MIRATHI YA KAKA sehemu ya 34
ILIPOISHIA TOLEO LILLOPITA...
“Tuendelee!” niliropoka mara baada ya kugutuka kutoka kwenye kuwaza kwa kina.
“Huo ulikuwa ni utangulizi tu, hivyo kama unataka kuwa mmoja kati ya matajiri wa dunia hii yakubali nitakayokuambia.” Aliongea Sharifa kisha akanyosha mkono wake kuichukua brificase iliyokuwa mezani.
SASA ENDELEA..........
Aliifungua brificase na kuniambia niangalie. Naam! Ilikuwa imesheheni fedha za kigeni, fedha ambazo zilikuwa zimebanwa katika maburungutu. Nilijikuta nikimeza mate baada ya kuviona vitita hivyo.
“Kama utakubaliana na ninachoenda kusema basi matumizi yako kwa siku yatakuwa ya pesa kama hizi.” Mwanadada huyo alizidi kunitamanisha japokuwa nilikuwa sijajua atakachokitaka kutoka kwangu.
Nilishusha pumzi huku nikiongeza umakini wa kumsikiliza. Nilizidi kuwa katika wakati mgumu kwa kujua kwamba kama nitamuendekeza sana msichana huyo basi pepo ya Mwenyezi Mungu nitakuwa nimeipa kisogo.
Hata hivyo nilijiambia ngoja kwanza nimsikilize, uamuzi si ulikuwa ni wangu bwana, kama ningetaka kukubali basi ningekubali na kama ningetaka kukataa basi ningekataa.
“Najua mwanzo ulikuwa ukinichukia sana, hasa hasa pale niliposimama mbele ya mahakama kutoa ushahidi juu ya kesi yako. Lakini sasa hivi hunichukii tena, hasa baada ya kukuokoa kutoka kwenye kunyongwa, uongo?”
“Ni kweli.”
“Mateso yote uliyokuwa ukiyapata tangu kifo cha marehemu kaka yako ulikuwa ukitumikia adhabu.”
Maneno hayo yalinishtua na kunifanya nigutuke.
“Adhabu! Adhabu kwa kosa lipi? Na kosa hilo nilikuwa nimemkosea nani?” Niliuliza.
“Kosa hukutenda wewe bali ni kaka yako James.”
“Alitenda kosa gani kaka yangu?”
“Usiwe na pupa, nipo hapa kukufunulia kila kitu hivyo nitakueleza siri nzito aliyokuwa nayo kaka yako.”
Hilo nalo lilikuwa neno; kujua kile kilichokuwa kimejificha nyuma ya pazia wakati wa uhai wa kaka James, nilizidi kuongeza umakini. Kikao chetu kilizidi kutia fora, sasa nikawa na shauku ya mambo matatu. Jambo la kwanza ni shauku ya kujua siri nzito iliyokuwepo kwa kaka James.
Jambo la pili lilikuwa ni shauku ya kujua masharti ambayo nilikuwa nimeambiwa nitapewa wakati natoroshwa gerezani. Jambi la tatu ni shauku ya kutaka kujua madhara yatakayonipata endapo ningeshindwa kutekeleza masharti hayo.
Sharifa alianza kunieleza habari ya kaka James. Habari ambayo iliyaamsha machungu ya moyo wangu, nikahisi maumivu makali yakipenya barabara kunako mtima wa moyo wangu.
Kaka James alipokuwa anamalizia masomo yake ya kidato cha nne aliambiwa na rafiki yake mmoja kuwa kuna mganga wa kikongo aliyekuwa kaingia nchini. Mganga huyo alikuwa akiwatengenezea watu dawa ya kupata utajiri.
Kutokana na tamaa za kutaka kupata utajiri, kaka James alimtaka rafiki yake huyo ampeleke kwa mganga huyo ili akatengenezewe dawa ya kuwa tajiri. Ndipo alipopelekwa.
Alipofika kwa mganga huyo aliambiwa kuwa masharti ya kupata utajiri ni lazima uingie maagano na majini. Maagano hayo yalikuwa ni maagano ya kafara za damu huku yakiwa katika madaraja matatu.
Daraja la kwanza lilikuwa ni kuwatoa kafara wazazi wako wote pamoja na ndugu yako mmoja wa damu. Ndugu aliyetakiwa katika daraja hili ni mdogo wako, kaka yako ama dada yako. Kama wote hao huna basi mjomba ama shangazi hutakiwa.
Baada ya hapo utajiri unaanza kwa kasi ya kawaida. Ukishakaa miaka mitano unatakiwa kutoa tena kafara ya mtoto wako wa kwanza pamoja na mama yake kama wewe ni mwanaume. Lakini kama ni mwanamke basi unatakiwa kumtoa mtoto wako wa kwanza pamoja na baba yake.
Ukishakamilisha kafara za daraja la kwanza na la pili unatakiwa sasa kuhamia kwenye daraja la tatu ambalo kafara yake huendelea mwaka hadi mwaka. Kafara katika daraja hili ni ya mtu yeyote ama awe mfanyakazi wako au anayetumia vitu vyako mfano abiria katika magari yako, mpangaji katika nyumba yako na kadhalika.
Masharti hayo ndiyo aliyopewa James naye akakubaliana nayo. Siku chake baada ya kuingia kwenye maagano yale ya kishetani wazazi wetu walikufa wote kwa mkupuo katika ajali ya kutisha.
Habari hii ndiyo iliyonitonesha majeraha yaliyokuwa yamejengeka ndani ya moyo wangu mithili ya donda ndugu. Kuanzia hapo nilianza kumchukia James na kumuona ni shetani mkubwa ambaye alikuwa anastahili kutupwa kwenye moto wa jehanamu.
Nilijikuta nahukumu wakati maandiko ya Mungu yanatuambia tusikuhumu ili na sisi tusije tukahukumiwa. Niliumia sana nilipoambiwa hiyo habari.
‘Ndiyo maana mambo ya kaka James yalianza kuwa safi mara baada ya vifo vya wazazi wetu.’ Niliwaza.
Wakati huo huo nikakumbuka swali, nikaona nimuulize huyo huyo Sharifa kwani hata yeye alikuwa ni mdau wa kafara hizo.
“Umesema kafara ya daraja la kwanza inahusisha wazazi wote wawili na ndugu mmoja wa damu, mbona sasa baba yangu alikufa wakati hakuwa baba wa kumzaa James?”
“Kwa kuwa alikuwa kamuoa mama mzazi wa James na pia alikuwa na mapenzi ya baba kwake, basi kafara yake ilifana.” Alijibu Sharifa.
Akaendelea kunieleza kosa la James lilikuja kutokea baada ya kutakiwa kutoa kafara nyingine ili kukamilisha kafara za kwenye daraja la kwanza. Hapo alitakiwa ndugu yake wa karibu; mdogo mtu, kaka mtu, shangazi ama mjomba.
Kwa bahati mbaya sana ndugu wa damu aliyekuwa yu ngali hai nilikuwa ni mimi peke yangu. Aliamua kukaidi kunitoa kafara kutokana na mambo mawili.
Jambo la kwanza ni upendo uliokuwepo baina yangu na yeye. Kusema kweli kaka James alikuwa ananipenda kupita kiasi, na ndiyo maana hakuwa tayari kunitoa kafara.
Jambo lingine lililomsababisha kaka James agome kunitoa kafara ni kwamba hapakuwa na ndungu mwingine wa karibu zaidi yangu mimi. Kama angenitoa kafara basi angebaki bila ndugu wa karibu katika dunia hii. Sasa kubaki bila ndugu wa karibu lilikuwa ni jambo gumu sana kwake.
Nadhani hata wewe mpenzi msomaji usingepata fursa ya kusimuliwa simulizi hii nzuri iliyojaa vitisho vya lejaleja na yenye kusisimua kwani ningekuwa tayari nimeshalala mauti.
Baada ya kuona kunitoa kafara haiwezekani, James aliacha kabisa kwenda kwa mganga aliyekuwa amemfanyia dawa ya kumpa utajiri huo wakati alitakiwa awe anaenda mara moja kwa mwezi kufanya ibada. Muda wa kukamilisha kafara ya daraja la kwanza ulipita huku akiwa hajakamilisha, akaongezwa muda wa ziada nao ukawa umepita.
Mganga alipoona James kapuuzia agano hilo aliamua kumripoti kwa wataalamu wake ambao ndiyo waliokuwa wanamwezesha kufanya uganga huo.
Wataalamu hao walikasirishwa sana na kitendo chake cha kujifanya mjanja na mwenye akili kuzidi wao waliokuwa wamempa maagizo yale. Ndipo walipoamua kumtoa duniani kwa staili ya kujiua mwenyewe ili akaonekane ana dhambi hata mbele za mwenyezi Mungu.
Japo kabla ya kutoa adhabu hiyo walitoa muda wa kutosha kwake wakitegemea labda angejirudi na kukamilisha agano lao, siku zilizidi kwenda bila ya mabadiliko yoyote ya kutaka kujirudi kwa James.
Tena alipoona kakaa muda mrefu bila kupatwa na matatizo yoyote ilhali alikuwa hajakamilisha kutoa kafara alijua kuwa huenda zile zote zilikuwa ni danganya toto tu na vitisho visivyokuwa na misingi yoyote. Baada ya muda wa nyongeza kuisha uhai wa James ukawa ni halali ya wataalamu hao.
Hayo ndiyo mambo yaliyosababisha kifo cha wazazi wangu pamoja na kaka yangu. Tamaa ya kaka yangu kupata mali nyingi kwa njia ya mkato ndiyo iliyagharimu maisha yake na ya wazazi wetu kwa ujumla. Habari hiyo yote mimi nilikuwa siijui ila Sharifa ndiye aliyekuja kuning’amua.
NINI KITAFUATIA? USIKOSE............!!!