Lowassa aingiza serikali matatani
Mwandishi wetu's picture
Na Mwandishi wetu - Imechapwa 10 March 2010
Edward Lowassa
MAAMUZI ya serikali yaliyotolewa wakati wa waziri mkuu aliyejiuzulu, Edward Lowassa, yataitia hasara ya zaidi ya Sh. 8 bilioni, MwanaHALISI lina taarifa.
Hasara hiyo inatokana na Mahakama Kuu, Kitengo cha Biashara kuiamuru serikali kulipa kiasi hicho kwa kampuni ya Empire Properties Limited, ambayo majengo yake yaliyoko jijini Dar es Salaam, yalibomolewa mwaka 2006.
Taarifa zinasema mwaka 2006, Lowassa aliamuru kufanyika ukaguzi wa majengo, hasa ya ghorofa, yaliyojengwa kiholela jijini Dar es Salaam na kuwachukulia hatua wanaohusika.
Jengo la Empire Properties Limited, lililopo makutano ya barabara ya Mwaya na Toure, Masaki yalikuwa miongoni mwa yaliyokaguliwa na hatimaye kuvunjwa kwa madai yalijengwa kinyume cha taratibu.
Lakini, kupitia hukumu ya kesi Na. 66 ya mwaka 2006 iliyosomwa 8 Januari mwaka huu, na Jaji A. Nchimbi aliamua kuwa uvunjwaji wa majengo hayo ulikuwa batili na sasa manispaa ya Kinondoni iliyoshiriki kuyavunja inatakiwa kulipa fidia.
Uamuzi wa mahakama unakuja wakati viongozi serikalini, Chama Cha Mapinduzi (CCM) na baadhi ya vyombo vya habari, wamekuwa wakijitahidi kumsafisha Lowassa kutokana na kashfa ya Richmond iliyosababisha ajiuzulu Februari 2008.
Malipo haya yaweza kuibua madai mapya dhidi ya Lowassa na halmashauri ya manispaa ya Kinondoni na kusababisha mradi wake wa kujisafisha kuwa mgumu zaidi au kukwama kabisa.
Wakati kesi ikinguruma, manispaa ilidai kwamba ujenzi wa majumba hayo ulikiuka kibali cha ujenzi. Majengo hayo ambayo hayakuangushwa yako Kitalu Na. 383, Masaki.
Kwa mujibu wa manispaa ya Kinondoni, kibali cha ujenzi kilichotolewa kwa kampuni hiyo chenye Na. 0000500 kilikuwa kwa ajili ya ujenzi wa jengo lisilozidi ghorofa tatu tu.
Lakini manispaa ilidai mahakamani kwamba kampuni hiyo ilikuja baadaye kujenga ghorofa nane, jambo ambalo lilikuwa kinyume cha kibali kilichotolewa.
Kati ya Mei 15 na 17 mwaka 2006, askari wa manispaa ya Kinondoni walianza ubomoaji huo kwa kuanzia na ukuta ambao nao walidai ulijengwa kinyume cha maagizo ya kibali.
Hata hivyo, katika mahakama hiyo, kampuni ya Empire iliwasilisha kibali Na. 0000600 kilichotolewa na manispaa hiyo, ambacho kinaonyesha kampuni hiyo ilipewa idhini ya kujenga jengo la ghorofa nane.
Manispaa ya Kinondoni inadai kwamba kibali hicho kilighushiwa na hakikutolewa na wao.
Lakini katika hukumu yake hiyo, Jaji Nchimbi amesema kuwa manispaa hiyo imeshindwa kuthibitisha kwamba kibali hicho kilikuwa batili.
Hiyo ilikuwa baada ya ushahidi wa wataalamu wa mambo ya maandishi kuithibitishia mahakama kwamba vibali hivyo vilitoka katika manispaa hiyo hivyo vilikuwa halali.
John Emmanuel Bunga, mmoja wa Watanzania wa kwanza kusomea mambo ya maandishi ya kughushi, ndiye alitoa ushahidi kuonyesha vibali hivyo viwili, Na. 500 na Na. 600, vyote vilitolewa na manispaa ya Kinondoni.
"Manispaa imeshindwa kuthibitisha kwamba kibali hicho kilighushiwa. Kwa sababu hiyo, naagiza Empire walipwe kiasi cha Sh 8,047, 814,000 kama fidia ya hasara iliyopatikana," alisema Jaji Nchimbi.
Pamoja na kiasi hicho cha fedha, Jaji Nchimbi pia aliamuru malipo ya riba ya asilimia 12 inayoanza kuhesabiwa tangu siku ambayo kesi hiyo ilifunguliwa hadi malipo ya mwisho yatakapofanyika.
Katika mwaka huu ambapo mapato ya serikali yamepungua kwa kiasi kikubwa na uchaguzi mkuu ukitarajiwa kutumia fedha nyingi, serikali haitarajiwi kuwa na uwezo wa kulipa.
Serikali itakuwa ikilipa Sh. 965,737,680 kila mwaka hadi itakapomaliza kulipa deni hilo lote.
Kampuni hiyo ya Empire ilikuwa imeomba kulipwa fidia ya Sh 14 bilioni kutokana na kuvunjiwa kwa majengo hayo.
Kiasi hicho kilitakiwa kufidia hasara ya vitu vilivyoharibiwa, hasara ya kukosa wapangaji, mkopo wa ujenzi ambao kampuni hiyo ilichukua ili iweze kujenga na riba ya hasara ya kifedha iliyopatikana.
Kwa mujibu wa mthamini wa majengo aliyetoa ushahidi mahakamani, majengo mawili yaliyokuwa kwenye kitalu hicho, yalibomolewa kwa kiwango cha asilimia 45 na 55.
Jaji Nchimbi alipunguza kiasi hicho hadi kufikia Sh. 8 bilioni kwa sababu Empire hawakusema kiasi cha mkopo kilichochukuliwa na pia ugumu wa kuthamamisha hasara ya kupangisha kwa vile majengo yalikuwa hayajaanza kutumika.
Jaji Nchimbi alisema kimsingi, kesi hiyo ilikuwa na mambo makuu manne; kubainisha iwapo ujenzi wa majengo hayo haukufuata maelekezo ya kibali, kubainisha iwapo ubomoaji huo ulifuata sheria, iwapo fidia inatakiwa kulipwa na ni kiasi gani kinahitajika kulipwa.
Kumekuwa na kauli tofauti kuhusu nani hasa alitoa amri kwa manispaa ya Kinondoani kuvunja majengo ya Empire.
Wakati kuna waliomtaja Lowassa moja kwa moja, wengine walisema alikuwa Ritha Mlaki aliyekuwa naibu waziri wa ardhi na maendeleo ya makazi.
Manispaa ya Kinondoni tayari imekata rufaa kupinga hukumu hiyo na rufani inatarajiwa kuanza kusikilizwa wiki hii.
Taarifa za ndani zinasema ofisi ya Lowassa kwanza ilitaka manispaa ya Kinondoni ivunje majengo ya Empire; lakini walipokataa, ofisi hiyo ikataka uongozi wa polisi kanda ya Dar es Salaam usimamie uvunjaji.
Ilikuwa baada ya polisi nao kukataa kushiriki kuvunja majengo ya Empire ndipo juhudi zilifanywa kuleta vijana wa Jeshi la Kujenga Taifa, Ruvu kuja kufanya kazi hiyo ambayo sasa itaigharimu serikali mabilioni ya shilingi.
Mwanzoni mwa mwaka huu, gazeti hili liliandika kuhusu namna Lowassa alivyoamuru malipo ya Sh. 10 bilioni kwa kiwanda cha General Tyre cha Arusha ambazo ni kama zimepotea.
Akiwa waziri mkuu, Lowassa aliamua kuanzisha mradi wa bei mbaya wa kutengeneza mvua kwa kutumia wataalam kutoka Thailand.
Kabla serikali haijatupa rasmi mpango huo, Lowassa alikuwa tayari amejiuzulu uwaziri mkuu na serikali ilikuwa imekwisha kulipa kiasi cha Sh. 10 milioni kwa ajili ya mradi huo wa Lowassa.