mizambwa
JF-Expert Member
- Oct 8, 2008
- 4,421
- 1,792
- Thread starter
- #21
MIRATHI YA KAKA sehemu ya 12
ILIPOISHIA SEHEMU ILIYOPITA......
“Afande, kama vipi richukue maerezo maana tayari rimeshazinduka.” Alisikika afande aliyekuwa ameshikilia bunduki akimwambia mwenzake ambaye alikuwa kashika faili mkononi.
“Hamna tabu afande, hata mimi nilikuwa ninalifikiria hilo kichwani mwangu.” Alijibu afande huyo.
SASA ENDELEA.......
Mara nilimuona afande huyo aliyekuwa kashikilia faili mkononi akivuta kiti chake na kusogea karibu kabisa na pale nilipokuwa nimelaza kichwa changu. Alifungua faili lake huku akiwa kashikilia kalamu mkononi.
Alianza kunihoji maswali kuhusiana na tukio zima la mauaji ya Kishoka, kila aliponiuliza nilimjibu, kila nilipomjibu aliandika kwenye karatasi iliyopo kwenye faili lake.
“Mnaishi wangapi katika hiyo nyumba?” lilikuwa ni baadhi tu ya maswali niliyokumbana nayo kutoka kwa kachero huyo. Swali hilo nililijibu kwa kusema kuwa tunaishi wawili tu katika hiyo nyumba, yaani mimi na Kishoka.
Mara aliniuliza uhusiano wangu na Kishoka, nami nilimjibu kuwa Kishoka ni mpangaji wangu katika nyumba yangu niliyorithi kutoka kwa marehemu kaka yangu, kaka James ambaye alikufa kifo cha kujiua mwenyewe kwa kujifyatulia risasi kichwani baada ya kumuua aliyekuwa mpenzi wake pamoja na jamaa aliyemfuma akilamba asali ya mapenzi kwa mpenzi wake huyo..
“Sasa kwa nini umeamua kumuua Kishoka?” Askari huyo alinifyatulia swali jingine. Nami nilimjibu bila kusita wala kujing’atang’ata kwamba mimi sijaua.
“Kama wewe hujaua, ni nani aliyemchinja Kishoka ilhali mnaishi wawili tu katika hiyo nyumba?”
Nilijitahidi kuwa makini sana katika maelezo yangu ili nisijikanganyekanganye halafu nikaonekana nimeua kweli. Niliamua kumtaja muuaji, nikasema kuwa ni msichana fulani ambaye alianza kunifanyia vioja tangu juzi nilipokutana naye ufukweni. Nilieleza jinsi mambo yalivyokuwa kati yangu na mwanadada huyo kule ufukweni.
Nilipoulizwa jina lake na mahali alipokuwa anaishi niliishia kusema sina nijualo juu yake. Nilijaribu kurudia tena kutoa maelezo jinsi nilivyokutana na msichana huyo, sikuwa namfahamu hata kidogo, lakini yeye alidai kuwa ananifahamu na kwa kunithibitishia hilo alinitajia hadi jina langu. Hakuishia hapo tu, aliongeza kuwa mpaka kwangu alikuwa anapajua hivyo akaniahidi atanitembelea kesho yake asubuhi.
“Ilipofika kesho yake asubuhi kweli alikuja?” Aliendelea kuhoji askari huyo huku akionekana kunisikiliza kwa makini sana.
“Ndiyo alikuja lakini vilikuwa ni vioja vitupu!”
“Uliweza kuonana naye na mkaongea nini?” Aliniuliza afande nami nikaanza kumdadavulia vile ilivyojitokeza tangu msichana huyo anafika pale getini, akakaribishwa na Kishoka lakini akakataa kuingia ndani.
Niliendelea kueleza jinsi msichana huyo alivyopotea kimazingara tusimuone alikoelekea. Nilizidi kuweka wazi kila kilichojitokeza mpaka wakati nilipokikuta kichwa cha Kishoka kikiwa kimetenganishwa na kiwiliwili chake. Nilimalizia kwa kusema kuwa muuaji si mimi bali ni huyo msichana ambaye kwa vyovyote vile si binadamu wa kawaida.
Askari huyo aliyakataa katukatu maelezo yangu na kuniambia kuwa mimi ni muongo na hayo maelezo yangu hayawezi yakanifikisha kokote, akasema jeshi la polisi haliamini ushirikina wala mazingazi. Akanitaka nieleze ukweli ili aone ni jinsi gani ataweza kunisaidia. Nilimwambia ukweli wangu ndiyo huo na sikuwa na maelezo mengine zaidi ya hayo.
Afande huyo nilimuona akifunga faili lake na kuniambia nijiandae kwenda kuozea jela. Alichodai ni kwamba laiti kama ningeeleza ukweli basi angeweza kunisaidia.
Nikiwa rumande machozi yalizidi kunitiririka bila kukauka utadhani chemichemi za mto Naili, chemichemi ambazo hutiririka bila kukauka misimu yote; iwe masika ama kiangazi. Mifereji ya machozi ilikuwa inatiririka kutoka machoni ikipitia mashavuni mpaka kwenye kidevu.
Harufu mbaya ya humo kwenye ‘gheto’ la watuhumiwa ilinifanya nipige chafya mara kwa mara. Nilijaribu kujikaza kiume nijizuie kulia lakini cha ajabu machozi yalizidi kunitoka. Nilikuwa sijawahi kuswekwa rumande hata siku moja tangu kuumbwa kwa misingi ya dunia.
Siku niliiona kama haiendi, masaa nayo yalikuwa kama yamesimama. Tangu saa tano za asubuhi baada ya kuruhusiwa hospitali niliingia humo, mpaka muda huu ambao nilikuwa nauhisi ni kama saa tisa za jioni nilikuwa nimeiva sawasawa. Kwa muda mchache huu ambao nilikuwa nimekaa ndani nilikuwa najiona kama nimekaa mwezi mzima.
Mawazo kibao yalikuwa yametawala kichwa changu; niliwaza biashara zangu zitasimamiwa na nani, zaidi ya yote kilichokuwa kinaniumiza kichwa ni hatima ya kesi yangu iliyokuwa inanikabili, kesi ya mauaji.
Ilipofika usiku nilizidi kuipata freshi, tena ni freshi ya mwaka. Sulubu iliyokuwemo kwenye ‘gheto’ la watuhumiwa haielezeki, yaani ni sulubu ya kufa mtu. Hapo ndiyo nilianza kuamini kuwa kweli rumande siyo kanisani ama msikitini.
Mbu walinishambulia si mchezo, nilijaribu kuwaua mmoja baada ya mwingine lakini wakawa hawaishi wala kupungua, suala la kupata usingizi walau dakika moja lilikuwa ni ndoto; tena ndoto yenyewe ni ndoto ya kuota mchana kweupe.
Siyo mbu peke yao walionipa kero usiku huo, kunguni na viroboto nao walizidi kuleta adha katika mwili wangu.
‘Kama rumande ya polisi tu hali ndiyo hii, kule gerezani sasa hali ikowaje?’ Nilizidi kutafakari huku nikiwa ‘buzy’ kupambana na wadudu hao wasiyokuwa na chembe ya adabu hata kidogo.
Niliwatumbua kwa hasira kila nilipowabahatisha wakigema damu yangu, lakini nao ndiyo kwanza walizidi kuongezeka utadhani walikuwa wakialikana.
‘Kwa mtindo kama huu kufikia asubuhi nitakuwa nimepoteza lita kadhaa za damu katika mwili wangu. Lakini chanzo cha mateso haya yote ni yule msichana aliyemuua mpangaji wangu Kishoka.’ Niliendelea kunung’unika peke yangu. Manung’uniko ambayo hayakuzaa matunda ya wokovu wa kesi yangu hata kidogo.
Hayawi hayawi mwisho yakawa, jogoo la kwanza nililisikia likiruka ‘bonanza’ kuashiria alfajiri inawadia. Mara nilisikia jogoo la pili na hatimaye la tatu. Kulionekana kupambazuka huku nikiumaliza usiku kwa kuutoboa, yaani namaanisha sikusinzia hata sekunde moja zaidi ya kupepesa macho pale ilipobidi.
Ikawa asubuhi, siku ambayo sikujua itaishaje. Nilitegemea kupandishwa kizimbani kwa mara ya kwanza ili kusomewa shauri lililokuwa linanikabiri. Lakini mambo yakawa sivyo.
Mara mlango ulipofunguliwa niliwaona askari wawili waliokuwa wameshikilia bunduki kila mmoja wamesimama mlangoni kisha wakanitaka nitoke. Nilipotoka walinifunga pingu mikononi kisha wakanitanguliza mbele mpaka kwenye chumba kimoja katika kituo hicho kisha mahojiano yakaanza upya.
JE, NINI KITATOKEA HUKO KATIKA MAHOJIANO? MUUAJI ATAJULIKANA? FUATILIA BAADAYE...