Huwezi Kuua Maiti -Erick Shigongo

Huwezi Kuua Maiti -Erick Shigongo

SEHEMU YA 61

“Hapa nilipo si rahisi kuniona ila nahitaji kuwa na mahali pa kuishi na safari hii nitaishi ardhini ambako hakuna mtu awaye yote ataniona hata wakija kunitafuta hawatanipata ninachohitaji ni maji na chakula, nitakaa ardhini kwa siku nne bila kutoka nje siku ya tano nitatoka nafikiri hali itakuwa shwari, kazi yangu sasa itakuwa ni kuunda jeshi tu!” Aliwaza bibi Nyanjige kisha kuanza kutafakari ni kwa njia gani angeweza kupata mahali pa kuishi.

“Kwanini nisichimbe ardhini?”Aliwaza bibi Nyanjige na kukubaliana na wazo hilo na bila kuchelewa alipiga mluzi wa ajabu kwa muda wa kama dakika tano hivi, walitokeza wanyama wawili wadogo na wafupi kimo cha Paka , walikuwana mikia mikubwa ya rangi nyeupe! Walikimbia mbio hadi miguuni kwa bibi Nyanjige na mmoja alimrukia mikononi akambeba kama mtoto!

Bibi Nyanjige alipiga tena mluzi wa aina nyingine na wadudu wale kama mshale walirukia ardhini na kuanza kuchimba ardhini! Udongo uliruka kama uliotupwa na mashine ya kuchimba kisima, katika muda wa kama dakika ishirini hivi hawakuonekana ardhini na shimo refu kupita kiasi lilishachimbwa ardhini!

Kazi hiyo iliendelea kwa muda kama masaa mawili ndipo bibi Nyanjige aliposikia mlio fulani wa wanyama hao kutoka shimoni aliielewa maana yake na kuanza kuteremka shimoni taratibu akikanyaga pembezoni mwa shimo hilo na kuzidi kushuka chini, ilimchukua muda wa masaa mawili kufika chini ambako aliwakuta wanyama hao wamelala kifundifundi ardhini! Walionyesha kuchoka.

Kulikuwa na kiza kila mahali ndani ya shimo hilo lakini kwa msaada wa macho ya wanyama hao ambao macho yao yalimulika kama tochi yenye mwanga mkali bibi Nyanjige aliweza kuona, hakuwa na tatizo la hewa kwani wanyama walitoa aina fulani ya hewa kutoka katika mapafu yao iliyoondoa gesi na hewa nzito shimoni.

Ni wanyama hao ndio waliomtunza bibi Nyanjige shimoni kwa siku zote tatu alizokaa shimoni alikula matunda na ni wanyama hao waliokwenda mtoni kunywa maji na kwenda kumtemea mdomoni aliposikia kiu.
 
SEHEMU YA 62

Wanajeshi kumi na mbili waliongizwa shimoni kuchunguza wote hawakurudi juu wala kutingisha kamba ili watolewe, hali hiyo ilizidi kuwatia wasiwasi wanajeshi wote.
“Hebu ngojeni niende mwenyewe inawezekana hawa vijana wanafanya mchezo humo ndani!”Alisema mkuu wa majeshi akafungwa kamba kiunoni na kuanza kushushwa taratibu kuelekea shimoni, mwili wake ulitetemeka kwa hofu.

Sababu ya mafunzo ya judo aliyoyapata huko China alikuwa tayari kwa lolote ambalo angekutana nalo ardhini, alipotua tu chini naye mzizi ulimzunguka shingoni kwa sababu hakuwa legelege alifanikiwa kuuondoa mzizi na kumtupa mtu aliyeweka mzizi huo shingoni pembeni, mara alisikia kitu kama mluzi na ghafla ukipigwa viumbe kama Paka vilimrukia usoni na kuanza kumng’ata na kumrarua vibaya usoni, lakini tayari alishaitingisha kamba na wanajeshi waliokuwa nje walianza kumvuta kwa nguvu.

“Jamani ni hatari!” Alisema baada ya kufika juu.
“Kuna nini?”
“Bibi……!” Kabla hajamaliza sentensi yake Kamanda alikata roho.
“Yaani bibi Nyanjige ndiye amemfanya hivi kamanda wetu kama yumo humu ndani basi hakuna la kufanya zaidi ya kutumbukiza bomu na huu ndio uwe mwisho wake!”

‘Lete bomu?”
“Hili hapa!”
“Na wenzetu waliomo ndani je?”
“Nina uhakika hao hawawezi kuwa hai, weka bomu shimoni tu!”Alisema msaidizi wa kamanda na bomu lilitupwa ndani ya shimo, kilichofuata hapo ni mlipuko mkubwa sana.

Itaendelea.
 
SEHEMU YA 63

Risasi za Msaidizi wa Mkuu wa 
Majeshi zilichimba sentimita 
chache kutoka kwenye kichwa cha bibi Nyanjige. bila shaka alidhamiria kumuua kutokana na maneno machafu aliyopewa.

Msaidizi yule wa Mkuu alikerwa na bibi Nyanjige kupita kiasi kutokana na maneno yake ya dharau. Pamoja na kuelewa ukweli kuwa bibi Nyanjige ana uwezo mkubwa na ameshalisumbua sana jeshi mpaka hapo walipompata, kitendo cha kuwatambia kwamba atawamaliza kilimchefua zaidi.

Dereva wake alisimama katika namna ya kumchunga bosi wake asichukue hatua mbaya ya mauaji. Hakuona sababu ya kumuua wakati kulikuwa na kila uwezekano wa kumchukua na kumpeleka jeshini.

Bibi Nyanjige kama ambaye alikuwa amesoma mawazo ya Msaidizi wa Mkuu yule wa majeshi. Alimtazama kwa sura ya dharau ya hali ya juu. Nia yake ikiwa ni kumjaza hasira zaidi Mkuu huyu ili ampige risasi.

Alikuwa radhi kufa kwa risasi, kuliko kufikishwa mbele ya wakuu wa majeshi ambao kutokana na jinsi alivyowaudhi na kuwachanganya, alijua lazima atapata mateso makubwa na mabaya sana. Njia bora aliyoiona ilikuwa ni kuendeleza bidii ya kuwaudhi wawili hawa, pengine lengo la kupigwa risasi na kufa pale pale lingekamilika na hivyo kumuepushia na sokomoko ambalo angelipata huko jeshini atakapopelekwa.

“Nyie Manguruwe pori!.. Nasema kama wanaume kweli vifyatueni hivyo vibunduki vyenu viniue niende zangu peponi. Mbwa wakubwa nyie. Kwanza vijanaume gani vinakuwa vipumbavu-pumbavu kama hivyo.

Mnamshikia bunduki bibi kizee kama mimi huku mnatetemeka! Niueni sasa mkione cha moto!-Washenzi wakubwa!!” Maneno haya yalimfanya Mkuu wa majeshi kukurupuka na kumnyang’anya bunduki dereva wake na kumwekea bibi Nyanjige kichwani, akataka kufyatua, dereva wake akamsukuma kidogo na kumnyang’anya bunduki.

Risasi iliyofyatuliwa kwa mara nyingine ikachimba ardhi badala ya kichwa.
“Kwa nini unanizuia?” Mkuu alimjia juu dereva wake ambaye aligwaya ghafla.
“Nasema kwa nini unanizuia? Huoni maneno anayoyasema mshenzi huyu yanavyochefua? Unafikiri huyu anafaa kufikishwa jeshini-keshatia hasara ngapi? Nani ana haja ya kumuona akiwa hai?”
 
SEHEMU YA 64

Bibi Nyanjige akaingilia kati akimwita Mkuu yule ambaye alielekea kuingia kwenye mtego wa bibi Nyanjige kwa kupandwa na jazba.
“We mwanamke!! Unamfokea mwenzako wakati nimeshakupa ruhusa ya kuniua na ...” Kabla hajaongeza neno zaidi, Msaidizi wa Mkuu wa Majeshi akatupa teke zito, likampata chini ya kidevu.

Bibi Nyanjige akatoa mguno mkubwa wa maumivu. Akajinyonganyoga pale sakafuni huku akihisi ladha yenye chumvi ya damu kutoka kinywani mwake. Akalia kwa uchungu wa maumivu yale.
Mkuu wa majeshi alimgeukia dereva. “Unaona.. Unaona?”

“Sikiliza Mkuu, huyu usimuue, hebu punguza hasira na ukumbuke maagizo tuliyopewa, kwamba tumfikishe huyu akiwa hai mbele ya Wakuu.”
“Amenitia hasira sana, hawezi kunidharau namna hii”.

Dereva aliinama kumwangalia bibi Nyanjige kama yu hai, maana teke alilopigwa na Mkuu wake lilikuwa ni zito kiasi kwamba bibi yule alijinyonga kidogo kisha akalala kimya.

Akagundua kwamba ameumia mno. Kwa kuchanganya na majeraha mengine aliyokuwa ameyapata kutokana na kipigo cha wamasai, Bibi Nyanjige sasa alikuwa hajiwezi. Alikuwa akivuja damu na kuvimba karibu mwili mzima, hii ilimfanya aanze kufikiria upya kuhusu namna ya kumpeleka kwa Wakuu wa Majeshi.
“Mkuu, huyu ameumia sana, tufanyeje?”
“Hawezi kutembea?” Mkuu ambaye alikuwa ameegemea gari na kuangalia upande mwingine, alionekana kupunguza makali ya hasira zake.

“Nadhani, buti ulilompiga ni kubwa sana kwa mtu kama huyu, anaweza kufa kabla ya kufikishwa Makao Makuu”.
“Unafikiria nini sasa?” Sauti ya Mkuu ilishapoa.
“Huyu anahitaji matibabu, Mkuu”
“Na akifia hospitali?”

“Tusifikiri hivyo mapema, maana kama suala ni kifo anaweza kufa hata wakati tuko njiani kumpeleka Makao Makuu.”
Mkuu aliendelea kubaki nyuma ya gari huku akili yake ikifanya kazi haraka haraka juu ya nini cha kufanya.
 
Back
Top Bottom