangwa washiriki wa gwaride hilo) kisha amguse bega mtuhumiwa.

"Huyo msichana aliweza kumgusa bega la kushoto huyo mtuhumiwa, akasema ni huyu ambaye alikuja Kigamboni kwa tajiri yangu, alinitishia bastola na kuniambia niondoke," alisema shahidi huyo.

Baada ya hatua hiyo, askari msimamizi wa gwaride alichukua karatasi akaandika majina yao wote walioshiriki katika gwaride hilo, wakasaini pamoja na mkaguzi wa gwaride, kisha wakaruhusiwa kuondoka na mtuhumiwa alichukuliwa na askari wa kike akarudishwa alikokuwa ametolewa.

Vivyohivyo na yule msichana aliyemtambua mtuhumiwa naye alichukuliwa na askari wa kike akaondoka.

Akiongozwa na mwendesha mashtaka, shahidi huyo alimsogelea mshtakiwa Miriam kisha akaionesha mahakama kwa kumuonyesha kidole kuwa ndiye mtuhumiwa aliyetambuliwa katika gwaride hilo.

Mahojiano na wakili wa mshtakiwa
Baada ya kumaliza ushahidi wake huyo, shahidi huyo alihojiwa maswali mbalimbali ya dodoso na Wakili wa mshtakiwa huyo, Peter Kibatala, katika kupima uthabiti wa ushahidi wake huo.

Kibatala: Alimpatia shahidi fomu aliyosaini baada ya gwaride la utambuzi, kisha akaanza kumuuliza maswali. Shahidi wakati unaongozwa na mwendesha mashtaka kutoa ushahidi hapa ulimwambia Jaji kwamba kwenye hii karatasi kuna namba zako za simu walizotumia kukuita?

Shahidi: Ndio

Kibatala: Ulimwambia Jaji kwamba ulitoa namba zako za simu ili wakikuhitaji (wasimamizi wa gwaride) wakupate?

Shahidi: Sikumwambia

Kibatala: Unajua Kiingereza

Shahidi: Hapana

Kibatala: Ulimwambia Jaji kwamba kabla ya kujaza hii fomu ofisa yule aliyesimamia gwaride la utambuzi alikufafanulia kilichomo?

Shahidi: Sikumwambia

Kibatala: Kwa hiyo hata nikikuonesha hii kwamba hapa wameandika eight, wakasaini hujui?

Shahidi: Mimi sijui Kiingereza

Kibatala: Wakati unajitambulisha umesema unaitwa Sophia Amiri Shemzigo, katika karatasi hii ni wapi Jaji na wazee wa Baraza wakisoma wataona kuna majina ya Sophia Amir Shemzigo?

Shahidi: Sophia Amir

Kibatala: Kuna Shemzigo hapo?

Shahidi: Hakuna

Kibatala: Wakati unatambulishwa ulimwambia Jaji kuwa hapa naona Sophia Amir lakini Sophia Amiri Shemzigo ni mtu mmoja yuleyule?

Shahidi: Sikumwambia

Kibatala: Shahidi wewe si mwanasheria wala polisi lakini kuna masharti ya lazima katika hili zoezi (gwaride la utambuzi). Ulimwambia Jaji kuwa wakati wa utambuzi huyu mtuhumiwa hakuwa na pingu?

Shahidi: Sikumwambia

Kibatala: Ulimwambia Jaji kuwa yule mama aliyetambuliwa alikuwa hana alama yoyote, hajavimba au kichubuka usoni?

Shahidi: Sikumwambia

Kibatala: Ulimwambia Jaji kwamba wewe huna uhusiano wowote na ofisa wa polisi hata wa kindoa?

Shahidi: Sikumwambia

Kibatala: Ulimwambia Jaji kwamba wewe hauna huba husuda na huyu dada?

Shahidi: Sijamwambia
Kibatala: Ulimwambia Jaji kwamba wewe ulikuwa humfahamu huyu mshtakiwa?

Shahidi: Sijamwambia

Kibatala: Shahidi, hii kesi umekuwa reported sana, ulimwambia Jaji kwamba utambuzi wangu (wake shahidi kwa mshtakiwa mahakamani ) hauhusiani na kuona picha yake kwenye magazeti?

Shahidi: Sikumwambia

Kibatala: Shahidi ulimwambia Jaji wale maafisa wa ukaguzi walimpa nafasi mtuhumiwa kumkataa yeyote pale?

Shahidi: Sikumwambia

Kibatala: Shahidi umesema tu binti aliyekuja alisema maneno kwamba huyu ndiye ambaye alikuja kwa tajiri yangu, alinitishia bastola na kuniambia niondoke, ni sahihi?

Shahidi: Ehee

Kibatala: Mwambie Jaji kama ulimsikia (hiyo binti) akitaja tarehe na mwaka (ambayo huyo mtuhumiwa alikwenda Kwa huyo bosi wake)

Shahidi: Hakutaja tarehe

Kibatala: Ulimsikia huyo dada akisema kuwa huyu namfahamu kwa sababu nilishawahi kumuona Mererani?

Shahidi: Anacheka

Kibatala: Mbona unacheka?

Shahidi: Sikumsikia.

Baada ya maswali hayo machache ya dodoso kutoka kwa Wakili Kibatala, Kiongozi wa jopo la waendesha mashtaka, Wakili wa Serikali Mwandamizi, Paul Kimweri, alimuuliza tena shahidi maswali ya kumuongoza kutoa ufafanuzi wa baadhi ya majibu aliyoyatoa wakati akihojiwa na Wakili Kibatala.

Wakili Kimwei: Shahidi umeulizwa kuhusiana na majina yako, hebu soma hiyo karatasi majina yako yaliyoandikwa ni yapi?

Shahidi: Sijakuelewa

Wakili: Majina yako ni nani?

Shahidi: Sophia Amir

Wakili: Jina lako la tatu ni lipi?

Shahidi: Shemzigo

Wakili: Wakili (Kibatala) amekuuliza kama unajua Kiingereza ukasema hujui, pamoja na kutokujua Kiingereza ukiangalia hapo jina lako unaliona?

Shahidi: Naliona

Wakili: Umeulizwa kuhusu kumtambua mshtakiwa kwenye vyombo vya habari . Kwa mara ya kwanza ulimtambua wapi?

Shahidi: Nilimtambua kwenye gwaride

Wakili: Sasa ieleze Mahakama iwapo hapa mahakamani umemtambua?

Shahidi: Nimemtambua

Wakili: Sasa Wakili amekuuliza kwamba yawezekana labda wewe una chuki, huba.

Kibatala: Sijamuuliza kuwa ana chuki nimemuuliiza kama alimwambia Jaji kwamba hana chuki, huba.

Baada ya Wakili Kibatala kupinga swali hilo, Wakili Kimweri alibadili swali na sasa akamtaka shahidi aelezee ni kwa nini hana chuki na mshtakiwa ambalo pia wakili Kibatala alipinga na Wakili Kimweri akamaliza maswali yake.

Jaji Kakolaki aliahirisha kesi hiyo mpaka leo itakapoendelea

CREDIT:MWANANCHI
 
Back
Top Bottom