Sky Eclat
JF-Expert Member
- Oct 17, 2012
- 57,595
- 215,272
=====
Dar es Salaam. Katibu Mkuu mpya wa Chadema, John Mnyika ameanisha vipaumbele vitano vya chama hicho kikuu cha upinzani nchini Tanzania kuelekea uchaguzi mkuu wa mwaka 2020.
Mnyika aliyeteuliwa na mwenyekiti wa chama hicho, Freeman Mbowe kuwa katibu mkuu Desemba 20, 2019 kuchukua nafasi ya Dk Vicent Mashinji ameeleza hayo leo Jumapili Desemba 22, 2019 katika mkutano wake na waandishi wa habari.
Amesema vipaumbele hivyo ni kudai tume huru ya uchaguzi, maandalizi ya wagombea kuelekea uchaguzi mkuu, ilani ya uchaguzi ya chama hicho na kuendeleza sera ya Chadema msingi na Chadema Digital.
Huku akiwashukuru wanachama waliopokea vyema uteuzi wake, mbunge huyo wa Kibamba amesema, “kazi kubwa ya chama cha siasa ni kushika dola, hili ndio lipo mbele yetu kwenye uchaguzi wa mwakani. Katika mkakati huu tumekuja na vipaumbele hivi vitano ambavyo vikitekelezwa kwa ufanisi Watanzania watarajie mabadiliko.”
Mnyika ametumia mkutano huo kumtaka Waziri wa Mambo ya Ndani, Kangi Lugola na Inspekta Jenerali wa Polisi (IGP), Simon Sirro kueleza alipo ofisa wa kitengo cha elimu kwa umma wa Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC), Tito Magoti anayeshikiliwa na polisi.
Licha ya Kamanda wa Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam, Lazaro Mambosasa kusema kuwa polisi wanamshikilia ofisa huyo, hajasema anashikiliwa kituo gani jambo linalolalamikiwa na uongozi wa kituo hicho.
Chanzo: Mwananchi