Huwezi Kuua Maiti -Erick Shigongo

Huwezi Kuua Maiti -Erick Shigongo

SEHEMU YA 16...

Kwa mara nyingine alipiga tena mluzi na kundi jingine kubwa la ndege aina ya Tai liliibuka na kuanza kuzizingira helkopta hizo lakini muda mfupi baadaye bibi Nyanjige alishangaa kuona ndege wengi wakianguka ardhini wakiwa wamekufa na kuijaza ardhi! Alishindwa kuelewa ni kitu gani kilitumika kufanya mauaji hayo ya ndege wake.

Alipomuokota ndege mmoja na kumnusa ndipo aligundua ndege wake waliuawa kwa sumu kali aina ya DDT! Helkopta zilizidi kusogea eneo alilokuwa na alishuhudia mipira ya maji ilimwaga aina Fulani ya maji maji na mvuke angani ndege wake wakazidi kuporomoka na hatimaye anga ikabaki wazi bila ndege hata mmoja.

Kifo cha ndege kilimtisha na alipoona hivyo alipiga mluzi kuamuru jeshi jingine liingie kazini na nzige wengi walivamia anga kwa makundi makundi lakini kama ilivyokuwa kwa ndege nzige nao waliporomoshwa kwa makundi makundi hadi ardhini.

Kuona hivyo bibi Nyanjige alianza kukata tamaa kwani aliona ni kiasi gani jeshi lake lilikuwa limepuputika, alikuwa amebaki na jeshi la tembo peke yake na hakujua kama tembo hao wangeweza kuhimili vishindo vya vita kali iliyokuwa mbele yake.

Wakati akiwaza hayo ghafla alianza kuwaona Tembo wakiduwaa na kuketi chini na hata yeye mwenyewe alianza kuhisi kulewa na muda mfupi baadaye bibi Nyanjige alipoteza fahamu kabisa na kulala ardhini, madawa yaliyokuwa yakimwaga na helkopta angani yalimlewesha bibi Nyanjige pamoja na Tembo wake. Kabla hajapoteza fahamu zake zote ni kitu kimoja tu alichowaza kichwani mwake. angefanywa nini baada ya kukamatwa KWA VIFO ALIVYOSABABISHA.
*
*

Meli zilizobeba askari wa nchi kavu wa Tanzania ziliingia katika mji wa Kalemii nchini Kongo na kubebwa katika magari tayari kwa safari ya kwenda msituni! Kulikuwa pia na vifaru vipatavyo sabini kwa ajili ya vita hiyo pia vilishushwa na kuendeshwa kuelekea msituni tayari kwa mapambano.

“Ni lazima akamatwe” Alisema kiongozi wa majeshi ya kongo yaliyojitolea kuyasaidia majeshi ya Tanzania mara baada ya kuwapokea askari wa Tanzania.
 
SEHEMU YA 17...

Tayari vita hiyo ilishachukuwa sura kubwa kuliko ilivyotegemewa kila askari alikuwa na hasira kali dhidi ya bibi Nyanjige na wengi walitamani kumwona huyo bibi aliyeitingisha dunia kwa uwezo wake mkubwa wa kushawishi wanyama kufanya mauaji ya kikatili, lilikuwa si jambo rahisi kuamini.

“Baada ya helkopta kumwaga sumu na kuwaua wadudu na pia kuwalewesha Tembo, ndege za kulipua mabomu zitapita na kuusambaratisha msitu baada ya kazi hiyo jeshi la nchi kavu litaingia msituni na kukamilisha kazi!” Alisema mkuu wa majeshi ya Tanzania.

Wakati jeshi la nchi kavu likiingia msituni ilitolewa amri kuwa helkopta zote zilizokuwa zikipita angani na kumimina sumu zisitishe zoezi hilo kwanza ili kutoa nafasi kwa ndege za kudondosha mabomu na ndege kama kumi hivi ziliruka na kuingia msituni ambako milipuko ya mabomu ilisikika kila mahali, wakati huo askari wa miguu waliendelea kutembea taratibu kuingia msituni.

Kwa jinsi mabomu yalivyolipuka hakuna mtu hata mmoja aliyeamini bibi Nyanjige angekuwa hai mpaka wakati jeshi la waenda kwa miguu linaingia msituni, kwani msitu ni kama uligeuzwa nje kuingia ndani! Ulifukuliwa kila mahali hapakuwa na mahali pa mtu kujificha.
“Ni lazima huyu bibi atakuwa amekufa lakini maiti yake ni ni lazima itafutwe twende nayo hadi Tanzania Rais wetu akaione bibi huyu amesababisha vifo vya watu wengi mno” Hayo ndiyo maongezi yaliyoendelea midomoni mwa askari wengi waliotembea kuingia msituni.

Baada ya mashambulizi ya mabomu yaliyodondoshwa na ndege nyingi angani, ilifuata hatua ya mwisho ya jeshi la nchini kavu kwa lengo la kwenda kupambana na tembo kama wangekuwa hai na kumkamata bibi Nyanjige ama kuitafuta maiti yake hadi ipatikane na kuondoka nayo! Kwa fikra za askari wengi vita hiyo ilikuwa imefika mwisho
 
SEHEMU YA 18...

Jeshi la askari wasiopungua elfu tano liliuvamia msitu huo mkubwa kwa ajili ya kazi hiyo, kila mahali walikopita walishangaa kuona idadi kubwa ya tembo wakiwa wamekufa na kusambazwa kabisa na mabomu lakini hawakumwona bibi Nyanjige mahali popote kila mtu aliamini bibi huyo alikufa katika mashambulizi hayo.
*
*

Hakikuwa kitu rahisi kwa bibi Nyanjige kufa kama walivyotegemea kwani dakika kama ishirini hivi kabla ya jeshi la nchi kavu halijauvamia msitu, bibi alirejewa na fahamu zake na kukuta kila upande wa mwili wake kuna Tembo mkubwa mnene aliyekufa na aliponyanyuka na kukaa kitako macho yake yalipambana na shimo kubwa lililochimbuliwa alijua hiyo ilikuwa ni kazi ya mabomu.

Aliendelea kusikia milipuko sehemu mbalimbali msituni, ndege zilikuwa zikidondosha mabomu, kwa hali hiyo ingawa alikuwa amelewa aliweza kunyanyuka na kujikongoja akipita katikati ya msituni chini ya miti michache iliyokuwa imebaki mbele alisimama alipoiona helkopta iliyoungua huku pembeni mwake kukiwa na maiti za wanajeshi wawili waliokuwa.

Wazo la kujiokoa lilimwijia kichwani mwake kwa sababu alijua wakati wowote angekamatwa, aliivamia moja ya maiti hizo na kuivua magwanda na kuyavaa na akachukua pia kofia na kuivaa kichwani mwake, alipomaliza tu kufanya hivyo alisikia nyasi nyuma yake zikitingishika na aliamini haukuwa upepo.

Walikuwa ni maaskari wa nchi kavu wa Tanzania! Walioibuka kutoka katikati ya nyasi wakiwa na silaha zao mikononi, moyo wa bibi Nyanjige uliingiwa na hofu kubwa na alianza kutetemeka akijua ni lazima angetiwa nguvuni na kuuawa. Pamoja na kuwa bibi kizee lakini alikuwa shupavu kuliko umri wake, alijiangusha karibu kabisa na maiti aliyoivua magwanda.

Kwa jicho la pembeni aliwashuhudia askari wakitembea kuelekea mahali ilipokuwa helkopita iliyoungua, kila mmoja wao alisikika akiongea kwa huzuni hasa walipoziona maiti zikiwa zimelala pembeni, wao waliamini miili yote mitatu iliyolala chini ilikuwa maiti hawakujua kama mtu waliyekuwa wakimsaka alikuwa miongoni mwa miili hiyo.
 
SEHEMU YA 19...

“Masikini hawa ni askari wetu kabisa. Hakyanani huyu bibi tukimtia mikononi tutamchanana vipande viwili!” Alisema mmoja wa askari hao kwa hasira huku akirukaruka kuonyesha hasira aliyokuwa nayo.
Wengi wa maaskari walipoziona maiti hizo walilia machozi kwa uchungu na kila mmoja wao alionyesha hasira aliyokuwa nayo juu ya bibi Nyanjige.

Bibi Nyanjige alisikia kila kitu kilichoongelewa na askari hao na kuzidi kuingia na hofu! Alibana mbavu ili asionekane akihema, alijua kama angegundulika ni lazima wangemuua kikatili kuliko ilivyowahi kutokea duniani.
“Sasa tufanye nini?” Mmoja wa maaskari alimuuliza mkuu wa jeshi.

“Tusonge mbele vijana wengine wachukue hizi maiti tatu wazipeleke hadi tulipoyaacha magari, wazipakie wakati tukisubiri utaratibu wa kuzirudisha nyumbani baada ya vita ya leo, sawa?” Alisema mkuu wa majeshi na vijana watatu walijitokeza wakaimana na kuibeba miili hiyo begani hakuna hata mmoja aliyehisi kuwa mmoja kati ya miili waliyoibeba ulikuwa ni wa mtu hai! Bibi Nyanjige alizidi kubana pumzi.

Alilala begani kwa mmoja wa maaskari hao bila kujitingisha huku akihema mara moja kila baada ya dakika moja ili asingundulike! Alijua kama mbavu zake zingecheza ni lazima askari angeshtuka na kupiga kelele na huo ndio ungekuwa mwisho wake.

Mpaka wanafika yalipokuwa magari na kuitupa miili hiyo ndani ya gari hakuna askari hata moja aliyehisi mwili mmoja kati ya walioipakia ulikuwa ni wa bibi Nyanjige tena akiwa hai.

Maaskari waliondoka mbio kuwafuata wenzao msituni na muda mfupi baadaye maiti zilizidi kusombwa na kurundikwa ndani ya gari huku bibi Nyanjige akiendelea kugandamizwa na kuumia! Maiti zaidi ya hamsini zilipangwa juu yake.

“Hawanipati ng’o”Aliwaza bibi Nyanjige huku akizididi kutiririkiwa na damu kutoka katika miili ya watu waliokufa.
 
SEHEMU YA 20...

Msako wa kumsaka bibi Nyanjige porini uliendelea kwa masaa karibu kumi na mbili bila mafanikio yoyote! Nyumba yake ilisambaratishwa na mashimo mengi yalifukuliwa akitafutwa lakini bado hakuonekana mahali popote wanajeshi walikata tamaa na kuamini alikuwa amekufa.

Miili mingi ya tembo wakiwa wamekufa ilionekana kila mahali msituni, ndege na nzige waliokauka pia walionekana ardhini ilikuwa si rahisi kuiona ardhi sababu ya wingi wa ndege na nzige walioifunika.
Siku hiyohiyo jioni iliamriwa maiti zote zilizokuwa zimekusanywa zisafirishwe kurudi Tanzania wakati kukiwa na mpango kamambe wa kuendelea na operesheni kumsaka bibi Nyanjige siku ya iliyofuata.

Baada ya kauli hiyo ya mkuu wa majeshi maiti zote zilianza kuhamishwa kutolewa kwenye gari na kufungwa katika mifuko maalum ya nailoni tayari kwa kusafirishwa kurudishwa Tanzania, bila kugundulika bibi Nyanjige alifungwa ndani ya mfuko na kupakiwa katika ndege maalum iliyoandaliwa.

Dakika kama mbili hivi baada ya kuwekwa katika mfuko wa nailoni akiwa amepangwa ndani ya ndege bibi Nyanjige alianza kukosa hewa! Alihisi angekufa sababu ya kukosa hewa safi, Kwa kutumia meno yake makali alitoboa tundu katika mfuko wake na kuitega pua yake kwenye tundu hilo akawa anavuta hewa taratibu kutoka nje.
*
*

Ndege ilipoingia Dar es Salaam saa nne ya usiku maiti zote zilipakuliwa na kupakiwa ndani ya gari maalum lililoandaliwa tayari kwa kuzipelekea chumba cha maiti cha hospitali ya jeshi iliyoitwa Military general hospital kuhifadhiwa katika chumba chenye baridi ili zisiharibike zikisubiri operesheni imalizike na wote waliokuwa wazikwe siku moja kwa heshima ya jeshi.

Masaa matatu baada ya kuingizwa katika chumba cha maiti baridi kali iliyokuwemo ndani ya chumba hicho ilimfanya bibi Nyanjige ahisi mwili wake ukiganda aligundua asingeweza kuendelea kuwa ndani ya chumba hicho kwa muda mrefu kabla roho yake haijatoka.
 
Back
Top Bottom