***
"Bado siamini kama amefanya hivyo," mtu mmoja alikuwa akifoka pia, akiwa kaketi katika kundi la watu wenye hasira na mshangao kama yeye. Mabega yao yalikuwa yakimeremeta kwa nyota ambazo zilipamba magwanda yao kudhihirisha madaraka yao.
"Amefanya, lakini siamini kama Joram ni mtu wa kutenda kitendo cha aibu kama hiki. Jambo la kusikitisha zaidi ni jinsi habari hiii ilivyovuja kiasi cha kuyafikia masikio ya adui zetu. Leo nimesikia habari hizo na Afrika Kusini," Kombora aliendelea kulalamika.
"Ujerumani pia imetangaza afande," mtu mmoja aliongeza.
"BBC vilevile," mwingine aliongeza.
"Unaona, basi? Unaona habari mbaya zinavyosafiri upesiupesi? Pamoja na kwamba Joram ametuasi kimsimamo tulikuwa na haki ya kumsetiri kwasababu ya vitendo vyake vya nyuma. Sasa nadhani hatuna tunachoweza kufanya. Maji yamekwishakumwagika, hayazoleki. Lililopo ni kutafuta uwezekano wa kumpata na kurudisha pesa zote, hasa za kigeni."
"Hilo ndio tatizo mzee," msaidizi wake mmoja alijibu. "Taarifa za mwisho zinathibitisha kuwa hayupo kabisa hapa nchini. Kuna dalili kuwa ametorokea nchi jirani kwa ndege ya kukodi."
"Lazima, lazima apatikane," Kombora alisisitiza. "Pesa alizochukua ni nyingi sana na zinahitajika sana. Hana haki ya kuzifuja kwa starehe zake binafsi. Wasiliana na nchi jirani zote. Wasiliana na Interpol. Waarifu kuwa tunamhitaji Joram kwa hali na mali. Maadamu siri imekwishafichuka, hakuna haja ya siri tena."
Baada ya majadiliano marefu jalada hilo lilifunikwa na kuletwa jingine ambalo lilikuwa “zito” Zaidi. Lilihusu mkasa au maafa yaliyotukia taifa pamoja na lile tishio la maisha na majumba muhimu. Walipima juhudi zao zote wakilinganisha habari mbalimbali. Haikuwepo dalili yoyote ya kujenga matumaini.
Kisha wakavirudia vifo vya watu wawili katika chumba kimoja cha hoteli hapa Jijini. Dalili zilionyesha kuwa marehemu walikuwa watu wasiofahamiana kabisa. Pekuapekua yao katika chumba hicho haikuwapatia kitu chochote zaidi ya mavazi ambayo yalionyesha kuwa yameshonwa nchi za nje. Nyaraka walizohitaji, ambazo zingeweza kuwasaidia, hawakuzipata. Ilielekea vifo hivi vingeingia katika yale majalada ambayo kesi zake hazikuwahi kutatuliwa. Hivyo, baada ya kuzitazama tena picha za marehemu wote, zilirudishwa katika majalada na kufungiwa.
Kikao kikaendelea.
***
"Kwanini umefanya hivyo, Joram?" Nuru aliendelea kufoka.
Joram, ambaye alionekana kimawazo yuko maili kadha wa kadha nje ya chumba hicho, alimtazama Nuru kwa muda. Kisha ikawa kama amemkumbuka. Tabasamu dogo likamtoka, likifuatwa na sauti nzito, "Ilikuwa lazima nifanye vile, iko siku utaelewa Nuru."
"Nitaelewa!" Nuru alifoka, "Nitaelewa nini, mwanamume mwenye heshima zake na hadhi yake duniani anapothubutu kuingia benki na kuiba pesa ambazo nchi na watu wake wote wanazitegemea? Siwezi kuelewa kabisa, Joram. Ambacho naweza kuelewa ni wewe kuondoka sasa hivi na kwenda zako ofisi ya Ubalozi wetu ukaombe radhi na kurudisha kila senti. Tafadhali fanya hivyo, Joram."
Hilo lilisababisha kicheko kwa Joram. "Nina haki ya kula pesa za Tanzania kama wengi wao wanavyozila, Nuru. Huoni watu wenye mishahara ya shilingi elfu mbili wanavyojenga majumba ya mamilioni? Unadhani wanazipata wapi bila ya wizi? Tofauti yangu na wao ni kwamba mimi nimeiba kimachomacho, wao wanaiba kisirisiri. Mwizi ni mwizi tu." Akasita kidogo kabla ya kuendelea, "Acha tuzitumie Nuru. Acha tuzifaidi. Hii ni nafasi pekee katika maisha yetu ambayo hatujaisahau. Jisikie starehe..."
"Siamini kama maneno hayo yanatamkwa na Joram Kiango. Kwanini umebadilika kiasi hicho Joram?"
Kabla Nuru hajapata jibu mlango uligongwa na kufunguka taratibu. James aliingia. Uso wake ulionyesha kuwa alikuwa na habari ambayo si nzuri sana. Baada ya kubadilishana salamu za kawaida aliwataka radhi na kumchukua Joram chemba.
"Kaka, samahani. Unajua pamoja na kujiita kwako Charles Morris, ni watu wachache sana ambao waliamini? Sura yako si ngeni kabisa hapa Kenya. Umetokea mara nyingi katika magazeti na televishani. Wewe ni yule mpelelezi mashuhuri Joram Kiango. Sivyo, kaka?"
Joram alipochelewa kumjibu, James aliendelea, "Ziko habari mbaya zilizotokea katika vyombo vya habari. Inasemekana umetoroka kwenu ukiwa umechukua fedha nyingi za kigeni. Kwa jinsi ninavyokufahamu nashindwa kuamini kama ni kweli. Lakini hilo si muhimu sana kwa sasa. Nilichofuata ni kukufahamisha kwamba sasa hivi wapelelezi wa hoteli hii wamekaa kikao wakilijadili suala lako. Waweza kutiwa msukosuko mkubwa. Kwa hiyo, nakushauri utafute mbinu yoyote ambayo itakufanya uokoe maisha yako. Nina ndugu yangu anayeishi Nyeri. Anaweza kukuficha kwa muda."
Joram alicheka na kumshukuru James. "Usijali rafiki yangu. Nitajua la kufanya. Kwa sasa niache nijipumzishe kidogo na kufikiria la kufanya." Baada ya hayo aliutia mkono wake mfukoni na kuutoa ukiwa umeshikilia noti kumi za mia mia ambazo zilidakwa na James kabla hazijamfikia. "Kajipatie bia mbili," alimwambia akigeuka na kurudi chumbani.
"Unaona Joram? Twende zetu ofisi ya Ubalozi," Nuru alimdaka juujuu kwa maneno hayo.
"Kufanya nini?" Joram alizungumza kwa upole kama kawaida yake. "Tutakwenda zetu tunakotaka. Sasa hivi uwe binti mtulivu na ufanye kama nitakavyokuambia, tafadhali. Baada ya dakika chache tutakuwa zetu angani tukielekea katika mji mwingine wenye starehe kuliko huu."
"Haiwezekani, Joram. Lazima ukaombe radhi na kurudisha pesa za watu," Nuru aliendelea kukanusha.
"Alikuwa ameishi na Joram kwa muda mrefu. Lakini alikuwa hajapata kumuona Joram anavyokasirika. Leo hii aliziona hasira zake. Aliiona nuru kali na tena baridi, ikijitokeza katika sauti yake ndogo, nzito, aliposema taratibu, "Haya. Nenda zako ofisi za Ubalozi. Chukua na pesa zetu uwapelekee."
***
Dakika mbili tatu baadae mzee mmoja wa kiume, mwenye mvi nyingi na ndevu za kutosha alionekana akitoka katika hoteli hiyo. Alikuwa kafatana na kijana wa kiume mwenye sura nzuri ambaye alikifunika kichwa chake kwa kofia pana na macho kwa miwani ya jua. Mikononi mwao walikuwa na mifuko yao. Wafanyakazi waliowatazama wakiondoka hawakuweza kukumbuka wageni hawa waliingia lini na iwapo walikuwa katika vyumba vipi. Waliwasindikiza kwa macho hadi walipotoka nje na kukodi teksi.
Kati ya wafanyakazi walioshuhudia wakiondoka ni James Kamau. Hata ndoto haikumjia kuwa alikuwa akiwatazama Joram Kiango na Nuru wakiondoka.
6
SAA chache walikuwa angani tena, katika Ndege ya Shirika la Ndege la Uingereza, wakielekea London kupitia Cairo, Misri.
Sasa habari za "Wizi wa Joram" zikiwa zimetapakaa duniani kote, zikienezwa na kila chombo cha habari, haikuwa kazi ndogo kwao kuipata fursa hii ya kuiacha nchi ya Kenya. Polisi mitaani na katika vituo vyote vya usafiri walikuwa macho wakimtazama kila mtu ambaye alielekea kufanana na Joram. Passport na vitambulisho vyao vilitazamwa kwa makini zaidi, huku maswali mengi yakiulizwa. Hata hivyo, Joram na Nuru walifaulu kupenya vizingiti vyote huku wakicheka kimoyomoyo, kwani askari hao hawakuwatazama kabisa kwa jinsi walivyojibadili kimavazi na kitabia, kinyume kabisa cha matarajio ya askari.
Nuru aliuficha uzuri wake kwa kuiondoa ile hali ya uvulana aliotoka nayo hotelini na kujivika nywele zilionekana nusu zingemezwa na mvi. Mavazi yake pia yalikuwa yale ambayo vijana wasingependa kuyatupia macho zaidi ya mara mbili. Jambo ambalo lilifanya wawe sawa na huyu mzee mkongwe aliyekuwa akitembea kidhaifu, mfuko mgongoni na mkwaju mkononi. Hali zao pia zilikuwa za wakazi halisi wa Nairobi. Hati zao za halali pamoja na picha zao zilifichwa vilivyo katika mifuko ya siri iliyokuwemo katika mfuko waliorithi toka kwa hayati Chonde.
Ndani ya ndege Joram alitulia akinywa bia aliyoletewa kwa utulivu, huku mara chache akimtupia Nuru maongezi mafupi mafupi. Baada ya muda ambao haukuwa mrefu alipitiwa na usingizi. Aliamka ndege ilipokuwa ikitua katika Uwanja wa Ndege wa Cairo. Misukosuko ya abiria wanaoshuka na kuingia ilipopungua walizungumza na Nuru maongezi machache ambayo dhamira yake kubwa ilikuwa kuwafanya watazamike kama watu wa kawaida wasio na dosari yoyote machoni mwa wasafiri wengine.
Safari ilipoanza tena Joram alikiweka kiti chake katika hali ya kulala akimwacha Nuru akipekua kitabu chake kutafuta alipokuwa ameishia. Ikiwa safari ndefu, ya kuvuka bahari kubwa kama hii ya Atlantic, Joram alikusudia kutumia vyema kufidia usingizi ambao hakuupata kiukamilifu alipokuwa Nairobi. Na ndivyo ilivyomtukia. Hakupata nafasi ya kuyafumbua macho yake kuyatazama maji mengi yaliyotapakaa kote. Alipoamshwa na Nuru na kutazama dirishani, alishangaa kuona wakizunguka juu ya Jiji la London wakisubiri kutua.
"Imekuwa safari fupi kuliko nilivyotegemea," alisema.
"Hata! Ilikuwa safari ndefu sana kama ilivyo," lilikuwa jibu la Nuru.
Taratibu, ndege ikashuka na kutua bila msukosuko wowote katika uwanja mashuhuri wa Heathrow. Pilikapilika za abiria kuchukua mizigo na kutaka kutoka mapema zikaanza. Joram na Nuru, wakiwa miongoni mwa abiria walioshuka mwisho, walichukua mizigo yao na kupita katika ofisi za forodha na abiria wengine waliokuwa wakisubiri usafiri.
Dereva mmoja, msichana, wa shirika la usafiri la Avis and Hertz, aliwafuata na kuwashawishi kuingia katika gari lake. Akawapeleka mjini katika Hoteli maarufu duniani ya Wilson Place ambapo walijipatia chumba maridadi. Mapokezi yakiwa ya kistaarabu, huduma za kistaarabu, na wahudumu waliosomea ustaarabu, yote yaliwafanya waone kama wako nyumbani badala ya ugenini, jambo ambalo liliwafanya wasijali chochote juu ya malipo makubwa yanayodaiwa na hoteli hiyo.
Kuna mzungu mmoja, mshairi, au mpenzi tu wa taifa lake ambaye aliwahi kusema: "When a man is tired of London, he is tired of life for there is all that life can afford," kwamba binaadamu anayekinaishwa na Jiji la London basi amekinaishwa na maisha kwa ujumla kwani London inacho kila kitu ambacho maisha ya binaadamu yanahitaji. Joram na Nuru wasingemwona mtu huyo kuwa mwongo sana. Pamoja na kwamba wote hawakuwa wageni sana wa jiji hili, macho yao yaliendelea kuvutwa na vitu mbalimbali siku yao ya pili walipoamua kuzunguka jijini.Walikodi gari lililowatembeza kila mahali kufuata matakwa yao. Kwanza, walipenda kuona mto ule maarufu unaougawa mji wa London, Thames. Waliyatazama maji yake yanayopita kwa utulivu pamoja na madaraja yake murua. Kisha walizunguka katika miji ya Kingstone, Bromley, Croyon na kwingineko, wakiona mambo tofautitofauti katika mitaa mashuhuri kama Oxford, Kingsway, Dean na Sheftebury. Usiku ulipoingia walikwenda katika jumba la Her Majesty kutazama michezo ya kuigiza.
"Kesho tutakwenda kutembea Epping Forest," Joram alimnong'oneza Nuru walipokuwa wakirudi hotelini kwao.
"Ningependa kuingia Richmond Park," Nuru alimjibu.
"Nilipokuja kozi hapa miaka minne iliyopita nilidhamiria kuingia lakini sijui ilikuwaje nikashindwa, safari hii nisingependa kushindwa tena."
"Huwezi kushindwa. Tuna muda na pesa. Tutafanya kila kitu ambacho roho itatutuma kufanya. Nafasi kama hii hutokea mara chache sana katika miaka ya maisha yote ya binaadamu."
Chumbani kwao walivua uzee na kuurudia ujana wao. Wakatazamana na kucheka kidogo. Kisha walikumbatiana na kuongozana kitandani. Muda mfupi baadaye Nuru alikuwa akikoroma taratibu, huku Joram akinyata kukiacha kitanda. Aliiendea mizigo yao na kuikagua kwa makini. Kila kitu kilikuwemo kama kilivyokuwa kimehifadhiwa. Akatoa kile kisanduku chenye vigololi na kuvitazama kwa makini. Kisha alivirudisha na kuchukua vitabu vyake ambavyo alikuwa akivisoma au kufanya majaribio ya maandishi na mahesabu kwa umakini na utulivu. Mara kwa mara alichana karatasi hii na kujaribu ile, mara akiacha kuandika na kuanza kusoma kwa umakini, kisha akianza tena kuandika.
"Siwezi kukusaidia mpenzi?"
Sauti ilimzindua Joram kutoka katika lindi hilo la shughuli iliyokuwa mbele yake. Aligeuka na kumtazama Nuru ambaye alitulia nyuma yake, uchi kama alivyozaliwa, macho yake yakitazama mahesabu katika karatasi za Joram.
"Samahani kwa kukuvuruga. Nimekuwa nyuma yako kwa zaidi ya saa nzima sasa. Nadhani hata hujui kuwa kumepambazuka."
Ndipo Joram alipotupa macho nje. Hakuamini. Nuru ya jua lililochomoza kitambo ilikuwa ikipenya dirishani kwa uangalifu. "Samahani Nuru. Usingizi ulinipaa ndipo nikaja mezani kupoteza muda," alisema akianza kufunika karatasi zake.
"Kupoteza muda?" Nuru alimwuliza. "Nimekutazama kwa muda mrefu sana. Hata kuna nyakati ambazo ulikuwa ukisema peke yako. Najua una jambo ambalo linakusumbua, jambo ambalo umeamua kuliweka siri rohoni mwako. Hutaki kunishirikisha. Huniamini hata kidogo! Sijui nifanye nini ili uniamini Joram!"
"Ndiyo. Afanye nini ili amwamini?" Joram alijiuliza. Msichana huyo ambaye ameacha kila kitu hata kazi na nchi yake ili awe pamoja naye! Msichana ambaye kuwa nae kumemsaidia sana katika kujifariji na msiba wa Neema na aibu aliyoipata kwa kushindwa kumuua Proper! Msichana ambaye majuzi tu aliyaokoa maisha yake kwa kumwua mtu ambaye angemwangamiza bila huruma! Zaidi ni msichana mzuri wa sura na tabia, msichana ambaye ni ndoto ya kila mwanaume!
“Sikia Joram, huwezi kukadiria kiasi gani nakuamini na kukutegemea. Sifai kuambiwa lolote. Kwako mimi ni mwanamke tu ninayefaa kwa mapenzi ya kimwili. Siwezi kuwa Neema ambaye alikuwa mwenzi wako kikazi ambaye kimwili hukuwahi kumgusa.”
“Sivyo Nuru.”
“Wala sifahi lolote hata kukusaidia katika hesabu za fizikia unazopiga au kusoma maandishi hayo na kuyalinganisha na hayo ya kijasusi kama unavyofanya. Sifai hata kwenda maktaba kukusaidia kupekua walao kitabu unachokihitaji.”
“Nuru!” Joram alifoka kwa sauti ambayo masikioni mwa mtu asiyemfahamu ingekuwa ya kawaida tu. “Nilidhani wewe ni mtu pekee unayeweza kunielewa. Nilidhani unaifahamu tabia na msimamo wangu. Sina tabia ya kuyachukua matatizo yangu na kuyabwaga mikononi mwa binadamu mwingine. Sijazowea kuchukua fumbo ambalo limenishinda kufumbua na kumwomba mtu mwingine anisaidie. Wala tabia hiyo siwezi kuianza leo. Hivyo, ninapokuambia sina la kukuambia maana yake sina la kukuambia. Nadhani umenielewa.”
"Nadhani nimekuelewa. Hata zile pesa ulizozipokonya City Drive, ambazo tunachezea sasa naamini ni fumbo jingine ambalo hukupenda kulifumbua. Sivyo mpenzi?"
Joram akatabasam, "Yaelekea mimi na wewe tutakuwa na safari ndefu kimaisha."
Wakashikana mikono na kurudi kitandani.
***
Baada ya kuzitawala na kuzinyonya sana nchi zetu nyingi za Kiafrika, na baada ya 'kutoa' uhuru shingo upande, Uingereza iliendelea kujifanya baba na mama wa makoloni yake ya awali. Falsafa hii ndiyo chanzo cha vijimsaada kadha wa kadha. Eti pia Uingereza ndiyo mtaalamu wa habari zinazohusu nchi zilizokuwa chini ya himaya yake. Na habari ambazo hupata nafasi katika vyombo vya habari mara nyingi huwa ni zile ambazo si nzuri sana kwa masikio ya wasikilizaji, yaani habari za aibu, kushindwa, rushwa udikteta, uzembe na kadhalika. Uteuzi huu wa habari hizo mbovu na kuacha zile njema ni ushahidi mwingine ambao huonyesha kuwa Uingereza ingependa kuendelea kuitawala Afrika hadi siku ya mwisho ya dunia.
Habari za wizi wa fedha za kigeni katika Tanzania zilikuwa tamu mno katika magazeti, redio na televisheni zote za Uingereza. Zilipambwa kwa wino na rangi mbalimbali na uongo ainaaina hata zikawa kubwa kuliko zilivyostahili kuwa. Hiyo ilitokana hasa na mwizi wa pesa hizo alivyokuwa mtu maarufu duniani. "Ndivyo walivyo waafrika..." liliandika gazeti moja."Kati yao hakuna mwaminifu..." Gazeti jingine lilipendekeza kuwa Tanzania isipate msaada wowote wa kimataifa bila ya pesa hizo kurudishwa. "Tunaamini kilichofanyika ni njama tu baina ya Joram na viongozi wa serikali yake," Televishen moja ilitangaza.
Habari hizo zilianza kuwa za kawaida machoni na masikioni mwa Joram na Nuru. Hawakuzijali wala kuzishughulikia. Hata hivyo, kuna gazeti hili ambalo liliwashtua zaidi. Mwandishi wake alikuwa amesafiri hadi Dar es Salaam ambako alifanya utafiti wake binafsi, akihonga hapa na kuiba habari pale hata akawa ameunganisha taarifa ambayo ilidai kuwa Joram alikuwa ametorokea Nairobi kwa ndege ya kukodi. Mwandishi huyo alisafiri hadi Nairobi ambako utafiti wake ulimfikisha katika chumba alichokuwa Joram na Nuru kwa majina bandia. "Kwa kila hali sasa hivi Joram yuko London," lilieleza gazeti hilo. "Dunia haiwezi kupumbazwa na hila zake za kujibadili sura na umbile. Kwa hali ilivyo, atakuwa akiishi katika hoteli kubwa kwa jina la bandia.”
"Imekuwa tabia ya kawaida," gazeti hilo liliendelea kueleza. "Kila wanapofanya madhambi yao huko kwao hukimbilia huku. London imejaa watu weusi ambao wanaishi wanavyotaka baada ya kufanya maovu - au mema ambayo yalionekana maovu - huko makwao. Wako wachoyo, wahujumu, wazembe, wanafiki na kadhalika. Wengi wameziacha nchi zao zikiwa masikini zaidi huku roho za watu zikiteketea katika vita na mauaji yasiyo na mwisho. Uingereza tunawakaribisha na kuishi nao kama binadamu wenzetu. Miongoni mwa watu hawa sasa yumo Joram Kiango, mtu aliyejifanya na akaaminika kuwa ana roho ya kipekee yenye upendo na ushujaa kama ngao kwa jamii yake. Kumbe alikuwa fisi katika ngozi ya kondoo. Huyu, Uingereza haiwezi kumstahamili. Lazima apatikane, ahukumiwe na kupokonywa kila senti aliyobaki nayo.”
Nuru alimaliza kuisoma habari hii huku akitetemeka kidogo. Lakini ilimshangaza alipoinua uso na kukutana na ule wa Joram ambao ulikuwa ukichekelea. Hilo lilimshangaza. Akiwa mtu ambaye ameishi na Joram kwa kipindi cha kutosha, alikuwa na hakika kuwa amemfahamu Joram vya kutosha. Asingelaghaika kama watu wengine kung'amua wakati gani anacheka kwa hasira na wakati upi anajifanya kuchukia hali amefurahi. Tabasamu hili, ambalo lilikuwa likiendelea kuchanua katika uso wa Joram, halikuwa tabasamu batili, bali tabasamu halisi, tabasamu ambalo huutembelea uso huu kwa nadra sana. Hivyo, ilimshangaza sana Nuru. Alimtegemea Joram kujisingizia kucheka huku rohoni akibabaika na kukata tamaa. Si kushangilia kama aliyepata tuzo au ushindi mkubwa baada ya shindano gumu.
"Sijakuelewa Joram, sidhani kama hii ni habari njema," alimwambia.
"Wala sidhani kama una haki ya kutegemea habari njema tangu ulipokubali kuandamana na mwizi mkubwa kama huyu," Joram alimjibu taratibu. Alipoona uso wa Nuru bado una maswali na dalili za kutoridhika, aliongeza, "Kinachonichekesha ni huyu Mwingereza anavyojifanya ana uchungu na nchi yetu kuliko sisi wenyewe. Utafiti aliofanya hautokani na moyo wake wa kuwajibika bali ni nguvu alizonazo kiuchumi, uwezo ambao ameuiba toka katika makoloni miaka nenda rudi." Alikohoa kidogo kabla ya kuongeza, “Hawawezi kunitisha kabisa. Nitaishi hapa nikistarehe katika jiji hili kubwa ambalo linapendeza kwa madini yaliyoibwa toka makwetu, yaliyochimbwa kwa jasho la babu zetu. Nitaondoka hapa tu tutakapokuwa tayari kuondoka. Sivyo, dada Nuru?"
"Nilichosema ni jinsi unavyoifurahia habari hii badala ya kuionea aibu. Sikutegemea. Au nakosea. Pengine hili ni fumbo jingine?"
Joram hakumjibu.