SEHEMU YA 42...
“Nafikiri na mimi nikitumia utaalam ule ule nitamnasa mmoja!” Aliwaza bibi Nyanjige na kusimama wima akiupima mwili wake nguvu.
“Niko bombaaa!” Alijitapa na kuamua kujaribu kutumia nafasi hiyo
Aliangaza macho yake pembeni na kuona mzizi mkubwa wa mti ukiwa chini, akajinyoosha na kwa kutumia nguvu nyingi aliukata na kuushika mkononi, ulikuwa mgumu na ulifanana kabisa na kamba.
Alipatwa na ujasiri wa ajabu na kujisogeza hadi pembeni kabisa mwa kichaka alichojificha na kuwashuhudia maaskari wakizidi kupita taratibu bunduki zao zikiwa mkononi, hakuwa na shida nao wote alimtaka mmoja tu! Alitulia akisubiri wa mwisho apite huyo ndiye alikuwa mlengwa.
Wengi walipita akamuona mmoja wao ambaye aliamini alikuwa wa mwisho akija taratibu, yeye alibeba mtambo mkubwa zaidi ya wenzake uliomuelemea kwa uzito! Alitembea peke yake akionekana kuchoka kupita kiasi na alikuwa legelege na mwenye afya mbovu.
“Huyu huyu ananitosha!” Aliwaza bibi Nyanjige huku akiweka mzizi wake vizuri, askari alipofika karibu yake bibi Nyanjige aliruka kwa kasi na kuuzungusha mzizi aliokuwa nao shingoni mwa askari kama ambavyo vibaka hufanya wanapomkaba mtu.
Mwanajeshi hakupiga kelele hata kidogo bali alianguka chini kimyakimya,macho yalimtoka vibaya askari, bibi Nyanjige naye akazidi kubana kwa mzizi kwa dakika kama mbili huku akiwaangalia wanajeshi wenzake waliozidi kutokomea bila kujua yaliyompata mwenzao! Bibi Nyanjige alijipongeza kwa kazi aliyoifanya.
Kwa haraka alimvutia askari huyo na kumwingiza ndani ya kichaka ambako alimbana zaidi na mzizi hadi akafa!
“Sasa mambo yameanza upya!” Alisema bibi huku akimvua askari huyo magwanda yake na kuyavaa mwilini mwake! Ingawa yalimbana sana aliyalazimisha. Kofia ya jeshi aliyovaa askari huyo ilikuwa kubwa kiasi kwamba bibi Nyanjige alipoiweka kichwani ilimfunika uso wake wote, haikuwa rahisi hata kidogo kumtambua.