Huduma bandari ya Dar Es Salaam hazijasimama, puuzeni uzushi

Irene Darton

Member
Feb 25, 2024
18
21
Jamii imepewa wito wa kupuuza taarifa zinazoenea hivi karibuni zikieleza kuwa shughuli za uendeshaji katika Bandari ya Dar es Salaam zimesimama badala yake inapaswa kufahamu kuwa Bandari hiyo imekuwa ikifanya kazi kwa saa 24 tena ikitumia teknolojia ya kisasa katika kurahisisha zoezi la utoaji wa huduma.

Akizungumza na wanahabari usiku wa kuamkia leo, Jumatatu, Machi 04.2024 akiwa Bandarini hapo Afisa utekelezaji Bandari ya Dar es Salaam kutoka idara ya Kichere Agapi Kasebele amesema Bandari hiyo haijawahi kusimamisha shughuli zake kwa sababu yoyote ile badala yake imekuwa ikiongeza wigo wa utoaji huduma kwa kutumia teknolojia ambazo zinasaidia wateja na wadau wa Bandari kwa ujumla wake kuhudumiwa kwa haraka tofauti na ilivyokuwa huko nyuma.

Amesema idara hiyo ya Kichere ambayo kwa kawaida inahusika na ushushaji wa mizigo kama vile Ngano, Sulphur, Mbolea nk kwa usiku huo pekee imekuwa ikishusha shehena ya Ngano ya tani 46,000 (Elfu Arobaini na Sita), ambayo kwa shifti moja (1) inashusha tani 3,000 (Elfu Tatu), huku kwa siku moja ambayo inahusisha shifti tatu (3) inaweza kushusha tani kati ya 9,000 (Elfu Tisa) hadi 10,000 (Elfu Kumi) huku akibainisha kuwa meli hiyo ya tani 46,000 inamaliza kushusha mzigo kati ya siku nne (4) hadi tano (5).

Kwa upande wake Mahmoud Ramadhan Makanyaga ambaye ni mfanyakazi wa kampuni ya Shipping line (Chinese - Tanzania Shipping Company) ameupongeza uongozi wa Bandari ya Dar es Salaam kwa kufanikisha urahisishaji wa kazi kwenye eneo hilo kwa kuwa kwa sasa meli zao zimekuwa zikimaliza kushusha mzigo kwa haraka pindi zinapotia nanga Bandarini hapo.

Ametolea mfano kuwa moja ya meli wanayoifanyia kazi iliyoingia Februari 28 mwaka huu ikiwa imebeba mizigo mchanganyiko, kwa sasa inamalizia kushusha mzigo kisha iondoke kurejea nchini China.

Baadhi ya wadau na watumiaji wa Bandari hiyo wakiwemo Mzee Bure Abdallah na Alexander Bukuku ambao ni madereva wamewaeleza wanahabari kuwa kwa sasa hawapati usumbufu katika kutoa mizigo yao badala yake wamekuwa wakihudumiwa kwa haraka, huku wakitumia fursa hiyo kupongeza uwekezaji uliofanyika kwenye mifumo ya kiutendaji (teknolojia) ambapo afisa wa eneo moja anaweza kuwasiliana na wa eneo jingine kwa haraka hasa kwenye masuala ya uhakiki na ukaguzi.

Naye, Juma Abdrehman Juma ambaye ni Afisa Mwandamizi kutoka mamlaka ya usimamizi wa Bandari nchini (TPA) kitengo cha General Cargo inayohusisha mizigo mchanganyiko amesema kwa usiku huo pekee Bandari ya Dar es Salaam inahudumia meli nne (4) kwa pamoja zikiwa zimebeba mizigo tofauti ikiwemo Magari, vyuma vya Reli, Mabomba, Makontena nk
 
Back
Top Bottom