Kanungila Karim
JF-Expert Member
- Apr 29, 2016
- 20,746
- 25,638
HADITHI: Sundi
MTUNZI: Ally Mbetu
SEHEMU: 01
SUNDI
Ndoa ni jumba lililo na pande mbili yaani nje na ndani.Aliye nje anatamani kuingia ndani na walio ndani wapo wanaofurahia kubakia na kutotamani kutoka nje lakini wengine kwao kama jehanamu wanatamani kutoka na waliotoka hawataki kurudi tena na wengine waliotoka kwa uzembe wao huenda kwa watalamu kuwapa dawa ambazo huwarudisha ndani.Vile vile wapo walio nje ambao wanatamani kuingia ndani lakini bahati hiyo hawana.Nao huangaika kwa waganga wa kienyeji au makanisani kuombewa ili nao waingie ndani na ndiyo nikasema ndoa inamitazamo miwili nje na ndani Ili kuyajua yote unagana na mtunzi ALLY MBETU
*********
Sundi akikaa pembeni ya mama yake akiwa amesongwa na mawazo juu ya siri ya ndoa ambayo kila kukicha ilimchanganya. Ilikuwa ni muda wa wiki tatu toka ampate mchumba kanisani aliyemuahidi kumuoa. Lakini swali lilikuja mbona mawazo yake ya awali ya kuomba usiku na mchana kuolewa umemtumbukia nyongo.
Baada ya kupata tu mchumba mtu wa kwanza kumpa taarifa alikuwa mama yake mdogo ambaye ndiye aliyekuwa shoga yake mkubwa. Siri zote alimpelekea yeye kabla ya kumfikia mama yake au dada zake, mama yake mdogo alikuwa mfanya biashara na hakuwa na mume baada ya kuikimbia ndoa yake baada ya manyanyaso ya mume na wifi zake.
Ndiye aliyemsimamia kila kitu katika masomo yake na kumnunulia akitakacho bila kuhoji kina gharama gani. Kitu kilichofanya Sundi amuone mama yake mdogo ni zaidi ya mama yake bali rafiki. Baada ya kuwa na mahusiano ya kimapenzi na kijana mmoja ambaye alimpenda kama alivyo mpenda.
Kijana yule alipofikia hatua ya kutaka kwenda kwao kujitambulisha, ndipo Sundi alipompelekea taarifa mama yake mdogo ili amsikie anasemaje. Siku hiyo alikwenda hadi kwa mama yake mdogo na kumueleza siri yake ya kupata mwenza.
Alimkuta mama yake mdogo akijiandaa kwenda kuoga baada ya kurudi kwenye shughuli zake za kutwa nzima. Mama yake alipomuona kwa uzoefu alimgundua mwanaye amekuja na kitu gani.
"Sundi mwanangu karibu.”
“asante mama.”
“Kwema?” alimuuliza huku akimtazama usoni.
Kwe,,,kwema ma' mdogo,” Sundi alibabaika kujibu.
“Hapana Sundi kuna kitu kunakusubumbua," mama yake alimwambia kwa sauti ya upole.
"Ma' mdogo umejuaje?"
"Mi' mkubwa ninajua mtu yupo katika hali gani pia we si mgeni kwangu."
"Ni kweli ma mdogo."
"Ehe una tatizo gani mwanangu kipenzi?"
"Ma' mdogo nimepata mchumba."
"Mchumba? Mmh, makubwa," kauli ile ilimshtua sana Sundi na kutaka kujua kwa nini mama yake mdogo amejibu vile.
"Ma' mdogo mbona unanitisha?"
"Sikutishi mwanangu mbona haraka sana?"
"Ma' mdogo miaka ishirini na tatu unaniona bado mdogo?"
"Tena sana."
"Ma' mdogo mbona da Monika kaolewa na miaka kumi na nane?" Sundi alimuuliza mama yake.
"Ni kweli dada yako kaolewa na miaka kumi na nane, lakini mwanangu ndoa mtihani ndoa ni vita ndoa ni jahanamu na ndoa ni pepo ya duniani."
"Una maana gani?"
"Mwanangu ndoa inahitaji ukomavu wa akili vilevile inahitaji bahati ya kuolewa na mwanaume akupendae mwenye mapenzi ya kweli mwenye utu moyoni mwake."
"Nina imani huyu niliyenaye ana mapenzi ya dhati kwangu."
"Hata mimi nilijua hivyo na kumuona baba yako mdogo ananipenda,lakini.."Ma mdogo alinyamaza na kuinama chini na kutulia kwa muda kiganja cha mkono wa kulia kikiwa juu ya paji la uso.
Alitulia kwa muda kitu kilichomshtua Sundi, lakini alikuwa mzito kumuhoji mama yake. Baada ya dakika kadhaa alisema huku mashavu yake yakiwa na michilizi ya machozi.
"Samahani mwanangu kwa hali iliyojitokeza, imenikumbusha miaka saba iliyopita nikiwa ndani ya ndoa yangu. Ndoa mwanangu ni kama jumba au ngome ambayo ina siri kubwa yaani nje na ndani, nikiwa na maana kuwa waliomo nje wanatamani kuingia ndani na waliopo ndani wanatamani kutoka nje.
Pia wapo waliotoka kwa makosa wanatamani kurudi tena ndani na waliopo nje hawataki kuingia ndani na wengine kama sisi yuliowahi kuwepo ndani hatutaki kurudi tena na wengine kama dada na mumewe wanaishi kama wapokwenye pepo ya dunia hawafikilii kutoka. Atatoka mmoja wao kwa kuchukuliwa na mauti kama walivyo apa mbele ya Mungu.
Mwanangu Sundi maisha ya dada yangu ambaye ni mama yenu na mumewe baba yenu ambaye ni shemeji yangu ndiyo yaliyonivuta na kutamani kuolewa. Kwa bahati nzuri nilibahatika kumpata mwanaume wa ndoto yangu mwenye hali nzuri kimaisha. Baada ya ndoa yangu iliyoacha simulizi midomoni mwa watu Eliza mimi niliyaanza maisha kama mke wa mtu..
Niliishi ndani ya jumba la kifahari kulala kitanda cha kifahari kutembelea gari la kifahari nilikula chakula nikitakacho na kujipamba kwa vito vyote vya gharama. Mwanangu na weupe huu nilikuwa kama malaika...
Ni kweli niliamini ndoa ni pepo ya duniani kwa maisha niliyoishi na mume wangu kwa kuonyesha mapenzi ya kweli na upendo ulioonekana dhahiri shairi. Nilipendeza machoni mwa watu mume wangu hakuwa mbaguzi wala kunihoji matumizi yangu.
Niliweza kufanya mambo mengi kwa siri bila kumjulisha, msiri mkubwa alikuwa mama yenu. Aliweza kuniwekea pesa na kufanikisha kuninunulia kiwanja ambacho aliwezesha kunijengea nyumba hii. pamoja na miladi yote unayo iona ni msaada wa mama yako. Basi mwanangu ndoa yangu ilidumu kwa mwaka mmoja na nusu tu ikaanza vituko, pale baba yako mdogo alipoanza visa. Na yote ilikuwa ni kutokana kuchelewa kupata mtoto na kuonekana mgumba, mwanzo mume wangu alikuwa upande wangu na kuwa pamoja na mimi kunipa moyo.
Japo upande wa wazazi wake hasa mama mkwe na wifi zangu walimshauri aniache. Msimamo wake ulinifanya nijione kweli nimepata mume wenye mapenzi ya kweli. Lakini ndugu zake walianzisha kampeni ya kumtafutia mwanamke wa pembeni ili kumpatia mtoto na kupata njia ya kunitoa ndani.
Kweli dua baya nalo hupokelewa baada ya kufanya siri ile mume wangu alifanikiwa kumbebesha ujauzito mke wa pembeni. Hapo ndipo nilipoanza kuiona nyumba mbaya mume wangu akaanza dharau hata kukubali dada zake waninyanyapae,japo mwanzo aliwakataza na kuwaonya.
Uliandaliwa mpango kabambe yaani siku ya kujifungua ndiyo siku ya mimi kutolewa ndani. Nilivaliwa kanga za mafumbo na kuimbiwa nyimbo nyingi zenye kutia kichefuchefu. Yote nilivumilia na yote manyanyaso nilimweleza mama yako ambaye alinipa moyo.
Alinieleza maisha ya ndoa yana misukosuko ambayo yanahitaji ujasiri wa hali ya juu na kuwa na moyo wa chuma hasa kuzingatia hali yangu ya kuchelewa kupata mtoto. Alinieleza kuwa nimsikilize mume wangu ndiye aliyeniweka ndani na ndiye mwenye maamuzi yote.
Siku moja nilipata taarifa ambazo zingeweza kusimamisha mapigo ya moyo wangu pale mtu wangu wa karibu aliponiletea taarifa.
"Shoga una habari gani za mumeo?"
"Hata sina."
"Basi mafumbo yote ya wifi zako na dharau za mumeo leo nimezipatia jibu."
"Jibu gani tena,mbona unanitisha?"
"Basi kama huna moyo siwezi kukueleza."
"Shoga moyo ninao bila huo moyo leo nisingekuwa hapa."
"Basi shoga kumbe mumeo ametafutiwa kisichana na sasa kina mimba ya miezi sita."
"Usiniambie!" nilihisi kuishiwa nguvu na mwili kunitetemeka hali iliyomtisha shoga yangu na kutaka kuacha kunisimulia
"Basi shoga naona mambo sio mazuri moyo wako mwepesi"
"Sio mwepesi hata wewe ungeshtuka malizia tu shoga"
"Basi mpango uliopangwa ni kuwa akijifungua tu na wewe out tena sio siri nashangaa we ndio hujui kila mmoja anakuonea huruma kwa kitendo cha kinyama wanachotaka kukutendea"
"Mungu wangu yaani wameisha kuwa Mungu wa duniani wananihuku sawa Mungu ndiye anayejua yote namuachia yeye"
Huwezi kuamini mwanangu wakati huo sikuwa Eliza yule mwenye mvuto wa kimalaika bali nilikuwa nimebakia mfupa na ngozi.Hata haki yangu ya ndoa nilipewa pale alipopenda.Kweli nilikuwa nimechokwa na mume wangu kwa kuniambia nimepoteza mvuto.
Mabadiliko ya hali yangu ilinifanya niingiwe na wasiwasi kwa kutokuziona siku zangu kwa mwezi wa pili. Wakati huo mwanamke wa pembeni alikuwa amabakiza mwezi mmoja ajifungue.Majibu ya uchunguzi wa afya yangu yalionyesha kuwa nimenasa yaani mjamzito.
Sikuamini niliamini Mungu ameyakomboa maisha yangu kwa kulifanya lile ambalo kwa mwanadfamu haliwezekani.Taarifa nilimfikishia Mume wangu,kwa kweli alishtuka na kusema
"Muongo mkubwa"
"Yaani mume wangu badala ya kufurahi kwa Mungu kusikiliza kilo chetu wewe unasema uongo"
"Hiyo sio dawa safari ipo pale pale"
"Mume wangu ulikuwa na lingine au hili hili?"
"Baada ya kunifanya nikose amani kwa familia yangu sasa unataka kunigombanishja kabisa"
"Mume wangu kukugombanisha kivipi?"
"Kwa kuwaeleza uongo"
"Mume wangu inamaana vyeti hivi vinasema uongo?"
"Nitaamini vipi labda umemuhonga daktari ili kukuokoa"
"Mume wangu sikulazimishi kukaa na mimi hata kama utaniacha leo basi uelewe umeniacha na ujauzito wako"
"Siamini twende wote hospitali"
Niliongozana na mume wangu hadi hospitali na kuchukuliwa vipimo mbele ya mume wangu na majibu yalimfanya mume wangu ahudhunike,lakini akuomba msamaha nilijua ni kiburi na ubabe.Bila kutarajia nilimwambia neno ambalo lilinitoka mdomoni
"Mume wangu nenda ukawaambie wamlete huyo walio muandaa"
"Wamlete nani na kina nani?"
"Unawajua"
"Naona umenikosea adabu"
"Na nitakukosea sana ninyi si miungu watu"
Maneno yalimuingia mume wangu na hakutaka kusema neno,tulipofika nyumbani aliondoka bila kuaga.Hapo mimi roho iliniuma na kujikuta nalia peke yangu,moyo uliniuma sana na kujiona sina thamani tena.
Nini kitaendelea?