Hadithi ya kusisimua: Vita ya wachawi

Hadithi ya kusisimua: Vita ya wachawi

Hatutakonda lakini fupi mno mkuu,vijana wanakubiga bao na hadithi zao,wanatupia mbilimbili kwa siku.
 
Mkuu mzizimkavu hadithi yako ni shedaahh duuh,ila kuna sehemu umenichanganganya kuhusu wahusika mbona majina ya baba yake ambakisye na Bupe yanafanana yaani wote ni andendeksye
Ufafanuzi mkuu
 
HADITHI YA KUSISIMUWA VITA YA WACHAWI-38

ILIPOISHIA:
Walijifikiria kwenda polisi kuzuia anachotaka kukifanya lakini walijiuliza wataeleza azuiwe kwa sababu gani ikiwa serikali haitambui ushirikina japokuwa viongozi wake wanategemea nguvu za giza kutawala. Baada ya kila kitu kukamilika, mganga alimfanyia dawa Andendekisye aliyenyanyuka na kushangaa kuona umati na kumuuliza mganga.
"Nimefikaje hapa?"
"Tulia utajua tu kwa vile mwisho wa ubaya ni aibu."
SASA ENDELEA...


Baada ya kuelezwa vile alipewa uji uliochanganywa na dawa na kuelezwa anywe kisha atulie. Mganga aliachana na Andendekisye na kuwageukia watu waliokuwa wamejaa na kusema kwa sauti ya juu yenye kusikika.
"Jamani nina imani jana makaburini kwa waliokuwepo waliona kila kitu kilichotokea pia katika misiba miwili iliyotangulia. Mnakumbuka nilieleza watu wafanye zoezi la kuharibu tunguri zao. Nina imani wengi hawaamini ila leo nitawaonesha kwa nini nilisema vile.
"Jana baada ya kueleza watu waachane na ushirikina, wapo wazee wangu ambao nawaheshimu sana walinifuata niache zoezi langu ili hali hii iendelee kijijini kwa watu kufanyishwa kazi kwenye mashamba ya watu. Watu kutupiga magonjwa bila sababu. Watu kulishwa vitu vichafu bila kujua.
"Vilevile watu kuuana kama mlivyoshuhudia vifo vya vita ya kichawi ya familia mbili. Hii imekuwa tabia ya watu wa maeneo ya karibu na mpakani kwenda Malawi kufuata uchawi ili kuwadhuru wenzao. Hii imekuwa ikiwaumiza watu wasio na uwezo wa kwenda huko kiasi cha kujiona wao ni miungu watu.
"Najua nitaondoka hapa kijijini lakini kabla sijaondoka nitaacha historia. Jana nilizungumzia wale nyoka na bundi na kuwaeleza usiku mpaka leo majibu yatapatikana na haya ndiyo majibu yake. Mzee wangu baada ya kumuua mtoto wa jirani yake kwa ugomvi wa kijinga aliona raha ya kuendelea kuua akishirikiana na mganga wake ambaye mimi namuona ni mchawi.
"Walipanga kuiteketeza familia ya Amangise lakini matokeo yake wamemuua mke wa mteja wake. Bado hawakushtuka kwa nini amemuua mkewe wakapanga kuja kutengeneza uchawi wao Tanzania kwa kutufanya waganga wa Tanzania hatujui kitu.
"Jana wametega bomu likamlipukia mganga. Na mwenzake anateswa na vivuli vya roho za watu alizozitoa bila hatia ambavyo vitaendelea kumtesa na asiposaidiwa ndiyo itakuwa chanzo cha kifo chake.
"Nilipanga kazi yangu kuifanya mwisho wa wiki lakini kwa dharura hii nimeonelea niifanye leo. Ila sitaifanya kama nilivyopanga, nitaifanya kwa mtindo mwingine kabisa. Kabla ya kuanza zoezi langu nilikuwa nataka nimuulize kaka yangu hapo mganga.
"Eti kaka wewe ni mwenyeji wa wapi?"
"Matipa Malawi."
"Umekuja hapa kufanya nini?"
"Kumtibu bwana Andendekisye."
"Nini kimekupata?"
"Hata mimi nashangaa kwa vile kimetokea ghafla."
"Naomba useme ukweli nini kimekuleta Tanzania na sababu ya kupatwa na tatizo la macho bila hivyo hurudi tena Malawi kwa vile muda wako wa kuishi unahesabika."
"Kwa kweli lazima niseme ukweli."
Mganga toka Malawi alielezea jinsi alivyofuatwa na Andendekisye na kumweleza kuwa jirani yake amemuua mwanaye hivyo naye aliomba kulipa kisasi, naye alifanya kama mteja wake alivyotaka na alimrudishia majibu. Mara ya pili alirudi tena na kutaka kummaliza jirani yake na mkewe lakini ilikuwa tofauti, uchawi walioufanya ulimrudia mwenyewe kwa kumuua mkewe bila kujua.
Pia alielezea jinsi alivyokuja Tanzania ili ammalize adui yao, lakini vilevile ilikuwa tofauti baada ya bundi na nyoka kutofanya kazi. Baada ya kushindwa ndipo alipotega mtego mwingine uliosababisha kupofuka macho.
Baada ya kumaliza maelezo yake yaliyowaacha watu midomo wazi, aliomba msaada wa matibabu ili apone macho.
"Najua nimefanya makosa, naomba unisaidie basi niweze kuona nirudi kwetu."
"Dawa niliyompa mwenyeji wako kuondoa maumivu ya macho ulikuwa uwezo wangu wa mwisho lakini kupofuka ni kazi ya Mungu, sina uwezo huo, hakuna wa kuyaponya macho yako."
"Basi naomba msaada wa kunirudisha nyumbani."
"Atakurudisha aliyekuleta."
"Mmh! Sawa."

Itaendelea jumatatu ijayo...............
 
HADITHI YA KUSISIMUWA VITA YA WACHAWI-39

ILIPOISHIA:
"Dawa niliyompa mwenyeji wako kuondoa maumivu ya macho ulikuwa uwezo wangu wa mwisho lakini kupofuka ni kazi ya Mungu, sina uwezo huo, hakuna wa kuyaponya macho yako."
"Basi naomba msaada wa kunirudisha nyumbani."
"Atakurudisha aliyekuleta."
"Mmh! Sawa."
SASA ENDELEA...


"Sasa ndugu nina imani mmesikia jinsi wanadamu tulivyo wabaya, nataka kuwaambia hapa katika kundi la watu kuna wachawi wengi wakubwa na watoto. Hapa kuna dawa nitaweka kwenye maji kila mmoja atakuja kunawa uso mchawi atajulikana."
Mganga alifanya mambo yake kwa kuweka maji kwenye beseni kisha alisema kuwa kama kuna mtu anayejihusisha na mambo ya kichawi basi atoke mbele na kujipaka maji yale.
"Jamani nataka watu waje wanawe maji haya."
Katika umati uliokuwa pale uwanjani, walitoka wachache ambao walifika na kunawa maji, lakini wengi walibakia wamesimama walipokuwa wamesimama na kumfanya mganga aseme kwa sauti:
"Kwa hiyo hawa ndiyo wasafi na ninyi wote mliobaki ni wachawi?"
Watu wote walikaa kimya, alimwita mtoto mmoja wa miaka saba aliyekuwa amesimama kifua wazi. Yule mtoto alisogea mbele kwa mganga ambaye alimwambia anawe yale maji lakini alikataa na kufanya watu washangae. Mganga alimuuliza:
"Kwa nini hutaki kunawa?"
"Nitaungua."
"Mbona hakuna moto."
"Beseni lote linawaka moto na maji nayaona yanachemka nitaungua."
Aliitwa mtoto mwingine na kuombwa anawe, alinawa bila tatizo lakini alipoambiwa tena yule mtoto aligoma na kusema ataungua. Watu waliokuwa wakiona kama utani, mganga alimwita mzee mmoja ambaye aligoma na kuamua kuondoka.
"Ndugu zangu nataka niwaambie kitu kimoja kijijini kwetu uchawi umetawala, ni kweli anachosema mtoto kuwa ameona moto kwa vile ni mchawi.
Huyu mtoto anatumiwa na bibi yake usiku katika kuwanga na ndiye dereva wa ungo. Naweza kumwona mtoto mdogo lakini usiku anafanya kazi kubwa ya kuwabeba magwiji wa kijiji hiki akiwemo bibi yake.
"Kama mnabisha ngoja nimuulize, eti jana usiku mlikwenda wapi?"
"Nigeria."
"Kufanya nini?"
"Bibi aliniambia kulikuwa na mkutano."
"Nini kiliwapata?"
"Tulipofika sehemu wanasema Kameruni, ungo ulianza kuyumba nilijitahidi kuuweka sawa lakini mmoja wetu alianguka."
"Bibi yako alifanya nini?"
"Alipata presha."
"Yupo wapi?"
"Yupo ndani anaumwa."
"Mmesikia?" Aliwauliza watu waliokuwa wameshika mdomo wasiamini kilichokuwa kikisimuliwa na yule mtoto.
"Ndiyo," waliitikia wote.
"Mmeona, sasa hebu jiangalieni wote," aliwaeleza watu waliokuwepo pale.
Watu wote walitazamana bila kujua mganga alikusudia nini. Baada ya muda aliwauliza.
"Jamani kuna mtu hakuvaa nguo hapa?"
"Hapana wote tumevaa," walijibu kwa pamoja.
"Basi nataka kuwaeleza hapa kuna watu zaidi ya kumi hawana nguo na wamekuja kujaribu ninachokifanya. Nataka kuwaeleza kuwa wanajisumbua zaidi ni kuumbuka, ndugu zangu hakuna faida ya uchawi zaidi ya kuishi maisha magumu huku ukiingilia kazi ya Mungu kuua na kutesa.
"Watu wamefilisika kutokana na mchezo wa chuma ulete bila kujua wanawafanyia watu kazi. Nina imani baada ya tukio la leo nitahamishwa kijijini kwa vile wenye nguvu wameshasema, lakini nataka kuwaeleza nitakachokifanya leo wachawi wote wataanza upya kutumia nguvu za kichawi kwa vile nitaua nguvu zao zote.
Kwa muda mfupi kila mtu ataona mabadiliko ya mwili wake kama hutolewa usiku na kugeuzwa farasi wa kubeba wachawi bila kujua. "Wagonjwa wenye maradhi yasiyoonekana yatapata ufumbuzi, wenye uzito kwenye kazi na biashara baada ya zoezi langu watashangaa mabadiliko yatakayotokea.
"Kila mwenye tatizo la kichawi ataona mabadiliko ila mwenye tatizo la kudra ya Mungu aendelee kumuomba atapona. Nilisema kuna watu wapo uchi hawana nguo inawezekana mnaona natania, kwa hiyo mnataka kumuona?"
"Ndiyooo!" Waliitikia wote.
"Sasa nitamtoa mmoja mbele ambaye amekuja kunipima," baada ya kusema vile alitembeza macho kwenye kundi la watu na kusema:
"Namuomba mwanamke mmoja mwenye kanga ili mtu akiumbuka awahi kumfunika ili kumsitiri."
Mwanamke mmoja alitoka mbele na kanga mkononi, baada ya kupita alimwita bibi mmoja aliyekuwa amesimama pembeni mkono amekunja ngumi. Lakini yule bibi alikataa, mganga aliwatuma vijana kumleta mbele. Walimbeba juujuu na kumpeleka mbele.
Baada ya kufikishwa yule bibi aliweka mkono mdomoni kama mwanamwali na kuangalia chini kama mtu mwenye aibu. Baada ya kufikishwa mganga alimuomba mwanamke mwingine afike mbele, alitoka mwanamke mwingine mbele.
"Sasa ninataka kuwaonesha kitu mnamjua huyu bibi?
"Hatumjui."
"Huyu ni mgeni ila ameletwa kwa ajili ya kukabiliana na mimi ndiyo maana nikasema wapo zaidi ya kumi wote mtawajua."
Baada ya kusema vile aliweka maji mdomoni na kumpulizia mwanamke aliyeitwa mara ya mwisho. Kisha aliwageukia watu na kuwauliza:
"Mmeona nini?"
"Hatujaona kitu."
"Huyu mama amevaa hajavaa?"
"Amevaa."
"Mama simama hapo, bibi simama hapa."
Yule bibi alisimama alipokuwa amesimama mwenzake kisha mganga alijaza maji kinywani na kumpulizia. Ghafla kukawa na sinema ya bure na kuwafanya watu wote wapige kelele baada ya yule bibi kubakia mtupu. Alimuomba mama aliyekuja na nguo amfunge kisha aliwageukia watu na kuwauliza.
"Mmeona?"
"Ndiyo."
"Basi huyu ni mmoja wa wachawi waliopo hapa japokuwa wapo wengine wamevaa, tunakaa nao lakini ni viumbe wabaya ndugu zetu wanapotea kumbe wamegeuzwa misukule. Ndugu zetu wengine wanakufa katika mazingira tata kumbe wazazi wetu wanawatoa sadaka ya nyama kwa vile wanakula nyama za watu. Hii imefanya nyumba nyingi ziwe tupu kwa ajili ya tamaa ya wazazi.

Itaendelea Alkhmisi ijayo...........


 
HADITHI YA KUSISIMUWA VITA YA WACHAWI-40

Ilipoishia wiki iliyopita.
Yule bibi alisimama alipokuwa amesimama mwenzake kisha mganga alibunda maji na kumpulizia. Ghafla kukawa na sinema ya bure na kuwafanya watu wote wapige kelele baada ya yule bibi kubakia mtupu. Alimuomba mama aliyekuja na nguo amfunge kisha aliwageukia watu na kuwauliza.
"Mmeona?"
"Ndiyo."
Sasa endelea...


"Basi huyu ni mmoja ya wachawi waliopo hapa japokuwa wapo wengine wamevaa tunakaa nao lakini ni viumbe wabaya ndugu zetu wanapotea kumbe wamegeuzwa misukule. Ndugu zetu wengine wanakufa katika mazingira tata kumbe wazazi wetu wanawatoa sadaka ya nyama kwa vile wanakula nyama za watu. Hii imefanya nyumba nyingi ziwe tupu kwa ajili ya tamaa ya wazazi.
"Lakini leo nitafanya nilichokitangaza huu ni wakati wa kila mtu kuleta uchawi wake hapa, una hiyari ya kuleta au kutoleta wenye kiburi leo ndiyo siku yao ya kuumbuka hadharani."

Kauli ile iliwafanya watu watazamane kila mmoja akimhofia mwenzake huenda ni mchawi. Upande wa wachawi walikuwa na tumbo moto huku wakiamini wanaumbuka.

"Leo nitakuwa na kazi moja ya kuua uchawi nyumba zote zenye uchawi pia kuua nguvu za watu wanaowatesa wenzao. Najua siwezi kumaliza ila wengi mtakutana nao wakiwa wamechanganyikiwa baada ya zoezi langu la usiku wa leo.
"Nina imani kwa zoezi langu watu wengi mtaona mabadiliko makubwa ya miili yenu kwa vile wengi mmekuwa mkitumika katika kuwafanyia kazi watu kama kulima na kubeba mizigo. Miili yenu mmekuwa kama mmebeba vitu vizito bila kujua.
"Pia sehemu zenu za biashara na kazi kuwa na nuru kutokana na kutiwa giza la kichawi. Nyumba zenu magonjwa hayaishi bila kujua wachawi kuna vitu wamechimbia mbele ya nyumba zenu.

"Kazi nitakayoifanya itaua kila kitu, narudia kusema kuwa maisha yangu yapo hatarini, ila nasema hawaniwezi zaidi ya kuzidi kuwaumbua. Mpango wao mmoja tu ndiyo unaoweza kufanikiwa wa kunifukuza, naamini nikiondoka mtawajua wabaya wenu ni kina nani."

"Namalizia kwa kumuomba Amangise na mkewe wapite mbele ili wamalize tofauti zao na jirani yao Andendekisye kwa vile kila mmoja alitumia kiburi cha nazi na matokeo yake mmepata hasara wote."
Baada ya kusema vile Amangise na mkewe walipita mbele na kusimama, mganga alisema:
"Mnajua sababu ya kukutana hapa ni kati ya ugomvi wa familia mbili ambazo umesababisha kupoteza watu wanne ambao wamekufa bila sababu kwa ubabe, familia ambazo walikuwa na ufumbuzi mwingine wa kutatua tatizo lao matokeo yao kukimbilia kurogana na kusababisha mauaji ya kutisha.

"Si hawa wapo watu wengi hapa kijijini ndiyo tabia zao, jambo dogo tu anavuka mpaka kwenda Malawi kuchukua uchawi na kuja kumuumiza mwenzake wakati suluhu si nguvu bali busara. Wengine ukiwaona ni wacha Mungu wazuri kwenye nyumba za ibada, wapo mstari wa mbele lakini wakitoka hapo wanavaa roho zao za kikatili na kuwanga usiku kucha.

"Kuna mtu simsemi ila kuanzia leo mtashangaa mashamba yake hayataendelea kulimwa kwa vile akiwatumia misukule wataonekana hana nguvu za kuwaficha tena. Na muda si mrefu watu mtawaona ndugu zenu ambao mlijua wamekufa na kuwazika lakini kumbe kilikuwa kiini macho watatoka katika nyumba walizofichwa kwa vile hakuna kizuizi cha kuwazuia tena.

"Sitamtaja mtu aliyefanya vile kwa sababu nitakuwa nimetengeneza vita lazima ndugu zao, lazima watu watauana na mimi nitakamatwa na jeshi la polisi kwa vile serikali haiamini uchawi japo asilimia kubwa ya viongozi wake wanaongozwa na nguvu za giza.
"Sasa nia yangu ni kuwaomba kuondoa tofauti zao kwa vile yaliyopita yamepita, Andendekisye kama ulivyoniahidi nataka uyatekeleze ukienda kinyume sitakuwepo. Amangise na mkewe hii ni fursa ya kudhihirisha kuwa mmesafisha mioyo yenu na kumrudia Mungu kwa kumsaheme jirani yenu.

"Napenda kuwaeleza sisi ni waganga lakini mganga wa kweli ni Mungu. Mkiishi kwa kumtegemea Mungu itawasaidia kuishi kwa furaha. Yapo magonjwa ya kawaida ambayo sisi waganga huyatibu lakini si ya kurogana."
Baada ya kusema vile Amangise na mkewe walisema wamejifunza kitu katika yaliyotokea na kusema wapo tayari kumsamehe Andendekisye kwa yote yaliyotokea. Naye Andendekisye huku akilia alisema ameona faida ya kumtegemea mwanadamu kuliko Mungu matokeo yake kampoteza mkewe na mwanaye.

Wote walikubali kusameheana na kufanya watu wote washangilie, baada ya zoezi lile kwisha. Mganga alimgeukia mganga kutoka Malawi na kusema:
"Ndugu yangu najua fani yetu ni kutibu watu ila umeigeuza na kuwa mchawi wa kuwaua watu na kuwatesa. Hili ulilokutana nalo ni funzo, nilitaka kukuacha uwe kipofu na usingepona sehemu yoyote unayojua kutokana kuwa mchawi na si mganga."
"Nakuahidi nikiweza kuona sitarudia tena kufanya nilichokifanya," mganga alitoa ahadi nzito.
"Umeua watu wangapi kwa mtindo huu?"
"Ni wengi ndugu yangu."
"Nakusaidia uone ukirudia macho yakifumba hayatafumbuka tena, wewe ni mganga tibu watu na si kuwaroga."
"Nitafanya kwa kila utakaloniagiza."

Mganga aliagiza maziwa mabichi yasiyochanganywa na kitu, aliweka dawa na kumpa mganga toka Malawi anawe. Alinawa na kuwashangaza watu kutoka vitu vyeusi kama udongo. Alipiga kelele za maumivu macho yaliuma zaidi ya mwanzo.
"Jamani nakufa au ndiyo unanimaliza?"
"Maumivu hayo ndiyo kupona kwako."

Aliendelea kunawa mpaka maziwa aliyonawa yakawa yanatoka na rangi yake ileile. Baada ya kumaliza kunawa alipewa maziwa mengine bila dawa ambayo alinawa na kuambiwa afumbue macho.
"Si..si..amini nimeona...nimeona..asante..asante," mganga toka Malawi alipiga magoti mbele ya mganga mwenzake.
"Kaka nyanyuka mimi sina hadhi ya kupigiwa magoti bali muumba wako, nataka kukwambia kitu kimoja chagua kitu kimoja uwe mchawi uwaroge watu au uwe mganga uwatibu watu."
"Nataka kuwa mganga."

"Basi achana na uchawi, babu yako mzee Msioka alikuwa mganga mkubwa sana, aliwasaidia watu hakuua wala kutesa, mwenye kazi ya kutesa na kuua ni Mungu tu kwa nini uingilie kazi yake?"
"Najua nimefanya makosa."

"Sasa wote mtakuja kunywa maji kwenye ndoo hii, atakayefanya uchawi wowote hataomba maji atakufa papohapo au kuwa kichaa kisichopona. Naomba vijana wahakikishe kila mtu anakunywa maji haya."
Zoezi lilianza kwa watu kunywa maji kidogokidogo, baada ya zoezi lile kwisha, mganga alipita nyumba baada ya nyumba huku akimwaga vitu.

Baada ya zoezi lile alirudi nyumbani kwake na kuacha gumzo kila kona. Mganga kutoka Malawi aliondoka siku ileile kurudi kwao huku akiamini yeye si mganga bali wapo waganga zaidi yake.
Hakuamini kijana mdogo kama yule kumuumbua lakini alimshukuru kwa huruma yake. Usiku wa siku ile baadhi ya wazee wenye imani ya kishirikina walioona wameumbuliwa walikodi vijana wa kijiji kile kumhamisha kinguvu yule mganga usiku uleule walihakikisha wanamtoa nje ya mji wa Kyela na kumwambia akirudi wanamuua. Zoezi lile lilifanyika kwa siri hakuna aliyejua huku nyuma nyumba yake ikatiwa moto.Je, nini kitaendelea?

Usikose kufuatilia Jumapili ijayo....................
 
Back
Top Bottom