RIWAYA: KISU CHENYE MPINI MWEKUNDU
MTUNZI: Ahmad Mussa Mniachi
SEHEMU YA KUMI
Aliondoka pale nyumbani huku akikabiliwa na mtihani mgumu kwa mke wa Gervas.
Atampata vipi ili amweleze ukweli wa mambo. Iwapo atamueleza kweli haitamletea
matatizo. Aliona wazi kuwa kuna hatari ya kushtakiwa kwa kueneza maradhi wakati
anajua wazi kuwa yeye ni muathirika. Lakini kama angeweka wazi kweli angepata ule
msaada? Angeupata vipi wakati Gervas alikataahata fedha. Kwanini Gervas ambaye
kafunga ndoa kanisani atake liwazo lingine nje ya ndoa? Labda haya ni malipo mazuri
ya usaliti. Hapana lazima nimuokoe mkewe, nitajibu nini mbele ya Mungu kama yule
mwanamke atakufa kwa ajili yangu? Alijiuliza maswali mengi bila kupata njia sahihi ya
kumnusuru mwanamke mwenzake.
Maandishi makubwa ya shule ya Sekondari Mbagala yalimzindua kutoka kwenye lindi
la mawazo. Akatembea moja kwa moja kuelekea ofisi ya mkuu wa shule. Alikuwa hajui
kama afurahi au ahuzunike. Kitendo cha kupata nafasi ile baada ya kuudhalilisha utu
wake kilimuumiza sana. Alitamani amfanye jambo baya Gervas ambaye alimfanyia
mambo yale bila hiyari yake upande mwingine ukamwambia kuwa hakuwa na sababu
ya kufanya yote yale adhabu aliyoipata ilitosha.
Akaingia moja kwa moja kwenye ofisi ya walimu. Hakukuwa na mwalimu yeyote,
akafuata kidirisha kidogo kilichoandikwa MAPOKEZI.
Habari yako dada.
Nzuri nikusaidie nini?
Naomba kuonana na mkuu wa shule.
Una tatizo gani?
kuna barua inabidi nimfikishie imetoka kwa Afsa elimu taaluma.
Ni barua ya kikazi au binafsi?
Ni barua ya kikazi.
Naomba hiyo barua. Akampa. Yule dada akaisoma kisha akagonga muhuri.
Nifuate. Akafungua mlango na kuja kule nje aliko mama Beda. Akamfuata.
kaa hapo. Akakaa sehemu iliyoandikwa wageni.
Akaingia kwenye ofisi iliyoandikwa MKUU WA SHULE . Baada ya dakika kama kumi
na tano yule dada akatoka. Akampa karatasi nyingine zipatazo nne. Mwanafunzi
amekubaliwa kujiunga lakini inabidi ujitahidi ndani ya wiki mbili awe amesharipoti.
Aliongea yule dada.
Ahsante.Alisikika mama Beda huku akipiga hatua kuiacha ofisi ile.
* * *
Muda wa masomo ulikuwa umeisha wanafunzi wa Zanaki walianza kuondoka
madarasani. Vick nisubiri nina maongezi kidogo na wewe. Alisikika kijana mmoja wa
kidato cha nne akimsimamisha Vick. Shikamoo. Aliamkia Vick
Aah. Noma hiyo hakuna mzee wa kuamkiwa hapa mambo.
Poa. Alijibu Vick huku moyo ukienda mbio.
Unajua Vick natafuta nafasi ya kuongea na wewe siku nyingi lakini siipati.
kwanza nani kakutajia jina langu?
Mtu ukimpenda tu lazima utajua jina lake.
unasema unatafuta nafasi ya kuongea na mimi, haya umeipata ongea basi? alisikika
Vick huku akianza kushikwa na hasira.
Neno langu ni fupi sana nakupenda Vick. Vick hakujibu badala yake alitoka mbio.
Vipi alikuwa anakuambia nini yule kaka mbona umetoka mbio? Aliuliza Zuwena
mwanafunzi aliyekuwa anasoma nae darasa moja.
Eti anasema ananipenda.
Mh. Mwenzangu kweli yule kaka ni fataki Ziada, Pili na mimi sote katutongoza
anataka amalize form one wote bora tumsemee kwa mkuu wa shule
Achana nae atatupotezea muda bure.
Wakafika getini kila mmoja akaelekea upande wake. Mbagalaa
Mbagalaa
Konda
alimshitua vick ambaye alikuwa kwenye dimbwi la fikra. Akakimbilia lile gari.
Ilikuwa ni safari ya dakika arobaini na tano kufika rangi tatu. Aliteremka pale kituoni
na kupanda kwenye daladala lililokuwa linaelekea kongowe. Mawazo yake yote
yalikuwa kwa Beda. Alitaka kujua kama mpango wa kupata shule umefanikiwa. Hivyo
alipofika nyumbani tu alibadili nguo haraka na kuondoka. Hakukumbuka hata kula.
Ulikuwa ni umbali wa dakika kama Thelathini kwa miguu lakini alijikuta akitumia
dakika ishirini tu.
Karibu Vick, ulikuwa unatamani kumuona mama yangu leo umemkuta. Alisikika
Beda akimkaribisha.
Oooh mwanangu huyo. mama Beda akamkumbatia Vick kwa furaha.
Karibu sana mwanangu.
Ahsante mama shikamoo.
Marahaba mwanangu hamjambo huko nyumbani?
hatujambo mama . Alijibu Vick huku akiminyaminya vidole vyake kwa haya.
Akatembea taratibu hadi pale alipokaa Beda wakapeana mikono.
Vipi umepata shule?
Nimepata Vick, Mungu atakulipa kwa wema ulionifanyia. aliongea kwa sauti ya
kunongona lakini ilifika kwenye masikio ya mama yake.
wapi?
Mbagala sekondari.
Hongera.
Ahsante.
Nilitaka kujua kama umepata shule, nashukuru kama umepata kwa heri.
Mbona mapema?
Hata chakula sijala nisije nikazusha maswali.
Ahsante kwa moyo wako mwema Akamuaga mama Beda, akaondoka
****
Alipanda ngazi taratibu kuelekea katika ofisi ya afisa elimu taaluma. Moyo wake
ulikuwa unapiga kwa kasi. Alijua wazi kuwa anayemwendea hayupo ofisini. Alikaa nje
ya ofisi muda mrefu akisubiri aondoke. Ni fursa hiyo ndiyo aliyoisubiri sana. Bahati
Ilikuwa upande wake kwani yule mtu aliondoka nusu saa kabla ya muda wa kazi
kumalizika. Hakutamani kabisa kuonana naye. Licha ya msaada aliompa bado
alimchukia kuliko mtu yeyote. Bila ridhaa yangu. Aliwaza kwa huku akisaga meno kwa
hasira.
Alikumbuka kuwa jana yake alikuwa hapa. Hakuwa na bahati kwani mlengwa alikuwa
miongoni mwa watu wa mwisho kutoka pale ofisini. Akafika hadi pale mapokezi
alipofikia siku ya kwanza. Ilikuwa ofisi ya mapokezi. Alimkumbuka vema yule dada
aliyempokea siku ya kwanza ingawa yule dada alimsahau mama Beda. Habari dada.
Alisalimia mama Beda.
Nzuri nikusaidie nini?
Naweza kumuona Mr. Gervas?
Hapana ameondoka, mpaka kesho.
Unaweza kunielekeza nyumbani kwake?
Anaishi Kimara baruti, si mbali sana kutoka kituoni. Kama unatoka kariakoo ukishuka
kituoni nenda upande wa kushoto, fuata mtaa wenye maduka mwisho kabisa utakuta
saluni imeandikwa Mama K uliza hapo au nenda mbele kuna kanisa la mabati pia
unaweza kuuliza hapo kanisani kwani mkewe ni mwekahazina hapo kanisani.
Sina swali amemaliza kazi. Aliwaza mama Beda huku moyoni akiwa na furaha kubwa.
Huyu dada kanisaidia sana sasa nina uhakika wa kumnusuru Mrs. Gervas. Aliendelea
kuwaza mama Beda. Akaondoka akiwa mwenye furaha kubwa sana.
Kimara baruti, kituo cha kwanza mtaa wenye maduka uliza Mama K saluni au kanisani,
kanisani ni kuzuri zaidi. Aliwaza huku akichukua beseni lake la matunda ambalo
aliliacha getini kwa mlinzi. Huyo, akaendelea kukata mitaa mbalimbali ya jiji hili lenye
kila aina ya raha na karaha. Akauza, akauza
. Alipofika Mtongani Beseni lilikuwa tupu.
Akapanda daladala ambalo lilimfikisha mbagala rangi tatu.
ITAENDELEA....