Hadithi ya umslopagaas

Hadithi ya umslopagaas

’Waniona?’’
Yule Mjivuni akajibu,

‘’Ndiyo, nakuona kitwana.’’

Umslopogaas akasema,

‘’Waliona hili?’’
akaweka Inkosikazi mbele ya macho yake.

Yule Mjivuni akasema,
‘’Ndiyo, kitwana, na ‘mchezo’ wako; ya nini?’’

Umslopogaas akasema,

‘’We Mjivuni mbwa, mpayapaya, wewe mjivuni, wewe mkamata wanawake kwa ‘mchezo ‘ huu nitavikongoa viungo vyako. Ni vyema ya kuwa u tarishi, ama sivyo, ninge vitawanya tawanya


story yote hapa napakubali sana
 
SURA YA KUMI NA TATU


Sasa nitatoa habari kidogo za watu hawa tuliowafikia. Habari hizi tulizijua kwa maarifa tuliyoyapata baadaye.

Nchi hii huitwa Zuvendi, na jina lake hutokana na Zu, maana yake ‘’rangi ya kimanjano’’ na ‘’Vendi’’ maana yake ‘’mahali au ‘’nchi.’’

Sikuweza kupata kujua sababu huitwa nchi ya Kimanjano, wala wenyeji wenyewe hawajui. Lakini hutaja sababu tatu, na mojawapo yoyote inatosha kulieleza jina lake.


Kwanza husemwa nchi ilipata jina hili kwa wingi wa dhahabu iliyopo; sababu ya pili ni kwa kuwa majani ya nchi, ambayo ni mazuri na matamu, hugeuka rangi ya kimanjano katika majira moja ya mwaka na sababu ya tatu inatoka katika hadithi ya kuwa zamani wenyeji walikuwa wenye rangi ya kimanjano, ikageuka kuwa nyeupe baada ya kukaa miaka mingi katika nchi za juu.


Nchi ya Zuvendi imezungukwa pande zote na misitu minene ya miiba, na kupita misitu hiyo ni maili nyingi za mabwawa na majangwa na milima mirefu. Kwa kifupi ni kama meza kubwa iliyoinuka juu ya nchi ya katikati ya Afrika.

Nchi yenyewe haina joto jingi na ardhi yake ni nzuri sana, na namna zote za nafaka na matunda na miti husitawi sana, na katika mabonde namna moja ya miwa huota.

Kila namna ya madini inapatikana kwa wingi humo, isipokuwa fedha ambayo ni kidogo tu katika milima ya kaskazini.

Ina maziwa makubwa matatu, lililo kuu ni lile tulilotokea ambalo huitwa Milosis, sawasawa na jina la mji mkuu tena yamo maziwa madogo mengi, mengine yana maji ya chumvi.

Wenyeji ni wengi, wapata milioni kumi au kumi na mbili, na walio wengi ni wakulima. Asili ya watu hawa siwezi kujua hakika, na maandiko ya habari zao ambazo huendelea kwa muda wa miaka elfu moja hayataji asili yao.

Ingawa watu walio wengi ni wakulima, lakini pamoja na hayo ni watu wapendao vita pia, na ingawa kwa namna nchi yao ilivyo hawawezi kupigana na mataifa mengine, lakini hupigana wao kwa wao mara kwa mara.

Kwa desturi mfalme au malkia huitawala nchi lakini makuhani wana nguvu nyingi, pia baraza ya wakuu lina nguvu, na kama ilivyo katika nchi nyingi za dunia, amri ya mtawala pengine inapingwa na wakuu wenye raia wengi chini yao.

Wakuu hao hupingana wao kwa wao au kufanya amani na wenzao kadiri wapendavyo, na pengine hata hugombana na watawala wao na kujifungia katika ngome zao mbali na mji mkuu wa Milosis, nao hushindana na watawala wao kwa muda wa miaka mingi.

Sisi tulipofika, mfalme alikuwa amekufa zamani za miaka miwili, naye alikuwa mfalme wenye nguvu nyingi akazipunguza nguvu za makuhani na wakuu.

Alipokufa watoto wake wanawake mapacha walitawazwa kama ilivyo desturi ya nchi hiyo, maana kama mmoja tu angalitawazwa, raia wengine wangalifanya ghasia.

Lakini watu wengi walifikiri ya kuwa shauri hili si zuri, wala haliwezi kudumu. Na kwa kweli wakuu wengine waliotamani uwezo zaidi walikuwa wakifanya hila kumuoa mmoja wapo wa malkia, ikadhaniwa kwamba vita vitatokea kwa sababu hiyo kabla hazijapita siku nyingi.


Sasa nitasimulia kidogo juu ya dini ya Zuvendi, ambayo ni kuliabudu jua tu. Dini hii ya kuliabudu jua inaingia katika desturi zote za Zuvendi, nayo hupeleka mizizi yake katika kila sheria na mila ya nchi.

Toka kuzaliwa kwao mpaka kufa kwao Wazuvendi hulifuata jua kwa kila jambo. Watoto wachanga huinuliwa na kuonyeshwa jua na kuwekwa wakfu kwa ajili yake, ambalo ni ‘’dalili ya wema, asili ya nguvu, na tumaini la milele.’’

Wazazi, huwaonyesha watoto wachanga jua na kuwaambia ya kuwa ni mungu mkarimu, nao huliabudu linapotoka na linaposhuka.

Tena, wanapokuwa wangali wadogo bado huchukuliwa na mama zao mpaka katika hekalu la jua lililo karibu.

Na huko, kwenye saa sita, miali ya jua inapoiangaza madhabahu ya dhahabu ya katikati na kuufifisha moto unaowaka huko, husikia makuhani waliovaa mavazi meupe wakiimba sifa za jua, na kuwaona watu wote wakisujudu na huku panda zinalia na kafara hutupwa katika moto ulio chini ya madhabahu.


Tena, wakiisha kua, ‘Huja hapa kutangazwa na makuhani kuwa sasa ni watu wazima, na kuwekwa wakfu kufanya matendo mema na vita; tena, ni hapa wanapowaleta mabibi arusi wao; tena ni hapa wanapowaleta kuachana nao kama hawawezi kupatana katika nyumba zao.

Basi, vivyo hivyo tokea mwanzo mpaka mwisho wa maisha yao, ndipo wanapoletwa juu ya jeneza na kuwekwa juu ya milango inayofunguliwa kuingilia chini mbele ya madhahabu ya mashariki, na miali ya mwisho ya jua linaposhuka na kuwaangazia nyusoni, makomeo huvutwa na mlango hufunguka; nao huanguka chini katika moto, ndio mwisho wao.


Makuhani wa Jua hawaoi. Huchaguliwa katika vijana waliowekwa wakfu na wazazi wao kufanya kazi hizo, nao hupewa riziki zao Serikalini.

Watu wenye daraja kubwa katika ukuhani huchaguliwa na mtawala, lakini wakisha pewa daraja, basi hawawezi kutolewa tena.

Na kwa kweli hao ndiyo wanaoitawala nchi. Makuhani ni chama kilichounganishwa imara, nao huapishwa kutii, tena huapa ya kuwa hawatatoa nje habari zozote za kazi yao, kwa hivi’.

Amri inayotolewa na kuhani mkuu huko Milosis hufuatwa mara ile bila kusita na kuhani wa mji wowote hata kama ni mbali mwendo wa maili mia tatu au nne.


Makuhani ni mahakimu na makadhi wa nchi, nao wakiisha kukata shauri haliwezi kupelekwa mbele isipokuwa mbele ya mkuu wa sehemu ile ya nchi, na toka kwake, hupelekwa mbele, ya mtawala mwenyewe nao wanazo nguvu juu ya mambo yote ya dini.


Pamoja na nguvu za kuharamisha watu ambayo ni nguvu kubwa sana.
Msingi mwingine wa nguvu za makuhani ni elimu, maana karibu elimu zote za nchi zi katika mikono yao tu!

Nao wanazo elimu nyingi za nyota pia, na kwa hivyo wanazo nguvu juu ya watu kwasababu wanaweza kubashiri habari ya kupatwa kwa mwezi na jua. Na pia habari za nyota nyingine zenye mikia.

Wako wakuu wachache tu wanaoweza kusoma na kuandika, lakini karibu makuhani wote wanaweza, na kwa hiyo watu huwadhania kuwa ni watu wenye elimu nyingi.

Kwa jumla yake, sheria za nchi ni za haki tena zina huruma, lakini zimeachana na zile za nchi zilizostarabika kwa namna nyinginezo.

Adhabu ya kifo inatokana kwa kumwasi mtawala au kujaribu kuikimbia nchi ambayo huhesabiwa kuwa ni kumwasi mtawala kwahiyo adhabu yake huwa ni ukumu ya kifo. Na kwa kudanganya yatima na wajane hukumu yake huwa ni kifo.


Namna ya kuwaua wakosaji hao ni moja tu! Nayo ni ya kutisha sana. Mkosaji hutupwa angali hai katika moto mkali ulio chini ya madhahabu mojawapo ya jua.

Kwa makosa yote mengine, pamoja na lile la kuwa mvivu, adhabu ni kupelekwa kufanya kazi katika majengo ya Serikali ambayo siku zote yanajengwa huko na huko katika nchi, nao pia hupingwa mara kwa mara kadiri ya makosa yao waliyoyafanya.


Wenyeji wanaruhusiwa kuoa zaidi ya mke mmoja, lakini kwa kawaida huona mke mmoja tu kwa sababu ya gharama. Kwa sheria mwanaumume lazima ampe kila mke nyumba ya peke yake.

Mke wa kwanza ni mke wa sheria, na watoto wake husemwa kuwa ni wa nyumba ya baba.

Watoto wa wake wengine huitwa watoto wa nyumba za mama zao. Lakini desturi hii si kuwatia aibu wale watoto wala mama zao. Tena, mke wa kwanza anaweza kufanya sharti anapoolewa ya kuwa mume wake hana ruhusa ya kuoa mke mwingine.

Lakini hawafanyi hivyo mara nyingi, bali ni wanawake walio na bidii katika desturi hii ya kutaka waume wao kuoa wake wengine, maana wanawake ni wengi kuliko wanaume, tena, Yule mke wa kwanza huwa kama ni mkubwa wa nyumba nyingi.

Kwa kawaida Wazuvendi ni watu wapole, wachangamshi, na wakarimu. Si stadi katika kufanya biashara, wala hawafikiri sana habari za fedha, hufanya kazi tu kupata chakula cha kutosha kuwasitawisha katika hali waliyozaliwa nayo. Biashara ya kawaida ni kubadilishana vitu.


Kazi iliyo kubwa ni kulima, lakini pia hufuga ng’ombe na farasi kwa uangalifu sana. Watu hutozwa kodi kubwa sana.

Serikali hutwaa theluthi ya mshahara wa kila mtu, na makuhani kadiri ya sehemu ishirini kwa moja ya ule uliobaki.

Lakini mtu ye yote akipatikana na misiba, basi, serikali humtunza kwa kadiri ya hali yake. Lakini kama ni mvivu , hupelekwa kufanya kazi ya serikali, na wakati huo serikali huwatunza wake zake na watoto wake.

Serikali hutengeneza njia na barabara zote na kujenga nyumba zote na kuzipangisha kwa watu.

Sasa je, watu hawa wamestarabika ama sivyo? Ni vigumu kusema kwa hakika. Majengo yao na sanamu zao ni nzuri kabisa nafikiri hakuna watu duniani wanaoweza kuwashinda kwa kazi hiyo.

Lakini hawana habari za kazi za sanaa nyingine zilizo katika nchi zilizostarabika. Vyombo vyao vya kufinyanga si vizuri, wala hawana habari za nguvu za mvuke wa maji, wala za umeme, wala za baruti, wala hawajui namna ya kupiga chapa vitabu.

Juu ya habari za dini yao, kweli pengine huliita jua ‘’Vazi la Roho’’ lakini kwa kweli huliabudu jua lenyewe.

Tena huliita ‘’Tumaini la milele ,’’ lakini naona maana yake si dhahiri. Wengine wao huamini kuwa kuna ukumu inayofuata baada ya kufa najua ndivyo anavyosadiki Nyleptha lakini ni dini ya moyo wake yeye, wala si kanuni ya dini ya nchi.
 
SURA YA KUMI NA NNE

Nilipoamka asubuhi baada ya kufika Milosis, saa yangu ilikuwa saa mbili na nusu. Nilikuwa nimelala muda wa saa kumi na mbili, nikaona nafuu kabisa.

Kweli, usingizi ni kitu cha Baraka sana! Ni tofauti hiyo inayofanyika kwenye usingizi wa saa kumi na mbili baada ya siku nyingi za kazi ngumu na hatari ni kama kulala hujifai kabisa na ukiamka tena umekuwa mtu mpya.

Niliketi kitandani, na kitu cha kwanza nilichoona ni rodi ya Bwana Good inanitazama. Nilijua ya kuwa amekwisha amka, anangoja niamke tu apate kuongea.


Hakika, alianza kusema, lakini hapa tulisikia panzia likivutwa na mtumishi aliingia chumbani, akafanya ishara kutujulisha ya kuwa amekuja kutuongoza kwenye mahali pa kuogea.

Tukamfuata kwa furaha, tukapelekwa kwenye hamam ya marumaru yenye maji maangavu yaliyo katikati yake, tukajitumbukiza ndani mara ile.


Tulipokwisha oga tulirudi chumbani tukavaa tukaenda chumba cha katikati tulimokula jioni, tukaona chakula kimeandaliwa tayari.

Kilikuwa chakula kizuri sana, ingawa siwezi kuieleza namna yake. Baada ya kula , tulitembea huko na huko kufurahia mazulia, na sanamu zililozochorwa katika mawe, tukifikiri mambo gani tena, yatakayo fuata!!

Basi, tulipokuwa tukifanya hivyo, askari mkubwa Yule aliyewekwa kutuangalia alifika, akatuamkia na kufanya ishara tumfuate, tukamfuata na huku tuna mashaka mengi moyoni, maana tulisikia ya kuwa wakati ume wadia wa kufika mbele ya kuhani mkuu kutoa sababu ya kuwaua wale viboko.

Lakini hatukuwa na njia nyingine ila kumfuata, na mimi niliona faraja nyingi kwa vile wale Malkia pacha walivyotuhaidi kutuokoa, nikijua ya kuwa wanawake kwa jinsi walivyo na mapenzi ya dhati, basi hawakosi njia ya kuyatimiza mapenzi yao.

Basi, tukamfuata kama kwamba tunapenda. Baada ya kupita katika vichochoro na katika ua wa nje tukafika kwenye milango ya jumba ya kuingilia barabara kubwa inayopanda kilima katikati ya Milosis na Hekalu la jua mwendo wa maili moja, kisha inakwendea upande wa pili wa hekalu mpaka kwenye ukuta wa nje wa mji…

Milango hii ni mikubwa sana ya shaba iliyonakshiwa vizuri. Katikati ya milango hii maana iko miwili pana handaki kadiri ya futi arobaini na tano lililojaa maji, lenye daraja la kulivukia. Daraja hilo linaweza kuinuliwa na liinuliwapo, jumba huwa mfano wa kisiwa kisichofikika.


Tulipotoka milangoni mara magari manne yakaja mbio, na kila gari lilikuwa likikokotwa na farasi wawili weupe.


Magari hayo ni ya mbao yenye magurudumu mawili yaliyozungushiwa chuma. Saisi hukaa katika kiti mbele, na ndani ya gari vimo viti vitatu.


Magari hayo ni mepesi lakini ni imara sana, na farasi ni wazuri mno, si wakubwa sana, ila ni wenye nguvu nyingi. Gari la kwanza na la mwisho yalikuwa na askari ndani yake.

Lakini yale mawili mengine yaliyokuwa katikati yalikuwa hayana mtu ndani isipokuwa saisi wanaoyaendesha. Basi, tulipelekwa kwenye magari hayo, tukaingia ndani, na mara ile yakaanza kwende mbio sana.

Baadaye kidogo tukaona Hekalu la jua, zuri ajabu, ambalo linaheshimiwa sana na Wazuvendi.

Utajiri na ustadi na kazi za vizazi vingi zilitumika kulijenga jengo hilo la ajabu, nalo lilikuwa limemalizwa zamani za miaka hamsini tu.

Hakuna kitu kilichomo katika nchi kilichotakiwa kulikamilisha hekalu hilo kisicholetwa na kutumika na jengo kwa kweli lilistahili bidii yote iliyotumika kulijenga.

Si kwa sababu ya ukubwa wake, maana yako majengo makubwa zaidi duniani, ila kwa sababu ya ukamilifu wa malingano yake, ukamilifu wa uzuri wa vitu vilivyotumika na ukamilifu wa sanaa za kazi.

Hekalu limesimama peke yake juu ya kilima, na kuzunguka ziko nyumba wanamokaa makuhani, na umbo la jengo lake ni la ua kubwa.

Sehemu ya katika ina dari ya kuba iliyofanana na jicho la ua, na katika pande zake ziko sehemu kumi na mbili zilizofanana na majani ya maua yanayotoka katika jicho lake, na kila sehemu imewekwa wakfu kwa ajili ya mwezi mmmoja wapo wa mwaka, na ndani yake huwekwa sanamu za ukumbusho wa watu maarufu waliokufa.


Upana wa duara iliyo chini ya kuba ni futi mia tatu, na urefu wa kwenda juu ya kuba ni futi mia nne, na urefu wa kila sehemu inayotoka katika sehemu hiyo ya katikati ni futi mia moja na hamsini, na urefu wa dari zake ni futi mia tatu; basi ile sehemu ya katikati iliyo kama jicho la ua imeinuka juu zaidi ya sehemu nyingine.

Mawe ya majengo ni marumaru nyeupe iliyolainishwa mpaka kung’aa, nayo yaonekana vizuri sana kwa sababu mawe ya nyumba na majengo ya mji ni mekundu.

Sehemu ya nje ya kuba, na dari za sehemu za hekalu zimefunikwa kwa mabati ya dhahabu na nchani kabisa mwa kila dari iko sanamu ya dhahabu ya mtu mwenye mabawa aliyeshika panda mkononi mwake, amesimama kama kwamba yu taari kuruka juu angani.


Madhabahu kubwa iko katikati chini ya kuba, na madhabahu nyingine ziko, moja upande wa magharibi, na moja upande wa mashariki.

Madhabahu ya katikati ni ya marumaru iliyofunikwa kwa dhahabu. Sura yake ni kama jua, na urefu wake kwenda juu ni futi nne, na uzingo wake ni futi thelathini na sita.

Katika pande zake iko namna ya milango kumi na miwili iliyopangwa kufanana na majani ya ua kuizunguka madhabahu ambayo ni kama jicho la ua.

Milango hiyo imefungwa kwa bawabu chini ya madhabahu, nayo hurudishwa na kufungwa juu ya madhabahu saa zote isipokuwa muda mfupi tu, yaani jua linapopenya katika tundu lililo katikati ya kuba.


Saa sita ya mchana, na kuangazia madhabahu katikati, basi, hapo milango hufunguka na madhabahu hufanana na ua lililochanua, na jua liishapo kupita, basi milango hufungiwa juu tena, liko neno jingine juu habari za madhabahu hiyo.

Hapa afadhali nieleze ya kuwa kila siku miali ya jua liangaziapo katikati ya madhabahu kuu, panda hupigwa, na jua hutolewa kafara iliyochomwa moto, pengine ni mzoga wa kondoo au wa ng’ombe, au pengine ni matunda au nafaka.


Madhabahu ya magharibi na ya mashariki zina sura ya nusu ya duara; zimewekwa kusimama karibu na ukuta wa hekalu.

Madhabahu hizi si nzuri kama ile ya katikati, ila hata hivyo ni za dhahabu ; na moto uliowekwa wakfu unawaka juu ya kila moja, na sanamu ya mtu mwenye mabawa imewekwa upande huu na huu wa kila madhabahu.


Nyuma ya madhabahu ya magharibi na ya mashariki ipo miali miwili ya dhahabu ukutani, na katikati yake liko dirisha jembamba refu.

Basi, jua litokapo asubuhi, miali yake ya kwanza hupenya katika dirisha lililo nyuma ya madhabahu ya mashariki na kupita mpaka katika madhabahu kuu na kuing’arisha dhahabu yake, kisha hupita na kuiangaza madhabahu ya magharibi.
 
Vile vile, jua lishukapo jioni, miali ya mwisho hupenya kati dirisha lililo katika ukuta nyuma ya madhabahu ya magharibi.

Na huing’arisha madhabahu ya katikati kisha hutua kwa muda kidogo juu ya madhabahu ya mashariki. Ni kama ahadi inayoweka mapambazuko ya jioni, na ahadi inayoweka jioni kwa mapambazuko.

Isipokuwa kwa madhabahu hizi tatu, nafasi iliyo chini ya kuba hili kubwa ni wazi kabisa, bila pambano lolote.

Basi, hili ndiyo namna lilivyo hekalu lile zuri, lakini siwezi kulieleza zaidi jinsi lilivyo la ajabu na utukufu.

Mlangoni pa hekalu, tulipokewa na kundi la skari walio onekana kuwa wapo chini ya amri ya kuhani. Tuka pelekwa katika sehemu moja ya hekalu tukaachwa humo muda wa nusu saa.

Hapa tulifanya shauri pamoja, tukatambua ya kuwa tumo katika hatari ya kupoteza maisha yetu, tukakusudia kujilinda tuwezavyo na kuyapigania vikali maisha yetu.

Uslopogaas alisema kuwa yeye atamuua Yule kuhani mkuu Agon kwa kumpasulia mbali kichwa kwa Inkosikazi.

Mahali tuliposimama tuliweza kuona umati wa watu waliokuwa wakihudhuria hekaluni, kama kwamba wanatazamia jambo kuu, nikahofia ya kuwa sisi tumo katika jambo hilo.

Basi, karibu na saa sita, kuhani alikuja akafanya ishara, na mkubwa wa askari alituashiria ya kuwa tunatakiwa kwenda mbele, tukaenda mbele kwa ujasiri tulivyoweza.

Mara tulitoka katika ile sehemu ya hekalu, tukapita katikati ya umati mkubwa wa watu waliokuwa wamehudhuria, mpaka tukawa tumesimama juu ya utando wa shaba ulio katika sakafu mbele ya madhabahu kuu kwa upande wake wa mashariki.

Kwa kadiri ya futi thelathini kuizunguka madhabahu, kamba zilifungwa ili kufanya nafasi na kuwazuia watu wasiingie ndani.

Na katika nafasi hiyo makuhani wengine walipangwa mfano wa duara, wameshika panda mikononi mwao, wamevaa mavazi meupe yenye mahazamu ya dhahabu, na mbele yetu, Agon kuhani mkuu, alikuwa amesimama amevaa kofia yake ya nakshi na urembo. Yeye pekee alikuwa amevaa kofia, bali wote wengine walikuwa vichwa wazi.


Tulisimama juu ya sehemu ile ya shaba, wala hatuna habari hata kidogo kuna nini chini yake kilichotengenezwa kwa ajili yetu.

Nilisikia sauti ikitoka chini sakafuni, lakini sikuweza kukisia ni kitu gani.
Basi, hapa kukawa kimya, nikatazama huku na huko niwaone wale Malkia wawili Nyleptha na Sorais. Nisiwaone.

Lakini niliona nafasi ipo wazi upande wa kulia, nikakisia ya kuwa nafasi ile imewekwa kwa ajili yao.

Tulingoja, na halafu tulisikia panda inalia mbali sana juu katika kuba. Kisha, tulisikia mnong’ono wa watu waliokuwapo, tukatazama tukaona Malkia wale wawili wanakuja pamoja.

Nyuma yao wakuu wengine waliandamana nikamwona Yule Nasta, na nyuma yao askari wapatao hamsini walifuata.

Nilifurahi sana nilipowaona askari wale. Basi, baada ya muda mfupi, walikuwa wamekwisha fika na kusimama mahali pao, Malkia wawili kwa mbele, na wakuu kwa upande wa kuume na wa kushoto, na askari wamejipanga katika mfano wa nusu duara nyuma yao.

Kasha, kukawa kimya kwa muda mrefu, na Nyleptha alinitazama; nikafikiri ya kuwa anajaribu kunijulisha habari, nikamwangalia sana.

Jicho lake lilitazama jicho langu, kasha likajongea, na kutazama ile sehemu ya shaba ambayo tulikuwa tumesimama juu yake, kasha, alikijongeza kichwa chake polepole upande.

Sikufahamu maana yake, akaifanya ishara ile ile tena. Ndipo nilipofahamu ya kuwa anatuonya tusisimame juu ya mlango huo wa shaba.

Akatazama tena, nikaona kuwa ndiyo maana yake hakika, yaani ya kuwa ipo hatari katika kusimama juu ya mlango huo.

Sir Henry alikuwa amesimama upande wangu mmoja na Umslopogaas upande wa pili.

Basi, niliyakaza macho sawasawa mbele yangu, lakini niling’ona kwa sauti ndogo sana kwanza kwa Kizulu, kisha kwa Kiingereza nikawaambia warudi nyuma kidogo kidogo mpaka wawe wamesimama juu ya sakafu wala si juu ya mlango wa shaba.

Basi, sote tulianza kujongea polepole kabisa polepole wala hapana mtu aliyetuona isipokuwa Nyleptha na Sorais tu.

Kisha, nilimtazama tena Nyleptha nika mwona anakiinamisha kichwa chake kidogo sana kama kwamba ananijulisha ya kuwa nimefanyaalivyotaka.

Basi, huku nyuma macho ya Agon yalikuwa yamekazwa mbele kuitazama madhabahu, kama kwamba ametoa kila wazo katika akili zake isipokuwa la kazi iliyoko mbele yake! Na macho yangu yalikuwa yamekazwa kuutazama mgongo wake.
 
Halafu alianza kuipunga mikono yake, akaanza kuimba kwa sauti iliyosikika hekaluni mwote.

Maneno aliyoimba yalikuwa yakulisifu jua.
Yalikuwa kama haya yanayofuata:

Kuna kimya juu ya uso wa Dunia na wa maji yake, Ndiyo kimya imeukalia uso wa maji kama ndege akaaye juu ya kiota chake.

Na kimya imekali kifua cha giza nene, juu sana angani tu nyota zinasema na nyota.
Dunia anataka kuzimia kwa kutamani na machozi yake yanatoka kwa ajili ya tamaa yake.
Usiku mwenye ukanda wa nyota huikumbatia isiridhike.


Imelala imefunikwa kwa ukungu kama maiti katika sanda, Imeinyosha mikono yake kuendelea masharikini.

Tazama! Mbali masharini iko dalili ya mwangaza.

Dunia imeiona na kujiinua, Inatazama toka chini ya kitanga cha mkono wake.
Ndipo malaika wako wakuu hutoka katika mahali pako Patakatifu, ee jua.
Huzitupa panga zao zenye moto katika jua na kuliunguza.


Hupanda mbinguni na kuzitupa chini nyota toka viti vyao vya kifalme.
Ndiyo, huzirudisha nyota ziinemetazo katika giza la usiku.


Hufanya mwezi kufifia kama uso wa mtu anayekufa.
Na tazama! Utukufu wako huja, ee jua!


Ee wewe uliye mzuri, hujivika kwa moto.
Mbingu pana ni njia yako, hupita juu yake kama gari.


Dunia ni bibi arusi wako. Huikumbatia nayo huzaa watoto, ndiyo, humpendeza naye hutoa mazao yake.

Wewe ni Baba wa wote na mtoaji uzima ee jua.

Watoto wadogo huinyosha mikono yao na kukua katika mwangaza wake, Wazee nao hutokea na wakikuona hukumbuka nguvu zao.
Wafu tu, ndio wanaokusahau, ee jua.


Ukasirikapo ndipo huficha uso wako.
Hujifunika na pazia la vivuli.


Ndipo Dunia huona baridi na Mbingu hufadhaika; Hutetemeka, na sauti yake ni kama sauti ya ngurumo Hulia, na machozi yao humiminika katika mvua;
Huguna, na pepo kali ni sauti ya kuguna kwao.


Maua hufifia, mashamba yenye mauuno husinyaa na kunyauka.
Wazee na watoto huenda mahali panapo wahusu.
Uchapo mwangaza wako, ee jua!


‘’Sema, u nini, ee uzuri usio na mfano nani aliyekuweka juu sana, ee kitisho cha joto?
Ulianza lini, na siku ya mwisho wako itakuwa lini?
Wewe ni vazi la roho mwenye uhai.


Hakuna aliyekuweka juu maana wewe ndiyo mwanzo.
Huna mwisho hata watoto wako watakapo sahauliwa .


Ndiyo, huna mwisho kabisa, maana wakati wako ni wa milele.

Umekaa juu katika nyumba yako ya dhahabu na kupima wakati.
Ee Baba Wa Uzima! Ee Jua Mfukuzaji wa Giza!’’


Basi, aliacha kuimba na ingawa maneno niliyotafsiri huoonekana kama si mazuri sana, lakini yale aliyoyasema yalikuwa mazuri ajabu; kisha, akatazama juu katika kipepeo cha kuba, akasema.

‘’Ee jua, ushuke juu ya madhabahu yako!’’

Aliposema maneno hayo, jambo zuri la ajabu lilitokea.
Mwali mmoja wa nuru ulipenya lile tundu katika kuba kama upanga wa moto mkali.

Ulitua juu ya milango ya dhahabu iliyofungwa juu ya madhabahu, ukatiririka juu yake, na ua lile tukufu lilifunuka kama kwamba limefunuliwa na mwangaza wake.

Lilifunuka polepole na milango ile ilipokuwa ikifunuliwa, na kuonyesha madhabahu ya dhahabu ambayo juu yake moto huwaka daima, makuhani walipiga panda zao, na watu wote walipaaza sauti zao, na sauti zao za kusifu zikapanda juu zikapiga kuba ya dari zikarudishwa tena katika kuta za marumaru.

Sasa madhabahu ya ua ilikuwa imefunuka , mwangaza wa jua ulitua juu ya ulimi wa moto mtakatifu, ukaupiga chini hata ukapepesuka na kuzama na kutoweka katika shimo ulimotokea.

Ulipokuwa ukitoweka , sauti za panda zilipaa tena, na Yule kuhani mzee aliinua mikono yake juu tena, akasema kwa sauti kubwa

‘’Twakutolea kafara ee Jua!’’

Nilimtazama Nyleptha tena; nikaona ya kuwa macho yake yamekazwa kuutazama mlango ule wa shaba wa chini, mbele ya madhabahu.

Nikasema, ‘’Jihadharini!’’ na nilipokuwa nikisema, nilimwona Agon anainama mbele na kugusa kitu juu ya madhabahu.

Na alipofanya hivyo, nyuso za watu wote ziligeuka nyekundu, kisha zikageuka nyeupe tena, nikasikia sauti ya kuvuta pumzi kutoka kwa watu wote.

Nyleptha aliinama mbele, akajificha macho yake kwa mikono yake kama hawezi kujizuia.

Sorais aligeuka akamnong’oneza mkubwa wa walinzi wa kifalme, ndipo sauti ya kukwaruza ilisikika, na mlango ule wa shaba katika sakafu ulifunguka mbele ya miguu yetu, na mahali pake palikuwapo shimo lenye moto mkubwa mkali sana chini ya madhabahu.

Tulitoa sauti ya hofu, tukaruka nyuma. Mara kukawa na ghasia nyingi sana, na sisi tulijipanga mgongo kwa mgongo.

Sote tulikuwa na bastola maana ingawa tulipokuwa tukitoka jumbani, tulinyang’anywa bunduki zetu, bastola tulikuwa nazo maungoni mwetu.

Watu hawa hawakujua bastola ni kitu gani. Tena, Umslopogaas alikuwa na shoka lake la vita, na sasa alilizungusha kichwani akatoa ukulele wa vita wa Kizulu uliozunguka zunguka hekaluni.

Basi, hapa makuhani ambao walikuwa wamenyang’anywa mawindo yao walifuta panga zao toka chini ya mavazi yao meupe, wakaturukia kama mbwa mwitu wanavyowarukia wanyama wanaojitetea.

Nikatambua ya kuwa ingawa iko hatari katika kutenda jambo lolote, lakini hata hivyo, lazima tujaribu kujitetea au tupotee.

Basi, mtu wa kwanza alipotujia naye alikuwa mtu mrefu mkubwa nilimpiga risasi ikampata, akaanguka mbele ya lile shimo la moto, akatumbukia ndani ya lile shimo la moto tulilowekewa sisi, na huku anapiga kelele.


Sijui kama ilikuwa kwa sababu ya kelele alizofanya au kwa sababu ya kishindo cha bastola na matokeo yake wale makuhani wengine walisimama kama wamepooza na kufadhaika kabisa.

Na kabla hawajaweza kujongea mbele tena, Sorais alitoa amri, na mara ile sisi pamoja na Malkia wawili na watu wakuu tulizungukwa na kundi la askari wenye silaha.

Basi, hata hapo makuhani walisita, na watu wote walisimama kama wanyama walioshtushwa, wasifanye hivi wala vile.

Sauti ya mwisho ya Yule kuhani aliyeangukia motoni ilififia, kukawa kimya kabisa katika hekalu.

Ndipo kuhani mkuu Agon alipogeuka, na uso wake ulikuwa kama wa shetani! Akawapigia ukulele wale Malkia akasema, ‘’Kafara itolewe.

Kufuru iliyotendeka na wageni hawa haitoshi na ninyi Malkia mtaingia nyinyi kama mnataka kuwaokoa watu hawa walio tenda uovu ule wa kuwaua wanyama wale waliowekwa wakfu.

Na sasa kuhani wa Jua pia amekufa, wamemuuawa kwa uchawi wao. Wageni hawa waliofika kama pepo za mbinguni toka wapi hatujui, wala hatuwajui ni nani!

Jihadharini ninyi Malkia namna mnavyojiingiza na kushughulika na utukufu wa mungu, hata mbele ya madhabahu yake.

Iko nguvu iliyo kuu kuliko nguvu zenu; iko haki iliyo juu kuliko haki yenu. Jihadharini wala msiinue mikono ya kufuru kuzipinga. Enyi Malkia, kafara itolewe.’’

Ndipo Sorais alijibu, na sauti yake ilikuwa ya utulivu, na kama ilivyokuwa siku zote kama kwamba anadhihaki: ‘’Ee Agon umesema kama ulivyotaka, nawe umesema kweli. Lakini ni wewe unayetaka kuinua mkono wa kufuru juu ya haki ya Mungu.

Kafara ya saa sita imekwisha timizwa! Jua limechagua kuhani wake awe kafara.’’
Basi, wazo hili lilikuwa la kigeni, na watu wote wakalikubali.

Sorais akaendelea: ‘’Watu hawa ni nani? Ni wageni walioonekana wanaelea juu ya ziwa. Nani amewaleta hapa? Walifika hapa namna gani? Unajuaje ya kuwa si watumishi wa Jua?

Je, huu ndio ukarimu unaotaka taifa letu liwape watu ambao bahati imewaleta kwetu, Je, ni vyema kuwatupa motoni? Ole wako! Ole wako! Ukarimu ni nini? Kumpokea mgeni na kumkaribisha vizuri! Kuyaganga majeraha yake, kumpa mahali pa kulala, na chakula.

Lakini malazi yako ni shimo la moto, na chakula chako ni joto la moto. Ole wako, nasema!’’

Hapa alinyamaza kidogo ili aone namna watu wanavyoyapokea maneno yake, na alipoona wanayapokea vizuri, akabadili usemi wake, na sasa ulikuwa wa kutoa amri.

‘’Haya! Jitengeni; wapisheni Malkia na wale wanao funikwa na mavazi ya Malkia.’’
Agon akayakaza meno yake, akasema: ‘’Je, ee Malkia nikikataa?’’

Sorais akajibu kwa kiburi: ‘’Basi hapo nitakata njia kwa walinzi wangu, ndiyo, hata mbele ya madhabahu takatifu na katikati ya miili ya makuhani wako.’’

Agon akafura kwa gadhabu ya kushindwa. Akawatazama watu kama kwamba anawasii wamsaidie, lakini aliona ya kuwa wako upande wa Malkia.

Wazuvendi ni watu wenye udadisi, tena wakarimu, ingawa walifikiri ya kuwa kuwapiga wale viboko waliowekwa wakfu ni kosa kubwa, lakini hawakutaka wageni wa kwanza walioonekana katika nchi yao watupwe katika shimo la moto, na kwa hivyo kukomesha nafasi ya kupata habari zetu kwa kuzungumza juu yetu.


Agon alipoona hivyo akasita, kisha , Nyleptha alisema kwa sauti yake nzuri, akasema: ‘’Kumbuka Agon, kama dada yangu Malkia alivyosema, labda, watu hawa pia ni watumishi wa Jua.

Wao hawawezi kujitetea maana ndimi zao zimefungwa. Mambo haya yawekwe mpaka watakapojifunza lugha yetu.

Nani anayeweza kuhukumiwa bila kusikilizwa? Watu hawa watakapoweza kujitetea, basi hapo tutaweza kuwahukumu.’’

Basi, hii ilikuwa njia ya akili ya kuokoka ingawa Yule mzee mkali kuhani hakuipenda, hana njia nyingine, akasema: ‘’Vyema, Ee Malkia.

Watu na waende kwa amani, nao watakapo weza kusema lugha yetu watapata nafasi ya kujitetea. Na mimi, hata mimi, nitaomba mbele ya madhabahu maradhi yasiingie katika nchi yetu kwa ajili ya kufuru iliyotendeka.’’

Basi maneno yake yalikubaliwa na wote, tukatoka hekaluni tumezungukwa na askari wa kifalme.

Lakini hatukupata kujua kwa siku nyingi habari za mambo yaliyotokea siku ile, na jinsi maisha yetu yalivyookolewa kwa shida nyingi kwa mikono ya ukatili ya makuhani wa Zuvendi, ambao wana nguvu hata karibu kuzishinda nguvu za Malkia.


Kama Malkia hawakufanya bidii kutulinda, tungaliuawa hata kabla hatujaingi katika hekalu la Jua.

Ile hila ya kututumbukiza katika shimo la moto tuwe kafara, ilibuniwa baada ya kujaribu kutuangamiza kwa njia nyingi nyingine ambayo sisi hatukuwa na habari nazo.
 
Back
Top Bottom