JIINI LA DARAJA LA SALENDA........EP.46.
"Muddy nipo hapa toka saa tano usiku baridi lote limeniishia nikijua haupo mbali, kumbe umekwenda kwa wanawake zako," Balkis alijiliza kiuongo.
"Nisamehe Ba..Ba..lkis," Muddy alijitetea baada ya kujua kuwa ameumbuka.
"Niambie ukweli ulikuwa wapi?"
"Nilikufuata kwenu."
"Kufanya nini, wakati niliondoa kwako hukuniambia kitu?"
"Nililipenda jumba lenu nilitaka kuliona kwa macho yangu nikiwa kwa nje."
"Si ungenieleza unataka kupajua kwetu ili nikupeleke kuliko kunichunguza au huniamini?"
"Nakuamini lakini basi tu, yaani nimechanganyikiwa, jumba kama lile sikuwahi kuliona hata mchana huwa silioni maeneo yale."
"Narudia tena, kwa nini usiniulize jumba letu lilipo? unaweza kulitafuta mwaka mzima na usilione."
"Naomba unisamehe kwa yote yaliyojitokeza."
"Muddy nilishakusamehe tangu siku ya kwanza nilipokuona ukipasuliwa moyo wako kwa kisu butu bila ya ganzi na mkeo wa bandia, niliamini mtupo uliotupwa haukujua ungeangukia wapi na muanguko wako ungekuwa mkubwa sana na usingesimama tena."
"Nashukuru Balkis kwa kuyaokoa maisha yangu, nisamehe kwa yote, siyo kwamba sikuamini la hasha, bali nilipenda kuuona utukufu wa utajiri wa familia yako. Bado nipo njia panda kujiuliza jumba zuri kama lile limejengwa lini maeneo yale."
"Maeneo gani?"
"Si pale pembeni ya njia panda ya kuelekea Masaki."
"Nataka nikutaadharishe kitu kimoja, yaani usije tena maeneo yale kwani baba yangu akikuona anaweza hata kukutoa uhai."
"Atanijuaje?"
"Mbona anakujua, aliponiuliza nilimdanganya, sasa kama atakuona tena maeneo yale lazima atajua namdanganya na atakufanyia kitu kibaya."
"Je, akinikuta kwenu?"
"Kwa sasa baba yupo, hivyo hutuwezi kwenda tena mpaka tutakapooana."
"Kwa hiyo utakuwa unakuja kulala hapa?"
"Ndiyo maana yake."
"Si umesema nyumba hii itapigwa bei itakuwaje?"
"Usiwe na wasiwasi kila kitu niachie mimi, ukitoka mahakamani nitakupeleka kwenye nyumba yako mpya."
"Nitashukuru mpenzi wangu."
Balkis baada ya kuingia ndani aliisikia nyumba ukinuka sana, aliogopa kusema kwa kuhofia kumuudhi mpenzi wake. Alitafuta mbinu ya kumuondoa Muddy ili afanye usafi ndani mle.
Alimtuma kitu ambacho alijua hawezi kukipata karibu, alijua nafasi ile ingempa fursa ya kuwaita wajakazi wake kufanya usafi kwa muda mfupi. Alimuomba samahani kabla ya kumtuma:
"Samahani mpenzi wangu."
"Bila samahani."
"Najua umechoka lakini naomba nikutume kitu."
"Nitume tu mpenzi wangu."
"Kwa vile nataka kufanya usafi, naomba kaninunulie udi sehal"
"Upo sehemu gani?" "Kwenye maduka wanayouza manukato utaupata."
"Hakuna tatizo wacha niwahi."
"Nioneshe ufagio."
Baada ya kumpa ufagio Muddy alitaka kuondoka na gari lakini Balkis alimkataza alijua akitembea kwa miguu atachukua muda mrefu kurudi kuliko akitumia gari.
"Unaweza kuupata karibu wala usitumie gari."
"Hakuna tatizo."
Muddy aliondoka na kumwacha Balkis akijifanya anafagia, baada ya kuondoka tu, aliacha kufagia na kujishika kwenye paji lake la uso. Haikuchukua sekunde wajakazi kumi walikuwa mbele yake wakiwa wamepiga magoti.
"Rabeka mwana wa mfalme una shida gani?" Waliuliza kwa pamoja.
"Nataka mfanye usafi wa nyumba yote, sitaki kusikia harufu mbaya kama hii."
Mara moja wajakazi walianza kusafisha nyumba nzima, ilikuwa ajabu waliondoka vitu vyote vya ndani na kuviweka vipya na vyenye thamani kwa muda mfupi, ndani pakabadilika, pakapendeza na kuvutia kila kona ya nyumba ilinukia kwa harufu nzuri.
Muddy alijikuta akitembea umbali mrefu kutafuta udi sehal, kila alipouliza watu hawakuujua. Alijikuta akikata tamaa na kuamua kurudi kumweleza Balkis kuwa udi wenye jina hilo kila alipouliza watu hawakuujua. Kutokana na kwenda umbali mrefu ilibidi wakati wa kurudi apande gari, jasho likimvuja kwa kutembea.
Alipofika nyumbani aliingia ndani lakini alishtuka kukuta nyumba yake ikiwa imebadilika na kupendeza sana, aliviona vitu tofauti kiasi cha kuamini kuwa alikuwa amekosea, hakukuwa kwake. Alitoka nje ili akaitafute nyumba yake lakini mlangoni alikutana na Balkis akiwa amebeba siagi na jam.
"Vipi mpenzi mbona nimekuona umeingia na unatoka?"
"Ha! Hapa ni kwangu?" Alishtuka.
"Eeh! Kwako, kwani vipi?"
"Umefanya usafi mkubwa hivi kwa muda gani?""Usinione nipo hivi mimi ni mwanamke wa shoka."
"Na mbona kuna vitu vipya?"
"Sasa kipi cha ajabu, yote haya nimeyapanga kwa muda mrefu, nilipokuwa nakuja kulala hapa. Nilimtuma mtu avilete vitu hivi, wakati unaondoka vilikuwa vinaingia."
"Sasa nyumba ikiuzwa?"
"Achana na wazo hilo hebu nenda kaoge ufungue kinywa."
Muddy hakujibu kitu alichukua taulo na kwenda kuoga, nyumba ilikuwa ikinukia kama ujinini kwa akina Balkis. Muddy alipotoka kuoga alikuta chai imeshatayarishwa juu ya meza, ilikuwa tamu ambayo Muddy aliwahi kuinywa nyumbani kwa akina Balkis tu.
Pamoja na kuisifia chai lakini Muddy kila alipomuangalia Balkis moyo wake haukuamini kama alikuwa na mwanamke mzuri kama yule tena tajiri mwenye mapenzi ya dhati kwake.
JIINI LA DARAJA LA SALENDA........EP.47.
"Muddy nihakikishie kuwa huwezi kurudiana na Ashura?"
"Nakuhakikishia kukupenda siku zote na kamwe sitarudiana na yule mwanamke muuaji." "Muddy unayosema yanatoka moyoni au mdomoni?"
"Yanatoka moyoni mwangu?"
"Ukinigeuka?"
"Nifanye lolote."
"Muddy kama unayosema ni kweli basi kitu nilichotaka kukifanya naachana nacho."
"Kipi hicho?"
"Nilitaka kusimamia kesi yako kuhakikisha hawachukui kitu chochote."
"Kwa nini usifanye hivyo?"
"Naacha ili maisha yako yakiwa mazuri mtu yeyote asikuguse."
"Kwa hiyo nitakuwa na maisha mazuri zaidi ya haya?" Muddy aliuliza.
"Mara kumi ya haya."
"Usiniambie!"
"Kwangu fedha si tatizo, ninachokitaka kutoka kwako ni mapenzi ya kweli, sihitaji kitu kingine."
"Nakuahidi utayapata hapa."
"Basi tegemea kuishi maisha ya raha mpaka kufa kwako."
"Asante mpenzi wangu," Muddy alisema huku akimkumbatia Balkis.
***
Muda ulipofika Muddy aliitwa mahakamani na hukumu ilikuwa ile ile ya kugawana mali. Kwa vile alishaelezwa na Balkis maisha yake baada ya hukumu, hakuchanganyikiwa baada ya kuelezwa yale. Baada ya hukumu ile, Muddy pia alitakiwa kumlipa fidia ya fedha ambayo ilimfanya asipate kitu katika mali zitakazouzwa, vikiwemo gari na nyumba.
Ashura alishangaa kumuona Muddy pamoja na pigo zito yupo katika hali ya kawaida. Baada ya hukumu Muddy alitoka nje ya mahakama na kwenda moja kwa moja kwa Balkis aliyekuwa akimsubiri. Muddy alishtuka kumuona Balkis akiwa pembeni ya gari la kifahari.
"Karibu mpenzi."
"Asante."
"Pole na masaibu yote."
"Asante," walikumbatiana, kitendo kile hakuna aliyekiona zaidi ya Muddy peke yake.
"Nina imani mambo yamekwenda kama nilivyokueleza?"
"Yaani umekuwa kama wewe ndiye uliyeyapanga yote, hakuna hata kimoja kilichokwenda kinyume."
"Basi huyo ndiye Ashura ambaye pia hilo si jina lake halisi."
"Una maana gani kusema hivyo?"
"Nitakueleza, kila mwanaume aliyemchezea mchezo huu anamjua kwa jina hili lakini jina halisi anaitwa Shuuna."
"Ina maana hata hayo majina aliyotumia kwa hao mabwana wa awali unayajua?"
"Nayajua."
"Alikuwa anaitwa nani?"
"Twende kwanza nyumbani ukapumzike, mengine tutazungumza tukifika."
Muddy aliingia kwenye gari na kuondoka, kabla ya kuingia kwenye gari Ashura alishtuka kumuona Muddy na mwanamke mrembo aliyejitambulisha kuwa ndiye mkewe siku aliyokwenda kwake kumuonya.
Alijikuta akikosa raha na kujiona wamefanya kazi bure sawa na kutwanga maji kwenye kinu. Waliona kama hawakufanya kitu na kujikuta akimuuliza mwanaume wake.
"Yule mwanamke mwenye fedha Muddy kamtoa wapi?" Ashura aliuliza.
"Hata mimi nashangaa, ni wazi wameanza uhusiano kipindi mkiwa wote."
"Ndiyo maana hata ilipotolewa hukumu hakushtuka."
"Hata mimi nilishangaa kuona anakubali kila kitu."
"Kwa hiyo tutakuwa tumefeli?"
"Hapana, hatujafeli kwani tulivyovitaka tumevipata, ila kuna biashara nyingine nzuri," mwanaume wa Ashura alisema.
"Biashara gani?"
"Tukafungue mashitaka ya kudai kuhujumiwa penzi lako lililosababisha muachane na mumeo wakati bado unampenda."
"Aisee, wazo zuri sana! Kweli wewe bwana mipango, sasa mpango huo tuufanye lini?"
"Kwanza tupajue wanapoishi ili tufanye mpango wa kufungua mashitaka."
"Hilo wazo, mbona mwaka huu tutatengeneza fedha mpaka zitukimbie."
"Hiyo ndiyo kazi yetu."
"Lakini Mussa kuna jambo nimekumbuka."
"Jambo gani hilo?"
"Unakumbuka yule mwanamke alivyotuonya kuhusu tabia yetu kuwa itatutokea puani?"
"Sasa wewe unamuogopa, atatufanya nini mwanamke yule?"
"Mmh! Nashangaa moyo unanienda mbio nilipomkumbuka."
"Si kwa vile amekuchukulia mumeo."
"Yule si mume wangu nilikuwa naye kibiashara zaidi."
"Basi mpango wa haraka ni kudili na Muddy kuhakikisha anaokota makopo."
JIINI LA DARAJA LA SALENDA........EP.48.
Wakati wakipanga kuchukua fedha za Balkis, muda huo Muddy alikuwa akikaribishwa kwenye jumba la kifahari.
"Karibu mpenzi wangu hapa ndipo kwako ishi kwa furaha na mapenzi ya kweli," Balkis alimkaribisha kwa sauti tamu.
"Ha! Siamini."
"Hata lile gari ni lako."
"Usiniambie!" Muddy alizidi kupigwa na butwaa.
"Ukweli ni huo, leo usiku kutakuwa na sherehe fupi ya kufunga ndoa yetu ili uweze kunitumia kihalali kama mkeo."
"Hakuna tatizo, asante sana mpenzi."
Muddy alishukuru kwa kupiga magoti huku machozi yakimtoka na kujiuliza bila ya Balkis maisha yake yangekuwaje baada ya kufanyiwa utapeli na Ashura.
****
Ashura na mwanaume wake baada ya kutoka mahakamani waliongozana na madalali kwenda kuuza mali za Muddy zikiwemo gari na nyumba siku ile ile, kutokana na mipango iliyopangwa mapema. Baada ya kufanikiwa kuuza gari na nyumba waliendelea kufurahia mafanikio yao kufuatia kazi yao ya utapeli na kujipanga kwa ajili ya kupambana na Balkis kuhakikisha wanapata fedha kupitia kwa Muddy.
Pamoja na kupata vitu walivyovitaka kutoka kwa Muddy, bado Ashura moyo wake ulikosa raha, alijiuliza atamtazamaje Muddy siku wakikutana kutokana kuonekana ameingia kwenye maisha mazuri tofauti na awali walipokuwa pamoja.
Baada ya kumuacha Muddy na kuonesha kuchanganyikiwa, alitegemea kusikia amejinyonga. Kufuatia kupona kifo hicho, Ashura alitegemea siku ya hukumu angemuona Muddy akitoka mahakamani na kuanza kuokota makopo, lakini ilikuwa ni kinyume na mategemeo yake.
Wasiwasi wake Muddy lazima angelipa kisasi, wazo lake lilikuwa kumuwahi kabla hajawahiwa yeye. Akiwa amekaa na mwanaume wake, Ashura alimueleza jambo:
"Mussa nina jambo linaniumiza akilini mwangu."
"Lipi tena mpenzi?"
"Nina wasiwasi na Muddy kutulipizia kisasi."
"Ni kweli hata mimi nilikuwa na wazo hilo."
"Sasa tufanye nini kabla hajafanya lolote, maana akitulia atajipanga na yule dada anaonekana ana fedha hivyo anaweza kutufanyia kitu kibaya."
"Ondoa hofu hawawezi kutufanya lolote zaidi ya sisi kuwamaliza wao."
"Hayo ndiyo maneno." Ashura alipata faraja.
***
Wakati Ashura na Musa wakipanga mipango yao, usiku wa siku ile ufukweni mwa Bahari ya Hindi maeneo ya Daraja la Salenda kulikuwa na sherehe kubwa ya harusi kati ya Balkis na Muddy. Katika kundi la watu wote waliokuwepo kwenye sherehe ile Muddy peke yake ndiye aliyekuwa mwanadamu, lakini waliobakia walikuwa majini.
Lakini hakuwajua kwa vile walikuwa katika maumbile ya kibinadamu, Muddy alimuoa rasmi Balkis na kuwa mkewe wa halali. Ilikuwa sherehe kubwa kuwahi kutokea katika maisha ya Muddy. Baada ya harusi walilala kwenye kitanda cha bembea kilichowabembeleza mpaka kunakucha.
*****
Taarifa ya ndoa ya Balkis ilifika chini ya bahari kwa Mfalme Barami Hudirud, kitendo kile kwake alikiona kama ni dharau kutoka kwa mwanaye kufunga ndoa na mwanadamu. Alimfuata mkewe aliyekuwa amekaa kwenye bustani akibembea kwenye kiti.
"Mama Balkis," alimwita kwa sauti ya juu iliyomshtua.
"Mtukufu Mfalme wa chini ya bahari, mbona sauti kali, kuna usalama?"
"Mwanao ananitafuta nini?"
"Kwani kafanya nini tena mtukufu mfalme?"?"Tunamkataza nini na anafanya nini?"
"Amefanya nini?"
"Anaweza kuvunja amri yangu?" Mfalme Barami alisema huku akipiga ngumi kifuani kwa hasira.
"Mume wangu, lakini si bado anaendelea kuleta vizazi vya wanawake?"
"Kwa nini ameolewa na mwanadamu?"
"Ha! Ndiyo kafanya hivyo!" Malkia Huleiya alishtuka.
"Eeh! Tena nasikia watwana na vijakazi walikuwepo kwenye harusi hiyo."
"Usiniambie!"
"Kwa jinsi alivyovunja amri yangu, wote waliohudhuria harusi ile watakutana na adhabu kali," alisema kwa hasira mpaka povu likamtoka mdomoni.
"Mume wangu usimguse mtu yeyote ni wewe uliyempa amri mwanao kwa watwana na vijakazi juu ya kuheshimu amri zake."
"Basi kama sivyo hivyo nitamtuma mtwana mkuu Muhuru akammalize huyo mwanaume."
"Bado hujatumia busara, kumbuka kosa lako lolote litatugharimu, kitendo cha kukataa kumuondoa mwanaume wa kwanza huku kilizua patashika na ulipotaka kumuua ulisikia alichosema mwanao. Hivi umuue huyu aliyefunga naye ndoa itakuwaje?"
"Sasa kuna haja gani kuendelea kuleta vizazi vya wanawake wakati ameishajiamulia kuolewa na mwanadamu?"
JIINI LA DARAJA LA SALENDA........EP.48...B
ILIPOISHIA:
"Bado hujatumia busara, kumbuka kosa lako lolote litatugharimu. Kitendo cha kutaka kumuondoa mwanaume wa kwanza huku kukiwa na patashika ulipotaka kumuua ulisikia alichosema mwanao. Hivi umuue huyu aliyefunga naye ndoa itakuwaje?"
"Sasa kuna haja gani kuendelea kuleta vizazi vya wanawake wakati ameshajiamulia kuolewa na binadamu?"
SASA ENDELEA...
"Labda ana sababu zake, ngoja akija tumuulize."
"Hakuna cha kumsubiri, tumtume Muhuru aende akamwite mara moja."
"Siamini, kama jana kafunga ndoa leo aje huku, hebu kuwa na subira mume wangu."
Walikubaliana kumsubiri ili aje awaeleze kwa nini amevunja amri ya mfalme wa bahari, tena akiwa binti wa mfalme.
BAADA YA MIEZI MIWILI
Maisha ya Muddy yalibadilika ghafla, kila aliyemuona alimshangaa. Mmoja kati ya watu waliomshangaa alikuwa ni Ashura aliyemuona akitoka super market akiwa ameongozana na Balkis katika mwonekano wa mahaba mazito. Roho ilimuuma na kujikuta akipata wivu wa kutaka kuwa na Muddy.
Aliamini kuwa kilio cha Muddy alichokitoa siku alipomuacha, kama angemuomba warudiane angeweza kukubali. Alipanga kumtafuta na kumuomba msamaha.
Ashura aliamua kumtafuta Muddy kwa udi na uvumba kila kona ya mji. Lakini alishangaa kila alipomuona Muddy na kumfuata alipomkaribia Balkis alitokea bila kujua ametokea wapi, kitu ambacho kilimkosesha amani ya moyo wake. Hata alipojaribu kumfuatilia kwa nyuma alimpotea kimiujiza. Aliamini njia rahisi ya kumrudisha mikononi mwake ni kwenda kwa mtaalam wake aliyekuwa anakaa Mbagala Kimbangulile, Mzee Chujio.
Aliwasha gari na kuelekea Mbagala kwa mtaalam ili akamvute tena Muddy kama alivyofanya mwanzo na kupelekea kuisahau familia yake. Alipofika Mtoni kwa Azizi Ali dada mmoja aliomba msaada kwenye gari lake. Hakutaka kumnyima lifti, alimsaidia.
"Unafika wapi dada yangu?" alimuuliza baada ya kuingia kwenye gari na kufunga mlango.
"Mbagala Zakheem," alijibu yule dada kwa sauti ya chini.
"Ooh! Mimi nafika mbele, nitakushusha kituoni."
"Nitashukuru."
Wakati safari ikiendelea mwanamke aliyeomba msaada alianzisha mazungumzo.
"Dada yangu huku ni mwenyeji?"
"Hapana nakwenda kumuona mtu mmoja Mbagala mwisho."
"Nani mganga Chujio?"
"Mmh!" Ashura alishtuka.
"Mbona umeshtuka?"
"Walaa, siendi huko."
"Lakini dada shida ya nini kumuendea Muddy kwa mganga wakati mmekwisha achana?" Kauli ile ilimshtua sana Ashura.
"Nani amekwambia mimi nakwenda kwa mganga, pia habari za Muddy nani kakueleza?"
Ashura alishtuka kujiona yupo uchi japo amevaa nguo, alijuta kumpa lifti yule mwanamke ambaye aliharibu safari yake yote.
"Ashura," mwanamke aliyepewa lifti kwenye gari alimwita jina lake.
"Ha! Umejuaje jina langu?" Ashura alizidi kumshangaa mtu aliyempa lifti kwa kumjua kwa mapana.
"Nijue unataka kufanya nini nitashindwa kujua jina lako? kwanza jina lako si Ashura."
"Kama siitwi Ashura naitwa nani?"
"Shuuna."
"Mungu wangu! Umenijuaje?"
Ashura nusura aliingize gari kwenye mtaro kwa mshtuko, ilibidi alisimamishe pembeni maeneo ya Mbagala Misheni.
"Kwani kuna siri, la muhimu achana na Muddy endelea na maisha yako, pia mpango wenu wa kumfuatilia Muddy na mkewe mtaokota makopo ninyi kabla ya huyo Muddy."
"Wewe ni nani?" Ashura alimuuliza huku jasho likimtoka.
"Mke wa Muddy," sauti ilijibu pembeni.
"Muongo...Ha!" Ashura alijibu huku akigeuka kumtazama aliyejiita mke wa Muddy, wakati huo manukato makali yalinukia ndani ya gari. Hakuamini kumuona mtu aliyempa lifti amebadilika na kuwa mke wa Muddy, Balkis.
"Punguza hofu, sipo hapa kwa shari bali kukuonya kwa kitu unachotaka kukifanya, kumbuka nilikuuliza mapema kuhusu kurudiana naye nawe ulinihakikishia hutarudiana naye tena.
"Sasa sikiliza Ashura, huenda utashangaa kuniona hapa. Sitaki kujieleza sana, ila ukitaka vita na mimi ambavyo najua hutaweza kushinda endelea na mambo yako. Nitakufanya kitu kibaya ambacho kitabakia katika kumbukumbu zako mpaka unafukiwa chini.
"Mwambie na mpumbavu mwenzako mpango unaopanga wa kutaka kuichukua mali yangu mtakufa kifo kibaya. Leo sikuja kwa shari nimekuja kistaarabu. Mara ya pili utashangaa na hutaamini kuwa ni mimi," Balkis alisema kwa sauti kali kidogo iliyomtisha Ashura.
JIINI LA DARAJA LA SALENDA........EP.49
ILIPOISHIA:
"Sasa sikiliza Ashura huenda utashangaa kuniona hapa, sitaki kujieleza sana ila ukitaka vita na mimi najua huwezi, nitakufanyia kitu kibaya ambacho kitabakia katika kumbukumbu yako mpaka unafukiwa chini.
"Mwambie na mpumbavu mwenzako kwamba mpango mnaoupanga wa kutaka kuzichukua mali zangu mtakufa kifo kibaya. Leo sikuja kwa shari bali kwa ustaarabu, mara ya pili utanishangaa, hutaamini kuwa ni mimi," Balkis alisema kwa sauti kali kidogo iliyomtisha Ashura. SASA ENDELEA...
Baada ya kusema maneno yale, Balkis aliufungua mlango wa gari na kutoka nje huku akifyonya kwa sauti kali, alipolizunguka gari akatoweka.
Baada ya kuondoka eneo lile, Ashura alishtuka kama mtu aliyetoka usingizini na kujiuliza alichokiona na kukisikia kama kilikuwa ni cha kweli au alikuwa akiota.
Wazo lililomjia haraka aliamini kabisa kuwa ile ilikuwa ni ndoto, aliamua kwenda kwa mganga kupata tiba ya kumrudisha Muddy mikononi mwake.
Alijishangaa mwanaume aliyemgeuza mradi amekuwa kero moyoni mwake kila dakika alijikuta akimpenda na kumtamani kuwa naye tena.
Aliendesha gari huku akiapa kutompa msaada kiumbe yeyote kwa kuhofia kukutana na matatizo ambayo bado aliamini kuwa ni ndoto.
Hakuamini kama mtu angeweza kugeuka mara mbili katika hali ya kawaida, kwake alijua ile ilikuwa ni ndoto mbaya tu.
Alipofika Mbagala Rangi Tatu alikata kushoto na kuelekea Kimbangulile, alipofika kwa mganga alishangaa kukuta watu wakiwa wamejaa kuonesha kulikuwa na jambo.
Alisimamisha gari mbali kidogo na nyumba ya mganga na kuteremka kisha akajisogeza kwenye kundi la watu ambapo kila mmoja alikuwa akisema lake. Alimsikia mmoja akisema;
"Lazima yule atakuwa ni jambazi aliyefanyiwa kitu kibaya na mganga."
"Hapana mbona hakutoka mle ndani yule lazima atakuwa ni jini tu."
Yalikuwa naneno yaliyomchanganya Ashura na kujiuliza mganga amefanya nini, ilibidi amwite pembeni dada mmoja ili apate kumhoji vizuri.
"Samahani dada yangu kuna nini?"
"Mmh! Kuna jambo limetokea linawachanganya watu wengi."
"Jambo gani?"
"Mzee Chujio ameuawa."
"Mzee Chujio gani?"
"Yule mganga."
"Mganga?" Ashura aliuliza kwa mshtuko.
"Eeh, unamfahamu?"
"Sasa dada yangu nani asiyemjua mzee Chujio sehemu hii?"
"Basi ndiyo hivyo, ameuawa katika mazingira ya kutatanisha."
"Una maana gani?"
"Nasikia kuna dada mmoja mrembo alikuja na kuingia ndani kwa mganga na kuwaacha wateja wachache wakiwa kwenye foleni. Lakini inasemekana hakutoka, baada ya wateja kusubiri kwa muda bila kusikia wakiitwa ndani waliamua kuingia lakini cha ajabu wakamkuta mganga amelala chini akiwa amekufa na kutoka funza mdomoni kama aliyefariki wiki moja iliyopita."
"Funza mdomoni?"
"Ndiyo."
"Sasa jamani mtu wa kutoka funza si mtu aliyekufa zaidi ya wiki?" Ashura alisema kwa mshtuko.
"Hapo ndipo watu walipochanganyikiwa na kuamini kuwa yule mwanamke mzuri alikuwa ni jini."
"Jini! mna maana gani?"
"Wanasema alikuwa mzuri sana, tena alikuwa akinukia na alipoingia ndani hakutoka."
"Alivaa nguo gani?"
"Mmh! Hebu muulize yule dada aliyesimama katikati ya watu," alimuonesha dada mmoja aliyekuwa akizungumza na watu huku akilia na kuweka mikono kichwani.
"Naomba uniitie."
Yule binti alimfuata yule dada aliyekuwa akizungumza huku akitokwa na machozi, baada ya kusogea karibu ya Ashura, ilibidi ajitambulishe kuwa ni mmoja wa wateja wa mzee Chujio mtu aliyemtegemea kwenye mambo yake.
"Samahani mdogo wangu hata mimi nilikuwa nimekuja kwa mzee Chujio lakini kuna habari zimenichanganya sana. Nini kimemsibu mganga wetu?"
"Dada yangu hata kuzungumza nashindwa, siku tano zilizopita mzee Chujio alinisaidia matatizo yaliyonitesa kwa miaka kumi. Dawa alizonipa zilinionesha yote aliyonieleza, dada yangu walimwengu ni wabaya, niliteswa na mke mwenza na kufikia hatua ya kunuka mwili mzima hata kukaa mbele za watu nilikuwa siwezi.
"Nilitengwa na watu, wanaume walinipenda kwa kuniona, lakini waliponisogelea walikuwa wakikimbia kutokana na harufu kali kama ya mzoga uliooza. Leo dada yangu nilikuwa nafuata dawa na kupatiwa kinga baada ya awali kuondolewa tatizo langu.
"Ajabu wakati nasubiri kuingia kwa mganga alipita dada mmoja mrembo na kuingia ndani bila kufuata foleni. Kwa vile ilikuwa ni zamu yangu nilitaka kumfuata ndani kumtoa kwani hakuonesha ustaarabu, lakini wenzangu walinisihi nikamuacha amalize shida yake ndipo nami niingie.
"Baada ya muda kidogo tulisikia watu wakibishana, kauli ya mganga ilikuwa ya juu akionesha kuna kitu hakukubaliana na yule mwanamke mrembo mwenye kunukia manukato.
"Mganga alisema hawezi kufundishwa kazi na mtu, mara tulisikia sauti ya yule mwanamke mrembo akisema kuwa hana jinsi ile ndiyo zawadi yake.
"Baada ya hapo kilipita kimya kirefu huku muda ukizidi kuyoyoma.
"Baada ya nusu saa bila kusikia mazungumzo wala yule mwanamke mrembo kutoka, niliamua kuingia ndani kujua kilichokuwa kikiendelea.
"Nilipoingia nikamkuta mganga akiwa amelala chini, kilichonishtua zaidi ni funza waliokuwa wakimtoka mdomoni kama mtu aliyekufa muda mrefu."
JIINI LA DARAJA LA SALENDA........EP.50
"Funza?" Ashura aliuliza tena japo taarifa ya kutoka funza alielezwa mapema.
"Funza dada, kama mtu aliyekufa muda mrefu."
"Unataka kuniambia kabla ya kutokea tukio lile ulionana naye?"
"Tena alitoka nje na mgonjwa aliyekwenda kumfanyia tiba nyuma ya nyumba yake, aliponiona alitaka kujua hali yangu, nilimweleza ninavyoendelea na kuniambia vitu vyote alivyovitafuta kwa ajili ya kazi yangu vimepatikana...Yaani..," Kufikia pale yule dada aliangua kilio mikono kichwani, Ashura aliingia kwenye kazi ya kumbembeleza.
"Mdogo wangu hebu nyamaza kwanza."
"Dada inauma, haiwezekani niwe miye, nimeteseka muda mrefu, napata tiba mganga anauawa katika mazingira ya utata," aliendelea kulia kilio cha kukata tamaa. Ashura, japo alijitahidi kujikaza na kumbembeleza kwa kumlalia kifuani, lakini moyoni alikuwa na maumivu makali kama angepata sehemu iliyojificha, basi naye angeangua kilio ambacho hakuna mtu ambaye angeweza kumbembeleza.
Kifo cha mzee Chujio kilikuwa pigo kubwa maishani mwake, ndiye aliyekuwa tegemeo lake katika mambo yote aliyoyafanya ya kuwatapeli wanaume kwa kuwapumbaza kwa dawa. Alijiuliza nani atakayemsaidia katika maisha yake baada ya kifo cha mzee Chujio ambaye alimgeuza kama Mungu wa pili.
"Unasema ulimuona?" Ashura kwa kuchanganyikiwa alijikuta akiuliza swali alilojibiwa awali.
"Ndiyo."
"Unasema alipoingia ndani hakutoka?"
"Ndiyo."
"Au wakati anatoka huyo mwanamke ulikuwa umesinzia?"
"Dada yangu kusinzia tusinzie wote tulio
kuwa tunasuburi huduma?"
"Alivaa nguo gani?"
"Gauni refu jekundu lenye maua shingoni na kifuani, sielewi maua yale ya rangi gani kutokana na kumeremeta."
"Mmh! Shingoni alikuwa na mkufu wenye herufi M?"
"Eeeh."
"Mtandio wake wa bluu yenye maua ya kumetameta?"
"Huo huo!"
"Ana kipini cha mkufu?"
"Eeeh dada, umemjuaje?"
"Mmh! Kazi ipo," Ashura aliguna na kusema kwa sauti ya chini.
"Kwani unamfahamu?"
"Kuna mtu nilikutana naye njiani uliponielezea alivyovaa nilikisia basi lazima atakuwa yeye."
"Kwa hiyo si jini kama watu wanavyomdhania?"
"Mmh! Sijajua, kwani hakuna mlango wa kutokea nyuma?"
"Dada kama wewe ni mteja wa mzee Chujio, chumba chake unakijua, mlango utoke wapi?"
"Mna uhakika hakutoka?"
"Angetoka tungemuona kama si mimi basi wenzangu wangemuona."
"Mmh! Nina wasiwasi alitoka hamkumuona."
"Sawa alitoka, kile kifo nacho cha muda mfupi mtu aoze na kutoka funza kwa sekunde chache kinatokana na nini?"
"Inawezekana alimnywesha sumu kali iliyomuozesha tumboni na kuzalisha funza."
"Mmh! Labda."
"Basi dada, acha nirudi zangu hata mimi nimechanganyikiwa sana."
"Sawa dada, lakini mimi ndiye nimechanganyikiwa hata kuliko familia yake."
Wakati huo polisi walifika kuchukua mwili wa marehemu, alishuhudia mwili wa mzee Chujio ukitolewa huku familia yake na wateja wakiangua vilio.
Ashura alishindwa kujizuia, alikimbilia kwenye gari lake na kujifungia, alilia hadi macho yakamvimba. Alijiuliza yule mwanamke atakuwa nani, japo ilikuwa vigumu kukubali kuwa Balkis ni jini, lakini mambo yaliyomtokea kwenye gari alipombadilikia kama kinyonga yalimfanya aanze kuamini kabisa mke wa Muddy ni jini.
"Mungu wangu Muddy atakuwa ameoa jini?" Alijikuta akipayuka kwa sauti.
"Haiwezikani lazima nifanye chini juu nimtoe kwenye balaa lile."
Ashura alijiingiza kwenye vita nyingine ya kujua hatima ya Muddy kwa Balkis kwa kuamini kuna njia ya kuyafukuza majini. Aliwasha gari lake na kurudi nyumbani.
*duh!!tamuje??
Etaendelea leo jioni.................