SURA YA KUMI NA TANO
Tulipokwisha okolewa katika mikono ya Agon na watu wake wa dini, tulirudi katika vyumba vyetu katika jumba la Malkia tukawa katika hali njema, Malkia wawili, watu wakuu na watu wenyewe walishindana wao kwa wao kutupa heshima na zawadi, jambo lile la kuwaua viboko lilisahauliwa, wala hatukutaka kuwakumbusha watu habari zake.
Asubuhi iliyofuata mambo yale yaliotokea hekaluni, walimu watatu wenye vitabu vya maandiko ya mkono na wino na kalamu wakaja wakatuashiria kuwa wameletwa kutufundisha.
Basi, tulijitahidi sana kujifunza kila siku muda wa saa nne. isipokuwa Umslopogaas, Umslopogaas alikataa kabisa, akasema kuwa yeye hataki kujifunza lugha ya kike.
Na mwalimu mmoja alipomwendea na kitabu na wino na kuvipunga mbele yake, ili kumvuta macho, aliondoka kwa ukali akapunga Inkosikazi mbele ya macho ya Yule mwalimu, na huu ulikuwa mwisho wa kujaribu kumshawishi kumfundisha lugha ya Kizuvendi.
Kila sehemu watu walikuja kutuamkia na kutazama bunduki na nguo zetu na vyombo vyetu, na hasa saa zetu zilizowafurahisha sana. Watu wengine, hasa vijana maridadi waliyaiga mavazi yetu.
Basi baada ya haya, tulianza kuvaa mavazi ya kienyeji kwa sababu hatukutaka, Kuendelea kuwavuta watu kututazama.
Tena na pia nguo zetu zilianza kuchakaa. Umslopogaas tu hakukubali kubadili namna ya mavazi yake. Tena tulijitahadi katika kujifunza lugha ya nchi, tukaendelea vizuri.
Basi, hivyo kila asubuhi tulitumia wakati wetu katika kujifunza na baada ya saa sita tulitumia wakati kujiburudisha.
Pengine tulikwenda kutazama mashimo ya kuchimbua dhahabu na marumaru, na pengine tulikwenda mwituni kuwinda pamoja na mbwa waliofugwa na walio fundishwa kwa ajili hiyo.
Siku nyingine tulikwenda kuwaamkia mabwana wakuu katika ngome zao, tukaiona miji ya wenyeji. Jioni tulikwenda kula pamoja na Malkia, si kila siku ila labda mara tatu nne kila jioni na, walipokuwa hawana wageni wengi, wala shughuli iliyohusu utawala.
Nadhani tabia ya kupendeza ya Nyleptha ilikuwa upole na kwa sababu alipenda kujua habari za mambo madogo madogo ya mtu mzuri kupita wote nishajua lakini hata hivi, kwa kweli nimwanamke anaependa kujifunza mambo mapya.
‘’Basi, vivyo hivyo miezi mitatu mingine ilipita sasa tulikuwa tumekwisha jua lugha ya Kizuvendi kwa kadiri, maana si lugha ngumu.
Na huku nyuma tulikuwa tunapendwa na watu wote na pia watu wa jumbani mwa Malkia walitupenda kirafiki, tukapata sifa ya kuwa watu wenye ustadi na busara.
Sir Henry aliweza kuwaonyesha namna ya kutengeneza kioo, na kwa msaada wa kitabu tulichokuwa nacho chenye habari za jua na mwezi na nyota, tuliweza kupata habari za namna nyota zitakavyo pangwa siku fulani habari hizi ziliwashinda wanajimu wao.
Tena tuliita mkutano wa watu wenye elimu tukawaonyesha namna, nguvu iliyomo katika mvuke wa maji inavyofanya kazi, na namna mashine za mvuke zinavyotengenezwa, watu hao wenye elimu walishangaa ushangao mkuu! Tukatengeneza vim vingine vya namna ile ile.
Basi, kwa sababu ya mambo hayo wenyeji walikusudia tusiruhusiwe kabisa kutoka katika nchi yao, tutakaa ya kuwa hata kama tukitaka kutoka, hatutaweza.
Tena, tulipewa heshima, tukapewa vyeo katika askari walinzi wa Malkia, tukapata vyumba maalum katika jumba la Malkia, tukapewa nafasi ya kutoa ushauri katika mambo ya utawala wa nchi.
Lakini ingawa anga ilionekana kuwa na rangi ya samawati, lakini kulikuwa na wingu kubwa kwenye upeo wa macho yetu.
Kweli, tulikuwa hatukusikia habari za viboko wale tena, lakini tulijua kuwa habari za kufuru yetu hazikusahauliwa, wala hasira na uadui ulioongozwa na kuhani mkuu Agon haujatulia bado.
Na kwa kweli ulikuwa unawaka kwa ukali zaidi kwa kuzidishwa na wivu. Maana tangu hapo makuhani walifikiriwa kuwa watu wenye elimu kubwa katika nchi.
Lakini watu walipoyaona maarifa yetu, nguvu zao zilielekea kuvunjika. Tena, hatari nyingine ilikwepo maana wakuu wengine wakiongozwa na Nasta walituonea wivu sana, na uadui wao ulielekea kububujika kabisa.
Nasta alikuwa ametumaini kwa muda wa miaka mingi kumwoa Nyleptha, lakini sasa mambo yamebadilika.
Nyleptha moyo wake haukwepo tena kwake! Na Nasta alikuwa mwepesi kutambua sababu yake ni nini.
Basi, katika hasira yake alimgeukia Sorais, akaona kuwa ni bora zaidi kuposa mlima kuliko Sorais! Kwakweli Sorais alikuwa mzuri sana napia ni jasiri lakini uliochangajika na uovu.
Basi, nasta aliwakumbuka watu wake elfu thelathini wenye panga walio tayari kufuata amri zake kutoka chini yake milimani na kuushambulia mji wa Milosis.
Lakini kwanza alikusudia kujaribu tena kumposa Nyleptha! Akafanya shauri la kumposa mbele ya baraza ya mwaka inayofanywa ili Malkia watie sahihi sheria zote zilizoamriwa nao, katika muda wa mwaka ule.
Basi, Nyleptha akapata habari, akatuambia usiku kabla ya siku ile ya kutia sahihi, na ingawa alifanya kama si kitu, nilitambua ya kuwa anaona hofu.
Sir Henry alijiuma midomo na kujaribu awezavyo lakini hakuweza kuficha fadhaa aliyoisikia. Nikamuuliza Nyleptha kama kwa udadisi, ‘’ Malkia atamjibu nini bwana Nasta?’’
Malkia akajikunia mabega. Akasema, ‘’Nitamjibuje Makumazahn? (maana tulijulikana kwa majina yetu ya kienyeji).
Sijui Mwanamke dhaifu anaweza kufanya nini na hali anajua kuwa Yule atakaye kumposa anao watu elfu thelathini wenye panga kuhimiza posa yake?’’ Akamchungulia Sir Henry katika kope zake ndefu.
Basi, hapo tuliondoka mezani kwenda katika chumba kingine, Sir Henry akanijia, akasema ‘’Njoo upesi Quatermain, nataka shauri lako. Sikiliza, Ingawa sijasema neno, hukosi umeona kuwa nampenda sana Nyleptha. Je, nifanye nini?’’
Kwa bahati nilikuwa nimekwisha yafikiri mambo hayo, nikaweza kumjibu upesi, nikasema, ‘’Lazima useme na Nyleptha usiku huu huu. Wakati wako ni sasa, ama sivyo, hutapata nafasi tena.
Sikiliza, Tuendapo katika chumba kile cha maongezi, umkaribie umnong’oneze umwambie akukute saa sita usiku karibu na sanamu ya Rademas mwisho wa sebule kuu. Mimi nitakuwapo kushika zamu, basi, wasaa ni sasa ama haupatikani tena.’’
Basi, tulikwenda katika chumba kingine. Nyleptha alikuwa amekaa ameiweka mikono yake mbele yake, na uso wake ulikuwa wa kuhuzunisha sana. Mbali kidogo Sorais alikaa anazungumza na Bwana Good kwa sauti yake ya pole pole.
Sasa wakati ulikuwa ukipita, nikajua ya kuwa baada ya dakika kumi na tano Malkia wataondoka kama ilivyo desturi yao, na Sir Henry bado hajapata nafasi ya kusema na Nyleptha kwa faragha, maana ingawa tulionana na Malkia mara nyingi, ilikuwa shida kuweza kusema na mmoja wao peke yake.
Nilifikiri sana kisha nikapata akili nikamwendea Sorais, nilijiinamisha mbele yake, nikasema, ‘’Tafadhali, Malkia, utuimbie watumishi wako.
Mioyo yetu ni mizito leo, utuimbie ewe bibi wa usiku.’’ (Ndilo jina wanalomwita wenyeji.) akajibu, ‘’Nyimbo zangu hazielekei kuuondoa uzito wa mioyo yenu Makumazahn. Lakini ukitaka nitaimba.
Akaondoka akaenda mezani akaichukua gambusi akaanza kuipiga kivivuvivu. Ndipo alipoanza kuimba, na sauti yake ilikuwa nzuri kama sauti ya ndege, lakini wimbo ulikuwa wa kuhuzunisha kabisa, na kiitikio chake pia kilikuwa cha huzuni sana.
Sauti yake ilipanda juu ikawa kama inayeyuka kwa mbali sana. Kisha, ilizidi tena, ikasafiri kama imejaa huzuni yote ya ulimwengu na taabu zote za wote waliopotea.
Ulikuwa wimbo wa ajabu mno, lakini sikupata nafasi nyingi ya kuusikiliza vizuri. Walakini baadaye niliyaandika maneno yake, nikajaribu kuyatafsiri. Kadiri nilivyoweza kuyatafsiri, ni kama haya yanayofuata:
Wimbo wa Sorais
Kama ndege mwenda pweke aliyepotea anavyoruka gizani.
Kama mkono ulioinuka buree kuikinga mauti wakati wa kufa.
Ndivyo yalivyo maisha! Maisha yanayotia upendo na pumzi wimboni.
Kama wimbo wa ndege uliojaa utamu usiotamkikana.
Kama roho inayofungulia milango mbinguni kwa ishara.
Ndivyo ulivyo upendo! Upendo utakaoanguka ukiisha vunjika..
Kama vishindo vya hatua za mashujaa wanaokwenda vitani.
Kama sauti ya ngurumo za umeme unapopasua mawinguni,
Ndivyo ulivyo uwezo! Uwezo utakaoanguka mavumbini mwishoni.
Maisha ni mafupi: hata hivyo vitu vyote vyaweza kutuacha.
Ni ndoto chungu usingizini wala hakuna awezaye kutuamsha,
Mpaka hatua za mauti! Mauti asubuhi au jioni zatupata.
Kiitikio.
Ndiyo, dunia ni nzuri asubuhi asubuhi asubuhi.
Lakini jua jekundu huzama damuni jua jekundu huzama damuni.
Basi Sorais alipoanza kuimba ubeti wa pili wa wimbo wake, niligeuka, nikamwambia Sir Henry kwa sauti ‘’Haya sasa nenda,’’ nilimwambia.
Niliweza kusikia kila neno alilolisema, maana moyo wangu ulifadhaika sana na kwa hiyo nilikuwa na mang’amung’amu. Akasema, ‘’Nyleptha! Nyleptha, naomba nisema nawe usiku huu huu, nakuomba usikatae.’’
Akajibu, ‘’Nawezaje kusema nawe? Malkia si kama watu wengine, nimezungukwa na walinzi na kuangaliwa kila ni endapo.’’
Sir Henry akasema, ‘’Sikiliza Nyleptha. Nitakuwapo mbele ya sanamu ya Rademas karibu na sebule kuu saa sita usiku. Makumahn na Umslopogaas watakuwapo ili kutulinda. Usikatae eh Malkia wangu.’’
Akajibu, ‘’Haiwezekani, ikawa kesho?’’ Sir Henry akamsii, ‘’ Tafadhali nakuomba iwe leo Malkia wangu!’’
Basi, hapo itikio la wimbo lilianza kuishia, na Sorais aligeuka pole pole.
Hapo Nyleptha akasema kwa haraka; ‘’Vyema, nitakuwapo, nawe usikose kuwapo pia.’’