Jenerali Ulimwengu: Hata kwenye upuuzi tuko dhaifu!

Dark City

JF-Expert Member
Oct 18, 2008
16,253
11,598
Nimeipenda makala ya Generali Ulimwengu ya week hii....

Soma mwenyewe hapa CLICK HERE Kwa nini tunataka ‘kuizairesha' nchi?: Katika upuuzi tutakuwa wapuuzi dhaifu

NIMESEMA mara nyingi kwamba tunahitaji kupunguza upuuzi katika maisha yetu na shughuli zetu kama jamii na kama taifa. Hii ina maana kwamba tunaenenda kipuuzi mno na ndiyo sababu kubwa ya kukosa maendeleo ambayo tunaweza kujivunia, tukiacha hayo maendeleo tunayolazimishwa tuyaangalie na wale wanaojisifu kwa kazi nzuri ambayo haionekani.
Upuuzi kwa kiasi fulani ni jambo jema. Kila mtu anayo haki ya kufanya upuuzi kidogo kama njia ya kujipumzisha, kujiliwaza na kujiburudisha baada ya kazi ngumu, ama ya mwili ama ya akili. Ndiyo maana hata katika jamii zilizoendelea sana katika ujenzi wa uchumi wapo watu ambao wanalipwa kwa mabilioni ya dola ili wapangilie upuuzi utakaowaburudisha wenzao waliotoka kwenye migodi na kazi nyingine za ngwamba. Kwa Marekani wengi wa watu wa aina hii wako Hollywood. Bara Hindi wako Bollywood.

Hata sisi hapa nchini tunao watu wa aina hiyo, hata kama sanaa yao haijakua kiasi cha kuzikaribia Hollywood na Bollywood. Na ni kweli kwamba wanatuburudisha na kutufurahisha kwa kiwango chao. Ni watu muhimu katika jamii kama ambavyo tulikumbushwa si muda mrefu uliopita alipofariki Kanumba.
Hata hivyo, hatutakiwi sote kuwa waburudishaji na watumbuizaji. Wengine hawana budi kufanya kazi nyingine ili taifa lisonge mbele, liweze kujilisha na kujilimbikizia amali kwa siku zijazo, kwa ajili ya vizazi vijavyo. Tukiwa sote ni watumbuizaji ni nani atatulisha, atatuvisha, atatujengea nyumba? Nasema, tunahitaji upuuzi kidogo, na tena huu ni upuuzi uliopangiliwa vyema, lakini upuuzi hautakiwi uwe ndiyo shughuli kuu ya jamii nzima.

Tukitaka kuangalia jamii iliyofanya upuuzi ukawa ndiyo shughuli kuu katika maisha yake, hatuhitaji kwenda mbali sana; tuiangalie Kongo, ambayo Joseph Mobutu aliita Zaire kwa kipindi kirefu akiwa mtawala wake. Kongo imejipambanua kwamba nchi ya upuuzi kabla ya uhuru wake mwaka 1960. Ilipoingiliwa na wazungu ilifanywa kuwa shamba binafsi la Mfalme Leopold II wa Ubelgiji, ambaye alichimba na kuchuma kila alichokitaka na alifanya kila aina ya unyama bila kuulizwa siyo tu na Wakongo bali pia hata Bunge la nchi yake. Kongo haikuwa koloni la Ubelgiji; lilikuwa ni kihamba cha Leopold.
Baada ya uhuru wanasiasa wapuuzi wakalumbana, wakazodoana, wakafukuzana, wakauana, hadi alipoibuka mshindi wa kinyanga'anyiro hicho kwa sura ya Jospeh Mobutu, ambaye aliboresha mbinu za wizi, uporaji, unyang'anyi, udhalimu na uuaji kiasi kwamba ikawa inajulikana kwamba hayo ndiyo maisha ya nchi ya Zaire na huo ndio utamaduni wake. Hiki ndicho kilikuja kujulikana kama Mobutism, u-Mobutu.

Kwa wananchi wa kawaida, hii ndiyo ilikuwa hali ya maisha, nao wakaichukulia hivyo ilivyokuwa na wakajichimbia katika wizi wao na unyang'anyi wao mdogo mdogo (small scakle thievery) ambao ulikuwa ni kiungo muhimu katika kufanikisha wizi mkubwa (large scale thievery) ya Mobutu na genge lake.

Isitoshe, katika kujiliwaza na kujisahaulisha madhila waliyoyapata muda wote, wakiwa ni shamba la Leopold na wakiwa ni shamba la Mobutu, wananchi wa nchi hiyo yenye utajiri kama El Dorado wakaingia katika shughuli ya kujitumbuiza kwa muziki na ngoma. Na hii ikawa ndiyo shughuli yao kubwa. Kongo ikajulikana kwa mambo manne makubwa: moja, utajiri mkubwa uliomnufaisha Mobutu na mafisi waliomzunguka, lakini hasa uliowanufaisha wazungu; pili, vita, fujo na vurumai zisizoisha; tatu, udhaifu wa serikali ambayo haikuonekana majimboni isipokuwa kwa uwapo wa askari wanaopora ili kupata ujira wao; nne, muziki, ngoma na burudani kama soka na ngono.
Taswira hii ya Kongo haijabadilika sana. Mwaka 1997 nilikuwa katika msafara wa Mwalimu Julius Nyerere aliyekwenda Kinshasa kwa mazungumzo na Rais Laurent Kabila. Katika wiki moja tuliyokaa Kinshasa jambo moja kubwa alilobaini ni kwamba Kabila na genge lake walikuwa wamefanikiwa kumfurusha madarakani Mobutu lakini wakabakiza u-Mobutu katika utawala wao. Kabila alikuwa ni Mobutu baada ya Mobutu, mrithi halali wa Leopold. Hadi leo hali haijabadilika sana, baada ya Kabila mdogo kumrithi baba yake aliyeuawa katika mazingira ya kunyang'anyana mali.

Pamoja na yote, K0ngo/Zaire ilipata mafanikio makubwa sana katika upuuzi uliopangiliwa. Haiwezekani kuzungumzia muziki barani Afrika bila kuitaja Kongo/Zaire; hata barani Uropa, wapenzi wa muziki ambao hawana asili ya Afrika wanatafuta muziki wa Kongo/Zaire. Aidha Wakongo ni wasanii katika mambo mengine pia, kama ushonaji wa nguo, ushonaji wa viatu, uchoraji na uchongaji. Pia ni wanasoka wazuri wanaosifika Ulaya ambako wanacheza katika ligi kubwa.
Mobutu, pamoja na kwamba alikuwa mshenzi, alifanya kazi kubwa ya kuhifadhi urithi wa kimuziki wa Kongo. Katika miaka ya 1970 nilikwenda mara kadhaa mjini Kinshasa na nikaweza kujikusanyia albamu kadhaa ya wanamuziki wa zamani wa Kongo, akina, Kabasele, Wendo na Boukaka, yote kwa sababu Mobutu alikuwa amefadhili kazi ya kukusanya nyimbo za zamani na kuziweka katika sahani za santuri.
Uhamasishaji wa vikundi vya ngoma na mapambio ya kumsifu Mobutu ulifikia viwango vya juu kabisa, kiasi kwamba watawala wa nchi nyingine, kama Gnassinbe Eyadema wa Togo, walianza kuiga walichokuwa wakifanya Wazaire katika kumsifu Mobutu. Hata sisi hapa nchini tulivutika na upuuzi huo kiasi kwamba wimbo wa "chama chetu cha Mapinduzi chajenga nchi" ulichukua mahadhi ya wimbo wa kumsifu Mobutu, "Tokobongisa Mobutu Sesse Seko."
Mobutu alifanikisha upuuzi kwa kiwango cha juu sana, na akaifanya nchi yake kuwa ya kipuuzi ambamo rasilimali za nchi zinaporwa na wageni wakisaidiwa na watawala wa nchi, huku wananchi wakiimba na kukata viuno wakimsifu Bwana Mkubwa. Nchi tajiri kwa rasilimali kuliko nchi nyingi duniani (ardhi nzuri yenye rutuba, misitu, maji, madini ya kila aina) lakini yenye wananchi siyo tu masikini lakini wasiokuwa na amani kutokana na vita za kila mara; lakini wanacheza ngoma, wanafurahi.

Wakichoka kuishi katika vurumai za nchini mwao wanaondoka, wanahamia katika nchi nyingine Afrika na ng'ambo ambako wanakwenda kuimba na kupiga muziki wa dansi, kushona nguo, na kusuka nywele. Kwa jinsi hii wamejipatia umaarufu mkubwa katika upuuzi wao. Laiti wangekuwa ni wapiga muziki mahiri, wanasanaa wakubwa na wasusi wa nywele wa kimataifa na papo hapo wakaiendeleza nchi yao katika kilimo na viwanda, tungelazimika kuwaheshimu kwa yote hayo na mimi nisingethubutu kuwaita wapuuzi ; kwa walivyo, ni wapuuzi waliofanikisha upuuzi wao kwa kiwango cha juu.

Hatari ninayoiona ni hii inayotunyemelea: Kwamba tunaelekea kuifanya nchi yetu kuwa Zaire bila kuwa na wanasanaa wa viwango vya Zaire. Tunataka kuwa wapuuzi bila kuwa na uwezo wa kufanya upuuzi ukafikia kiwango cha kutupatia sifa kama wapuuzi. Hii haitakuwa rahisi, na hii ina maana kwamba hata katika upuuzi tutakuwa wapuuzi dhaifu; hatutawafikia Wazaire kwa upuuzi.
Hii ni kwa sababu nchi yetu inayo misingi ya kitaifa iliyowekwa na waasisi wa taifa hili. Misingi hiyo inakataa nchi yetu kugeuzwa kihamba cha mtu au watu wachache; ni kihamba chetu sote, na wala si chetu kiasi hicho, kwani tumepewa dhamana tu ya kukihifadhi na kukiendeleza kwa ajili ya vizazi vijavyo, kwa niaba ya Watanzania tusiowajua, kwa sababu hawajazaliwa.
Tunao watoto tayari ambao kila wakituchunguza tunavyoenenda ki-Zaire hawaoni mustakabali wao na wa watoto wao; wanatuuliza maswali, tunashindwa kuwajibu; wanaasi, hatuelewi.
Tungekuwa na busara ya kusikiliza vyema wanachosema, tungezisikia sauti za watoto watakaozaliwa mwaka 2099, wakisaili: Mbona mnaigeuza nchi yetu Zaire? Tungesikiliza sauti hizo tungekomesha huu Uzaireshaji (Zairesation) wa nchi yetu, tungekuwa watu makini wenye viwango vidogo tu (vile vya lazima) vya upuuzi.
 
Makala hii bomba. Tatizo ni kwamba ni kwa ajili ya watu wenye kiwango cha juu cha uelewa. Maana Ulimwengu kuwashukia mafisi na mafisadi wetu walioko madarakani wakifanya sanaa huku watanzania nao wakikata viuno kushangilia upuuzi wao wakati nchi inaibiwa. Kweli wapuuzi si wazaire tu bali hata watanzania ambao hupenda kufanya vitu vya muhimu vya hovyo na vya hovyo muhimu. Shukrani Ulimwengu kwa makala iliyokwenda shule.
 
I always like this dude, huwa haogopi makunyanzi ya walioko kwenye madaraka- ukienda hovyo lazima akulime tu. Mzee wa kiwira anamjua vizuri ilibidi akimbilie kumnyang'anya uraia lakini haikusaidia kitu jembe liliendelea kutifua tu!!!!
 
Makala hii bomba. Tatizo ni kwamba ni kwa ajili ya watu wenye kiwango cha juu cha uelewa. Maana Ulimwengu kuwashukia mafisi na mafisadi wetu walioko madarakani wakifanya sanaa huku watanzania nao wakikata viuno kushangilia upuuzi wao wakati nchi inaibiwa. Kweli wapuuzi si wazaire tu bali hata watanzania ambao hupenda kufanya vitu vya muhimu vya hovyo na vya hovyo muhimu. Shukrani Ulimwengu kwa makala iliyokwenda shule.

Hivi mtu akikufanyia vitu vya hovyo halafu ukamkenulia meno, mtu wa hovyo zaidi ni yupi??

Nadhani watanzania tunahitaji kuelewa hili!!
 
Kwa mtazamo wa huyu Mnyarwanda muziki ni "upuuzi" na kuthubutu kukashifu tasnia nzima ya burudani kuwa nayo tunashindwa!

Kweli mgema akisifiwa tembo hulitia maji, mwandishi huyu mkongwe kakosa maneno sawia na kuamua kumwaga kashfa na bado anaambiwa yupo "deep!"

Kweli serikali hii ipo "auto pilot" ujinga ujinga kama huu mbona hakumfanyia Mkapa?
 
Upuuzi !!!!

Its true kwamba tunafanya upuuzi, its true kwamba mengi yafanyikayo ni upuuzi lakini tusiite hata mazuri ni upuuzi.., he is right in some scenarios lakini tusisahau kwamba what matters is making a living, kwahio si vema kuita skills za mtu ni upuuzi.. Upuuzi wa Mobutu hauwezi kupunguza sifa za Franco, Pepe Kalle wala Papa Wemba
 
Kwa mtazamo wa huyu Mnyarwanda muziki ni "upuuzi" na kuthubutu kukashifu tasnia nzima ya burudani kuwa nayo tunashindwa!

Kweli mgema akisifiwa tembo hulitia maji, mwandishi huyu mkongwe kakosa maneno sawia na kuamua kumwaga kashfa na bado anaambiwa yupo "deep!"

Kweli serikali hii ipo "auto pilot" ujinga ujinga kama huu mbona hakumfanyia Mkapa?

...kuna sehemu kasema kama hayo yangeendana na mapinduzi ya viwanda na kilimo, asingeita upuuzi!
 
Upuuzi !!!!
kwahio si vema kuita skills za mtu ni upuuzi.. Upuuzi wa Mobutu hauwezi kupunguza sifa za Franco, Pepe Kalle wala Papa Wemba

...kweli inahitaji akili kuelewa. Wakati nchi na mali zinaporwa, sie twakata mauno na kushangilia. Eti tusiitwe wapuuzi! Khaaa!!!
 
Kama alivosema Father of All, hii inahitaji mtu mwenye uelewa wa hali ya juu. Maana nimesoma na bado nadiriki kukiri kuwa bado najiuliza kama hasa nimeelewa vile Ulimwengu alilenga uelewa uwe.

As much as namkubali sana Jenrali Ulimwengu somehow naona hii article kaenda extreme in trying to make his point kwa kui label 'upuuzi' hio entity... Nashindwa kuelewa ni kwa nini ka label "Upuuzi" kwenye sector ambayo ingawa imelenga burudani zaidi ina manufaa yake makubwa tu kwa taifa kwa serkali na wananchi wenyewe kwa pande zote. Je amekuwa inspired na hasira tokana na kujihusisha kwa mkuu wa kaya na mtoa burudani ambae kwa kiasi kikubwa ni maarufu kwa kuuza sura? au ni kweli anaona kama hio sector ni upuuzi?

Labda alieelewa vema atudadafulie... Na kwa serkali yetu hii unaposema kui "Zaire" nchi yetu ina maana regardless ya tabia za Kiongozi mkubwa wa nchi kukumbatia upuuz (as per his say) pia in some way anakataliana na tabia ya wachache kuimiliki hii nchi badala ya majority... Hapo inanipa maswali kama akina J. Makamba pia ni walengwa...
 
Last edited by a moderator:
Mkuu MIA, ila kuna matumaini ya watanzania kushituka sasa hivi. binafsi naguswa sana na kazi iliyofanywa na chadema ya kuwaamsha watanzania. Haya majambazi ya ccm bila kuyawekea spidi gavana (KUYANG'OA MADARAKANI), hakyanani yatakula kila kitu. siku hizi hata kuulizwa tu hayataki, ukiyauliza yanakutishia kukuua(wauaji).



Tuendeleeni kuwaelimisha watanzania, ili waelimike waling'oe madarakani hili li-serikali la ccm MAONGO/MAFISADI/MAJAMBAZI/WAUAJI.
 
...kweli inahitaji akili kuelewa. Wakati nchi na mali zinaporwa, sie twakata mauno na kushangilia. Eti tusiitwe wapuuzi! Khaaa!!!
Kwahio ulitaka hao wakata mauno na wanaoshangilia (ili kupata pesa na kuwaburudisha wenzao) wajiue au waanze kulia na kusaga meno...

Lets not deflect the blame na upuuzi wa wengine kwa watu wengine.., hao wakata mauno na washangiliaji are the only heroes wapuuzi ni mafisadi, wanasiasa wasiofanya kazi zao, waajiriwa wasiowajibika n.k. The only so called wapuuzi (waburudishaji) are the only professionals I can see as far as the article is concerned.

Sisemi kwamba hakuna wapuuzi au upuuzi haufanyiki ila hapa amekosea sana kusema upuuzi unafall in this category ningemuelewa angesema UPUUZI wa TANZANIA sasa hivi upo kwenye Siasa ambapo all professionals wanakimbilia kwenye Siasa badala ya maendeleo.., but this so called wakata viouno na washangiliaji I might say they are the only heroes and their job if done right is a multi billion dollar business
 
Kama alivosema Father of All, hii inahitaji mtu mwenye uelewa wa hali ya juu. Maana nimesoma na bado nadiriki kukiri kuwa bado najiuliza kama hasa nimeelewa vile Ulimwengu alilenga uelewa uwe.

As much as namkubali sana Jenrali Ulimwengu somehow naona hii article kaenda extreme in trying to make his point kwa kui label 'upuuzi' hio entity... Nashindwa kuelewa ni kwa nini ka label "Upuuzi" kwenye sector ambayo ingawa imelenga burudani zaidi ina manufaa yake makubwa tu kwa taifa kwa serkali na wananchi wenyewe kwa pande zote. Je amekuwa inspired na hasira tokana na kujihusisha kwa mkuu wa kaya na mtoa burudani ambae kwa kiasi kikubwa ni maarufu kwa kuuza sura? au ni kweli anaona kama hio sector ni upuuzi?

Labda alieelewa vema atudadafulie... Na kwa serkali yetu hii unaposema kui "Zaire" nchi yetu ina maana regardless ya tabia za Kiongozi mkubwa wa nchi kukumbatia upuuz (as per his say) pia in some way anakataliana na tabia ya wachache kuimiliki hii nchi badala ya majority... Hapo inanipa maswali kama akina J. Makamba pia ni walengwa...

Hata mimi sina hakika kama nimemuelewa vizuri, ila kajaribu kusema baadhi ya mambo tuliyoyasema kwa Kanumba tunaonekana wabaya...Tuliona kama vile jamii inaelekea ndiko siko. Inawezekanaje watu makini wakamiminika kumsindikiza msanii na kumsahau mtu ambaye alikuwa mkuu wa majeshi wa nchi??

Katika kuendesha maisha ya kila siku, kuna mambo siyo ya lazima (huwezi kufa au kupata madhara makubwa kwa kuyakosa). Mfano wa mambo haya ni burudani za aina zote. Pamoja na kwamba sijafurahia neno alilolitumia, ila kwa namna fulani naweza kumuelewa kwa sababu ni kama vile tumeweka kipaumbele kwenye mambo yasiyo ya lazima na kuacha mambo muhimu. Na katika hali kama hiyo, tunaweza kusema tumefanya upuuzi na kwa maana hiyo, tunaendekeza mambo ya kipuuzi!!

Nadhani siyo rahisi kuelewa makala kama hizi, na endapo ukihisi kwamba umekuwa offended!
 
Kwahio ulitaka hao wakata mauno na wanaoshangilia (ili kupata pesa na kuwaburudisha wenzao) wajiue au waanze kulia na kusaga meno...

Lets not deflect the blame na upuuzi wa wengine kwa watu wengine.., hao wakata mauno na washangiliaji are the only heroes wapuuzi ni mafisadi, wanasiasa wasiofanya kazi zao, waajiriwa wasiowajibika n.k. The only so called wapuuzi (waburudishaji) are the only professionals I can see as far as the article is concerned.

Sisemi kwamba hakuna wapuuzi au upuuzi haufanyiki ila hapa amekosea sana kusema upuuzi unafall in this category ningemuelewa angesema UPUUZI wa TANZANIA sasa hivi upo kwenye Siasa ambapo all professionals wanakimbilia kwenye Siasa badala ya maendeleo.., but this so called wakata viouno na washangiliaji I might say they are the only heroes and their job if done right is a multi billion dollar business


Inawezekana uko sahihi,

Hivi ulishawahi kujiuliza, kwa nini karibia kila mzazi humzuia mwanae kujiingiza kwenye mambo ya usanii??
 
Just to make my point clear naomba angalia na hapa

Ndiyo maana hata katika jamii zilizoendelea sana katika ujenzi wa uchumi wapo watu ambao wanalipwa kwa mabilioni ya dola ili wapangilie upuuzi utakaowaburudisha wenzao waliotoka kwenye migodi na kazi nyingine za ngwamba. Kwa Marekani wengi wa watu wa aina hii wako Hollywood. Bara Hindi wako Bollywood.

Hapo inaonekana kwamba the works of art / talent ni some sort of upuuzi au some minor work.., ambapo sio kweli kila kazi ina faida zake.., kwahio hapa nadhani kwa mfano wa juu tungesema mpuuzi ni yule ambaye hafanyi kazi zake bali anakuwa mtu wa burudani au kuangalia burudani na sio mtoa burudani..

Kwahio kama wakuu wa nchi wanakula bata badala ya kufanya kazi basi wapuuzi ni wakuu wa nchi na sio mtoa bata (bali mla bata bila kuzalisha bata)
 
Hata mimi sina hakika kama nimemuelewa vizuri, ila kajaribu kusema baadhi ya mambo tuliyoyasema kwa Kanumba tunaonekana wabaya...Tuliona kama vile jamii inaelekea ndiko siko. Inawezekanaje watu makini wakamiminika kumsindikiza msanii na kumsahau mtu ambaye alikuwa mkuu wa majeshi wa nchi??

Katika kuendesha maisha ya kila siku, kuna mambo siyo ya lazima (huwezi kufa au kupata madhara makubwa kwa kuyakosa). Mfano wa mambo haya ni burudani za aina zote. Pamoja na kwamba sijafurahia neno alilolitumia, ila kwa namna fulani naweza kumuelewa kwa sababu ni kama vile tumeweka kipaumbele kwenye mambo yasiyo ya lazima na kuacha mambo muhimu. Na katika hali kama hiyo, tunaweza kusema tumefanya upuuzi na kwa maana hiyo, tunaendekeza mambo ya kipuuzi!!

Nadhani siyo rahisi kuelewa makala kama hizi, na endapo ukihisi kwamba umekuwa offended!

Kuna watu wakiongea kitu unajuwa wanamaanisha… Ulimwengu ni mtu ambae siku zote yuko within logic and reason. Hio article nimeisoma, ina ujumbe mzito BUT nimeona niiangalie more like a critique than tu kuikubali kama ilivo kwa mimi kuweza elewa na faidika nayo. Huwa nasoma makala zake once in a while na huwa hazinipi shida katika kumpata…

Kwa maelezo yako ulotoa (hasa paragraph ya pili); imeonesha kuwa nimeelewa vema kama wewe pia umeelewa hivo. Kama ulivosema na nakubaliana nawewe kuwa hajatumia neno zuri. Hata hivo nadhani shida sana sio kuendekeza kwa hayo mambo; shida ni kitendo cha kuwa na audacity ya ku-entertain vitu kama entertainment in a time ambayo taifa inakumbana na matatizo kila Nyanja, kila sector, ndani/nje and between hizo Nyanja na sector… Sad.

Tukija upande wa mfano wako wa Kanumba... Lets just not go there! Words can not suffice at the moment.
 
Inawezekana uko sahihi,

Hivi ulishawahi kujiuliza, kwa nini karibia kila mzazi humzuia mwanae kujiingiza kwenye mambo ya usanii??
You always need plan B.., usanii mara nyingi ni very competitive na unatumia kipaji / mwili wako as kitendea kazi na mara nyingi ukishindwa hapa kama hauna plan B unaweza kujikuta umeumia..

kwahio wazazi wengi they are right hususan huku bongo kitabu kwanza usanii baadae (kazi nyingine zina security zaidi) lakini kama una talent kama kina Michael Jackson, Tiger Woods, Bolt au Messi nadhani kutokufata talent yako itakuwa ni kufanya kosa kubwa.., lakini hata ukiwa Messi sio vibaya hata ukapata elimu ya watu wazima au evening studies just in case ukivunjika mguu uweze kuwa hata karani...

Sasa tukirudi hapo kwenye article sidhani watu wanaojitahidi kufanya zoezi na kuwa kama Messi ni wapuuzi bali wale ambao kazi yao ni kufagia barabara na kusafisha mitaro hawafanyi kazi zao bali wanamshangilia Messi ndio wapuuzi (one is doing his job and another is not)
 
You always need plan B.., usanii mara nyingi ni very competitive na unatumia kipaji / mwili wako as kitendea kazi na mara nyingi ukishindwa hapa kama hauna plan B unaweza kujikuta umeumia..

kwahio wazazi wengi they are right hususan huku bongo kitabu kwanza usanii baadae (kazi nyingine zina security zaidi) lakini kama una talent kama kina Michael Jackson, Tiger Woods, Bolt au Messi nadhani kutokufata talent yako itakuwa ni kufanya kosa kubwa.., lakini hata ukiwa Messi sio vibaya hata ukapata elimu ya watu wazima au evening studies just in case ukivunjika mguu uweze kuwa hata karani...

Sasa tukirudi hapo kwenye article sidhani watu wanaojitahidi kufanya zoezi na kuwa kama Messi ni wapuuzi bali wale ambao kazi yao ni kufagia barabara na kusafisha mitaro hawafanyi kazi zao bali wanamshangilia Messi ndio wapuuzi (one is doing his job and another is not)

Nakubaliana na wewe Mkuu,

Messi anayefanya kazi yake vizuri au Mr Bean, hawezi kuwa mpuuzi. Au mtu kama Drogba anayetumia mapato yake kutoa misaada ya kijamiii hawezi kuwa mpuuzi.

Ila nadhani kuna watu ambao wanafanya kazi kuingiza wakijivika uhusika wa akina Drogba, Messi na Mr Bean na hao ndio wapuuzi....Ila mwisho wa siku, wanajaribu kuchafua kazi nzuri ya akina Drogba... Na bahati mbaya, watu wengi tulio na akili za kawaida tunajikuta kwenye dilema ya kujua mpuuzi hasa ni nani kati ya hao!!

Sijui kama nimeeleweka vizuri!!

Babu DC!!
 
Back
Top Bottom