WAZIRI MKUMBO ATEMBELEA KIWAANDA CHA KELIN WOOD EAST AFRICAN, AONYESHA KURIDHIKA NA UWEKEZAJI MKOANI NJOMBE
Waziri wa Uwekezaji, Viwanda na Biashara, Mhe. Prof. Kitila Mkumbo,alipata fursa ya kutembelea kiwanda cha KELIN WOOD EAST AFRICAN kilichopo mkoani Njombe halmashauri ya Wilaya ya Njombe na kujionea mwenyewe uwekezaji mkubwa unaofanywa katika kuongeza thamani ya mazao ya misitu. Ziara hiyo ilifanyika tarehe 24 Machi, 2025, akiwa ameambatana na Mkuu wa Mkoa wa Njombe, Mhe. Anthony Mtaka.
Akizungumza baada ya kutembelea kiwanda hicho, Mhe. Prof. Mkumbo alielezea kuridhika kwake na juhudi za kiwanda hicho katika kuongeza thamani ya mazao ya miti, ikiwemo uzalishaji wa bidhaa kama Ringboard na Siljng board. Waziri alisisitiza kuwa uwekezaji huu unachangia kwa kiasi kikubwa katika kukuza uchumi wa mkoa na kutoa ajira kwa vijana, hasa katika maeneo ya vijijini.
"Tunashuhudia Njombe ya viwanda sasa, na hii ni alama kubwa sana ya maendeleo. Uwekezaji huu umefungua milango ya ajira kwa vijana wetu na kuinua uchumi wa wakulima. Ni mfano mzuri wa namna ambavyo mazingira rafiki ya uwekezaji yanavyoweza kuleta maendeleo ya haraka," alisema Prof. Mkumbo.
Mhe. Prof. Mkumbo pia aliongeza kuwa serikali itaendelea kuwekeza katika miundombinu na sera zinazohamasisha uwekezaji katika viwanda vya ndani, akielezea furaha yake kwa kuona kiwanda cha KELIN WOOD EAST AFRICAN kikiendeleza uzalishaji wa bidhaa zenye manufaa kwa uchumi wa mkoa na taifa kwa ujumla.