Huwezi Kuua Maiti -Erick Shigongo

Huwezi Kuua Maiti -Erick Shigongo

SEHEMU YA 30...

Bibi Nyanjige alizidi kutetemeka ndani ya Khanga aliyojifunika kichwani, alielewa wazi hapakuwa na njia yoyote ya kujiokoa kutoka mikononi mwa wanajeshi waliokuwa wakimsaka! Aliamini mwisho wa uhai wake ulikuwa umefika na kilichokuwa kikimsubiri mbele yake hakikuwa kingine zaidi ya kamba shingoni, alijua kwa mauaji aliyoyafanya ni lazima angenyongwa na kufa!

“Ehne! Wewe mama hebu jifunuee hicho kilemba chako!” Mwanajeshi mmoja alimwambia mwanamke aliyekaa kiti kilichokuwa mbele ya kiti cha bibi Nyanjige na aliyekuwa akifuata baada ya mama huyo alikuwa bibi Nyanjige mwenyewe! Bila ubishi mama huyo alijifunua kilemba chake na kuuacha uso wake wazi, hakufanana na mtu waliyekuwa wakimtafuta.

“Haya wewe mwanamke mwenye khanga kichwani hapo kwenye kona hebu ondoa hiyo khanga yako!” Alisema askari huyo.
Pamoja na ushujaa wake bibi Nyanjige alisikia nguo zake za ndani zikilowana, tayari mkojo ulishampenya! Alijadili kwa muda mrefu kuhusu kuitoa khanga kichwani au la kwani alijua kufanya hivyo kungemfanya akamatwe! Na kukamatwa kwake kungemaanisha kifo.

“Wee mwanamke husikii unajifanya kusinzia siyo?” Askari aliuliza kwa ukali.
“Ah bwanae hebu tuachane nao hawa twende chini tukasubiri magari mengine!” Askari mmoja alisema baada ya kuona taa za gari zikimulika kutoka kwa nyuma yao na wote kwa pamoja waliteremka hadi chini kuliwahi gari lililokuwa likija.

Kitendo hicho cha askari kilimfanya bibi Nyanjige ashushe pumzi ndani ya khanga aliyojifunika, hakuamini kama sakata hilo lilikuwa limekwisha! Kwa mara ya kwanza katika maisha yake alijikuta akiamini kuwa Mungu husikia kilio cha wenye shida.
“Hapo ndio nilishakufa!”

Dereva aliliondoa gari huku akilalamika kwa kupotezewa muda wake, walitumia kama dakika thelathini eneo hilo moja! Hata watu wengine ndani ya basi walisikika wakilalamikia kitendo hicho, bibi Nyanjige naye aliendelea kuhema kwa nguvu ndani ya khanga yake, hakuwa tayari kujifunua kwa kuogopa kugundulika kwani tayari kila mtu ndani ya basi hilo alikuwa na habari juu ya kusakwa kwake.

Itaendelea.
 
SEHEMU YA 31...

“Maaskari wengine bwana yaani walitegemea bibi Nyanjige wampate humu? Yule bibi ni hatari bwana, yule ni gaidi si mtu wa kukamatwa ovyoovyo! Badala ya kumtafuta huko huko Kongo eti wanakuja kuweka kizuizi hapa Chalinze! Wamechanganyikiwa nini?” Alifoka dereva wakati akiliondoa basi kwa kasi ili kufidia muda uliopotea wakati wa kukaguliwa!

Dereva alikuwa na sababu ya kuondoka kwa kasi kwa sababu maagizo aliyopewa na tajiri yake yalikuwa ni kuwahi kurudi Dar es Salaam ili kuja kuchukua watalii kuwapeleka Mbuga za Mikumi, aliliendesha basi kwa kasi ambayo mara nyingi huwa haitumiwi na magari yaliyobeba maiti. *****************

Macho ya binadamu hayana pazia! Ilikuwa si rahisi kwa watu wote waliokuwa msibani Kigamboni kutomgundua bibi Nyanjige. Msichana mmoja alimwona bibi Nyanjige na kumfananisha lakini hakuwa na uhakika sana na macho yake.
Aliporejea nyumbani baada ya gari kuondoka na maiti kuelekea Kilimanjaro, aliliona tangazo katika luninga likitangaza msako wa bibi Nyanjige, kwa sura aliyoiona hakuwa na sababu ya kutoyaamini macho yake tena! Alikuwa na uhakika asilimia mia kuwa mtu aliyemwona msibani alikuwa bibi Nyanjige.

Alipiga kelele kwa nguvu na kushangilia alijua zawadi iliyotolewa kwa mtu yeyote ambaye angefanikisha kukamatwa kwa bibi Nyanjige ilikuwa yake.
“Baba nimemwona huyu bibi anayetangazwa msibani!”
“Wewe mtoto unaota au unataka kuchanganyikiwa?” Baba yake aliuliza.
“Sio hivyo baba ni kweli alikuwa msibani na tulitoka nae chumba cha maiti!”
“NI lazima utakuwa umefananisha!”

“Hapana baba nina uhakika asilimia mia moja, mimi siyo mtoto!”
“Alivaa nguo gani?”
“Alivaa gauni hilihili lenye rangi ya kijivu na nyekundu analoonekana nalo kwenye televisheni ila lilikuwa mchafu kupita kiasi!” Alisema binti huyo akilionyesha gauni pekee la bibi Nyanjige katika Luninga picha yake iligandishwa ili watu wamwone vizuri.

“Huyu bibi ni mtu hatari popote atakapoonekana basi akamatwe na mtu atakayewezesha kukamatwa kwake atapatiwa zawadi”Ilisema sehemu ya habari hiyo.
“Baba tupige simu kwa polisi?” Binti alimweleza baba yake.

Itaendelea.
 
SEHEMU YA 33...

“Wewe mtoto una uhakika na unachokisema?”
“Ndiyo!”
“Sasa na hao polisi watampataje kama ameondoka na basi kwenda Kilimanjaro?”
“Wanaweza kulifuatilia basi alilopanda!”
Dakika mbili baadaye msichana huyo alikuwa kwenye simu akiongea na polisi juu ya mahali alikokuwa bibi Nyanjige, hata polisi wenyewe walionekana kutoyaamini maneno ya binti huyo.
“Binti una uhakika lakini? Usije kulisumbua jeshi la polisi bure?”
“Ni uhakika!”

“Kwa hiyo yupo wapi?”
“Ameondoka masaa matatu yaliyopita kupelekea maiti huko Marangu Moshi, kama mtaweza kulifuatilia gari lililobeba maiti basi mtakuwa mmempata!”
“Kweli?”
“Ndiyo!”
“Namba za basi walililopanda unaifahamu?”
“Ni TZO 8507!”

“Ok! Ahsante!” Alishukuru askari na kumuaga binti huyo akimpa uhakika kuwa kama bibi Nyanjige angekamatwa huko alikosema basi yeye ndiye angepewa pesa yote iliyoahidiwa kama zawadi, bila kupoteza hata sekunde mbili baada ya kuongea na simu maaskari walinyanyua simu ya upepo na kuanza kuwasiliana na maaskari waliokuwa maeneo ya Chalinze.

“Unanipata afande, ova!”
“Ndiyo ninakusoma, ova!”
“Yule bibi! Yule bibi! Yumo ndani ya basi dogo linalosafirisha maiti kwenda Marangu, ova! Basi dogo lililobeba maiti!”
“Namba zake ni ngapi?”
“TZO 8507,hakikisheni mnamkamata, ova!”
“Mungu wang....!”Alisema askari wa upande wa Chalinze.
“Niniii? Kuna nini kwani?”

Askari aliyekuwa makao makuu hakupata jibu lolote kutoka upande wa pili, askari aliyekuwa akiongea nae alihisi baridi kali ikipita katikati ya uti wake wa mgongo! Mikono yake ilikufa ganzi na simu ya upepo ilianguka chini!

“Vipi?” Mwenzake aliyekuwa jirani alimuuliza hata yeye pia hakumpa jibu zaidi ya kumwambia kuna matatizo yametokea.
Gari lenye namba zilizotajwa ndio lililokuwa limepita kama saa nzima kabla ya simu hiyo ya upepo kupigwa!

Hawakuamini kama bibi Nyanjige alikuwa ndani ya basi hilo kwani waliwakagua karibu watu wote ndani ya basi hilo isipokuwa mtu mmoja tu!
“Nafikiri aliyekuwa amejifunika khanga kwenye kiti cha mwisho kabisa nyuma ya basi, niliyetaka kumwamsha halafu wewe ukasema tuachane alikuwa bibi Nyanjige sasa tutafanya nini?”
 
Jaman hapo kwenye no msijari ipo sawa tu nimeshindwa kuedit
 
SEHEMU YA 34...

“Hakuna kingine isipokuwa kufuatilia mpaka tulipate basi hilo tumkamate na kumrejesha Dar es Salaam vinginevyo tutaonekana wazembe na kusababisha matatizo makubwa!”
Maaskari wote walikubaliana na kuingia ndani ya gari lao lililokuwa limeegeshwa pembeni na kwa kasi ya ajabu walianza kuondoka kuelekea mbele hofu yao kubwa ilikuwa kufukuzwa kazi na hiyo ndiyo iliwafanya wawe na usongo wa kulipata basi hilo na kumkamata bibi nyanjige, walikuwa wamefanya uzembe mkubwa ambao ungefanya wahusishwe na rushwa na kwa kosa hilo wangepoteza kazi zao.

“Hapana jamani mimi nahisi hiki kibibi ni kichawi, sasa pale kilitokea kitu gani mpaka tusimfunue kilemba chake kichwani?”:
“Hata mimi sielewi lakini kwa spidi waliyokuwa nayo ni lazima tutawapata tu!” ****************
Barabara ya Chalinze Segera ni miongoni mwa barabara zilizotengenezwa vizuri kupita zote nchini Tanzania! Ilikuwa ni barabara ya lami na aliyeitengeneza lami hiyo alikuwa ni mtaalam kweli kweli kwani ilikuwa ni mkeka wa nguvu! Magari yote yalipita katika barabara hiyo yalikimbia hadi kilometa mia mbili kwa saa.

Baada ya basi kuondoka eneo lilipokamatiwa dereva aliliendesha kwa kasi ya ajabu kiasi cha kuwatisha abiria, abiria wote walikuwa kimya roho zao zikiwa mikononi ilikuwa si rahisi kuamini gari hiyo ilikuwa ikisafirisha maiti! Dereva alipoangalia mshale wa kuonyesha kasi aligundua ulikuwa umegota mwisho!
Alishtuka lakini aliziamini tairi za gari lake zilikuwa na siku tatu tu tangu ziwekwe!

“Kanyaga moto mwanangu!” Kondakta wake alimchochea!
“Usiwe na shaka babu hii ni nenda ugaruke mwanangu!” Aliitikia dereva.
Bibi Nyanjige alikuwa bado amejifunika na khanga yake kichwani, kasi hiyo ilimshtua lakini hakuwa na la kufanya, aliendelea kumshukuru Mungu kwa kumuokoa! Mara kwa mara alijitingisha kama vile alikuwa na kwikwi za kilio, hakuongea kitu na mtu yeyote ndani ya basi, alijifanya mtu mwenye huzuni kupita wengine wote!
 
SEHEMU YA 35...

Kilometa kama hamsini na tano mbele yao basi lao lilikuwa likipandisha mlima na mbele yao lilikuwepo lori kubwa na tela lake lililokuwa likienda kwa mwendo wa taratibu sana, dereva wa basi lao alikerwa na kasi hiyo ya lori na kuamua kulipita kwa mwendo wa kasi.
Aliamua kufanya hivyo bila kujua kuwa mbele kulikuwa na lori jingine likija tayari walikuwa wamefika darajani!

Akiwa katikati ya lori alilokuwa akilipita alishtukia akikutana uso kwa uso na lori lililokuwa likija mbele yake, alijitahidi kukwepa na kugongwa mbavuni,basi lake lilianza kuyumba kutoka upande mmoja wa barabara hadi mwingine akielekea darajani.
Abiria ndani ya gari walianza kupiga kelele, ikabidi bibi Nyanjige ajifunue na kukuta watu wote ndani ya basi wakiwa wamesimama wima huku wakilia! Dereva alionekana kuchanganyikiwa.

Ghafla mlipuko mkubwa ulisikika tairi lilikuwa limepasuka! Basi likatoka barabarani na kuanza kuingia kwenye mtaro, mbele kidogo lilipinduka na kutumbukia katika daraja refu ambalo chini yake ulipita mto mkubwa uliokauka maji.

“Jamani ajali imetokea anayeweza kujiokoa afanye hivyo!” Ilikuwa ni sauti ya dereva.
Dirisha la upande wake lilipasuka, pamoja na uzee aliokuwa nao bibi Nyanjige alijivuta akatokeza nje na kusimama wima dirishani akiwa ameshika keria ya basi kwa juu!

“Stering hauwawi bwana!” Alisema bibi Nyanjige na kabla gari halijfika chini alirukia upande wa pili na kutua kwenye nyasi, alihisi kiuno chake kuteguka.

Akiwa hapo alishuhudia basi likijibamiza chini na kuzunguka kama mara tatu hivi ardhini, hakusikia tena kelele ndani ya basi ikawa kimya kabisa!

Hali iliyomfanya aamini kuwa watu wote ndani ya basi walikuwa wamekufa lakini sekunde chache baadaye alishuhudia watu wawili wakitoka ndani ya basi huku damu nyingi zikiwavuja, hawakuishi sana kwani walipotembea hatua chache mbele walianguka chini.
 
Back
Top Bottom