SEHEMU YA 51...
Magari matatu yakiwa na askari wapatao sitini yaliondoka makao makuu ya jeshi kwenda kijiji cha Kiambali, kwa sababu walimfahamu bibi Nyanjige na maajabu yake waliondoka na silaha za kutosha, kila mwanajeshi akiwa na bunduki yake na pia mabomu.
“Kama ni yeye basi mkamlete akiwa hai!”
“Sawa mkuu!”
*
*
Kutoka jijini Dar es Salaam hadi kijiji cha Kiambali kupitia Kibaha, Chalinze ulikuwa ni mwendo wa masaa manne waliingia kijijini hapo majira ya saa nane mchana! Wote walishangazwa na hali waliyoikuta, ng’ombe waliokuwa wakikimbia huku na kule mikia ikiwa imenyooka, walionekana kama wamepatwa na kichaa mamia ya watu walikuwa wamelala ardhini wakivuja damu na wengine walikuwa wakichomwa kwa pembe za ng’ombe ardhini, wengi walikuwa wamekufa.
Dereva aliegesha gari lake na wanajeshi walianza kushuka taratibu kutoka garini bunduki zao zikiwa tayari kufanya kazi, ghafla walishitukia kundi kubwa la ng’ombe kama mia mbili likija kwa kasi kuelekea mahali walipokuwa wamesimama,wanajeshi wote walihisi hatari.
“Jamani hawa ng’ombe hawana kichaa kweli?” Maaskari waliulizana na kuwageukia vijana wa kimasai.
“Nyie vijana vipi hawa ng’ombe wenu?”
“Hata sisi hatuelewi kabisa tuliacha hali ni shwari kabisa hapa kijijini sijui kimetokea nini!”
Wakati wakiongea hayo tayari ng’ombe walishafika na kuanza kuwashambulia wanajeshi kwa pembe zao kali, walijaribu kupiga risasi lakini haikusaidia ng’ombe walizidi kuja mbio, baadhi ya wanajeshi walirusha hata mabomu yalipolipuka yaliua ng’ombe wachache!Makundi mengine makubwa zaidi ya ng’ombe yalizidi kujitokeza na kuwashambulia wanajeshi! Kifupi hali ilitisha.
Wakati yote hayo yakitokea mkuu wa majeshi alikuwa bado hajateremka garini, hali aliyoishuhudia ilimtisha, badala ya kushuka alijikuta akifunga mlango wa gari zaidi! Hakuna kilichokuwepo zaidi ya kujiokoa na alilazimika kumwamuru dereva aliondoe gari kuokoa maisha yao.
Ni wao tu wawili waliokoka hata vijana wa kimasai pia walikufa katika mashambulizi hayo ya ng’ombe! Lilikuwa ni tukio la ajabu katika historia ya Tanzania.