SEHEMU YA 15
...Asubuhi ya siku hiyo msitu ulikuwa kimya kabisa, ni ndege tu waliopiga kelele wanyama wengine walikuwa kimya! Tembo wengi walikusanyika katikati ya msitu wakiwa wameiweka nyumba ya bibi Nyanjige katikati kuhakikisha usalama wake.
Ndege aina ya Tai ambao idadi yao ilikuwa si rahisi kuifahamu walionekana wakiruka angani, walikuwa tayari kwa hatari yoyote ambayo ingetokea na walikuwa na ufahamu kuwa wakati wowote msitu ungeweza kuvamiwa tena.
Kwa amri waliyopewa na bibi Nyanjige kama wangevamiwa Tembo na nzige wangeendelea na vita vya nchi kavu na ndege aina ya Tai, Kunguru na mwewe wangeendelea na vita vya angani wakipambana na na ndege zilizotegemewa kuuvamia msitu. Hali ya vita ilinukia kila mahali,kilichokuwa kikisubiriwa wakati huo ni kuwasili kwa maadui.
Masaa machache baadaye miungurumo wa ndege za kivita ilisikika angani upande wa mashariki, bibi Nyanjige aliponyanyua uso wake kuangalia angani aliziona ndege kumi zikipita na alipozisoma kwenye mabawa yake aliliona neno TAN na zilikuwa na nembo ya Twiga nyuma yake alijua ndege hizo zilikuwa ni za jeshi la Tanzania.
Bila kuchelewa alipiga mluzi kwa sauti ya juu ili kuashiria kuwa sasa mambo yalikuwa tayari na palepale makundi yote ya ndege waliokuwa wakizunguka angani walizizingira ndege zote tatu na kuziweka katikati kisha wakaanza kutoboa vioo vya ndege hizo kwa mbele na kuingia hadi ndani ambako walianza kuwashambulia marubani kabla hawajafanya jambo lolote.
Ndege walifanya hivyo kwa ndege ya kivita moja baada ya nyingine hatimaye ndege zote kumi zilianguka chini na kulipuka! Mamia ya ndege pia walilipuliwa na moto.
*
*
Bibi Nyanjige aliyekuwa bado yu katikati ya kundi kubwa la tembo alishuhudia mashambulizi ya ndege wake na kuhisi ushindi! Lakini ghafla alishtuka alipoona helkopta tano zikiruka kutoka upande mwingine wa msitu na vitu kama mipira ya maji ilichungulia kutoka ndani ya helkopta hizo, alijua tayari vita nyingine ilikuwa imefika.